Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 117

Mlo wa Jioni wa Bwana

Mlo wa Jioni wa Bwana

MATHAYO 26:21-29 MARKO 14:18-25 LUKA 22:19-23 YOHANA 13:18-30

  • YUDA ATAMBULISHWA KUWA MSALITI

  • YESU AANZISHA MLO WA UKUMBUSHO

Mapema jioni ya leo, Yesu aliwafundisha mitume wake somo la unyenyekevu kwa kuwaosha miguu. Sasa, inaelekea ni baada ya mlo wa Pasaka, anaponukuu maneno ya kinabii aliyosema Daudi: “Mtu niliyekuwa na amani naye, ambaye nilimwamini, aliyekuwa akila mkate wangu, amekiinua kisigino chake dhidi yangu.” Kisha anafafanua hivi: “Mmoja wenu atanisaliti.”—Zaburi 41:9; Yohana 13:18, 21.

Mitume wanatazamana na kila mmoja wao anauliza: “Bwana, je, ni mimi?” Hata Yuda Iskariote anauliza pia. Petro anamwambia Yohana ambaye amekaa kando ya Yesu hapo mezani, aulize mtu huyo ni nani. Basi Yohana anamuegemea Yesu na kumuuliza “Bwana, ni nani?”—Mathayo 26:22; Yohana 13:25.

Yesu anajibu hivi: “Ni yule ambaye nitampa kipande cha mkate ninachochovya.” Yesu anachovya kipande cha mkate katika bakuli lililo mezani na kumpa Yuda akisema: “Mwana wa binadamu anaenda zake, kama ilivyoandikwa kumhusu, lakini ole wake mtu atakayemsaliti Mwana wa binadamu! Ingekuwa afadhali kama mtu huyo hangezaliwa.” (Yohana 13:26; Mathayo 26:24) Kisha Shetani anamwingia Yuda. Tayari mwanamume huyu amepotoka, sasa anajitoa ili kufanya mapenzi ya Ibilisi na hivyo anakuwa “mwana wa maangamizi.”—Yohana 6:64, 70; 12:4; 17:12.

Yesu anamwambia Yuda: “Kile unachofanya, kifanye upesi zaidi.” Kwa kuwa Yuda ndiye aliyekuwa akitunza sanduku la pesa, baadhi ya mitume wanafikiri Yesu anamwambia: “‘Nunua vitu tunavyohitaji kwa ajili ya sherehe,’ au kwamba anapaswa kuwapa maskini kitu fulani.” (Yohana 13:27-30) Badala yake, Yuda anaenda kumsaliti Yesu.

Jioni hii ya mlo wa Pasaka, Yesu anaanzisha mlo mwingine tofauti kabisa. Anachukua mkate, anatoa sala ya shukrani, anaumega, na kuwapa mitume wake wale. Anasema: “Huu unamaanisha mwili wangu, ambao utatolewa kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka.” (Luka 22:19) Mkate huo unapitishwa, nao mitume wanakula.

Sasa Yesu anachukua kikombe cha divai, anatoa sala ya shukrani, na kuwapitishia. Kila mmoja wao anakunywa kutoka kwenye kikombe ambacho Yesu anasema hivi kukihusu: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.”—Luka 22:20.

Basi, Yesu anaanzisha ukumbusho wa kifo chake ambao wafuasi wake wanapaswa kukumbuka siku ya Nisani 14 kila mwaka. Mwadhimisho huo utawakumbusha kile ambacho Yesu na Baba yake wamefanya ili kuwawezesha watu wenye imani wakombolewe kutoka kwa hukumu ya dhambi na kifo. Mwadhimisho huu ni mkuu kuliko Pasaka ilivyo kwa Wayahudi, kwa sababu unakazia kukombolewa kikweli kwa wanadamu wanaoamini.

Yesu anasema kwamba damu yake “itamwagwa kwa ajili ya wengi ili wasamehewe dhambi.” Kati ya wengi ambao watasamehewa ni mitume wake waaminifu na wengine walio kama hao. Hao ndio watakaokuwa pamoja naye katika Ufalme wa Baba yake.—Mathayo 26:28, 29.