Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Namna Gani Unaweza Kusaidia Kutia Nguvu Umoja Wetu wa Kikristo?

Namna Gani Unaweza Kusaidia Kutia Nguvu Umoja Wetu wa Kikristo?

“Kutoka katika yeye mwili wote kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane.” WAEFESO 4:16.

NYIMBO: 53, 107

1. Ni jambo gani lenye limeonekana katika kazi za Mungu tangu mwanzo?

YEHOVA na Yesu wamekuwa katika umoja tangu mwanzo wa uumbaji. Yehova alimuumba Yesu mbele ya kuumba vitu vingine vyote. Kisha, Yesu alitumika pamoja naye na ‘alikuwa kando yake akiwa stadi [fundi] wa kazi.’ (Methali 8:30) Watumishi wa Yehova pia wanafanya kazi katika umoja. Kwa mufano, Noa pamoja na familia yake walijenga safina. Kisha, Waisraeli walifanya kazi pamoja ili kujenga tabenakulo, kubomoa sehemu zake, na kuihamisha. Kwenye hekalu, Waisraeli waliimba na kutumia vyombo vya muziki pamoja ili kumusifu Yehova kwa muziki wenye kupendeza. Watu wa Yehova waliweza kufanya mambo hayo yote kwa sababu walifanya kazi katika umoja.—Mwanzo 6:14-16, 22; Hesabu 4:4-32; 1 Mambo ya Nyakati 25:1-8.

2. (a) Kutaniko la Kikristo la wakati wa mitume lilikuwa na jambo gani la pekee? (b) Tutajibia maulizo gani?

2 Wakristo wa wakati wa mitume pia walifanya kazi katika umoja. Mutume Paulo alieleza kwamba Wakristo hao walikuwa na uwezo na kazi mbalimbali, lakini walikuwa na umoja. Wote walimufuata Yesu Kristo, Kiongozi wao. Mutume Paulo aliwalinganisha na sehemu mbalimbali za mwili zenye kufanya kazi pamoja. (Soma 1 Wakorintho 12:4-6, 12.) Lakini, tuseme nini juu yetu leo? Namna gani tunaweza kufanya kazi pamoja katika mahubiri, katika kutaniko, na katika familia?

KUFANYA KAZI PAMOJA KATIKA MAHUBIRI

3. Mutume Yohana aliona nini?

3 Wakati wa mitume, mutume Yohana aliona katika maono malaika 7 wenye walikuwa wanapiga tarumbeta zao. Wakati malaika wa 5 alipiga tarumbeta yake, mutume Yohana aliona ‘nyota iliyokuwa imeanguka kutoka mbinguni mupaka duniani.’ “Nyota” hiyo ilitumia funguo ili kufungua mulango wa shimo murefu na lenye kuwa na giza. Kwanza, moshi mukubwa ulitoka katika shimo hilo, na kisha kikundi cha nzige kiliruka kutoka katika moshi huo. Nzige hao hawakuharibisha miti na mimea, lakini walishambulia watu wenye hawakuwa na “muhuri [alama] wa Mungu juu ya mapaji ya nyuso zao.” (Ufunuo 9:1-4) Mutume Yohana alijua kwamba kikundi cha nzige kinaweza kuharibisha sana miti na mimea, kama vile zilifanya katika inchi ya Misri wakati wa Musa. (Kutoka 10:12-15) Nzige wenye mutume Yohana aliona wanafananisha Wakristo watiwa-mafuta wenye wamekuwa wakihubiri ujumbe muzito juu ya dini ya uongo. Na mamilioni ya watu wenye kuwa na tumaini la kuishi katika dunia wamejiunga nao. Wanafanya pamoja kazi hiyo ya kuhubiri. Kazi hiyo imesaidia watu wengi waachane na dini ya uongo na utawala wa Shetani.

Tunahubiri katika dunia yote kwa sababu tunafanya kazi katika umoja

4. Watu wa Yehova wako na kazi kubwa gani leo, na ni jambo gani tu linaweza kuwasaidia kufanya muzuri kazi hiyo?

4 Tumepewa kazi ya kuhubiria watu “habari njema” katika dunia yote mbele mwisho ufike. Hiyo ni kazi kubwa sana! (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Tunapaswa kualika wale wote wenye kuwa na “kiu” wakunywe “maji ya uzima,” ni kusema, tunapaswa kufundisha watu wote wenye wanapenda kusikiliza kweli za Biblia. (Ufunuo 22:17) Lakini, tunaweza kufanya kazi hiyo ikiwa tu ‘tunaunganishwa pamoja kwa upatano’ na kuwa na umoja na ndugu na dada katika kutaniko.—Waefeso 4:16.

5, 6. Wakati tunahubiri, namna gani tunatumika katika umoja?

5 Ili tufikie watu wengi zaidi, kazi yetu ya kuhubiri inapaswa kupangwa muzuri. Maagizo yenye tunapewa katika kutaniko letu yanatusaidia kufanya kazi hiyo. Kisha kumaliza mukutano kwa ajili ya mahubiri, tunaenda kuzungumuza na watu juu ya habari njema ya Ufalme. Tunawatolea pia vichapo vyenye kutusaidia kuelewa Biblia. Kwa hiyo, katika dunia yote tumetolea watu mamilioni ya vichapo. Wakati fulani tunaombwa kufanya kampanye za pekee za kuhubiri. Wakati unafanya kazi hiyo, unatumika katika umoja na mamilioni ya ndugu na dada katika dunia yote wenye wanahubiri ujumbe huo-huo! Unatumika pia pamoja na malaika wenye kusaidia watu wa Mungu katika kazi ya kuhubiri habari njema.—Ufunuo 14:6.

6 Tunafurahi sana wakati tunasoma katika Kitabu cha Mwaka habari juu ya matokeo ya kazi ya kuhubiri katika dunia yote! Fikiria pia namna tunafanya kazi katika umoja wakati tunaalika watu katika dunia yote wafike kwenye mikusanyiko yetu. Kwenye mikusanyiko hiyo, sisi wote tunafundishwa mafundisho moja. Hotuba, michezo yenye kutegemea Biblia, na maonyesho yanatutia moyo tumutumikie Yehova kulingana na uwezo wetu. Tunaungana pia na ndugu na dada zetu wa dunia yote wakati tunakuwa kwenye Ukumbusho wa kila mwaka. (1 Wakorintho 11:23-26) Ili kuonyesha shukrani yetu kwa jambo lenye Yehova ametufanyia na kutii amri ya Yesu, tunakusanyika pamoja siku ileile, ni kusema, tarehe 14 mwezi wa Nisani kisha jua kushuka. Pia, majuma fulani mbele ya Ukumbusho, tunafanya kazi pamoja ili kualika watu wengi zaidi wakusanyike pamoja na sisi wakati wa tukio hilo la maana sana.

7. Wakati tunatumika pamoja, tunaweza kutimiza nini?

7 Nzige moja hawezi kuharibisha sana miti na mimea. Vilevile, mutu moja hawezi kuhubiria watu wote. Lakini kwa sababu tunafanya kazi katika umoja, tunakuwa na uwezo wa kuhubiria mamilioni ya watu juu ya Yehova na kusaidia wamoja kati yao wamusifu na kumuletea heshima.

KUFANYA KAZI PAMOJA KATIKA KUTANIKO

8, 9. (a) Mutume Paulo alitumia mufano gani ili kufundisha Wakristo waendelee kuwa na umoja? (b) Namna gani tunaweza kuungana mukono katika kutaniko?

8 Mutume Paulo alifasiria Wakristo wa muji wa Efeso namna mambo yamepangwa katika kutaniko, na alisema kwamba wote katika kutaniko wanapaswa kukomaa katika mambo yote. (Soma Waefeso 4:15, 16.) Alitumia mufano wa mwili ili kuonyesha kwamba kila Mukristo anaweza kusaidia kutaniko liendelee kuwa na umoja na kumufuata Yesu, Kiongozi wa kutaniko. Mutume Paulo alisema kwamba sehemu zote za mwili zinafanya kazi pamoja ‘kupitia kila kiungo [kiunganishi] ambacho kinatoa kile kinachohitajiwa.’ Kwa hiyo, sisi wote tunapaswa kufanya nini iwe tuko vijana ao wazee, iwe tuko na afya muzuri ao tuko wagonjwa?

Namna gani unaweza kusaidia kutaniko liendelee kuwa na umoja?

9 Yesu ameweka wazee ili waongoze kutaniko, na anapenda tuwaheshimie na kutii muongozo wenye wanatutolea. (Waebrania 13:7, 17) Inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo wakati fulani. Lakini tunaweza kumuomba Yehova atusaidie. Roho yake takatifu inaweza kutusaidia tutii muongozo wowote wenye wazee wanatutolea. Pia, tujue kwamba ikiwa tunakuwa wanyenyekevu na tunatii wazee, ndugu na dada katika kutaniko letu watapata faida kubwa. Kutaniko letu litakuwa na umoja, na tutapendana sana na ndugu na dada zetu.

10. Namna gani watumishi wa huduma wanasaidia kutaniko likuwe na umoja? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

10 Watumishi wa huduma pia wanasaidia kuendeleza umoja katika kutaniko. Wanatumika sana ili kusaidia wazee, na tunashukuru sana kwa kazi yote yenye wanafanya. Kwa mufano, wanahakikisha kwamba kuko vichapo vingi vya kutumikisha katika kazi ya kuhubiri, na wanakaribisha wageni wenye kufika kwenye mikutano yetu. Pia, wanatumika sana ili kutunza Jumba la Ufalme na kulisafisha. Wakati tunaunga mukono ndugu hao, tunakuwa na umoja na tunamutumikia Yehova katika njia yenye kupangwa muzuri.—Linganisha na Matendo 6:3-6.

11. Vijana wanaweza kufanya nini ili kusaidia kutaniko likuwe na umoja?

11 Wazee fulani wametumikia kutaniko kwa bidii kwa miaka mingi. Lakini, pengine hawaweze tena kufanya mengi zaidi kwa sababu ya uzee. Ndugu wenye wangali vijana wanaweza kuwasaidia. Wanaweza kupewa madaraka zaidi katika kutaniko ikiwa wamepata mazoezi. Pia, wakati watumishi wa huduma wanatumika sana, wanaweza kuwa wazee kisha muda fulani. (1 Timotheo 3:1, 10) Vijana fulani wenye kuwa wazee wamefanya maendeleo zaidi. Leo ni waangalizi wa muzunguko na wanasaidia ndugu na dada katika makutaniko mengi. Tunashukuru wakati vijana wanajitoa kwa kujipendea ili kutumikia ndugu na dada.—Soma Zaburi 110:3; Mhubiri 12:1.

KUFANYA KAZI PAMOJA KATIKA FAMILIA

12, 13. Ni nini inaweza kusaidia wote katika familia waungane mukono?

12 Ni nini inaweza kutusaidia tukuwe na umoja katika familia yetu? Ni kufanya ibada ya familia kila juma. Wakati wazazi na watoto wanapitisha wakati pamoja ili kujifunza juu ya Yehova, wanapendana tena zaidi. Wakati huo, wanaweza kufanya mazoezi ya mambo yenye watasema katika mahubiri, na hilo litasaidia kila mumoja wao akuwe tayari kabisa kwa ajili ya mahubiri. Na wakati wanasikia maelezo yenye kila mumoja wao anatoa juu ya kweli na kuona kwamba wote katika familia wanamupenda Yehova na wako tayari kumupendeza, hilo linawasaidia wakaribiane tena zaidi.

Wakati bibi na bwana wanamupenda Yehova na kumutumikia pamoja, wanakuwa na furaha na umoja katika ndoa yao

13 Namna gani bibi na bwana wanaweza kuungana mukono? (Mathayo 19:6) Wakati wote wawili wanamupenda Yehova na kumutumikia pamoja, wanakuwa na furaha na umoja katika ndoa yao. Wanapaswa pia kupendana kama vile Abrahamu na Sara, Isaka na Rebeka, na Elkana na Hana. (Mwanzo 26:8; 1 Samweli 1:5, 8; 1 Petro 3:5, 6) Wakati bibi na bwana wanapendana, wanakuwa na umoja na wanamukaribia Yehova zaidi.—Soma Mhubiri 4:12.

Ibada ya familia inaweza kusaidia vijana na wazee wakaribiane zaidi (Picha hii inapatana na fungu la 12, 15)

14. Ikiwa bibi ao bwana yako haiko Shahidi wa Yehova, unaweza kufanya nini ili ndoa yenu iendelee kuwa nguvu?

14 Biblia inasema waziwazi kwamba hatupaswe kuoa ao kuolewa na mutu mwenye haiko Shahidi wa Yehova. (2 Wakorintho 6:14) Lakini, kuko ndugu na dada wenye wameoa ao kuolewa na mutu mwenye haiko Shahidi wa Yehova. Wamoja kati yao walijifunza kweli kisha kuoa ao kuolewa, lakini bibi ao bwana yao hakufikia kuwa Shahidi wa Yehova. Inawezekana wengine walioa ao kuolewa na Shahidi wa Yehova, kisha bibi ao bwana yao akamuacha Yehova. Katika hali hizo, Wakristo wanajikaza sana ili kufanya ndoa yao iendelee kuwa nguvu kwa kutii mashauri ya Biblia. Inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo wakati fulani. Kwa mufano, dada Mary na David, bwana yake, walimutumikia Yehova pamoja. Kisha, David aliacha kukusanyika. Lakini dada Mary aliendelea kujikaza kuwa bibi muzuri na kuonyesha sifa za Kikristo. Pia, aliwafundisha watoto wake 6 juu ya Yehova na hakuacha kuenda kwenye mikutano na mikusanyiko. Kisha miaka mingi, watoto wake walikomaa na kuondoka nyumbani. Lakini dada Mary aliendelea kumutumikia Yehova hata kama haikuwa mwepesi kufanya hivyo. Wakati huo, David alianza kusoma magazeti yenye dada Mary alimuachia. Kisha, David alianza tena kuenda kwenye mikutano fulani. Sikuzote mujukuu (munkana) wake wa miaka 6 alikuwa anamuchungia nafasi, na ikiwa David hakufika, mutoto huyo alikuwa anamuambia hivi: “Tate (nkambo) haukufika leo kwenye mikutano.” Kisha miaka 25, David alimurudilia Yehova; sasa yeye na bibi yake ni wenye furaha kwa sababu wanamutumikia tena Yehova pamoja.

15. Namna gani bibi na bwana wenye wamefanya miaka mingi katika ndoa wanaweza kusaidia wale wenye wameoana hivi karibuni?

15 Shetani anashambulia familia leo. Ndiyo sababu bibi na bwana wenye kuwa Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuungana mukono. Hata kama umekuwa katika ndoa tangu miaka mingi ao umeoa ao kuolewa hivi karibuni, ufikirie mambo yenye unaweza kusema ao kufanya ili ndoa yako ikuwe nguvu. Ikiwa mumekuwa katika ndoa tangu miaka mingi, munaweza kuwa mufano muzuri kwa wale wenye wameoana hivi karibuni. Pengine munaweza kuwaalika kwenye ibada yenu ya familia. Wataona kwamba bibi na bwana wanapaswa kupendana na kuwa na umoja hata kama wamefanya miaka mingi katika ndoa ao wameoana hivi karibuni.—Tito 2:3-7.

‘TUENDE JUU KWENYE MULIMA WA YEHOVA’

16, 17. Watumishi wa Mungu wenye kuwa na umoja wanangojea nini?

16 Wakati Waisraeli walikuwa wanaenda kwenye sikukuu zao huko Yerusalemu, waliungana mukono. Walikuwa wanatayarisha vitu vyote vyenye walikuwa navyo lazima kwa ajili ya safari. Kisha, walisafiri pamoja na kusaidiana. Wote walimusifu Yehova na kumuabudu pamoja kwenye hekalu. (Luka 2:41-44) Kwa sababu tunajitayarisha leo ili kuishi katika dunia mupya, tunapaswa kuwa na umoja na kujikaza sana ili tuungane mukono. Unaweza kufikiria njia fulani zenye unaweza kutumia ili uendelee kufanya hivyo zaidi?

17 Watu wa ulimwengu huu hawasikilizane na wanapigana. Lakini sisi tunamushukuru Yehova kwa sababu ametusaidia tukuwe na amani na tuelewe kweli! Katika dunia yote, watumishi wake wanamuabudu katika njia yenye kumupendeza. Pia, kuliko wakati mwingine wowote, katika siku hizi za mwisho, watumishi wa Yehova wanaishi katika umoja. Kama vile tu nabii Isaya na Mika walitabiri, tunaenda pamoja kwenye ‘mulima wa Yehova.’ (Isaya 2:2-4; soma Mika 4:2-4.) Wakati unaokuja, tutafurahi sana wakati watu katika dunia yote ‘wataunganishwa pamoja kwa upatano’ ili kumuabudu Yehova pamoja!