Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yesu Alifanana Kabisa Namna Gani?

Yesu Alifanana Kabisa Namna Gani?

Hakuna mutu mwenye kuwa na picha ya Yesu. Hakusimama ili akamatwe picha ao kuchorwa. Hata hivyo, kwa miaka mingi, ameonyeshwa katika michoro ya wachoraji wengi.

Bila shaka, wachoraji hao hawakujua namna Yesu alifanana kabisa. Desturi, imani ya kidini, na mapendezi ya watu wenye waliomba watengenezewe picha, zimechochea kila mara wachoraji kuhusu namna wanafanya picha ya Yesu. Hata hivyo, picha na michoro yao inaweza kuchochea, ao hata kuharibu mawazo ya watu kuhusu Yesu na mafundisho yake.

Wachoraji fulani walichora Yesu akiwa mwenye kuonekana kama mwanaume zaifu, mwenye kuwa na nywele za murefu na ndevu zenye hazina afya nzuri, ao mwenye kuwa na huzuni nyingi. Katika picha zingine, Yesu anaonekana kuwa wa ajabu, mwenye kupambwa na mwangaza wa muviringo juu ya kichwa chake, ao mwenye hahangaikie watu wenye kumuzunguka. Kwa kweli, picha hizo zinamufananisha Yesu muzuri? Namna gani tunaweza kujua ukweli? Njia moja ni kuchunguza habari za Biblia zenye kutusaidia kuelewa namna pengine Yesu alifanana. Habari hizo zinaweza kutusaidia pia kuwa na mawazo yenye kufaa juu yake.

“ULINITAYARISHIA MWILI”

Pengine Yesu alisema maneno hayo katika sala wakati wa ubatizo wake. (Waebrania 10:5; Mathayo 3:13-17) Mwili huo ulifanana namna gani? Miaka 30 hivi mbele ya hapo, malaika Gabrieli alimwambia Maria hivi: “Utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, . . . Mwana wa Mungu.” (Luka 1:31, 35) Kwa hiyo, Yesu alikuwa mwanaume mukamilifu, kama vile Adamu wakati aliumbwa. (Luka 3:38; 1 Wakorintho 15:45) Yesu alipaswa kuwa mwanaume mwenye umbo nzuri, na inawezekana alifanana Maria, mama yake mwenye alikuwa Muyahudi, katika mambo fulani.

Tofauti na Waroma, Yesu alikuwa na ndevu, kama vile ilikuwa desturi ya Wayahudi. Ndevu hizo zilikuwa alama ya utukufu na heshima; hazikuwa za murefu ao zenye hazitunzwe. Bila shaka, Yesu alitunza ndevu zake, na nywele zake zilikatwa muzuri. Ni Wanaziri tu, kama vile Samsoni, ndio hawakukata nywele zao.​—Hesabu 6:5; Waamuzi 13:5.

Katika sehemu kubwa ya miaka 30, Yesu alikuwa seremala na alifanya kazi yake bila vyombo vya kisasa vyenye kutumia umeme. (Marko 6:3) Kwa hiyo, alipaswa kuwa na mwili wenye nguvu kabisa. Mwanzoni mwa utumishi wake, akiwa peke yake, ‘aliwafukuza hekaluni wale wote wenye kondoo na ngombe, akamwanga sarafu za waliokuwa wakibadili pesa na kupindua meza zao.’ (Yohana 2:14-17) Iliomba kuwa mwanaume wa nguvu ili kufanya hivyo. Yesu alitumia mwili wake wenye Mungu alimutayarishia ili kutimiza utume wake wenye alipewa na Mungu. Alisema hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Iliomba kuwa na nguvu nyingi ili kuzunguka Palestina yote kwa miguu na kutangaza ujumbe huo.

“NJOONI KWANGU, . . . NAMI NITAWABURUDISHA NINYI”

Sura ya Yesu yenye kuchangamuka na namna yake ya kutendea watu vilipaswa kufanya mualiko wake uvutie kabisa watu wenye “kutaabika na kulemewa na mizigo.” (Mathayo 11:28-30) Shauku na fazili yake vilihakikisha ahadi yake ya kuburudisha watu wenye walikubali kufundishwa naye. Hata watoto walipenda kuwa karibu na Yesu, kwa sababu Biblia inasema hivi: “Akachukua watoto akawakumbatia.”​—Marko 10:13-16.

Hata kama Yesu alipatwa na maumivu makali mbele ya kufa, hakujulikana kuwa mutu wa huzuni-huzuni. Kwa mufano, alisaidia wakati wa karamu ya ndoa huko Kana kwa kugeuza maji kuwa divai nzuri. (Yohana 2:1-11) Katika vipindi vingine alitoa somo zenye haziwezi kusahauliwa.​—Mathayo 9:9-13; Yohana 12:1-8.

Zaidi ya yote, mahubiri ya Yesu yalifanya wasikilizaji wake wafurahie sana tumaini la uzima wa milele. (Yohana 11:25, 26; 17:3) Wakati wanafunzi wake 70 walimwambia mambo yenye walifurahia katika kazi yao ya kuhubiri, akakuwa na “shangwe” na akasema: ‘Mushangilie kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.’​—Luka 10:20, 21.

‘INGAWA HIVYO, NINYI HAMUPASWI KUWA HIVYO’

Viongozi wa dini wa wakati wa Yesu walitunga njia za kuvuta uangalifu wa watu juu yao na kufanya watu wakubali mamlaka yao. (Hesabu 15:38-40; Mathayo 23:5-7) Tofauti nao, Yesu alifundisha mitume wake ‘wasipige ubwana’ juu ya wengine. (Luka 22:25, 26) Kwa hiyo, aliwashauri hivi: ‘Mujihazari na waandishi ambao hupenda kutembea wakiwa wamevaa kanzu na hupenda salamu katika masoko.’​—Marko 12:38.

Tofauti nao, Yesu alichangana na kikundi cha watu, na wakati fulani hakutambuliwa. (Yohana 7:10, 11) Hata kati ya mitume wake 11 waaminifu, hakuwa na umbo lenye kuwa tofauti sana nao. Musaliti Yuda alitumia busu, “ishara waliyokubaliana,” ili kutambulisha Yesu kwenye kikundi cha watu.​—Marko 14:44, 45.

Kwa hiyo, hata kama mambo mengi kuhusu Yesu hayajulikani, ni wazi kwamba hakufanana namna anachorwa mara nyingi. Lakini, jambo la maana zaidi kuliko kujua namna alifanana kabisa, ni mawazo yenye tuko nayo juu yake.

“BADO MUDA KIDOGO ZAIDI NA ULIMWENGU HAUTANIONA TENA”

Yesu alikufa na kuzikwa siku yenye alisema maneno hayo. (Yohana 14:19) Alitoa uzima wake kuwa “fidia [ao, bei ya ukombozi] badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Katika siku ya tatu, Mungu alimufufua “katika roho” na kumuruhusu ‘afunuliwe’ kwa wanafunzi wake fulani. (1 Petro 3:18; Matendo 10:40) Sasa, Yesu alifanana namna gani wakati alitokea wanafunzi wake? Inaonekana ilikuwa tofauti kabisa na namna alionekana mbele ya kifo chake, kwa sababu hata wanafunzi wake hawakumutambua mara moja. Maria Magdalene alimufananisha na mutunza-bustani; na katika njia yenye kuenda Emau, wanafunzi wawili walimuona kuwa mugeni.​—Luka 24:13-18; Yohana 20:1, 14, 15.

Namna gani tunaweza kumuwazia Yesu leo? Miaka 60 kisha kifo cha Yesu, mutume mupendwa Yohana aliona maono kuhusu Yesu. Yohana hakuona mutu mwenye kufa juu ya musalaba. Lakini aliona “Mufalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,” ni kusema, Mufalme wa Ufalme wa Mungu, mwenye hivi karibuni, atashinda maadui wa Mungu, wakuwe ni mashetani ao wanadamu, na kuletea wanadamu baraka za milele.​—Ufunuo 19:16; 21:3, 4.