Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 120

Kuzaa Matunda Kama Matawi na Kuwa Rafiki za Yesu

Kuzaa Matunda Kama Matawi na Kuwa Rafiki za Yesu

YOHANA 15:1-27

  • MZABIBU WA KWELI NA MATAWI

  • JINSI YA KUENDELEA KUKAA KATIKA UPENDO WA YESU

Yesu amekuwa akiwatia moyo mitume wake waaminifu kwa mazungumzo yanayogusa moyo. Muda umesonga, labda ni usiku wa manane. Sasa Yesu anatoa mfano wenye kuchochea:

Anaanza hivi: “Mimi ndiye mzabibu wa kweli, naye Baba yangu ndiye mkulima.” (Yohana 15:1) Mfano wake unafanana na jambo lililosemwa karne nyingi mapema kuhusu taifa la Israeli, ambalo liliitwa mzabibu wa Mungu. (Yeremia 2:21; Hosea 10:1, 2) Hata hivyo, Yehova analikatilia mbali taifa hilo. (Mathayo 23:37, 38) Basi Yesu anazungumzia jambo jipya. Yeye ndiye mzabibu ambao baba yake amekuwa akiupalilia tangu alipomtia mafuta Yesu kwa roho takatifu mwaka wa 29 W.K. Lakini Yesu anaonyesha kwamba mzabibu huo haumwakilishi yeye peke yake, anaposema:

“[Baba yangu] huliondoa kila tawi ndani yangu lisilozaa matunda, naye hulisafisha kila tawi linalozaa matunda, ili lizae matunda zaidi. . . . Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa matunda likiwa peke yake lisipobaki katika mzabibu, vivyo hivyo hamwezi kuzaa matunda msipokaa katika muungano pamoja nami. Mimi ndiye mzabibu; nanyi ndio matawi.”—Yohana 15:2-5.

Yesu amewaahidi wanafunzi wake kwamba baada ya yeye kuondoka, atamtuma msaidizi, yaani, roho takatifu. Baada ya siku hamsini na moja, mitume na watu wengine wanapokea roho hiyo, na basi wanakuwa matawi ya mzabibu huo. Na “matawi” yote yanapaswa kubaki katika muungano na Yesu. Ili kutimiza jambo gani?

Anaeleza hivi: “Yeyote anayekaa katika muungano pamoja nami, nami katika muungano pamoja naye, huyo huzaa matunda mengi; kwa maana bila mimi hamwezi kufanya lolote kamwe.” Matawi hayo—wafuasi wake waaminifu—wangezaa matunda mengi, kwa kuiga sifa za Yesu, na kuwahubiria wengine kuhusu Ufalme wa Mungu, na kufanya wanafunzi wengi. Namna gani mtu asipobaki katika muungano na Yesu na akose kuzaa matunda? Yesu anaeleza hivi: “Ikiwa yeyote hakai katika muungano pamoja nami, atatupwa.” Kwa upande mwingine, Yesu anasema: “Mkikaa katika muungano pamoja nami, na maneno yangu yakae ndani yenu, ombeni chochote mnachotaka nanyi mtapewa.”—Yohana 15:5-7.

Sasa Yesu anazungumzia jambo ambalo amelitaja mara mbili—kushika amri zake. (Yohana 14:15, 21) Anafafanua njia muhimu ambayo wanafunzi wake wanaweza kuthibitisha kwamba wanafanya hivyo: “Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile ambavyo nimeshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.” Hata hivyo, zaidi ya kumpenda Yehova Mungu na Mwana wake kuna mengi yanayohusika. Yesu anasema: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda. Hakuna mtu aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu atoe uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya mambo ninayowaamuru.”—Yohana 15:10-14.

Baada ya saa chache, Yesu ataonyesha upendo wake kwa kuutoa uhai wake kwa ajili ya wote wanaomwamini. Mfano wake unapaswa kuwachochea wafuasi wake waonyeshane upendo kama huo wa kujidhabihu. Upendo huo ndio utakaowatambulisha, kama Yesu alivyosema hapo awali: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.”—Yohana 13:35.

Mitume wanapaswa kutambua kwamba Yesu anawaita “rafiki.” Anaeleza sababu ya kuwaita hivyo: “Nimewaita rafiki, kwa sababu nimewajulisha mambo yote niliyosikia kutoka kwa Baba yangu.” Huo ni uhusiano wenye thamani sana—kuwa marafiki wa karibu wa Yesu na kujua mambo ambayo Baba alimwambia! Hata hivyo, ili wafurahie uhusiano huo, ni lazima ‘waendelee kuzaa matunda.’ Ikiwa watafanya hivyo, Yesu anasema: “hata mkimwomba Baba jambo lolote katika jina langu, [atawapa].”—Yohana 15:15, 16.

Upendo kati ya “matawi” hayo, yaani, wanafunzi wake, utawasaidia kuvumilia mambo yatakayotokea. Anawaonya kwamba ulimwengu utawachukia. Ingawa hivyo, anawafariji hivi: “Ikiwa ulimwengu unawachukia, kumbukeni kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, . . . kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia.”—Yohana 15:18, 19.

Akieleza zaidi sababu itakayofanya ulimwengu uwachukie, Yesu anaongezea hivi: “Watawatendea mambo yote haya kwa ajili ya jina langu, kwa sababu hawamjui Yule aliyenituma.” Yesu anasema kwamba miujiza yake, inawahukumu wale wanaomchukia: “Kama singefanya kati yao kazi ambazo hakuna mwingine aliyezifanya, hawangekuwa na dhambi; lakini sasa wameniona, nao wamenichukia mimi na pia Baba yangu. Kwa kweli, chuki yao inatimiza unabii.—Yohana 15:21, 24, 25; Zaburi 35:19; 69:4.

Yesu anaahidi tena kutuma msaidizi, roho takatifu. Wafuasi wake wote wanaweza kupata nguvu hizo na zinaweza kuwasaidia kuzaa matunda, yaani, ‘kutoa ushahidi.’—Yohana 15:27.