Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unamukimbilia Yehova?

Unamukimbilia Yehova?

‘Yehova anaikomboa nafsi ya watumishi wake; wala hakuna yeyote kati ya wale wanaomukimbilia atakayehesabiwa kuwa na hatia.’​—ZAB. 34:22.

NYIMBO: 8, 54

1. Kwa sababu ya zambi, watumishi wengi waaminifu wa Mungu wanajisikia namna gani?

‘MASIKINI mimi!’ (Rom. 7:24) Watumishi wengi waaminifu wa Mungu wamesema maneno kama hayo ya mutume Paulo. Sisi wote tunapatwa na matokeo ya zambi yenye tuliriti, na wakati matendo yetu hayaonyeshe tamaa yetu ya kumupendeza Yehova, tunaweza kuhuzunika. Wakristo fulani wenye wamefanya zambi nzito wameona hata kuwa Mungu hawezi kuwasamehe kabisa.

2. (a) Namna gani Zaburi 34:22 inaonyesha kuwa watumishi wa Mungu hawapaswe kujisikia sana kuwa wenye hatia? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii? (Ona kisanduku “ Somo ao Vifananishwa?”)

2 Hata hivyo, Maandiko yanatuhakikishia kuwa wale wenye kumukimbilia Yehova hawana sababu ya kujisikia sana kuwa wenye hatia ao kujihukumu. (Soma Zaburi 34:22.) Kumukimbilia Yehova kunatia ndani nini? Tunapaswa kukamata hatua gani ili tufaidike na rehema ya Yehova na musamaha wake? Tunaweza kupata majibu kwa maulizo hayo kwa kuzungumuzia mupango wa miji ya makimbilio katika Israeli ya zamani. Kwa kweli, mupango huo uliwekwa wakati wa agano la Sheria, lenye lilibadilishwa kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Lakini, kumbuka kuwa Sheria hiyo ilitoka kwa Yehova. Mupango wa miji ya makimbilio unatusaidia kujua namna Yehova anaona zambi, watenda-zambi, na toba. Kwanza tuzungumuzie miji hiyo ilikuwa na kusudi gani na namna mambo yalikuwa yanatendeka katika miji hiyo.

‘MUJIPE WENYEWE MIJI YA MAKIMBILIO’

3. Namna gani Waisraeli walimutendea mutu mwenye aliua mwenzake kwa makusudi?

3 Yehova aliona kila tendo la kuua mutu kuwa jambo nzito katika Israeli ya zamani. Mutu mwenye angeua mwingine kwa makusudi alipaswa kuuawa na mwanaume wa karibu wa jamaa ya mutu mwenye alikufa. Mutu huyo aliitwa, ‘Mulipiza-kisasi cha damu.’ (Hes. 35:19) Kufanya hivyo, kulilipa damu ya mutu mwenye hana kosa mwenye alikuwa ameuawa. Kumuua bila kukawia mutu huyo kulifanya Inchi ya Ahadi isichafuliwe, kwa sababu Yehova alitoa amri hii: ‘Nanyi musiichafue inchi muliyo ndani yake [kwa kumwanga damu ya mwanadamu]; kwa sababu damu ndiyo inaichafua inchi.’​—Hes. 35:33, 34.

4. Mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia, alitendewa namna gani katika Israeli?

4 Lakini, namna gani Waisraeli walishugulikia mutu mwenye aliua, lakini hakufanya hivyo kwa makusudi? Hata kama hakufanya hivyo kwa makusudi, mutu mwenye aliua mwenzake alikuwa na kosa la kumwanga damu yenye haina kosa. (Mwa. 9:5) Hata hivyo, kwa rehema, aliruhusiwa kukimbia kutoka kwa mutu mwenye kulipiza kisasi cha damu na kuenda katika muji moja kati ya miji sita ya makimbilio. Angepata ulinzi huko. Mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia alipaswa kubakia katika muji wa makimbilio mupaka kifo cha kuhani mukubwa.​— Hes. 35:15, 28.

5. Namna gani mupango wa miji ya makimbilio unatusaidia kumujua Yehova muzuri zaidi?

5 Mupango wa kuchagua miji ya makimbilio haukuletwa na mwanadamu. Yehova yeye mwenyewe alimuamuru Yoshua hivi: “Sema na wana wa Israeli, uwaambie, ‘Mujipe wenyewe miji ya makimbilio.’” Miji hiyo ilipewa “hali ya utakatifu.” (Yos. 20:1, 2, 7, 8) Kwa sababu ni Yehova yeye mwenyewe ndiye aliomba miji hiyo ichaguliwe ili kutumiwa kwa njia ya pekee, tunaweza kujiuliza hivi: Namna gani mupango huo unatusaidia kuelewa muzuri kabisa rehema ya Yehova? Na unatufundisha nini juu ya namna tunaweza kumukimbilia leo?

“NAYE . . . ATASEMA MANENO YAKE MASIKIONI MWA WANAUME WAZEE”

6, 7. (a) Wazee walikuwa na daraka gani katika kuhukumu mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia? Eleza. (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.) (b) Sababu gani mukimbizi alipaswa kuzungumuza na wazee?

6 Kisha kumuua mwenzake bila kukusudia, kwanza mukimbizi alipaswa ‘kusema maneno yake masikioni mwa wanaume wazee’ kwenye mulango wa muji wa makimbilio ambamo alikimbilia. Alipaswa kukaribishwa muzuri. (Yos. 20:4) Kisha wakati fulani, alitumwa kwenye wazee wa muji ambamo mauaji yalitendeka, na wazee hao walipaswa kuhukumu jambo hilo. (Soma Hesabu 35:24, 25.) Mukimbizi angeweza kurudia katika muji wa makimbilio kisha tu wazee kuonyesha kuwa hakuua kwa makusudi.

7 Sababu gani mukimbizi alipaswa kuzungumuza na wazee? Kwa sababu walipaswa kufanya taifa la Israeli liendelee kuwa safi na kumusaidia mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia afaidike na rehema ya Yehova. Mutu mumoja mwenye elimu ya Biblia aliandika kuwa ikiwa mukimbizi hangeenda kuzungumuza na wazee, “maisha yake yalikuwa katika hatari.” Aliongezea hivi: “Damu yake ilikuwa kwenye kichwa chake mwenyewe, kwa sababu hakutumia mipango ya usalama yenye Mungu alikuwa ameweka kwa ajili yake.” Mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia angesaidiwa, lakini alipaswa kutafuta musaada huo na kuukubali. Ikiwa hangetafuta kimbilio katika muji moja kati ya miji yenye Yehova alichagua, mutu wa jamaa wa karibu wa mutu mwenye alikufa aliruhusiwa kumuua.

8, 9. Sababu gani Mukristo mwenye amefanya zambi nzito anapaswa kutafuta musaada wa wazee?

8 Leo, Mukristo mwenye alifanya zambi nzito anapaswa kutafuta musaada kwa wazee wa kutaniko ili wamusaidie. Sababu gani kufanya hivyo ni jambo la maana sana? Kwanza, daraka la wazee la kushugulikia zambi nzito, ni mupango kutoka kwa Yehova, kama vile Neno lake linaonyesha. (Yak. 5:14-16) Pili, mupango huo unamutia nguvu mutenda-zambi abakie katika ulinzi wa Mungu na aepuke tabia ya kufanya zambi. (Gal. 6:1; Ebr. 12:11) Tatu, wazee wamepewa mugawo na mazoezi ya kusaidia watenda-zambi wenye kutubu, kuwasaidia kupunguza huzuni yao na kuwasaidia wasiendelee kujihukumu. Yehova anaita wazee hao kuwa ‘mahali pa kujificha kutokana na zoruba ya mvua.’ (Isa. 32:1, 2) Kwa kweli mupango huo unaonyesha kabisa rehema ya Mungu.

9 Watumishi wengi wa Mungu wamepata kitulizo kwa sababu wametafuta na kupata musaada wa wazee. Kwa mufano, ndugu mumoja mwenye kuitwa Daniel, alifanya zambi nzito, lakini kwa miezi fulani alisita kuzungumuza na wazee. Anasema hivi: “Kisha kupita wakati mwingi, niliwaza kuwa wazee hawangeweza tena kufanya jambo lolote juu yangu. Lakini, sikuzote niliendelea kukumbuka, na kungojea matokeo ya matendo yangu. Na wakati nilikuwa ninasali kwa Yehova, niliona kuwa mbele ya kusema kila jambo nilipaswa kuomba musamaha kwa sababu ya zambi yenye nilikuwa nimefanya.” Mwishowe, Daniel alitafuta musaada wa wazee. Wakati anakumbuka, anasema hivi: “Kusema kweli, niliogopa kuzungumuza nao. Lakini kisha hapo, nilijisikia kuwa mutu fulani alikuwa ameondoa muzigo muzito kwenye mabega yangu. Sasa, ninajisikia kuwa ninaweza kusali kwa Yehova bila kitu chochote cha kunizuia.” Leo, Daniel iko na zamiri safi, na hivi karibuni aliwekwa kuwa mutumishi wa huduma.

‘NAYE ATAKIMBILIA MOJA LA MIJI HIYO’

10. Mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia alipaswa kukamata hatua gani ili aonyeshwe rehema?

10 Mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia alipaswa kutenda ili aonyeshwe rehema. Alipaswa kukimbilia katika muji wa makimbilio wenye ulikuwa karibu zaidi. (Soma Yoshua 20:4.) Kwa kweli, mukimbizi hangekataa kufanya hivyo; ili aendelee kuishi alipaswa kujikaza sana ili afike katika muji huo na kubakia ndani! Alipaswa kujinyima kabisa ili afanye hivyo. Alipaswa kuacha kazi yake ya kimwili, nyumba yake ya muzuri, na uhuru wake wa kufanya safari, na kubakia huko mupaka kifo cha kuhani mukubwa. * (Hes. 35:25) Lakini kuacha mambo hayo yote kungeleta matokeo ya muzuri. Ikiwa mukimbizi angeondoka katika muji huo, hilo lingeonyesha kuwa hauzunikie damu yenye alikuwa amemwanga, na maisha yake mwenyewe yangekuwa katika hatari.

11. Mukristo mwenye kutubu anapaswa kufanya nini ili kuonyesha kuwa hazarau rehema ya Mungu?

11 Ili kufaidika na rehema ya Mungu, mutenda-zambi mwenye kutubu anapaswa kutenda pia. Tunapaswa kuacha kabisa tabia ya kufanya zambi; hatupaswe kukimbia tu zambi nzito lakini pia zambi ndogo-ndogo zenye kutuongoza mara nyingi kwenye zambi nzito. Mutume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu ili kueleza matendo ya Wakristo wenye walitubu katika Korintho. Aliandika hivi: ‘Kule kuhuzunishwa kwenu kwa njia ya kimungu, kulitokeza katika ninyi hali ya bidii kubwa kama nini, ndiyo, kujiondolea wenyewe hatia, ndiyo, gazabu [hasira], ndiyo, woga, ndiyo, kutamani, ndiyo, bidii, ndiyo, kurekebisha kosa!’ (2 Kor. 7:10, 11) Wakati tunajikaza kuacha kabisa tabia ya kufanya zambi, hilo linaonyesha Yehova kuwa tunahuzunika juu ya jambo lenye tulifanya, na hatuzarau rehema yake.

12. Mukristo anaweza kuacha nini ili aendelee kufaidika na rehema ya Mungu?

12 Mukristo anapaswa kuacha nini ili aendelee kufaidika na rehema ya Mungu? Anapaswa kuwa tayari kuacha kabisa mambo yenye anapenda ikiwa mambo hayo yanaweza kumuchochea kufanya zambi. (Mt. 18:8, 9) Ikiwa marafiki fulani wanakuchochea ufanye mambo yenye kumuchukiza Yehova, utaacha kufanya urafiki pamoja nao? Ikiwa ni vigumu kwako kunywa pombe kwa kiasi, uko tayari kuepuka hali zenye zinaweza kukuchochea kunywa kupita kiasi? Ikiwa unapiganisha tamaa ya mubaya ya mambo ya uasherati, unaepuka filme, adresi za Internete, ao mambo mengine yoyote yenye yanaweza kuchochea mawazo machafu? Ukumbuke kuwa, mambo yote yenye tunajinyima ili tubakie washikamanifu kwa Yehova haiko ya bure. Hakuna jambo lenye kuumiza zaidi kuliko kujisikia kuwa hatukubaliwe na Yehova. Na hakuna jambo lenye kufurahisha zaidi kuliko kujisikia kuwa tuko katika ‘fazili [zake] zenye upendo mupaka wakati usio na kipimo.’​—Isa. 54:7, 8.

‘ITAKUWA KWENU MAKIMBILIO’

13. Sababu gani mukimbizi angejisikia kuwa salama, na mwenye furaha katika muji wa makimbilio? Eleza.

13 Kisha kufika katika muji wa makimbilio, mukimbizi alipata usalama. Juu ya miji hiyo, Yehova alisema hivi: ‘Itakuwa kwenu makimbilio.’ (Yos. 20:2, 3) Yehova hakuomba mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia ahukumiwe mara ya pili kwa ajili ya kosa lilelile; na hakuruhusu mutu mwenye kulipiza kisasi cha damu aingie katika muji ili kuua mukimbizi huyo. Kwa hiyo, mukimbizi hakupaswa kuogopa hata kidogo kuwa atauawa. Wakati alikuwa katika muji, alikuwa salama chini ya ulinzi wa Yehova. Muji huo haukukuwa gereza kwa mukimbizi. Katika muji huo, angeweza kufanya kazi, kusaidia wengine, na kumutumikia Yehova katika amani. Ndiyo, angeweza kuwa na maisha ya muzuri na yenye furaha!

Ukuwe hakika juu ya musamaha wa Yehova (Picha hii inapatana na fungu la 14-16)

14. Mukristo mwenye ametubu anaweza kuwa hakika juu ya jambo gani?

14 Watumishi fulani wa Mungu wenye wamefanya zambi nzito lakini wametubu wamejisikia kuwa wako “katika gereza” kwa kujihukumu, hata kujisikia kuwa Yehova ataendelea kuwaona kuwa wamechafuliwa na zambi nzito. Ikiwa unajisikia hivyo, tafazali ukuwe hakika kuwa wakati Yehova anakusamehe, unaweza kujisikia salama katika rehema yake! Daniel, mwenye tulizungumuzia hapo mbele, alijionea ukweli wa jambo hilo. Kisha wazee kumurekebisha na kumusaidia akuwe na zamiri safi, alisema hivi: “Nilijisikia kuwa ninaweza kupumua tena. Kisha mambo kushugulikiwa muzuri, zamiri yangu haikukuwa tena na sababu ya kunihukumu. Wakati zambi inasamehewa, inasamehewa kabisa. Kama vile Yehova alisema, anaondoa mizigo yako na anaiweka mbali na wewe. Hautaiona tena hata kidogo.” Kisha kuwa katika muji wa makimbilio, mukimbizi hangeogopa tena kuwa mutu mwenye kulipiza kisasi cha damu angekuja kumuua. Vilevile, kisha Yehova kusamehe zambi yetu, hatupaswe kuogopa kuwa ataikumbuka tena ao kutuhukumu juu ya zambi hiyo.​—Soma Zaburi 103:8-12.

15, 16. Kwa sababu Yesu ni Mukombozi na Kuhani Mukubwa, namna gani hilo linakusaidia utumainie rehema ya Mungu?

15 Kwa kweli, tuko na sababu kubwa ya kutumainia rehema ya Yehova kuliko Waisraeli. Kisha mutume Paulo kuonyesha huzuni yake ya kushindwa kutii Yehova kwa ukamilifu, alisema hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Rom. 7:25) Ndiyo, hata kama alikuwa anapiganisha tamaa za zambi na kusumbuliwa na matendo yake ya zamani yenye alikuwa ametubu, Paulo alitumainia musamaha wa Mungu kupitia Yesu. Yesu, Mukombozi wetu anasafisha zamiri zetu na kutupatia amani ya moyoni. (Ebr. 9:13, 14) Kwa sababu yeye ni Kuhani Mukubwa, ‘anaweza pia kuwaokoa kwa ukamili wale wanaomukaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.’ (Ebr. 7:24, 25) Ikiwa daraka la kuhani mukubwa lilihakikishia Waisraeli kuwa zambi zao zingesamehewa, daraka la Kuhani wetu Mukubwa, Yesu, linapaswa kutuhakikishia hata zaidi kuwa ‘tutapokea rehema na kupata fazili zisizostahiliwa kuwa musaada kwa wakati unaofaa.’​—Ebr. 4:15, 16.

16 Kwa hiyo, ili umukimbilie Yehova, unapaswa kuwa na imani katika zabihu ya Yesu. Usikubali tu kuwa faida ya zabihu ya ukombozi inasaidia watu wengi sana. Lakini, ukuwe na imani kuwa zabihu ya ukombozi inakuletea faida wewe mwenyewe. (Gal. 2:20, 21) Ukuwe na imani kuwa zabihu ya ukombozi ni musingi wa musamaha wa zambi zako. Ukuwe na imani kuwa zabihu ya ukombozi inakutolea tumaini la kuishi milele. Zabihu ya Yesu ni zawadi yenye Yehova anakutolea.

17. Sababu gani unapenda kumukimbilia Yehova?

17 Miji ya makimbilio inaonyesha rehema ya Yehova. Kupitia mupango huo, Mungu hakazie tu utakatifu wa uzima lakini pia anaonyesha namna wazee wanatusaidia, kutubu kikweli maana yake nini, na sababu gani tunaweza kuwa hakika kuwa Yehova anasamehe kabisa. Unamukimbilia Yehova? Hakuna nafasi ingine kwenye tunaweza kupata usalama! (Zab. 91:1, 2) Katika habari yenye kufuata, tutaona namna gani miji ya makimbilio inaweza kutusaidia kuiga mufano mukubwa zaidi wa Yehova wa kuonyesha haki na rehema.

^ fu. 10 Kulingana na vitabu fulani vya Wayahudi, familia ya karibu ya mutu mwenye aliua mwenzake bila kukusudia ilikuwa inamufuata katika muji wa makimbilio.