Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 88

Mabadiliko Katika Hali ya Tajiri na Lazaro

Mabadiliko Katika Hali ya Tajiri na Lazaro

LUKA 16:14-31

  • MFANO WA TAJIRI NA LAZARO

Yesu amekuwa akiwashauri wanafunzi wake kuhusu kutumia utajiri wa kimwili. Lakini si wanafunzi peke yao wanaomsikiliza. Mafarisayo pia wako hapo na wanapaswa kufuata ushauri wa Yesu. Kwa nini? Kwa sababu ‘wanapenda pesa.’ Wanaposikia mambo anayosema Yesu ‘wanaanza kumdhihaki.’—Luka 15:2; 16:13, 14.

Hata hivyo, Yesu haogopeshwi na jambo hilo. Anawaambia: “Mnajitangaza kuwa waadilifu mbele ya wanadamu, lakini Mungu anaijua mioyo yenu. Kwa maana kitu kinachoheshimiwa sana na wanadamu kinamchukiza Mungu.”—Luka 16:15.

Kwa muda mrefu Mafarisayo ‘wameheshimiwa sana na wanadamu,’ lakini sasa ni muda wa mabadiliko, muda wa kubadili kabisa mambo. Watu wanaoheshimiwa sana walio na utajiri wa vitu vya kimwili, mamlaka ya kisiasa, na ushawishi wa kidini watashushwa. Watu wa kawaida wanaotambua uhitaji wao wa kiroho watainuliwa. Yesu anaonyesha wazi kwamba mabadiliko makubwa yanatendeka anaposema:

“Sheria na Manabii walikuwa mpaka Yohana. Tangu wakati huo, habari njema za Ufalme wa Mungu zinatangazwa, na watu wa namna zote wanajitahidi kuufikia. Kwa kweli, ni rahisi zaidi kwa mbingu na dunia kupitilia mbali kuliko sehemu yoyote ya herufi ya Sheria kukosa kutimia.” (Luka 3:18; 16:16, 17) Maneno ya Yesu yanaonyeshaje kwamba mabadiliko yanafanyika?

Viongozi wa dini wa Kiyahudi wanadai kwa kiburi kwamba wanafuata Sheria ya Musa. Kumbuka kwamba Yesu alipomponya kipofu huko Yerusalemu, Mafarisayo walisema hivi kwa kiburi: “Sisi ni wanafunzi wa Musa. Tunajua kwamba Mungu alizungumza na Musa.” (Yohana 9:13, 28, 29) Kusudi moja la Sheria iliyotolewa kupitia Musa lilikuwa kuwaelekeza watu wanyenyekevu kwa Masihi, yaani, Yesu. Yohana Mbatizaji alimtambulisha Yesu kuwa Mwanakondoo wa Mungu. (Yohana 1:29-34) Kuanzia kwa huduma ya Yohana, Wayahudi wanyenyekevu, hasa walio maskini, wamekuwa wakisikia kuhusu “Ufalme wa Mungu.” Naam kuna “habari njema” kwa wote wanaotaka kuwa raia wa Ufalme wa Mungu na kufaidika kutokana nao.

Sheria ya Musa haijakosa kutimizwa; badala yake, imewaelekeza kwa Masihi. Isitoshe, wajibu wa kuifuata unakwisha. Kwa mfano, Sheria ilikubali talaka kwa sababu mbalimbali, lakini sasa Yesu anaeleza kwamba “kila mtu anayempa talaka mke wake na kuoa mwingine anafanya uzinzi, na yeyote anayemwoa mwanamke aliyepewa talaka na mumewe anafanya uzinzi.” (Luka 16:18) Maneno hayo yanawakasirisha sana Mafarisayo wanaopenda kutunga sheria!

Sasa Yesu anasimulia mfano unaokazia mabadiliko makubwa ambayo yanafanyika. Unawahusu watu wawili—ambao cheo, au hali za kila mmoja wao zinabadilika sana. Unapochunguza mfano huo, kumbuka kwamba kati ya wale wanaosikiliza ni Mafarisayo wanaopenda pesa na ambao wanaheshimiwa sana na watu.

Yesu anasema: “Kulikuwa na tajiri ambaye alikuwa akivaa mavazi ya zambarau na kitani, na alifurahia maisha ya kifahari siku kwa siku. Lakini mtu fulani aliyekuwa akiombaomba aliyeitwa Lazaro, alikuwa akiletwa kwenye lango lake. Alikuwa na vidonda mwili mzima, naye alikuwa akitamani kula mabaki yaliyoanguka kutoka kwenye meza ya yule tajiri. Ndiyo, pia, mbwa walikuwa wakija na kuramba vidonda vyake.”—Luka 16:19-21.

Mafarisayo wanapenda pesa, basi je, kuna shaka kuhusu watu ambao Yesu anazungumzia anapomtaja yule “tajiri”? Viongozi hao wa dini ya Kiyahudi pia wanapenda kuvaa mavazi ya kifahari ya bei ghali. Na zaidi ya utajiri ambao huenda wanao, wanaonekana kuwa matajiri kutokana na mapendeleo na nafasi walizo nazo. Naam, kuwalinganisha na mtu aliyevalia mavazi ya kifalme ya zambarau kunaonyesha hali yao ya kuheshimika, na kitani cheupe kinawakilisha jinsi wanavyojiona kuwa waadilifu.—Danieli 5:7.

Viongozi hao matajiri wenye kiburi wanawaonaje watu wa kawaida walio maskini? Kwa dharau wanawaona kuwa am ha·’aʹrets, au watu wa nchi (dunia), ambao hawajui Sheria wala hawastahili kufundishwa Sheria. (Yohana 7:49) Hilo linaonyesha hali ya ‘maskini aliyeitwa Lazaro,’ ambaye anatamani “kula mabaki yaliyoanguka kutoka kwenye meza ya yule tajiri.” Kama Lazaro aliyejaa vidonda, watu wa kawaida wanadharauliwa, kana kwamba ni wagonjwa kiroho.

Hali hiyo ya kuhuzunisha imekuwa ikiendelea kwa muda sasa, lakini Yesu anajua kwamba wakati umefika wa mabadiliko makubwa katika hali ya wale walio kama yule tajiri na wale walio kama Lazaro.

MABADILIKO KATIKA HALI YA TAJIRI NA LAZARO

Yesu anaendelea kufafanua mabadiliko hayo makubwa. Yesu anasema: “Baada ya muda yule mtu aliyekuwa akiombaomba akafa, malaika wakambeba na kumpeleka kando ya Abrahamu. Pia, yule tajiri akafa na kuzikwa. Akiwa Kaburini akatazama juu, akiteseka sana, akamwona Abrahamu kwa mbali na Lazaro akiwa kando yake.”—Luka 16:22, 23.

Wale wanaomsikiliza Yesu wanajua kwamba Abrahamu alikufa zamani na yuko Kaburini. Maandiko yanaonyesha wazi kwamba mtu aliye Kaburini, au Sheoli, hawezi kuona wala kuzungumza, kutia ndani Abrahamu. (Mhubiri 9:5, 10) Basi, viongozi hao wa kidini wanafikiri Yesu anamaanisha nini anaposimulia mfano huo? Anafundisha nini kuhusu watu wa kawaida na viongozi wa dini wanaopenda pesa?

Yesu ametaja mabadiliko aliposema ‘Sheria na Manabii walikuwa mpaka Yohana, lakini tangu wakati huo habari njema za Ufalme wa Mungu zinatangazwa.’ Basi, kupitia kazi ya kuhubiri ya Yohana na Yesu Kristo, Lazaro na tajiri wanakufa kuhusiana na hali zao za zamani, nao wanapata hali mpya kuhusiana na Mungu.

Hasa watu wanyenyekevu na maskini wamekuwa na njaa kiroho kwa muda mrefu. Lakini wanasaidiwa wanapokubali ujumbe kuhusu Ufalme uliohubiriwa kwanza na Yohana Mbatizaji kisha na Yesu. Mwanzoni, walikula ‘mabaki yaliyoanguka kutoka kwenye meza ya kiroho’ ya viongozi wa kidini. Sasa wanalishwa kweli muhimu za Kimaandiko, hasa mambo mazuri sana ambayo Yesu anafundisha. Ni kana kwamba mwishowe wako katika nafasi ya pekee machoni pa Yehova Mungu.

Kinyume chake, viongozi wa kidini walio matajiri na mashuhuri wanakataa kukubali ujumbe wa Ufalme ambao Yohana alitangaza na ambao Yesu amekuwa akihubiri kotekote nchini. (Mathayo 3:1, 2; 4:17) Hata wanakasirishwa na kuteswa na ujumbe huo unaozungumzia hukumu inayowaka kama moto kutoka kwa Mungu. (Mathayo 3:7-12) Viongozi wa kidini wanaopenda pesa wangefurahi ikiwa Yesu na wanafunzi wake wangeacha kutangaza ujumbe wa Mungu. Viongozi hao ni kama tajiri katika ule mfano, anayesema: “Baba Abrahamu, nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake katika maji aupoze ulimi wangu, kwa maana ninateseka sana katika moto huu mkali.”—Luka 16:24.

Lakini haitakuwa hivyo. Wengi kati ya viongozi wa kidini hawatabadilika. Walikataa “kumsikiliza Musa na Manabii,” yaani, maandishi ambayo yalipaswa kuwaongoza wamkubali Yesu kuwa Masihi wa Mungu na Mfalme. (Luka 16:29, 31; Wagalatia 3:24) Wala hawajinyenyekezi na kukubali kufundishwa na maskini wanaomkubali Yesu na walio na kibali cha Mungu. Kwa upande wao, wanafunzi wa Yesu hawawezi kulegeza msimamo au kupunguza uzito wa ukweli ili tu kuwafurahisha viongozi wa kidini na hivyo kuwapa kitulizo. Katika mfano wake, Yesu anaeleza ukweli huo kupitia maneno ambayo “Baba Abrahamu” alimwambia yule tajiri:

“Mwanangu, kumbuka wewe ulikuwa na vitu vingi vizuri maishani, naye Lazaro aliteseka sana. Hata hivyo, sasa anafarijika lakini wewe unateseka. Isitoshe, kuna shimo kubwa kati yetu nanyi, hivi kwamba wale wanaotaka kuvuka kutoka hapa kuja kwenu hawawezi, wala watu hawawezi kuvuka kutoka huko na kuja kwetu.”—Luka 16:25, 26.

Ni jambo la haki na linalofaa kwamba mabadiliko hayo makubwa yamefanyika! Yanatokeza mabadiliko ya hali kati ya viongozi wa kidini wenye majivuno na watu wanyenyekevu wanaokubali nira ya Yesu na mwishowe kuburudishwa na kulishwa kiroho. (Mathayo 11:28-30) Mabadiliko hayo yatakuwa wazi zaidi baada ya miezi kadhaa agano la Sheria litakapokoma na agano jipya kuanza. (Yeremia 31:31-33; Wakolosai 2:14; Waebrania 8:7-13) Mungu atakapomwaga roho yake takatifu siku ya Pentekoste 33 W.K., itakuwa wazi kabisa kwamba wanafunzi wa Yesu ndio walio na kibali cha Mungu, bali si Mafarisayo na wafuasi wao wa kidini.