Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 1

Wapokea Ujumbe Kutoka kwa Mungu

Wapokea Ujumbe Kutoka kwa Mungu

LUKA 1:5-33

  • MALAIKA GABRIELI ATABIRI KUZALIWA KWA YOHANA MBATIZAJI

  • GABRIELI AMWAMBIA MARIA KWAMBA YESU ATAZALIWA

Kwa kweli tunaweza kuiona Biblia nzima kuwa ujumbe kutoka kwa Mungu. Baba yetu wa mbinguni ametupatia Biblia ili ituongoze. Hata hivyo, fikiria ujumbe au matangazo mawili ya pekee yaliyoletwa zaidi ya miaka 2,000 iliyopita. Ujumbe huo uliletwa na malaika anayeitwa Gabrieli, ambaye ‘husimama karibu mbele za Mungu.’ (Luka 1:19) Hali zilikuwaje malaika huyo alipoleta ujumbe huo muhimu?

Ni karibu mwaka wa 3 K.W.K. Malaika Gabrieli anapeleka wapi ujumbe wa kwanza? Katika vilima vya Yudea, inaelekea si mbali kutoka Yerusalemu, ambako anaishi nabii wa Yehova anayeitwa Zekaria. Yeye na mke wake, Elisabeti, wamezeeka, na hawana watoto. Ni zamu ya Zekaria kutumikia akiwa kuhani katika hekalu la Mungu huko Yerusalemu. Zekaria akiwa hekaluni, Gabrieli anatokea ghafla karibu na madhabahu ya uvumba.

Ni wazi kwamba tukio hilo linamshtua Zekaria. Lakini malaika huyo anamtuliza Zekaria kwa kusema, “Usiogope, Zekaria, kwa sababu dua yako imesikiwa vema, na mke wako Elisabeti atakuzalia mwana, nawe utamwita Yohana.” Gabrieli anaongezea kwamba Yohana “atakuwa mkuu mbele za Yehova” na ‘atamwandalia Yehova watu waliotayarishwa.’—Luka 1:13-17.

Ni vigumu kwa Zekaria kuamini maneno hayo. Kwa nini? Kwa sababu ya umri wake na umri wa Elisabeti. Basi Gabrieli anamwambia: “Utakaa kimya, hutaweza kuongea mpaka siku ambayo mambo hayo yatatendeka, kwa sababu hukuamini maneno yangu.”—Luka 1:20.

Wakati huohuo, watu walio nje wanashangaa kwa nini Zekaria amekaa ndani muda mrefu sana. Mwishowe anatoka, lakini hawezi kuongea. Zekaria anatoa tu ishara kwa mikono yake. Ni wazi kwamba ameona jambo la kustaajabisha hekaluni.

Baada ya Zekaria kumaliza utumishi wake hekaluni, anarudi nyumbani kwake. Muda mfupi baadaye, Elisabeti anapata mimba! Kwa miezi mitano, anaposubiri mtoto wake azaliwe, Elisabeti anakaa nyumbani mbali na watu.

Kisha Gabrieli anatokea mara ya pili. Anamtokea nani? Anamtokea mwanamke kijana ambaye hajaolewa anayeitwa Maria, na ambaye anaishi upande wa kaskazini katika eneo linaloitwa Galilaya, katika jiji la Nazareti. Malaika anamwambia nini? Anasema: “Umepata kibali cha Mungu.” Kisha Gabrieli anamwambia Maria: “Tazama! utapata mimba na kuzaa mwana nawe utamwita Yesu.” Gabrieli anaongezea: “Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi, . . . naye atatawala akiwa Mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na Ufalme wake hautakuwa na mwisho.”—Luka 1:30-33.

Unaweza kuelewa jinsi Gabrieli alivyoliona kuwa pendeleo kupeleka ujumbe au matangazo hayo mawili. Tunaposoma mengi zaidi kuhusu Yohana na Yesu, tutaona wazi kwamba ujumbe huo kutoka mbinguni ulikuwa muhimu sana.