Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kataa Mawazo ya Ulimwengu

Kataa Mawazo ya Ulimwengu

‘Mujihazari [mukuwe waangalifu]: labda kuna mutu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mutupu . . . wa ulimwengu.’​—KOL. 2:8.

NYIMBO: 38, 31

1. Ni shauri gani lenye mutume Paulo aliandikia Wakristo wenzake? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

INAWEZEKANA kabisa kuwa mutume Paulo aliandika barua yake kwa Wakolosai mwishoni mwa kifungo chake cha kwanza katika Roma, ao katika mwaka wa 60 mupaka wa 61 hivi, kisha kuzaliwa kwa Yesu. Aliwaambia kuwa ni jambo la maana wakuwe na “utambuzi wa kiroho.” (Kol. 1:9) Pia Paulo alisema hivi: ‘Ninasema jambo hili ili mutu yeyote asiwadanganye ninyi kwa hoja [maneno] zenye kushawishi. Mujihazari: labda kuna mutu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mutupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya musingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.’ (Kol. 2:4, 8) Paulo alieleza pia sababu gani mawazo fulani yenye yalikuwa yameenea hayakukuwa sawa na sababu gani watu wenye hawakamilike wanaweza kuchochewa na mawazo ya ulimwengu. Kwa mufano, yanaweza kufanya mutu ajione kuwa mwenye hekima ao wa hali ya juu kuliko wengine. Barua hiyo ilikuwa na kusudi la kuwasaidia ndugu na dada wakatae mawazo ya ulimwengu na matendo ya mubaya.​—Kol. 2:16, 17, 23.

2. Sababu gani tutachunguza mifano ya mawazo ya ulimwengu?

2 Mawazo ya ulimwengu yanazarau ao yanapunguza uzito wa kanuni za Yehova na ikiwa tunachochewa nayo yanaweza kuregeza polepole imani yetu. Leo, sisi wote tunaweza kuambukizwa na mawazo ya ulimwengu. Yanakaziwa kwenye televizyo, Internete, kwenye kazi, ao kwenye masomo. Katika habari hii, tutazungumuzia mambo yenye tunaweza kufanya ili kuzuia mawazo hayo yasidanganye akili yetu. Tutachunguza mifano tano ya mawazo ya ulimwengu na namna gani tunaweza kuepuka mawazo hayo.

TUKO NA LAZIMA YA KUMUAMINI MUNGU?

3. Watu wengi wanachochewa na wazo gani, na sababu gani?

3 “Ninaweza kuwa mutu muzuri bila kumuamini Mungu.” Katika inchi nyingi, ni jambo la kawaida kusikia watu wanasema kuwa hawamuamini Mungu; wanajiona kuwa watu wenye hawana dini yoyote. Pengine hawakuchunguza kwa uangalifu ili kujua ikiwa Mungu iko ao hapana, lakini wanachochewa na wazo la kuwa na uhuru wa kufanya mambo yenye wanapenda. (Soma Zaburi 10:4.) Wengine wanaweza kujiona kuwa wako na hekima ya ulimwengu wakati wanasema hivi: “Ninaweza kuwa na kanuni za juu za mwenendo bila kumuamini Mungu.”

4. Namna gani tunaweza kufikiri na mutu mwenye kuamini kuwa hakuna Muumbaji?

4 Ni jambo lenye kupatana na akili kuamini kuwa hakuna Muumbaji? Kama mutu anategemea sayansi ili kujua kabisa ikiwa uzima uliumbwa ao hapana, anaweza kuvurugika na habari zenye haziko wazi. Lakini kwa kweli, jibu liko mwepesi. Ikiwa nyumba inapaswa kujengwa na mutu fulani, vitu vyenye kuwa na uzima vinapaswa kabisa kuwa viliumbwa na mutu fulani! Kwa kweli, chembe ndogo sana zenye uzima zenye kuwa katika dunia ni za ajabu sana kuliko nyumba yoyote kwa sababu zinaweza kufanya mambo yenye nyumba haiwezi kufanya, ni kusema, kutengeneza chembe zingine. Kwa hiyo, chembe hizo ziko na namna ya kuchunga habari na kufanya kopi ya habari zenye kuhitajiwa ili kutengeneza chembe zingine zenye kuzifanana. Ufundi wa chembe hizo zenye kuwa na uzima ulitoka wapi? Biblia inajibia hivi: ‘Kila nyumba inajengwa na mutu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.’​—Ebr. 3:4.

5. Tunaweza kusema nini juu ya wazo la kuwa mutu anaweza kuamua mambo yenye kuwa sawa bila kumuamini Mungu?

5 Tunaweza kusema nini juu ya wazo la kuwa mutu anaweza kuamua mambo yenye kuwa sawa bila kumuamini Mungu? Neno la Mungu linaonyesha kuwa watu wenye hawaamini wanaweza kuwa na kanuni fulani za muzuri. (Rom. 2:14, 15) Kwa mufano, wanaweza kuheshimia wazazi wao na kuwapenda. Lakini ikiwa hawafuate kanuni za Yehova, wanaweza kukamata maamuzi ya mubaya. (Isa. 33:22) Leo, watu wengi wenye kufikiri muzuri wanakubali kuwa hali za mubaya sana zenye kuwa katika dunia zinaonyesha kabisa kuwa mwanadamu iko na lazima ya musaada wa Mungu. (Soma Yeremia 10:23.) Kwa hiyo, tunapaswa kuepuka kufikiri kuwa mutu anaweza kuamua kabisa mambo yenye kuwa sawa bila kumuamini Mungu na kufuata kanuni zake.​—Zab. 146:3.

TUKO NA LAZIMA YA DINI?

6. Watu wengi wako na mawazo gani juu ya dini?

6 “Unaweza kuwa na furaha hata kama hauko katika dini fulani.” Watu wengi wanapendezwa na wazo hilo la ulimwengu kwa sababu wanaona kuwa dini inachokesha watu na haina maana. Pia dini nyingi zinafanya watu wasimukaribie Mungu kwa sababu zinafundisha moto wa mateso, zinaomba sadaka, na zinahubiri mambo ya politike. Ndiyo sababu watu wengi zaidi wanaona kuwa wanaweza kuwa na furaha hata kama hawako katika dini fulani! Watu hao wanaweza kusema hivi: “Ninapendezwa na mambo ya Mungu, lakini sipendi kujiunga na dini fulani.”

7. Namna gani dini ya kweli inaleta furaha?

7 Ni kweli kwamba mutu anaweza kuwa na furaha hata kama haiko katika dini fulani? Bila shaka, mutu anaweza kuwa na furaha bila kuwa katika dini ya uwongo, lakini mutu anaweza kuwa na furaha kabisa ikiwa iko na urafiki pamoja na Yehova, mwenye Biblia inaonyesha kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11) Kila kitu chenye Mungu anafanya kinatuletea faida. Watumishi wake wako na furaha kwa sababu wanatumia maisha yao ili kusaidia wengine. (Mdo. 20:35) Kwa mufano, fikiria namna ibada ya kweli inafanya familia ikuwe na furaha. Ibada ya kweli inatufundisha kuheshemia bibi ao bwana yetu, kuona naziri za ndoa kuwa takatifu, kuepuka uzinifu, kukomalisha watoto muzuri, na kuonyesha upendo wa kweli. Kwa hiyo, ibada kama hiyo inaunganisha watu katika makutaniko yenye kuwa na furaha na familia ya ndugu na dada katika dunia yote yenye kuwa na furaha.​—Soma Isaya 65:13, 14.

8. Namna gani Mathayo 5:3 inaweza kutusaidia kuelewa ni nini inaletea watu furaha?

8 Namna gani tunaweza kuona wazo la ulimwengu lenye kuonyesha kuwa mutu anaweza kuwa na furaha bila kumutumikia Mungu? Fikiria ulizo hili: Ni nini inaletea watu furaha? Watu fulani wanapata furaha katika kazi ya kimwili, michezo, ao katika mambo ya kujifurahisha. Wengine wanapata furaha kwa kuhangaikia familia ao marafiki wao. Hata kama mambo hayo yanaweza kuleta furaha, maisha yetu yako na kusudi kubwa zaidi lenye kutuletea furaha yenye kuendelea. Tofauti na wanyama, tunaweza kufikia kumujua Muumbaji wetu na kumutumikia kwa uaminifu. Tumeumbwa katika njia hiyo, ili tupate furaha wakati tunafanya hivyo. (Soma Mathayo 5:3.) Kwa mufano, waabudu wa kweli wanapata furaha na kutiwa moyo sana wakati wanakutana pamoja ili kumuabudu Yehova. (Zab. 133:1) Pia, wanafurahia umoja wa familia ya ndugu na dada ya duniani pote, maisha yenye kuwa safi, na tumaini lenye furaha.

TUKO NA LAZIMA YA KANUNI ZA MWENENDO?

9. (a) Watu wengi wako na mawazo gani juu ya ngono katika ulimwengu huu? (b) Sababu gani Neno la Mungu linakataza kufanya ngono inje ya ndoa?

9 “Kuko ubaya gani wa kufanya ngono inje ya ndoa?” Watu wanaweza kutuambia hivi: “Mutu anapaswa kufurahia maisha. Kuko ubaya gani wa kufanya ngono inje ya ndoa?” Wazo la kuwa Mukristo anapaswa kuona uasherati kuwa jambo la kawaida, ni wazo la mubaya. Sababu gani? Kwa sababu Neno la Mungu linakataza uasherati. * (Soma 1 Wathesalonike 4:3-8.) Yehova iko na haki ya kutuwekea sheria kwa sababu yeye ndiye alituumba. Sheria ya Mungu inaruhusu tu kufanya ngono kati ya mwanaume na mwanamuke wenye kuoana na ni sehemu ya mupango wa ndoa. Mungu anatupatia sheria kwa sababu anatupenda. Zinatuletea faida. Familia zenye kuheshimia sheria hizo zinakuwa na upendo, heshima, na usalama. Mungu anachukia mutu mwenye kuvunja sheria zake kwa makusudi.​—Ebr. 13:4.

10. Namna gani Mukristo anaweza kuepuka kabisa uasherati?

10 Neno la Mungu linatufundisha namna ya kuepuka uasherati. Njia kubwa ya kufanya hivyo ni kuwa waangalifu juu ya mambo yenye tunaangalia. Yesu alisema hivi: ‘Kila mutu ambaye anaendelea kumutazama mwanamuke na kumutamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake. Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, liongoe ulitupilie mbali nawe.’ (Mt. 5:28, 29) Kwa hiyo, Mukristo anapaswa kuepuka kuangalia pornografia ao kusikiliza miziki yenye kuwa na maneno ya machafu. Mutume Paulo aliandikia Wakristo wenzake hivi: ‘Muviue viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati.’ (Kol. 3:5) Pia, tunapaswa waangalifu juu ya mambo yenye tunafikiria na mambo yenye tunazungumuzia.​—Efe. 5:3-5.

TUNAPASWA KUFUATIA KAZI YA MUZURI YA KIMWILI?

11. Sababu gani tunaweza kuchochewa kufuatia kazi ya muzuri ya kimwili?

11 “Kufuatia kazi ya muzuri ya kimwili kunaleta furaha.” Watu wengi wanatuchochea tufuatie kazi ya kimwili katika maisha yetu. Kazi hiyo inaweza kutufanya tutazamie kujulikana, kupata cheo, kuwa na utajiri. Kwa sababu watu wengi wanafuatia sana kazi ya kimwili katika maisha yao, Mukristo pia anaweza kufikia kuwa na mawazo kama hayo.

12. Kazi ya muzuri ya kimwili inaleta furaha?

12 Ni kweli kwamba kazi ya muzuri yenye kukutolea cheo na kukufanya ukuwe mwenye kujulikana sana inaweza kukuletea furaha ya kuendelea? Hapana. Ukumbuke kuwa tamaa ya kupenda kutawala wengine na kupenda kujulikana sana ndiyo mambo yalimuchochea Shetani, lakini iko na hasira na hana furaha. (Mt. 4:8, 9; Ufu. 12:12) Wakati tunalinganisha furaha yenye kuendelea yenye mutu anapata wakati anasaidia watu wafaidike na hekima ya Neno la Mungu ili wafikie kupata uzima wa milele, kazi ya kimwili inaweza tu kutuletea furaha yenye kuwa na mipaka. Zaidi ya hilo, roho ya ulimwengu huu inaendelea kuchochea watu sana. Inachochea watu wakuwe na roho ya mashindano, inaleta wivu, na mwishowe inaonekana kuwa ni “kufuatilia upepo.”​—Mhu. 4:4.

13. (a) Tunapaswa kuona kazi ya kimwili namna gani? (b) Kulingana na barua yenye mutume Paulo aliandikia Wathesalonike, ni nini ilimuletea furaha kubwa?

13 Kwa kweli, tunapaswa kutimiza mahitaji yetu ya kimwili, na hakuna ubaya wa kufanya kazi yenye tunapenda. Lakini kazi ya kimwili haipaswe kuwa jambo na maana sana katika maisha yetu. Yesu alisema hivi: ‘Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamuchukia mumoja na kumupenda yule mwingine, ama atashikamana na mumoja na kumuzarau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.’ (Mt. 6:24) Wakati tunakaza akili yetu juu ya kumutumikia Yehova na kufundisha wengine Neno lake, tunapata furaha kubwa sana. Mutume Paulo ni mumoja kati ya watu wenye walijionea jambo hilo. Zamani katika maisha yake, alikuwa amefuatia kazi ya muzuri sana katika dini ya Kiyahudi, lakini alipata furaha ya kweli wakati alianza kufanya kazi ya kufanya wanafunzi na kujionea namna watu wanaitikia ujumbe wa Mungu na namna ulibadilisha maisha yao. (Soma 1 Wathesalonike 2:13, 19, 20.) Hakuna kazi ingine yenye kuleta furaha kama hiyo.

Kusaidia watu wafaidike na hekima ya Neno la Mungu kunaleta furaha yenye kuendelea (Picha hizi zinapatana na fungu la 12, 13)

TUNAWEZA KUMALIZA MAGUMU YA MWANADAMU?

14. Sababu gani mutu anaweza kupendezwa na wazo la kuwa mwanadamu anaweza kumaliza magumu yake?

14 “Wanadamu wanaweza kumaliza magumu yao.” Watu wengi wanaweza kuchochewa na wazo hilo. Sababu gani? Ikiwa ni kweli, inaweza kumaanisha kuwa mwanadamu hana lazima ya muongozo wa Mungu na kuwa anaweza kufanya mambo yenye anapenda. Pia, wazo la kuwa mwanadamu anaweza kumaliza magumu yake linaweza kusadikisha wengi kwa sababu, kulingana na uchunguzi fulani, vita, jeuri, magonjwa, na umasikini vinaendelea kupunguka. Ripoti moja inasema hivi: “Hali ya wanadamu inaendelea kuwa muzuri zaidi kwa sababu wanadamu wameamua kufanya ulimwengu ukuwe nafasi ya muzuri ya kuishi.” Maelezo hayo yanaonyesha kuwa mwanadamu anakaribia kumaliza magumu yenye yamemusumbua kwa miaka mingi? Ili kupata jibu, tuzungumuzie kwa uangalifu magumu hayo.

15. Ni mambo gani yenye kuonyesha kuwa magumu ya mwanadamu yanaendelea kuongezeka?

15 Vita: Inakadiriwa kuwa watu milioni 60 ao zaidi walikufa wakati wa Vita ya Kwanza na Vita ya Pili ya Ulimwengu. Kwa kweli, tangu Vita ya Pili ya Ulimwengu, wanadamu hawajajifunza namna ya kuepuka vita. Kufikia mwaka wa 2015, hesabu ya watu wenye waliacha makao yao kwa sababu ya vita ao kwa sababu ya kuteswa ilikuwa imeongezeka na kufikia watu milioni 65 hivi. Imekadiriwa kuwa watu 12 400 000 waliacha makao yao katika mwaka wa 2015 tu. Jeuri: Hata kama aina fulani ya jeuri imepunguka katika maeneo fulani, aina ingine ya jeuri inaendelea kuongezeka sana, kama vile jeuri kupitia Internete, jeuri nyumbani, na ugaidi (terorisme). Zaidi ya hilo, watu wengi wanaamini kuwa rushwa [kata-midomo] imeongezeka zaidi katika ulimwengu muzima. Wanadamu hawawezi kumaliza jeuri. Magonjwa: Wanadamu wamepata dawa kwa ajili ya magonjwa fulani. Lakini ripoti moja yenye ilitolewa katika mwaka wa 2013 ilionyesha kuwa kila mwaka watu milioni kenda wenye kuwa chini ya miaka 60 wanakufa kwa sababu ya ugonjwa wa kupooza, kansere, magumu ya kupumua, na ugonjwa wa sukari. Umasikini: Kulingana na Benki ya Dunia, hesabu ya watu wenye kuwa masikini sana katika Afrika tu imeongezeka kutoka watu milioni 280 katika mwaka wa 1990 mupaka milioni 330 katika mwaka wa 2012.

16. (a) Sababu gani ni Ufalme wa Mungu tu ndio unaweza kumaliza magumu ya wanadamu? (b) Ni baraka gani zenye Isaya na mwandikaji mumoja wa zaburi walitabiri?

16 Watu wenye mamlaka wenye kusimamia mambo ya feza na wenye kuwa katika politike ni wenye kujipenda wenyewe. Ni wazi kwamba, watu hao wenye mamlaka hawawezi kumaliza, vita, magonjwa, na umasikini; ni Ufalme wa Mungu tu ndio utamaliza mambo hayo. Fikiria mambo yenye Yehova atafanyia wanadamu. Vita: Ufalme wa Mungu utaondoa mambo makubwa yenye kuchochea vita, ni kusema, tabia ya watu kujipenda wenyewe, rushwa, kupenda sana inchi, dini ya uwongo, na Shetani mwenyewe. (Zab. 46:8, 9) Jeuri: Ufalme wa Mungu tayari unafundisha mamilioni ya watu kupendana na kutumainiana na hakuna serikali ingine yenye kufanya hivyo. (Isa. 11:9) Magonjwa: Yehova atabariki watu wake kwa kuwapatia afya kamilifu. (Isa. 35:5, 6) Umasikini: Yehova atamaliza umasikini na atapatia watu wake utajiri wa kiroho na wa kimwili, maisha yenye kuwa ya maana zaidi kuliko utajiri wowote.​—Zab. 72:12, 13.

‘MUJUE JINSI MUNAVYOPASWA KUJIBIA’

17. Namna gani unaweza kukataa mawazo ya ulimwengu?

17 Ikiwa unasikia wazo la ulimwengu lenye linaweza kutia imani yako katika hatari, tafuta mambo yenye Neno la Mungu linasema juu ya habari hiyo na uzungumuzie jambo hilo pamoja na Mukristo mwenzako mwenye kuwa na uzoefu. Uchunguze sababu gani wazo hilo linaweza kukupendeza, sababu gani wazo hilo ni la uwongo, na namna gani unaweza kukataa wazo hilo. Kwa kweli, sisi wote tunaweza kujilinda juu ya mawazo ya ulimwengu kwa kutii shauri la mutume Paulo lenye alipatia kutaniko la Kolosai: ‘Muendelee kutembea kwa hekima kuelekea wale walio inje . . . Mujue jinsi munavyopaswa kumujibu kila mutu.’​—Kol. 4:5, 6.

^ fu. 9 Kisha kusoma Yohana 7:53–8:11 watu wengi wamefikia kusema kuwa mutu mwenye hana zambi ndiye anaweza tu kumuhukumu mutu mwenye alifanya uzinifu. Lakini watu wengi hawajue kuwa maandiko hayo yaliongezwa na hayakukuwa sehemu ya maandishi ya kwanza-kwanza yenye yaliongozwa na roho ya Mungu. Ndiyo sababu maandiko hayo hayakuwekwa katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya sasa ya Kiingereza. Lakini sheria yenye Mungu alipatia taifa la Israeli ilisema hivi: ‘Ikiwa mwanamume atapatikana akilala na mwanamuke aliye na mume, wote wawili watauawa.’​—Kum. 22:22.