Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 114

Kristo Akiwa na Mamlaka Awahukumu Kondoo na Mbuzi

Kristo Akiwa na Mamlaka Awahukumu Kondoo na Mbuzi

MATHAYO 25:31-46

  • YESU ATOA MFANO WA KONDOO NA MBUZI

Akiwa kwenye Mlima wa Mizeituni, Yesu ametoka tu kusimulia mfano wa mabikira kumi na mfano wa talanta. Anamaliziaje jibu lake kwa swali la mitume kuhusu ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo? Anamalizia kwa kutoa mfano wa mwisho, unaohusu kondoo na mbuzi.

Yesu anaanza kwa kueleza jinsi hali itakavyokuwa, anaposema: “Mwana wa binadamu atakapokuja katika utukufu wake, pamoja na malaika wote, ataketi kwenye kiti chake cha ufalme chenye utukufu.” (Mathayo 25:31) Hakuna shaka yoyote kwamba yeye, yaani, Yesu ndiye mhusika mkuu katika mfano huo. Mara nyingi amejiita “Mwana wa binadamu.”—Mathayo 8:20; 9:6; 20:18, 28.

Mfano huo utatimizwa wakati gani? Utatimizwa Yesu “atakapokuja katika utukufu wake” pamoja na malaika na kuketi kwenye “kiti chake cha ufalme chenye utukufu.” Tayari alikuwa amezungumza kuhusu “Mwana wa binadamu [kuja] juu ya mawingu ya mbinguni akiwa na nguvu na utukufu mwingi” pamoja na malaika zake. Jambo hilo lingetokea wakati gani? “Mara tu baada ya dhiki.” (Mathayo 24:29-31; Marko 13:26, 27; Luka 21:27) Basi, mfano huo utatimizwa wakati ujao Yesu atakapokuja akiwa na utukufu. Kisha atafanya nini?

Yesu anaeleza hivi: “Mwana wa binadamu atakapokuja . . . , mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi. Naye atawaweka kondoo kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto.”—Mathayo 25:31-33.

Kuhusu kondoo ambao wanawekwa upande wenye kibali, Yesu anasema: “Ndipo Mfalme atawaambia wale walio kwenye mkono wake wa kuume: ‘Njooni, ninyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, urithini Ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu.’” (Mathayo 25:34) Kwa nini kondoo wanapata kibali cha Mfalme?

Mfalme anaeleza hivi: “Nilikuwa na njaa mkanipa chakula; nilikuwa na kiu mkanipa kinywaji. Nilikuwa mgeni mkanikaribisha vizuri; nilikuwa uchi, mkanivika nguo. Nilikuwa mgonjwa mkanitunza. Nilikuwa gerezani mkanitembelea.” Kondoo hao, “waadilifu,” wanapomuuliza mfalme jinsi walivyofanya mambo hayo mazuri anawajibu hivi: “Kwa kadiri ambavyo mlimtendea aliye mdogo zaidi kati ya hawa ndugu zangu, mlinitendea mimi.” (Mathayo 25: 35, 36, 40, 46) Hawafanyi matendo hayo mazuri wakiwa mbinguni kwa maana huko hakuna wagonjwa au watu wenye njaa. Bila shaka, matendo hayo yanafanywa kwa ajili ya ndugu za Kristo hapa duniani.

Namna gani mbuzi ambao wanawekwa upande wa kushoto? Yesu anasema hivi: “Kisha [Mfalme] atawaambia wale walio kwenye mkono wake wa kushoto: ‘Ondokeni kwangu ninyi mliolaaniwa, nendeni katika moto wa milele aliotayarishiwa Ibilisi na malaika zake. Kwa maana nilikuwa na njaa, lakini hamkunipa chakula, nilikuwa na kiu, lakini hamkunipa kinywaji. Nilikuwa mgeni, lakini hamkunikaribisha; nilikuwa uchi, lakini hamkunivika nguo; nilikuwa mgonjwa na nilikuwa gerezani lakini hamkunitunza.’” (Mathayo 25:41-43) Mbuzi wanastahili hukumu hiyo kwa sababu hawakuwatendea kwa fadhili ndugu za Kristo hapa duniani, kama walivyopaswa kufanya.

Mitume wanajifunza kwamba wakati huo ujao wa hukumu utakuwa na matokeo ya kudumu, yaani, ya milele. Yesu anawaambia: “Ndipo [Mfalme atawaambia]: ‘Kwa kweli ninawaambia, kwa kadiri ambavyo hamkumtendea mmoja wa hawa wadogo zaidi, hamkunitendea mimi.’ Hao watakatiliwa mbali milele, lakini waadilifu watapata uzima wa milele.”—Mathayo 25:45, 46.

Jibu la Yesu kwa swali la mitume linawapa wafuasi wake mambo mengi ya kufikiria, likiwasaidia kuchunguza mitazamo na matendo yao.