Hamia kwenye habari

Muziki Unaoimbwa Katika Lugha Nyingi

Muziki Unaoimbwa Katika Lugha Nyingi

Ni jambo ngumu sana kutafsiri wimbo mmoja tu kutoka lugha moja hadi nyingine. Kutafsiri kitabu kizima chenye nyimbo 135 ni kazi ngumu hata zaidi.

Mashahidi wa Yehova wamefaulu kufanya hivyo na katika kipindi cha miaka mitatu wametafsiri kitabu chao kipya cha nyimbo, Mwimbieni Yehova, katika lugha 116. Kwa kuongezea, nyimbo 55 katika kitabu hicho zimetafsiriwa katika lugha 55 nyingine. Na bado nyimbo hizo zitatafsiriwa katika lugha nyingine nyingi.

Kutafsiri na Kuandika Nyimbo

Tayari Mashahidi wa Yehova wanatafsiri vitabu vya kuwasaidia watu kuelewa Biblia katika lugha 600 hivi, na 400 hivi kati ya hizo zinapatikana kwenye Intaneti. Lakini kutafsiri kitabu cha nyimbo hutokeza matatizo ya kipekee. Kwa nini? Kwa sababu muziki katika kitabu Mwimbieni Yehova, haubadiliki hata ingawa maneno ya nyimbo hizo yametafsiriwa katika lugha nyingi.

Kutunga maneno yawe wimbo ni tofauti kabisa na kutafsiri maandishi katika gazeti. Kwa mfano, wanapotafsiri gazeti la Mnara wa Mlinzi katika lugha nyingine, watafsiri hujitahidi kuwasilisha maana yote ya Kiingereza kwa usahihi kadiri wawezavyo. Lakini wanafuata utaratibu tofauti wanapotafsiri nyimbo.

Jinsi Nyimbo Zinavyotafsiriwa

Watafsiri hutumia mbinu tofauti wanapotafsiri nyimbo kuliko ile wanayotumia wanapotafsiri machapisho mengine kwa sababu maneno ya nyimbo yanapaswa kuwa yenye maana, yenye kupendeza, na yanayoweza kukumbukwa kwa urahisi.

Maneno yanayotumiwa katika wimbo wa sifa yanapaswa kuwa rahisi hivi kwamba mwimbaji anaweza kuelewa kwa urahisi maana na kusudi la kila fungu la maneno. Katika kila lugha, maneno yanapaswa kuingiana na muziki na kwenda sambamba, kana kwamba ni maneno yaliyotungwa na mwimbaji.

Watafsiri hutimizaje jambo hilo? Badala ya kutafsiri moja kwa moja maneno ya nyimbo za Kiingereza katika kitabu Mwimbieni Yehova Sifa, watafsiri wameagizwa waandike maneno yao wenyewe ambayo yatawasilisha maana na hisia zilizo katika nyimbo za Kiingereza. Ingawa lengo la watafsiri ni kuwasilisha wazo la Kimaandiko lililo katika kila wimbo, wao hutumia maneno ya kawaida katika lugha yao ambayo yataeleweka na kukumbukwa kwa urahisi.

Hatua ya kwanza ilikuwa kutafsiri wimbo wa Kiingereza neno kwa neno. Kisha, Shahidi aliye na ujuzi wa kuandika maneno ya nyimbo alisahihisha tafsiri hiyo kwa kuandika maneno yenye kupendeza na yenye maana katika lugha mpya. Kwa kuwa sikuzote watafsiri hutaka kudumisha maana sahihi ya Kimaandiko, wao pamoja na wasahihishaji wa makala husahihisha makosa yoyote ya mwandikaji wa maneno ya nyimbo.

Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote walijawa na shangwe walipopokea kitabu hicho kipya cha nyimbo, na watu wanakitazamia kwa hamu katika lugha nyingine nyingi.