Hamia kwenye habari

Mwanzo Sasa Kinapatikana Katika Lugha ya Ishara ya Marekani

Mwanzo Sasa Kinapatikana Katika Lugha ya Ishara ya Marekani

VIZIWI walipunga mikono yao kushangilia tangazo hili lenye kusisimua: “Mtafurahi kujua kwamba kazi ya kutafsiri baadhi ya vitabu vya Biblia vya Maandiko ya Kiebrania [Agano la Kale] inaendelea. Kazi ya kurekodi [video] ya kitabu cha Mwanzo imekamilika!”

Tangazo hilo lilitolewa wakati wa hotuba ya mwisho katika makusanyiko yaliyofanywa na Mashahidi ya Yehova na kutolewa katika Lugha ya Ishara ya Marekani (ASL).

Katika mwaka wa 2005, Mashahidi wa Yehova walianza kutafsiri Biblia Takatifu-Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Lugha ya Ishara ya Marekani, wakianza na kitabu cha Mathayo. Kufikia mwaka wa 2010, vitabu vyote 27 ambavyo kwa kawaida huitwa Agano Jipya vilikuwa vimetafsiriwa katika Lugha ya Ishara ya Marekani.

Isitoshe, Mashahidi wa Yehova wametafsiri baadhi ya vitabu vya Biblia katika lugha nyingine tano za ishara.

Kwa nini wanafanya kazi hiyo yote? Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba maandishi yanayochapwa kwenye kurasa yanategemea lugha inayozungumzwa ambayo viziwi wengi hawajawahi kujifunza kamwe. Tafsiri ya Biblia katika lugha ya ishara iliyo sahihi na rahisi kueleweka, huwezesha viziwi wengi kuelewa Neno la Mungu na kujenga uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Watu wameipokea jinsi gani tafsiri hii ya Biblia?

Kijana mmoja kiziwi alisema hivi: “Kitabu cha Mathayo kilipotolewa miaka michache iliyopita, nilihisi huo ulikuwa uthibitisho wa kwamba Yehova Mungu ananipenda kibinafsi, na kutolewa kwa kitabu cha Mwanzo kumenihakikishia hilo. Yeye anahakikisha kwamba ninapata kumjua vizuri.”

Mwanamke mmoja kiziwi alieleza hisia zake katika njia hii: “Ishara zinaeleweka vizuri na zimejaa hisia! Nimekuja kuipenda sana Biblia. Naona kwamba Yehova anataka nisome Neno lake kwa kuchunguza muktadha, mstari kwa mstari, ili niweze kumjua kwa ukamili zaidi. Ishara zenye kueleweka zinagusa moyo wangu na kuniwezesha kumweleza Mungu hisia zangu za ndani kabisa ninaposali.”