Hamia kwenye habari

Maktaba Unayoweza Kubeba Mkononi

Maktaba Unayoweza Kubeba Mkononi

Oktoba 7, 2013 Mashahidi wa Yehova walizindua programu inayoitwa Maktaba ya JW (JW Library) inayoweza kutumiwa kwenye vifaa vya mkononi vya kisasa vya mawasiliano. Mashahidi walibuni programu hiyo ili itumiwe katika kusoma na kujifunza Biblia. Programu hiyo inayotolewa bila malipo, ina tafsiri sita za Biblia katika lugha ya Kiingereza, kutia ndani tafsiri ya Biblia ya King James Version na Biblia iliyofanyiwa marekebisho ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, toleo la mwaka wa 2013.

Kwa Nini Ilibuniwa?

Mamilioni ya watu wanafanya kazi na kuwasiliana wakitumia simu, kompyuta ndogo za kisasa za mkononi (tablet), na vifaa vingine kama hivyo. Kwa kuwa tayari watumiaji wa vifaa hivyo wangeweza kusoma na kujifunza Biblia kwenye tovuti ya jw.org, kwa nini Maktaba ya JW ilibuniwa?

Kwanza, baada ya kuisakinisha programu hiyo katika kifaa chako, hutahitaji huduma za Intaneti ili ufurahie kuitumia. Pili, imeundwa katika njia ya kwamba msomaji anaweza kutafuta Maandiko kwa njia rahisi sana ili ajifunze Biblia kikamili zaidi. Jinsi gani?

Maktaba ya JW Inamsaidia Mtu Ajifunze Biblia

Unapoifungua Maktaba ya JW mara ya kwanza, maktaba hiyo huanza kwa kuorodhesha vitabu vya Biblia. Unapobofya kwenye kitabu fulani cha Biblia, utaona sehemu inayofuata ikionyesha orodha ya sura za kitabu kilichochaguliwa. Kwa njia hiyo, ni rahisi sana kufungua mstari au sehemu fulani ya sura unayotaka kwa sekunde chache tu. Isitoshe, Maktaba ya JW ina mambo kadhaa yatakayokusaidia unapojifunza Biblia:

  • Maelezo ya chini yanayoonyesha maana kadhaa na habari zaidi kuhusu jambo linalotajwa.

  • Marejeo ya pambizoni yanayokuelekeza kwenye mistari mingine ya Biblia inayohusiana na jambo unalojifunza.

  • Kipengele cha kutafuta habari ambacho kinamsaidia mtumiaji apate sehemu zote ambapo neno au kifungu cha maneno anachotafuta kinapatikana.

  • Utangulizi wa yaliyomo unaopatikana mwanzoni mwa kila kitabu cha Biblia.

  • Jedwali linaloonyesha mwandikaji wa kila kitabu cha Biblia, mahali kilipoandikwa, wakati uandikaji ulipokamilika na vilevile muda uliohusika.

  • Rangi maridadi za ramani, chati mbalimbali kutia ndani zile zinazoonyesha miaka na matukio, na michoro mbalimbali.

Kama ilivyo na machapisho yote ya Mashahidi wa Yehova, Maktaba ya JW inatolewa bila malipo. Tayari maktaba hiyo inayopatikana bila malipo na inayotegemezwa kwa michango ya hiari, imepakuliwa zaidi ya mara milioni moja. (2 Wakorintho 9:7) Kwa nini usiitumie maktaba hiyo wewe mwenyewe na ujionee faida yake?

Programu hiyo ina mambo mengine yaliyoongezwa mnamo Januari 2014 ambayo yanatia ndani kijitabu Kuyachunguza Maandiko kila Siku na kitabu cha nyimbo kinachotumiwa na Mashahidi wa Yehova.