Hamia kwenye habari

Kampeni ya Ulimwenguni Pote Yatangaza JW.ORG

Kampeni ya Ulimwenguni Pote Yatangaza JW.ORG

Katika mwezi wa Agosti 2014, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote waligawanya trakti ya kuwafahamisha watu kuhusu jw.org. Kwa sababu hiyo, idadi ya watu ambao walitembelea tovuti hiyo iliongezeka kwa zaidi ya asilimia 20 katika mwezi huo, kufikia karibu milioni 65. Ulimwenguni pote, karibu watu 10,000 waliomba funzo la Biblia kupitia tovuti hiyo​—zaidi ya asilimia 67 kwa kulinganisha na mwezi uliotangulia! Kampeni hiyo iliwasaidia watu kila mahali kupata msaada.

Msaada kwa watu wanaotafuta majibu ya maswali muhimu zaidi maishani

Shahidi mmoja nchini Kanada alimsalimu Madeline ndani ya lifti na kumwonyesha trakti iliyokuwa ikitumiwa kwa ajili ya kampeni hiyo, Tutapata Wapi Majibu ya Maswali Muhimu Maishani? Madeline alisema kwamba usiku uliotangulia alisali kwa bidii Mungu amsaidie apate majibu ya maswali kama hayo. Hapo awali alikuwa amepiga simu kwenye makanisa kadhaa kuomba mtu amfundishe Biblia, lakini hakuna mtu aliyewahi kumtembelea. Muda mfupi baadaye alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova.

Msaada kwa wale wasioifahamu Biblia

Nchini Filipino, Rowena alizungumza na mwanamume Mchina aliyekuwa amesimama nje ya mkahawa fulani. Alimpa trakti na kumweleza kwamba Mashahidi wa Yehova wanataka kuwasaidia watu wajifunze Biblia bila malipo.

Mwanamume huyo alisema kwamba yeye hajawahi kuona Biblia. Mazungumzo yao yalimchochea kuhudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Baadaye alisema kwamba alitaka kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia na kwamba ataipakua kutoka katika tovuti yetu.

Msaada kwa viziwi

Guillermo, Shahidi ambaye ni kiziwi nchini Hispania, alikutana na Jorge ambaye pia ni kiziwi. Zamani wote wawili walikuwa katika shule moja. Jorge alisema kwamba mama yake alikuwa amekufa karibuni, na hilo lilimfanya awe na mashaka na maswali mengi. Guillermo alimpa trakti iliyokuwa ikitolewa katika kampeni hiyo na kumweleza jinsi ambavyo angeweza kupata habari katika lugha ya ishara kwenye tovuti hiyo ya jw.org, ambayo ingejibu mengi kati ya maswali yake. Pia, Guillermo alimwalika Jorge ahudhurie mkutano katika Jumba la Ufalme. Alihudhuria, na tangu wakati huo, Jorge hajakosa hata mkutano mmoja, ingawa anaishi kilomita 60 kutoka kwenye Jumba la Ufalme.

Msaada kwa wanaoishi maeneo ya mbali

Kwa gharama kubwa sana, waume wawili na wake zao wanaoishi Greenland walisafiri kwa saa sita katika mashua ndogo ili kufika kwenye kijiji kilicho na wakaaji 280. Walihubiri, wakagawa trakti, na kuonyesha video iliyo kwenye jw.org katika Lugha ya Greenland. Pia, walianzisha funzo la Biblia pamoja na wenzi fulani wa ndoa. Sasa wanaongoza funzo hilo mara mbili kwa juma kupitia simu.

Jitihada hizo hazikufanywa katika maeneo hayo ya Kaskazini tu. Mashahidi nchini Nikaragua walipanga kuwagawia trakti hiyo watu wanaozungumza Kimayangna katika msitu wa eneo la Karibea. Baada ya kusafiri kwa saa 20 bila kusimama ndani ya basi kuukuu katika barabara iliyojaa mashimo, walitembea kwa saa 11, nyakati nyingine katika maji yenye matope yenye kina ili kufika katika vijiji hivyo. Walipofika, waligawa trakti hizo na kuonyesha video katika Kimayangna, jambo ambalo liliwashangaza na kuwafurahisha sana watu katika eneo hilo.

Estela alimpa trakti mwanamume mmoja aliyekuwa akitembelea mji mdogo kwenye msitu wa mvua nchini Brazili. Mwanamume huyo alipokea trakti hiyo, akaitia mfukoni, lakini hakupendezwa sana nayo. Alipokuwa akirudi nyumbani, injini ya mashua yake ilizima naye akashindwa kuendelea na safari. Alipokuwa akisubiri msaada, mwanamume huyo alisoma trakti hiyo. Akitumia simu yake, aliingia kwenye tovuti ya jw.org, ambapo alisoma makala kadhaa na kupakua video kadhaa. Siku chache baadaye, mwanamume huyo alikutana na mume wa Estela na kumwomba amshukuru Estela kwa kumpa trakti hiyo. Alisema hivi: “Makala nilizosoma mashua yangu ilipokuwa imekwama kwenye mto, zilinituliza hadi mashua nyingine ilipokuja kuniokoa. Watoto wangu wanapenda video za Caleb. Nitaendelea kutembelea tovuti ya jw.org.”