Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 92

Watu Kumi Wenye Ukoma Waponywa​—Mmoja Ashukuru

Watu Kumi Wenye Ukoma Waponywa​—Mmoja Ashukuru

LUKA 17:11-19

  • YESU AWAPONYA WATU KUMI WENYE UKOMA

Yesu anavuruga mipango ya Sanhedrini ya kutaka kumuua anaposafiri kwenda jiji la Efraimu, lililo upande wa kaskazini mashariki hivi wa Yerusalemu. Anakaa huko na wanafunzi wake, akiwa mbali na maadui wake. (Yohana 11:54) Hata hivyo, Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. inakaribia, kwa hiyo Yesu anasafiri tena. Anasafiri kuelekea kaskazini kupitia Samaria hadi Galilaya, safari yake ya mwisho katika eneo hilo kabla ya kifo chake.

Hapo awali katika safari yake, Yesu akiwa anasafiri kutoka kijiji kimoja kwenda kingine, anakutana na watu kumi wenye ukoma. Katika hatua fulani, ugonjwa huo unaweza kufanya sehemu za mwili ziharibike hatua kwa hatua, kama vile sehemu za vidole vya mikono na miguu, au masikio. (Hesabu 12:10-12) Sheria ya Mungu inasema kwamba mtu mwenye ukoma anapaswa kusema hivi kwa sauti “Mimi si safi, mimi si safi!” na kwamba aishi akiwa ametengwa.—Mambo ya Walawi 13:45, 46.

Kwa hiyo, wale watu wenye ukoma wanasimama mbali kidogo na Yesu. Hata hivyo wanapaza sauti kubwa: “Yesu, Mwalimu, tuhurumie!” Anapowaona watu hao wenye ukoma, Yesu anawaamuru: “Nendeni mkajionyeshe kwa makuhani.” (Luka 17:13, 14) Kwa hiyo, anaheshimu Sheria ya Mungu, ambayo inawapa makuhani mamlaka ya kutangaza kwamba watu waliokuwa na ukoma wamepona. Wanaweza kuanza kuishi tena na watu wasio na ukoma.—Mambo ya Walawi 13:9-17.

Watu hao kumi wenye ukoma wana uhakika kwamba Yesu ana nguvu za kufanya miujiza. Wanaanza safari ya kwenda kuwaona makuhani, hata kabla hawajapona. Wakiwa njiani, wanapata thawabu kwa sababu ya kumwamini Yesu. Wanaanza kuona na kuhisi kwamba wamepona!

Tisa kati ya watu hao wenye ukoma waliotakaswa wanaendelea na safari yao. Mmoja hafanyi hivyo. Mwanamume huyo, Msamaria, anarudi kumtafuta Yesu. Kwa nini? Anathamini sana jambo ambalo Yesu amemfanyia. Mtu huyo aliyekuwa na ukoma ‘anamtukuza Mungu kwa sauti kubwa,’ akitambua kwamba kwa kweli Mungu ndiye amemponya. (Luka 17:15) Anapompata Yesu, anaanguka mbele yake, na kumshukuru.

Yesu anawaambia hivi wale waliomzunguka: “Wote kumi walitakaswa, sivyo? Basi, wako wapi wale wengine tisa? Je, hakuna mwingine aliyerudi ili kumtukuza Mungu isipokuwa mtu huyu wa taifa lingine?” Kisha Yesu anamwambia Msamaria huyo: “Simama uende; imani yako imekuponya.”—Luka 17:17-19.

Kwa kuwaponya watu hao kumi wenye ukoma, Yesu anaonyesha kwamba anaungwa mkono na Yehova Mungu. Kwa sasa mmoja kati ya wale kumi si kwamba ameponywa kupitia matendo ya Yesu tu, bali pia huenda yuko kwenye njia ya uzima. Hatuishi wakati ambao Mungu anamtumia Yesu kufanya miujiza kama hiyo. Hata hivyo, tukiwa na imani katika Yesu, tunaweza kuwa kwenye njia ya uzima—uzima wa milele. Je, tunaonyesha kwamba tuna shukrani kama Msamaria huyo alivyofanya?