Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Uige Haki na Rehema ya Yehova

Uige Haki na Rehema ya Yehova

‘Mufanye hukumu kwa haki ya kweli; na mutendeane kwa fazili zenye upendo na rehema.’​—ZEK. 7:9.

NYIMBO: 125, 88

1, 2. (a) Namna gani Yesu aliona Sheria ya Mungu? (b) Namna gani waandishi na Mafarisayo walitumia mubaya Sheria?

YESU alipenda Sheria ya Musa. Na alikuwa na sababu ya kufanya hivyo! Sheria hiyo ilitoka kwa Mutu wa maana sana katika maisha yake, ni kusema, Yehova, Baba yake. Yesu alipenda sana sheria ya Mungu; hilo lilitabiriwa katika Zaburi 40:8, inasema hivi: ‘Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako iko ndani yangu.’ Kwa maneno na matendo, Yesu alihakikisha kuwa Sheria ya Mungu ni kamilifu, yenye faida, na kwamba kila jambo lenye kuandikwa katika Sheria hiyo litatimia.​—Mt. 5:17-19.

2 Kwa hiyo, Yesu alipaswa kuhuzunika sana wakati aliona namna waandishi na Mafarisayo wanatumia mubaya Sheria ya Baba yake! Walishikilia sana mambo madogo-madogo fulani ya Sheria, ndiyo sababu Yesu aliwaambia hivi: ‘Ninyi munatoa sehemu ya kumi ya munanaa na dili na bizari.’ Kwa hiyo, walikuwa na tatizo gani? Aliongezea hivi: “Lakini mumepuuza [mumezarau] mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.” (Mt. 23:23) Tofauti na Mafarisayo hao wenye walijiona kuwa waadilifu, Yesu alielewa mambo makubwa yenye kukaziwa katika Sheria hiyo, ni kusema, sifa za Mungu zenye kuonekana katika kila amri.

3. Tutazungumuzia nini katika habari hii?

3 Sisi Wakristo hatuko chini ya agano la Sheria. (Rom. 7:6) Hata hivyo, Yehova aliweka Sheria hiyo katika Neno lake, Biblia kwa ajili yetu. Haiko ili tukazie mambo madogo-madogo ya Sheria hiyo, lakini ili tutambue na kutumikisha, “mambo mazito zaidi,” ni kusema, kanuni za maana zenye kutegemeza amri za Sheria hiyo. Kwa mufano, ni kanuni gani zenye tunaweza kupata katika mupango wa miji ya makimbilio? Katika habari yenye kutangulia tuliona mambo yenye tunajifunza kutokana na hatua zenye mukimbizi alikamata. Lakini, miji ya makimbilio inatufundisha pia juu ya Yehova na namna tunaweza kuiga sifa zake. Kwa hiyo, katika habari hii tutajibia maulizo tatu: Namna gani miji ya makimbilio inaonyesha rehema ya Yehova? Miji hiyo inatufundisha nini juu ya namna anaona uzima? Namna gani inaonyesha haki yake kamilifu? Katika kila hali, tafuta namna unaweza kumuiga Baba yako wa mbinguni.​—Soma Waefeso 5:1.

‘MIJI ITAKAYOWAFAA NINYI’ ​—HILO LILIONYESHA REHEMA

4, 5. (a) Ni nini ilifanywa ili ikuwe mwepesi kufika katika miji ya makimbilio, na sababu gani? (b) Hilo linatufundisha nini juu ya Yehova?

4 Ilikuwa mwepesi kufika katika miji hiyo sita ya makimbilio. Yehova aliamuru Waisraeli wachague miji hiyo kwenye ngambo zote za Muto Yordani. Sababu gani? Ili mukimbizi yeyote aweze kupata kimbilio haraka na mahali penye kufaa. (Hes. 35:11-14) Barabara za kuenda katika miji ya makimbilio zilitengenezwa kila mara ili ziendelee kuwa katika hali ya muzuri. (Kum. 19:3) Kulingana na vitabu vya Wayahudi alama fulani zilikuwa zinawekwa katika njia ili kuongoza mutu mwenye kukimbilia katika miji hiyo. Kwa sababu kulikuwa miji ya makimbilio, mutu mwenye aliua bila kukusudia, hakulazimika kukimbilia katika inchi ingine kwenye angechochewa kuabudu miungu ya uwongo.

5 Fikiria jambo hili: Yehova mwenye alikuwa ametoa amri kuwa mutu mwenye kuua kwa makusudi alipaswa kuuawa, alihakikisha kuwa mutu mwenye aliua mutu mwingine bila kukusudia anapewa nafasi ya kuonyeshwa huruma na kulindwa! Mutu mumoja aliandika hivi juu ya jambo hilo: “Mambo yote yalipangwa muzuri sana, kwa njia ya mwepesi sana kadiri iliwezekana. Hilo lilionyesha neema ya Mungu.” Yehova haiko muamuzi mwenye hana huruma mwenye anatamani sana kupatia watumishi wake malipizi. Lakini, ni “tajiri katika rehema.”​—Efe. 2:4.

6. Namna gani mawazo ya Mafarisayo yalikuwa tofauti na rehema ya Mungu?

6 Lakini, Mafarisayo hawakuwa tayari kuonyesha rehema. Kwa mufano, kulingana na vitabu vya Wayahudi, ikiwa mutu anafanya kosa ileile zaidi ya mara tatu, hawakuwa tayari kumusamehe. Yesu alionyesha wazi mawazo yao juu ya wakosaji kwa kueleza mufano wa Mufarisayo mwenye alisali hivi: ‘Ee Mungu, ninakushukuru ya kuwa mimi si kama wale watu wengine, wanyanganyi, wasio waadilifu, wazinzi [wazinifu], ao hata kama mukusanya-kodi huyu,’ mukusanya-kodi mwenye alikuwa anasali kwa unyenyekevu ili Mungu amuonyeshe rehema. Sababu gani Mafarisayo hawakuwa tayari kuonyesha rehema? Biblia inasema kuwa “waliona [watu] wengine kama si kitu.”​—Lu. 18:9-14.

Unafanya wengine wajisikie huru kukuomba musamaha? Ukuwe mwepesi kukaribiwa (Picha hii inapatana na fungu la 4-8)

7, 8. (a) Wakati mutu fulani anakukosea, namna gani unaweza kumuiga Yehova? (b) Sababu gani tunapaswa kuwa wanyenyekevu ili kusamehe wengine?

7 Uige Yehova, hapana Mafarisayo. Uonyeshe huruma. (Soma Wakolosai 3:13.) Njia moja ya kufanya hivyo ni kufanya wengine wajisikie huru kukuomba musamaha. (Lu. 17:3, 4) Ujiulize hivi: ‘Ninasamehe watu wenye wamenikosea hata kama wamefanya hivyo mara nyingi? Niko tayari kufanya amani na mutu mwenye amenikosea ao mwenye amenikwaza?’

8 Kusamehe wengine kunaonyesha kuwa tuko wanyenyekevu. Mafarisayo walishindwa kusamehe kwa sababu waliona wengine kuwa wa hali ya chini. Lakini, sisi Wakristo, tunapaswa kuwa wanyenyekevu kwa ‘kuwaona wengine kuwa ni bora kuliko’ sisi na kuwa tayari kuwasamehe. (Flp. 2:3) Utamuiga Yehova na kujikaza kuwa munyenyekevu? Ikiwa tuko wanyenyekevu, itakuwa mwepesi kwa wengine kutuomba musamaha na itakuwa mwepesi kwetu kusamehe wengine. Ukuwe tayari kuonyesha rehema na usikuwe mwepesi kukasirika.​—Mhu. 7:8, 9.

UHESHIMIE UZIMA, NA ‘HATIA YOYOTE YA DAMU ISIKUWE JUU YAKO’

9. Namna gani Yehova alikazia katika akili ya Waisraeli utakatifu wa uzima wa mwanadamu?

9 Kusudi kubwa la miji ya makimbilio lilikuwa kulinda Waisraeli juu ya hatia ao deni la damu. (Kum. 19:10) Yehova anapenda uzima na anachukia ‘mikono [ya muuaji] inayomwanga damu isiyo na hatia.’ (Met. 6:16, 17) Kwa sababu yeye ni Mungu mwenye haki na mutakatifu, hangeachilia hata mutu mwenye aliua mwengine bila kukusudia. Ni kweli kwamba mutu mwenye aliua mwengine bila kukusudia alionyeshwa rehema. Hata hivyo, alipaswa kuendea wazee, na ikiwa alionwa kuwa aliua bila kukusudia, alipaswa kubakia katika muji wa makimbilio mupaka kifo cha kuhani mukubwa. Hilo linamaanisha kuwa pengine angepitisha maisha yake yote katika muji huo. Matokeo hayo makubwa yalikumbusha Waisraeli wote utakatifu wa uzima wa mwanadamu. Ili kuheshimia ule mwenye aliwapatia uzima, walipaswa kuepuka jambo lolote lenye lingetia uzima wa mutu mwengine katika hatari.

10. Kulingana na Yesu, namna gani waandishi na Mafarisayo walionyesha kuwa hawakuhangaikia uzima?

10 Tofauti na Yehova, waandishi na Mafarisayo walionyesha kuwa hawaheshimie uzima. Namna gani? Yesu aliwaambia hivi: ‘Muliuondoa ufunguo wa ujuzi. Ninyi wenyewe hamukuingia, na wale wanaoingia muliwazuia!’ (Lu. 11:52) Wao ndio walipaswa kufunulia wengine maana ya Neno la Mungu na kuwasaidia watembee katika barabara yenye kuongoza kwenye uzima wa milele. Lakini, waliongoza watu mbali na ‘Wakili Mukubwa wa uzima,’ Yesu, na kuwaongoza katika njia yenye kuongoza kwenye uharibifu wa milele. (Mdo. 3:15) Kwa sababu waandishi na Mafarisayo walikuwa na kiburi na walijipenda wenyewe, hawakuhangaikia uzima wa wanadamu wenzao. Walikuwa wabaya na hawakukuwa na rehema hata kidogo!

11. (a) Namna gani mutume Paulo alionyesha kuwa aliona uzima namna Mungu anauona? (b) Ni nini itatusaidia kuwa na mawazo kama ya mutume Paulo juu ya kazi ya kuhubiri?

11 Namna gani tunaweza kuepuka kuwa na mawazo kama ile ya waandishi na Mafarisayo na kumuiga Yehova? Tunapaswa kuheshimia uzima na kuuona kuwa zawadi ya maana sana. Mutume Paulo alifanya hivyo kwa kutoa ushahidi kwa ukamili. Kwa hiyo, alisema hivi: “Mimi ni safi kutokana na damu ya watu wote.” (Soma Matendo 20:26, 27.) Hata hivyo, Paulo hakuhubiri kwa sababu ya kuepuka kuwa na deni la damu ao kwa sababu alipaswa kufanya hivyo. Lakini alipenda watu na aliona kuwa uzima wao ni wa maana. (1 Kor. 9:19-23) Sisi pia tunapaswa kujikaza kuona uzima namna Mungu anauona. Yehova ‘anataka wote wafikie toba.’ (2 Pet. 3:9) Halafu wewe? Unaweza kutambua kuwa kukomalisha sifa ya rehema katika moyo wako kutakuchochea kuhubiri kwa bidii na utapata furaha kubwa kadiri unaendelea kufanya hivyo.

12. Sababu gani watu wa Mungu wanaona usalama kuwa ni jambo la maana?

12 Pia tunaweza kuona uzima namna Yehova anauona kwa kuhangaikia usalama wetu. Tunapaswa kujikaza kutembeza na kutumika kazi katika hali ya usalama, hata wakati tunajenga, tunatunza, ao tunaenda kwenye nafasi zetu za kufanyia ibada. Tusione kuwa kutimiza mambo fulani, feza, ao kumaliza kazi fulani mbele ya wakati kuwa mambo ya maana kuliko usalama na afya yetu. Mungu wetu mwenye haki anafanya sikuzote mambo yenye kuwa sawa na yenye kufaa. Tunapenda kumuiga. Zaidi sana wazee wanapaswa kujikaza kuhangaikia usalama wao na wa wale wenye kutumika pamoja nao. (Met. 22:3) Kwa hiyo, ikiwa muzee anakukumbusha kanuni na maagizo fulani juu ya usalama, usikilize shauri lake. (Gal. 6:1) Uone uzima namna Yehova anauona, na “hatia yoyote ya damu isikuwe juu yako.”

‘HUKUMU . . . KULINGANA NA HUKUMU HIZI’

13, 14. Wazee Waisraeli walipaswa kufanya nini ili kuonyesha haki ya Yehova?

13 Yehova aliomba wazee Waisraeli waige kanuni yake ya juu ya haki. Kwanza wazee walipaswa kuchunguza mambo kwa uangalifu. Pia, mbele ya kuamua ikiwa ataonyeshwa rehema ao hapana, wazee walipaswa kufikiria kwa uzito nia, mwelekeo, na mwenendo wa zamani wa muuaji. Ili kuiga haki ya Mungu, walipaswa kutafuta kujua ikiwa mukimbizi alitenda “kwa sababu ya chuki” na ‘ikiwa alimuvizia.’ (Soma Hesabu 35:20-24.) Ikiwa iliomba kuwe ushuhuda, kulipaswa kuwa mashahidi wawili ao zaidi ili kuhakikisha kuwa aliua kwa makusudi.​—Hes. 35:30.

14 Kwa hiyo, kisha kuchunguza mambo kwa uangalifu, wazee walipaswa kuchunguza pia mutu huyo, hapana tu tendo hilo. Walikuwa na lazima ya utambuzi, ni kusema, uwezo wa kuona mambo yenye hayaonekane waziwazi na kuelewa muzuri mambo. Zaidi ya yote, walikuwa na lazima ya roho takatifu ya Yehova, yenye ingewasaidia kutenda kwa utambuzi, rehema, na haki.​—Kut. 34:6, 7.

15. Namna gani mawazo ya Yesu yalikuwa tofauti na ya Mafarisayo juu ya watenda-zambi?

15 Mafarisayo walikazia zaidi mambo yenye mutenda-zambi alikuwa amefanya kuliko kuangalia ikiwa mutenda zambi alikuwa mutu wa namna gani. Wakati Mafarisayo walimuona Yesu anakula chakula katika nyumba ya Mathayo, waliuliza wanafunzi wake hivi: ‘Kwa nini mwalimu wenu anakula pamoja na wakusanya-kodi na watenda-zambi?’ Yesu aliwajibia hivi: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu [munganga], bali wenye kuugua [kugonjwa] ndio wanaomuhitaji. Muende, basi, mukajifunze maana ya jambo hili, ‘ninataka rehema, wala si zabihu.’ Kwa maana nilikuja kuwaita, si watu waadilifu, bali watenda-zambi.” (Mt. 9:9-13) Yesu alikuwa anatetea watu wenye kufanya makosa mazito? Hapana kabisa. Kwa kweli, ujumbe mukubwa wa Yesu ulitia ndani kuomba watenda-zambi watubu. (Mt. 4:17) Hata hivyo, Yesu alitambua kuwa wamoja kati ya ‘wakusanya-kodi wengi na watenda-zambi’ walipenda kubadilika. Walikuwa katika nyumba ya Mathayo haiko ili kula tu chakula. Lakini, wengi wao walikuwa wanamufuata Yesu. (Mk. 2:15) Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, Mafarisayo wengi walishindwa kuona mambo yenye Yesu aliona katika watu hao. Tofauti na Mungu mwenye haki na rehema mwenye walikuwa wanasema kuwa wanamuabudu, Mafarisayo waliwaita wanadamu wenzao kuwa watenda-zambi na kuwahukumu kuwa hawangeweza kubadilika.

16. Halmashauri ya hukumu inapaswa kujikaza kutambua jambo gani?

16 Leo, wazee wanapaswa kuhakikisha kuwa wanamuiga Yehova, mwenye ‘kupenda haki.’ (Zab. 37:28) Kwanza wanapaswa “kupeleleza na kuuliza habari kabisa” ili kuhakikisha kuwa mutu amefanya zambi kabisa. Ikiwa mutu amefanya zambi, watashugulikia jambo hilo kulingana na muongozo wa Maandiko. (Kum. 13:12-14) Wakati wako katika halmashauri ya hukumu, wanapaswa kuchunguza kwa uangalifu ikiwa Mukristo mwenye alifanya zambi nzito anatubu. Sikuzote, haionekane waziwazi ikiwa mutu anatubu ao hapana. Kutubu kunatia ndani mawazo ya mutu, mwelekeo wake, na hali ya moyo wake. (Ufu. 3:3) Mutenda-zambi anapaswa kutubu ili aonyeshwe rehema. *

17, 18. Namna gani wazee wanaweza kutambua toba ya kweli? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

17 Yehova na Yesu wanaweza kusoma katika mioyo ya watu, lakini wazee hawawezi kufanya hivyo. Kwa hiyo, ikiwa wewe ni muzee, namna gani unaweza kufikia kutambua ikiwa mutu anatubu kutoka moyoni? Kwanza, usali kwa Yehova na kumuomba hekima na utambuzi. (1 Fal. 3:9) Pili, uchunguze Neno la Mungu na vichapo vya mutumwa mwaminifu ili kukusaidia kutofautisha “huzuni ya ulimwengu” na “kuhuzunishwa . . . kwa njia ya kimungu,” ni kusema, toba ya kweli. (2 Kor. 7:10, 11) Uchunguze namna Maandiko yanazungumuzia watu wenye kutubu na watu wenye kukosa kutubu. Namna gani Biblia inaeleza namna walijisikia, mawazo yao, na mwenendo wao?

18 Mwishowe, ujikaze kufikiria hali yote ya mutu. Fikiria maisha ya mutenda-zambi, nia yake na mipaka yake. Kuhusu Yesu, kichwa cha kutaniko la Kikristo, Biblia ilitabiri hivi: “Hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.” (Isa. 11:3, 4) Nyinyi wazee muko wachungaji wenye kuwa chini ya uongozi wa Yesu, na atawasaidia kuhukumu kama vile yeye anahukumu. (Mt. 18:18-20) Tuko wenye shukrani sana kwa sababu tuko na wazee wenye wanajikaza sana kufanya hivyo. Tunapendezwa na bidii nyingi yenye wanafanya ili kuonyesha rehema na haki katika makutaniko!

19. Miji ya makimbilio imekufundisha mambo gani yenye umepanga kutumikisha?

19 Sheria ya Musa ilionyesha “picha ya ujuzi na ya ile kweli” juu ya Yehova na kanuni zake za uadilifu. (Rom. 2:20) Kwa mufano, miji ya makimbilio inafundisha wazee kufanya “hukumu kwa haki ya kweli,” na inatufundisha sisi wote namna ya ‘kutendeana kwa fazili zenye upendo na rehema.’ (Zek. 7:9) Hatuko tena chini ya Sheria. Lakini, Yehova hajabadilika, anaendelea kuona sifa yake ya haki na rehema kuwa za maana kwake. Tuko na pendeleo kubwa sana la kuabudu Mungu mwenye alituumba kwa mufano wake, mwenye tunaweza kuiga sifa zake, na mwenye tunaweza kukimbilia!

^ fu. 16 Ona “Maulizo ya Wasomaji Wetu” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 9, 2006, ukurasa wa 30.