Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mutu Mwenye Kuonyesha “Ukarimu Atabarikiwa”

Mutu Mwenye Kuonyesha “Ukarimu Atabarikiwa”

TANGU zamani, kutoa zabihu kumekuwa sehemu ya maana sana ya ibada ya kweli. Waisraeli walitoa zabihu za wanyama, na Wakristo wamejulikana siku zote kuwa wenye kutoa ‘zabihu ya sifa.’ Lakini, kuko zabihu zingine zenye kumupendeza Mungu. (Ebr. 13:15, 16) Zabihu hizo zinaleta furaha na baraka, kama vile mifano yenye kufuata inaonyesha.

Hana, mutumishi mwaminifu wa zamani wa Mungu, alipenda sana kuwa na mutoto mwanaume lakini hakukuwa na uwezo wa kuzaa watoto. Katika sala, alifanya naziri kwa Yehova kwamba ikiwa anazaa mutoto mwanaume, ‘atamutoa kwa Yehova siku zote za maisha yake.’ (1 Sam. 1:10, 11) Kisha wakati fulani, Hana akapata mimba, na akazaa mutoto mwanaume na kumupatia jina la Samweli. Kisha Samweli kuachishwa kunyonya, Hana alimupeleka kwenye tabenakulo, kama vile tu alikuwa ametoa naziri. Yehova alimubariki Hana kwa sababu ya roho yake ya kujitoa. Alipata pendeleo la kuzaa watoto wengine tano, na Samweli akakuwa nabii na muandikaji wa Biblia.​—1 Sam. 2:21.

Kama Hana na Samweli, leo Wakristo wako na pendeleo la kutumia maisha yao katika utumishi mutakatifu kwa Muumbaji wao. Yesu aliahidi kuwa tutabarikiwa sana kwa sababu ya kila jambo lenye tunajinyima ili kumuabudu Yehova.​—Mk. 10:28-30.

Wakati wa mitume, mwanamuke mumoja Mukristo mwenye kuitwa Dorkasi alijulikana sana kwa sababu ya “matendo mema na zawadi za rehema,” ni kusema, zabihu zenye alitoa ili kusaidia wengine. Hata hivyo, jambo la kuhuzunisha ni kwamba, “alishikwa na ugonjwa akafa,” hilo lilihuzunisha sana kutaniko. Wakati wanafunzi walisikia kwamba Petro alikuwa katika eneo hilo, walimuomba akuje bila kukawia. Wazia furaha yenye walikuwa nayo wakati Petro alimufufua Dorkasi; huo ndio ulikuwa ufufuo wa kwanza wenye ulifanywa na mutume wenye kuandikwa katika Biblia! (Mdo. 9:36-41) Mungu alikuwa hajasahau zabihu za Dorkasi. (Ebr. 6:10) Habari juu ya ukarimu wake imeandikwa katika Neno la Mungu ili kutuonyesha mufano wa muzuri wenye tunaweza kuiga.

Vilevile mutume Paulo alituachia mufano wa muzuri sana kwa kutumia wakati wake kwa ukarimu na kuhangaikia sana watu. Wakati aliandikia ndugu zake Wakristo katika Korintho, Paulo alisema hivi: “Kwa upande wangu mimi nitatumia kwa furaha zaidi na kutumiwa kabisa kwa ajili ya nafsi zenu.” (2 Kor. 12:15) Mambo yenye Paulo alijionea yalimufundisha kuwa kujitoa kwa ajili ya wengine kunaletea mutu furaha, lakini pia jambo la maana zaidi, kunaleta baraka za Yehova na kukubaliwa naye.​—Mdo. 20:24, 35.

Ni wazi kwamba, Yehova anapendezwa wakati tunatumia wakati na nguvu yetu ili kuendeleza faida za Ufalme na kusaidia Wakristo wenzetu. Lakini kuko njia zingine zenye tunaweza kutumia ili kutegemeza kazi ya kuhubiri Ufalme? Ndiyo! Zaidi ya matendo yetu ya upendo, tunaweza kumuheshimia Mungu kwa kutoa michango ya kujipendea. Michango hiyo inatumiwa ili kuendeleza kazi ya kuhubiri katika dunia yote, kazi hiyo inatia ndani kutegemeza wamisionere na watumishi wengine wa wakati wote. Zaidi ya hilo, kutayarisha na kutafsiri vichapo na video, kutoa misaada wakati wa misiba, na ujenzi wa Majumba ya Ufalme; kazi hizo zote zinategemezwa na michango yetu ya kujipendea. Tunaweza kuwa hakika kuwa mutu mwenye kuonyesha “ukarimu atabarikiwa.” Zaidi ya hilo, wakati tunamutolea Yehova vitu vyetu vya maana, tunamuheshimia.​—Met. 3:9; 22:9.

Telefone: 0998189791 ao 0815551000

“Association Les Témoins de Jéhovah” no 75, 13ème Rue, Industriel, Limete-KINSHASA, République Démocratique du Congo.