Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Imba kwa Sauti Yenye Shangwe!

Imba kwa Sauti Yenye Shangwe!

‘Ni vema kumupigia Mungu wetu muziki.’​—ZAB. 147:1.

NYIMBO: 9, 138

1. Kuimba kunatusaidia kufanya nini?

MWANDIKAJI mumoja wa nyimbo mwenye kujulikana sana alisema hivi: “Wakati unasikia maneno, hilo linakuchochea kuwaza. Wakati unasikia muziki, unajisikia kwa njia fulani. Lakini wakati unaimba, maneno yanagusa moyo wako.” Nyimbo zetu zinamutolea sifa, Yehova Baba yetu wa mbinguni na zinaonyesha kuwa tunamupenda. Ndiyo sababu kuimba ni sehemu ya maana sana ya ibada safi, iwe tuko peke yetu wakati tunaimba ao tuko pamoja na watu wa Mungu katika kutaniko.

2, 3. (a) Watu fulani wanaweza kujisikia namna gani juu ya kuimba kwa sauti kubwa pamoja na kutaniko? (b) Tutajibia maulizo gani?

2 Lakini, uko na mawazo gani juu ya kuimba kwa sauti kubwa pamoja na kutaniko? Unasikia haya ya kufanya hivyo? Katika desturi fulani, wanaume wanaweza kusikia haya ya kuimba mbele ya watu wengi. Mawazo hayo yanaweza kuwa na matokeo juu ya kutaniko lote, zaidi sana ikiwa wale wenye kuongoza wanatafuta visababu vya kukosa kuimba ao wanafanya mambo mengine wakati wengine katika kutaniko wanaimba.​—Zab. 30:12.

3 Ikiwa tunaona kabisa kuwa kuimba ni sehemu ya ibada yetu, tutaepuka kabisa kutoka inje ao kukosa kuwa kwenye sehemu hiyo ya mikutano yetu. Kwa hiyo, kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Niko na mawazo gani juu ya kuimba kwenye mikutano yetu ya ibada? Namna gani ninaweza kumaliza vizuizi vyenye vinaweza kunizuia kuimba kwa shangwe? Na ninaweza kufanya nini ili niimbe kwa moyo wangu wote nyimbo zetu?’

KUIMBA NI SEHEMU YA MAANA YA IBADA YA KWELI

4, 5. Ni mipango gani ilifanywa kwa ajili ya kuimba katika ibada katika Israeli ya zamani?

4 Tangu zamani, waabudu waaminifu wa Yehova wametumia muziki ili kumusifu Yehova. Ni jambo lenye kupendeza sana kujua kuwa wakati taifa la Israeli la zamani lilikuwa linamutumikia Yehova kwa uaminifu, kuimba ilikuwa sehemu ya maana ya ibada yao. Kwa mufano, wakati alifanya matayarisho juu ya utumishi kwenye hekalu, Mufalme Daudi alipanga Walawi 4000 ili watoe muziki wa sifa. Kati yao 288 “waliozoezwa nyimbo kwa Yehova, wote wakiwa wajuzi [mafundi].”​—1 Nya. 23:5; 25:7.

5 Wakati hekalu lilitolewa kwa Yehova, muziki na nyimbo zilichukua nafasi ya maana sana. Biblia inatuambia hivi: ‘Na ikawa kwamba mara tu wapiga-tarumbeta na waimbaji walipokuwa kama mutu mumoja kwa kutokeza sauti moja isikike katika kumusifu na kumushukuru Yehova, na mara tu walipopaaza sauti kwa tarumbeta na kwa matoazi na kwa vyombo vya nyimbo na kwa kumusifu Yehova, . . . utukufu wa Yehova uliijaza nyumba ya Mungu wa kweli.’ Kwa kweli hilo lilikuwa tukio lenye kutia nguvu imani kabisa!​—2 Nya. 5:13, 14; 7:6.

6. Ni mipango gani ya pekee yenye ilifanywa kuhusu kuimba wakati Nehemia alikuwa gavana wa Yerusalemu? Eleza.

6 Wakati Nehemia aliongoza Waisraeli waaminifu katika kazi ya kujenga upya kuta za Yerusalemu, alipanga pia waimbaji Walawi wenye kuwa na vyombo vyenye kuenea vya kupiga muziki. Wakati ukuta huo ulitolewa kwa Yehova, muziki wa pekee wenye uliimbwa, ulichangia sana ili tukio hilo likuwe lenye furaha. Wakati huo, kulikuwa “makundi mawili makubwa ya waimbaji ya kutoa shukrani.” Makundi hayo ya kuimba yalitembea pande tofauti na kukutana kwenye ukuta wenye ulikuwa karibu na hekalu ili waweze kuimba kwa sauti yenye ingesikika mupaka sehemu za mbali. (Neh. 12:27, 28, 31, 38, 40, 43) Kwa kweli, Yehova alifurahi sana kusikia namna waabudu wake wanamuimbia sifa kwa shangwe.

7. Namna gani Yesu alionyesha kuwa ni jambo la maana kuimba katika ibada ya Kikristo?

7 Wakati kutaniko la Kikristo lilianzishwa, nyimbo ziliendelea kuwa sehemu ya maana ya ibada ya kweli. Katika usiku mumoja wa maana zaidi katika historia ya wanadamu, Yesu na mitume wake waliimba nyimbo kisha Yesu kuanzisha Chakula cha Bwana cha Mangaribi.​—Soma Mathayo 26:30.

8. Namna gani Wakristo wa wakati wa mitume walituachia mufano wa kuimba katika ibada?

8 Wakristo wa wakati wa mitume walituachia mufano muzuri wa kuimba pamoja ili kumusifu Mungu. Hata kama mara nyingi walikusanyika katika nyumba za watu, nyumba hizo za kawaida hazikuwazuia kumuimbia Yehova kwa bidii. Mutume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu ili kutolea ndugu zake Wakristo maagizo haya. Aliandika hivi: ‘Muendelee kufundishana na kuonyana kwa zaburi, sifa kwa Mungu, nyimbo za kiroho kwa neema, mukimuimbia Yehova mioyoni mwenu.’ (Kol. 3:16) Nyimbo zenye kuwa katika kitabu chetu cha nyimbo ni “nyimbo za kiroho za [kuimbwa] kwa neema” kabisa. Ni sehemu ya chakula cha kiroho chenye kutolewa na ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara.’​—Mt. 24:45.

NAMNA YA KUMALIZA WOGA WA KUIMBA

9. (a) Ni nini inaweza kuzuia watu fulani kuimba kwa shangwe kwenye mikutano na mikusanyiko yetu? (b) Namna gani tunapaswa kumuimbia Yehova sifa, na ni nani wenye wanapaswa kuonyesha mufano? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

9 Tuseme nini ikiwa watu hawazoee kuimba katika familia yenu, katika desturi yenu, ao mahali kwenye unaishi? Kupitia teknolojia ya sasa, unaweza kusikiliza nyimbo za waimbaji wenye kuwa na ufundi wa kuimba. Lakini, unaweza kusikia haya ao kuvunjika moyo wakati unalinganisha sauti yako na sauti za waimbaji hao wa ulimwengu huu. Hilo halipaswe kukuzuia kumuimbia Yehova sifa. Lakini, uinue kitabu chako cha wimbo, uinue kichwa chako, na kuimba kwa moyo wako wote! (Ezra 3:11; soma Zaburi 147:1.) Leo, katika Majumba mengi ya Ufalme, maneno ya wimbo yanaonyeshwa kwenye skrini ao écran, na hilo linatusaidia kuimba kwa sauti kubwa. Ni jambo lenye kupendeza pia kuwa sehemu ya kuimba nyimbo za Ufalme imewekwa kwenye programu ya Masomo ya Huduma ya Ufalme kwa ajili ya wazee. Hilo linaonyesha kuwa ni jambo la lazima wazee waonyeshe mufano wakati kutaniko linaimba.

10. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa woga unatuzuia kuimba kwa sauti kubwa?

10 Jambo moja lenye kuzuia watu wengi kuimba kwa sauti kubwa ni woga. Pengine ni kwa sababu wanaogopa kusimama ao pengine wanaogopa kuwa hawana sauti za muzuri. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kuwa wakati tunasema, ‘sisi sote tunajikwaa [tunakosea] mara nyingi.’ (Yak. 3:2) Lakini, hilo halituzuie kusema. Kwa hiyo, hatupaswe kuruhusu sauti zetu zenye hazikamilike zituzuie kumuimbia Yehova sifa.

11, 12. Ni mashauri gani fulani yanaweza kutusaidia kuimba muzuri zaidi?

11 Pengine tunaogopa kuimba kwa sababu hatujue muzuri namna ya kuimba. Lakini, tunaweza kufanya maendeleo juu ya namna yetu ya kuimba kwa kufuata mashauri fulani ya musingi. *

12 Unaweza kujifunza namna ya kuimba kwa sauti yenye nguvu na yenye kuwa kubwa kwa kupumua muzuri. Kama vile moto wa umeme unafanya taa iwake, kupumua muzuri kunafanya sauti yako ikuwe na nguvu wakati unazungumuza ao wakati unaimba. Unapaswa kuimba kwa sauti kubwa kama ile yenye unatumia wakati unasema ao hata kwa sauti kubwa zaidi. (Ona mashauri yenye kupatikana katika kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ukurasa wa 181 mupaka wa 184, chini ya kichwa kidogo “Pumua Vizuri.”) Kwa kweli, kuhusu kuimba sifa, wakati fulani Maandiko yanaambia waabudu wa Yehova wapige “vigelegele vya shangwe.”​—Zab. 33:1-3.

13. Namna gani tunaweza kuongeza uwezo wetu wa kuimba? Eleza.

13 Wakati wa ibada ya familia ao wakati uko peke yako, ujaribu kufanya hivi: Uchague wimbo moja wenye unapenda sana katika kitabu chetu cha wimbo. Soma maandishi ya wimbo kwa sauti ya juu, na bila kuogopa. Kisha, utumie sauti ileile ili kusema maneno yote yenye kuwa katika mustari moja wa wimbo kwa kupumua mara moja. Kisha uimbe mustari huo kwa kutumia sauti ileile yenye kuwa na nguvu. (Isa. 24:14) Sauti yako ya kuimba itakuwa na nguvu, na hilo ni jambo la muzuri. Usiache sauti yako ikufanye uogope ao kusikia haya!

14. (a) Namna gani kufungua sana kinywa chetu kunaweza kutusaidia wakati tunaimba? (Ona kisanduku “ Namna Unaweza Kuimba Muzuri Zaidi.”) (b) Ni mashauri gani juu ya kumaliza magumu ya kuimba yenye umeona kuwa yenye kufaa?

14 Hautaimba kwa sauti ya nguvu ikiwa haufungue kabisa kinywa chako. Kwa hiyo, shauri lingine ni kufungua sana kinywa chako kuliko namna unazoea kukifungua wakati unaongea. Unapaswa kufanya nini ikiwa unaona kuwa hauna sauti yenye nguvu ao uko na sauti ya juu sana? Unaweza kupata mashauri yenye kufaa juu ya magumu hayo katika kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ukurasa wa 184, katika kisanduku chenye kichwa, “Kushinda Matatizo Fulani Hususa.”

IMBA SIFA KWA MOYO WAKO WOTE

15. (a) Ni tangazo gani lenye lilifanywa kwenye mukutano wa kila mwaka wa 2016? (b) Sababu gani kitabu cha nyimbo kilitafsiriwa upya?

15 Ilikuwa furaha sana kwenye mukutano wa kila mwaka wa 2016 wa shirika Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania wakati Ndugu Stephen Lett wa Baraza Lenye Kuongoza alitangaza kutolewa kwa kitabu kipya cha nyimbo, chenye kichwa ‘Mwimbieni Yehova kwa Shangwe’ chenye tungepata hivi karibuni na kukitumia kwenye mikutano yetu. Ndugu Lett alieleza kuwa kusudi moja la kufanya kitabu kipya cha wimbo lilikuwa kukipatanisha na Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya sasa. Iliomba kuondoa ao kutafsiri upya maneno fulani yenye hayapatikane tena katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya sasa yenye ilitolewa mwaka wa 2013. Pia, nyimbo za mupya zenye kuzungumuzia kazi yetu ya kuhubiri na nyimbo zenye kuonyesha shukrani yetu juu ya zabihu ya ukombozi zimeongezwa katika kitabu hicho. Pia, kwa sababu kuimba ni sehemu ya maana ya ibada yetu, Baraza Lenye Kuongoza lilipenda kufanya kitabu kizuri chenye kuwa na jalada lenye kufanana na jalada la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya sasa.

16, 17. Ni mabadiliko gani ya muzuri yenye yalifanywa katika kitabu kipya cha nyimbo?

16 Ili kufanya kitabu ‘Mwimbieni Yehova kwa Shangwe’ kikuwe mwepesi kutumiwa, nyimbo zinapangwa kulingana na vichwa vya habari. Kwa mufano, nyimbo 12 za kwanza zinazungumuzia Yehova, zingine 8 zenye kufuata zinazungumuzia Yesu na zabihu ya ukombozi na kuendelea. Kwa mufano, kuko index ya nyimbo yenye itasaidia musemaji achague muzuri wimbo wa kutumia kwa ajili ya hotuba.

17 Ili kusaidia kila mutu aimbe kwa moyo wake wote, maneno fulani ya wimbo yamebadilishwa ili mawazo yaeleweke waziwazi na maneno yenye haitumiwe tena kwa ukawaida yameondolewa. Kwa mufano, ilifaa kabisa kubadilisha wimbo wenye kichwa “Linda Moyo Wako” na kuufanya kuwa “Tuulinde Moyo Wetu.” Sababu gani? Kwa sababu zamani, wakati mutu alikuwa anaimba wimbo huo, alikuwa anaambia wengine mambo yenye wanapaswa kufanya. Hilo lingekuwa jambo ngumu kwa wapya, wale wenye kupendezwa na kweli, vijana, na dada wenye wanahuzuria mikutano na mikusanyiko yetu. Kwa hiyo, kichwa na maneno ya wimbo huo vilibadilishwa.

Mufanye mazoezi ya kuimba wakati wa ibada ya familia (Picha hii inapatana na fungu la 18)

18. Sababu gani tunapaswa kujua muzuri nyimbo zenye kuwa katika kitabu kipya cha nyimbo? (Ona maelezo ya chini.)

18 Nyimbo nyingi zenye kuwa katika kitabu ‘Mwimbieni Yehova kwa Shangwe’ ziko kama sala. Nyimbo hizo zinaweza kukusaidia kumuambia Yehova mambo yote yenye kuwa katika moyo wako. Zingine zitasaidia ‘kutuchochea katika upendo na matendo mazuri.’ (Ebr. 10:24) Bila shaka, tunapenda kujua muzuri muziki, namna ya kuimba, na maneno ya nyimbo zetu. Unaweza kufanya hivyo kwa kusikiliza nyimbo zenye kuimbwa zenye kupatikana kwenye adresi yetu ya Internete jw.org. Wakati unajifunza nyimbo hizo nyumbani, unaweza kujua namna ya kuimba bila kuogopa na kuimba kwa moyo wako wote. *

19. Namna gani kutaniko lote linaweza kumuabudu Yehova moja kwa moja?

19 Ukumbuke kama kuimba ni sehemu ya maana ya ibada yetu. Ni njia kubwa ya kuonyesha upendo na shukrani yetu kwa Yehova. (Soma Isaya 12:5.) Wakati unaimba kwa shangwe, utatia pia wengine moyo waimbe bila kuogopa. Kwa kweli, wote katika kutaniko, vijana, wazee, na wale wenye kupendezwa na kweli, wanaweza kujiunga na sisi kwenye aina hiyo ya kumuabudu Yehova moja kwa moja. Kwa hiyo, usijizuie kuimba kwa moyo wako wote. Lakini, utii muongozo huu wa mwandikaji mumoja wa zaburi mwenye aliongozwa na roho ya Mungu ili kuimba hivi: “Mwimbieni Yehova!” Ndiyo, uimbe basi kwa sauti yenye shangwe!​—Zab. 96:1.

^ fu. 11 Ili kupata mashauri zaidi juu ya namna ya kufanya sauti zetu zikuwe muzuri zaidi wakati wa kuimba, ona programu ya Mwezi wa 12 ya mwaka wa 2014 ya JW Télédiffusion (kwenye sehemu KUTOKA STUDIO YETU).

^ fu. 18 Ili kutusaidia tukuwe na hamu ya kuimba, kila kipindi cha mukusanyiko kinafunguliwa na sehemu ya muziki wa dakika kumi. Muziki huo uko na kusudi la kutayarisha moyo na akili yetu juu ya programu yenye kufuata. Kwa hiyo, tunatiwa moyo kukaa kwenye viti vyetu wakati muziki unaanza na kusikiliza kwa uangalifu programu hizo za muziki.