Hamia kwenye habari

Kuhitimu kwa 134 kwa Shule ya Gileadi—“Igeni Imani Yao”

Kuhitimu kwa 134 kwa Shule ya Gileadi—“Igeni Imani Yao”

Darasa la 134 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) lilihitimu siku ya Jumamosi, Machi 9, 2013, katika kituo cha elimu cha Mashahidi wa Yehova huko Patterson, New York. Shule hii huwazoeza wahudumu wenye uzoefu wa Mashahidi wa Yehova ili wawe na matokeo zaidi katika huduma yao. Watu 9,912 walihudhuria programu hiyo kutia ndani marafiki, watu wa familia, na wageni wengine.

Mwenyekiti wa programu hiyo alikuwa Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Aliwakumbusha wasikilizaji kuhusu programu ya kuanzishwa kwa Shule ya Gileadi, miaka 70 iliyopita Februari 1, 1943. Katika tukio hilo, Nathan Knorr, msimamizi wa shule hiyo, alifafanua kusudi lake aliposema: “Lazima kuwe na mamia ya maelfu zaidi ambao wangeweza kufikiwa [na habari njema za Ufalme wa Mungu] ikiwa kungekuwa na wafanyakazi wengi zaidi shambani. Kwa neema ya Bwana, kutakuwa na wengi zaidi.” Je, Ndugu Knorr alikosea?

Fikiria jambo hili. Muda mfupi baada ya shule hiyo kuanzishwa, Ndugu Knorr alitembelea nchi ya Mexico akitafuta maeneo ambayo wamishonari waliohitimu Shule ya Gileadi wangeweza kutumwa. Akiwa huko, makutaniko yote katika eneo la kilomita 240 kuzunguka Mexico City yalialikwa kwenye mkutano, na watu 400 walihudhuria. Leo, karibu miaka sabini imepita tangu wamishonari wa kwanza walipoenda Mexico kutoka Gileadi, na ikiwa mkutano huo ungefanywa tena leo, zaidi ya watu 200,000 wangehudhuria.

“Ni Nini Kilicho Mkononi Mwako?” Anthony Griffin, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, alitoa hotuba yenye kichwa hicho kilichotegemea andiko la Kutoka 4:2. Katika simulizi hilo, Mungu alimwuliza Musa: “Ni nini hicho kilicho mkononi mwako?” Musa alijibu: “Fimbo.” Yehova alitumia fimbo hiyo kama ishara ya mamlaka na kazi aliyompa Musa. (Kutoka 4:5) Musa alifanikiwa alipotumia mamlaka yake kumtukuza Mungu, lakini alimkosea Mungu alipoitumia kujitukuza na kuwakemea ndugu zake, kama alivyofanya huko “Meriba.”​—Hesabu 20:​9-​13.

Ndugu Griffin alilinganisha fimbo ya Musa na mazoezi ya kiroho ambayo wanafunzi wa Gileadi wamepokea na akawasihi wasitumie elimu yao kuwakandamiza wengine. Badala yake aliwashauri hivi: “Tumieni kile mlichopewa kumsifu na kumheshimu Yehova, nanyi mtaendelea kuwa baraka kwa wale mnaowatumikia.”

“Kumbukeni Mana.” Ndugu Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza alikazia masomo manne yafuatayo tunayoweza kujifunza kutokana na mana ambayo Mungu aliwapa Waisraeli kimuujiza walipokuwa jangwani.

  • Endelea kufanya kazi kwa bidii. (Hesabu 11:8) Ili waweze kunufaika na mana, Waisraeli walihitaji kufanya haraka kuikusanya na kuitayarisha kabla ya kuila.​—Kutoka 16:21.

  • Usilalamike kamwe kuhusu maandalizi ya Yehova. (Hesabu 11:​5, 6) Waisraeli walinung’unika kuhusu mana. Lakini Yehova aliona kuwa wananung’unika dhidi yake mwenyewe. Kama ilivyokuwa kuhusu mana, chakula cha kiroho tunachopata hakitusisimui wakati wote, hata hivyo huwa chenye lishe nyakati zote. Sikuzote tunapaswa kuthamini maandalizi yote ambayo Yehova anatupa.

  • Uwe na uhakika kabisa kwamba Yehova atakupa mahitaji yako. Yehova aliwapa Waisraeli mana kila siku, na siku iliyotangulia sabato alihakikisha kwamba walipata kiwango maradufu. (Kutoka 16:22-​26) Sisi pia, tuna uhakika kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu.​—Mathayo 6:​11.

  • Tukikosa kutii hatutapata baraka yoyote. (Kutoka 16:19, 20, 25-​28) Waisraeli waliojaribu kuokota mana siku ya Sabato hawakupata chochote bali walikosa kibali cha Yehova, na walipookota na kuhifadhi mana kwa ajili ya siku inayofuata katika zile siku sita za juma mana hiyo ilishambuliwa na funza na kutoa harufu mbaya sana.

Ndugu Lett aliwahimiza wanafunzi wakumbuke masomo tunayojifunza kutokana na mana, kwa sababu Yehova ‘atawafungulia malango ya mbinguni na kuwamwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’​—Malaki 3:​10.

“Jiandae kwa Maisha Katika Ulimwengu Mpya.” William Samuelson, ambaye anasimamia Idara ya Shule za Kitheokrasi, alieleza kwamba ingawa tunahisi tuko tayari, au tunatamani maisha katika mfumo mpya ujao, lazima tujitayarishe vizuri. Ili mtu ajitayarishe vizuri anahitaji “utimamu wa akili.”​—1 Petro 4:7.

Tunaonyesha kwamba tuna utimamu wa akili kwa jinsi tunavyoshughulika na hali yetu ya kutokamilika. Hatupaswi kumlaumu Shetani au ulimwengu huu ulio chini yake kwa sababu ya makosa yote tunayotenda, labda tukifikiri kwamba tutayarekebisha makosa hayo katika ulimwengu mpya baada ya Mungu kuondoa uvutano mbaya. Hata sasa, tunaweza kupinga tabia mbaya, kama vile ubinafsi, kwa kujitahidi “kuvaa utu mpya.”​—Waefeso 4:​24.

“Acha Kutumia Kalamu Yako.” Mark Noumair , mwalimu wa shule ya Gileadi, alitumia mfano wa kalamu kueleza jinsi ‘tunavyopenda kujiandikia mambo yanayotuhusu maishani.’ Hata hivyo, ‘tunaacha kutumia kalamu zetu’ kwa kumruhusu Yehova atuandikie mambo hayo.

Kisa cha Mfalme Sauli ni mfano wa kutuonya katika jambo hili. Alianza utawala wake akiwa mnyenyekevu na mwenye kiasi. (1 Samweli 10:22, 27; 11:13) Punde si punde alianza ‘kujiandikia mambo yake mwenyewe’ kwa kufanya mambo aliyofikiria kuwa sahihi na kujitukuza. Mungu alimkataa kwa sababu ya kutotii.​—1 Samweli 14:24; 15:10, 11.

Licha ya kwamba wanafunzi wamekuwa waaminifu hadi kufikia sasa, Ndugu Noumair aliwakumbusha kwamba walihitaji kuendelea kufanya kazi ya Mungu jinsi Mungu anavyotaka ifanywe. Aliwaonya wanafunzi hivi: “Msifikiri kwamba kwa kuwa Mungu anatutumia basi tuna kibali chake.” Kwa mfano, Musa alishindwa kufuata maagizo ya Mungu alipotokeza maji kimuujiza kutoka kwenye mwamba. Alipata maji, lakini hakupata baraka ya Yehova.​—Hesabu 20:​7-​12.

“Kufanya Kazi Pamoja na Malaika Katika Kazi ya Kuhubiri.” Katika hotuba yake mwalimu wa Shule ya Gileadi Sam Roberson alikazia andiko la Ufunuo 14:​6, 7. Kisha aliongoza sehemu ya maigizo ya wanafunzi ya mambo ambayo walijionea walipokuwa wakihubiri. Kwa mfano, mwanafunzi mmoja alimhubiria muuguzi mmoja wa hospitali alipokuwa akipata nafuu baada ya kufanyiwa upasuaji. Muuguzi huyo ametokea Peru, kwa hiyo mwanafunzi huyo alianza mazungumzo kwa kumwonyesha picha kwenye Tovuti ya jw.org kuhusu kazi ya kuhubiri huko Chachapoyas , Peru. Jambo hilo lilimfanya muuguzi huyo pamoja na mume wake waanze kujifunza Biblia.

“Umenipumbaza . . . Hivi Kwamba Nikapumbazika.” (Yeremia 20:7) Allen Shuster, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani, aliwahoji ndugu wawili na wake zao kutoka katika darasa hilo. Wanafunzi hao walihisi kwamba ‘wamepumbazwa’ na Yehova. Jinsi gani? Mwanzoni waliogopa kwamba masomo yangekuwa magumu. Hata hivyo, mara tu shule hiyo ilipoanza, walipata msaada mkubwa sana uliowanufaisha. Dada Marianne Aronsson alieleza jinsi alivyothamini mazoezi aliyopokea kwa kusema hivi: “Sikuzote nitakuwa na jambo lenye kuvutia la kujifunza​—Nimetambua kwamba kila mstari katika Biblia ni kama hazina.”

“Igeni Imani Yao.” Ndugu David Splane wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya msingi ya programu hiyo. Hotuba yake ilitegemea andiko la Waebrania 13:7, linalosema: “Wakumbukeni wale ambao wanaongoza katikati yenu, ambao wamelisema neno la Mungu kwenu, nanyi mnapotafakari jinsi mwisho wa mwenendo wao unavyokuwa, igeni imani yao.” Wale ‘walioongoza’ kazi ya Mashahidi wa Yehova miaka 70 iliyopita walionyeshaje imani?

Mnamo Septemba 24, 1942, ndugu Nathan Knorr aliitisha mkutano wa wasimamizi wa mashirika mawili yanayotumiwa na Mashahidi wa Yehova na akapendekeza kuanzishwa kwa shule mpya, yaani, Gileadi, ili kuwazoeza wamishonari kuongoza kazi ya kuhubiri kwenye maeneo mapya. Hata hivyo, hali haikuwa nzuri wakati huo. Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vimepamba moto na hivyo ingekuwa vigumu au isingewezekana kuwatuma wamishonari kwenye maeneo mengi. Zaidi ya hilo, mfumo wa uchumi wa ulimwengu ulikuwa umeporomoka kipindi cha miaka ya 1930, na tengenezo lilikuwa na pesa ya kuendesha shule hiyo kwa miaka mitano tu. Ingawa hali ilikuwa hivyo, ndugu hao walionyesha imani walipofikia kauli moja na kupitisha pendekezo hilo.

Wahitimu wa madarasa ya mapema wa shule hiyo ya Gileadi walionyesha imani tunayoweza kuiga. Waliridhika na waliepuka kupenda pesa. (Waebrania 13:​5, 6) Wahitimu hao walihisi kwamba huenda hawangeweza kuziona familia zao tena kwa sababu washiriki wa familia zao hawangeweza kupata nauli ya kuwalipia ili watembelee nyumbani kwao tena. Isitoshe, wamishonari wengi hawakuwaona washiriki wa familia zao kwa miaka 10 au 15 baada ya kwenda kwenye migawo yao. Walikuwa na uhakika kwamba Yesu angeendelea kuwategemeza wao na familia zao kama tu alivyokuwa akifanya siku zote.​—Waebrania 13:8.

Darasa la kwanza la Gileadi, 1943

Baada ya kusimulia matatizo ambayo baadhi yao walipata walipokuwa wakihubiri katika nchi za kigeni hata kabla ya kuhudhuria Shule ya Gileadi, Ndugu Splane aliwaambia hivi wanafunzi: “Enyi wanaume na wanawake vijana, mnaendeleza historia tunayojivunia ya miaka 70 ya wanaume na wanawake ambao tayari wamehudhuria Shule ya Gileadi. . . . Furahieni kumtumikia Yehova mahali popote pale.”

Ndugu Splane alimalizia sehemu yake kwa kuonyesha picha za slaidi za wanafunzi 77 wanaotumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Marekani, kutia ndani wanafunzi wawili wa darasa la kwanza lililofanyika mwaka 1943. Picha hizo ziliambatana na sauti ya nyimbo zilizotumiwa na Mashahidi wa Yehova kwenye ibada yao katika kipindi cha miaka 70 iliyopita.

Baada ya wanafunzi kupokea diploma zao, mwanafunzi mmoja alisoma barua ya shukrani ya wanafunzi hao. Ndugu Sanderson alihitimisha programu hiyo kwa kusisitiza kwamba ijapokuwa miaka 70 imepita, maelezo aliyotoa Ndugu Knorr alipozungumza na wanafunzi wa darasa la kwanza la Gileadi bado yana maana kubwa sana leo: “Kokote kule mtakakokwenda, kumbukeni kwamba ninyi ni . . . wahubiri wa Ufalme; na kwamba hilo ndilo pendeleo kubwa sana alilowahi kukabidhiwa mwanadamu yeyote yule duniani, la kuimba sifa za Mungu sasa kabla ya vita vya Har-Magedoni. . . . Maadamu umekabidhiwa pendeleo hilo la kuhubiri, basi, hubiri.”