Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Usiache Jambo Lolote Likuzuie Kupata Zawadi

Usiache Jambo Lolote Likuzuie Kupata Zawadi

‘Musiache mutu yeyote awanyanganye tuzo [zawadi].’​—KOL. 2:18.

NYIMBO: 122, 139

1, 2. (a) Watumishi wa Mungu wanangojea kupata zawadi gani? (b) Ni nini itatusaidia kuendelea kukaza macho yetu juu ya zawadi? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

KAMA mutume Paulo, Wakristo watiwa-mafuta wako na tumaini la ajabu sana la kupata “tuzo la mwito [mualiko] wa Mungu wa kwenda juu.” (Flp. 3:14) Wanangojea kutumika pamoja na Yesu mbinguni katika Ufalme wake na kusaidia kufanya wanadamu wote kuwa wakamilifu. (Ufu. 20:6) Muradi huo wenye Mungu amewaalika kufuatia ni wa ajabu kabisa! Kondoo wengine wako na tumaini lenye kuwa tofauti. Wanangojea kupata zawadi ya uzima wa milele katika dunia, hilo ni tumaini lenye kuleta furaha kabisa!​—2 Pet. 3:13.

2 Ili kusaidia Wakristo watiwa-mafuta waendelee kuwa waaminifu na kupata zawadi yao, Paulo aliwatia moyo hivi: ‘Muendelee kukaza akili zenu juu ya mambo yaliyo juu.’ (Kol. 3:2) Walipaswa kukaza akili zao juu ya tumaini lao la ajabu la kupata uriti wao huko mbinguni. (Kol. 1:4, 5) Kwa kweli, kufikiria baraka zenye Yehova amewekea watumishi wake wote kunawasaidia waendelee kukaza akili zao juu ya zawadi, iwe wako na tumaini la kuishi mbinguni ao la kuishi duniani.​—1 Kor. 9:24.

3. Paulo alionya Wakristo wenzake juu ya hatari gani?

3 Pia mutume Paulo aliwaonya Wakristo wenzake juu ya hatari zenye zinaweza kuwazuia kupata zawadi. Kwa mufano, aliandikia Wakristo katika Kolosai juu ya Wakristo wa uwongo wenye walikuwa wanapenda kukubaliwa na Mungu kwa kufuata Sheria kuliko kuwa na imani katika Kristo. (Kol. 2:16-18) Pia mutume Paulo alizungumuzia hatari zenye zinaendelea kuwa hata katika siku zetu zenye zinaweza kutuzuia kupata zawadi. Kwa mufano, alizungumuzia namna ya kupinga tamaa za mubaya, namna ya kumaliza matatizo kati ya ndugu na dada zetu, na namna ya kupambana na matatizo ya familia. Mashauri yake juu ya mambo hayo ni ya maana sana kwetu. Kwa hiyo, tuzungumuzie basi mashauri fulani yenye upendo yenye kupatikana katika barua yenye Paulo aliandikia Wakolosai.

MUUE TAMAA ZA MUBAYA

4. Sababu gani tamaa za mubaya zinaweza kutuzuia kupata zawadi?

4 Kisha kukumbusha ndugu zake juu ya tumaini lao la ajabu, Paulo aliandika hivi: ‘Kwa hiyo, muviue viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye mazara, na kutamani.’ (Kol. 3:5) Tamaa za mubaya zinaweza kuwa nguvu na zinaweza kutufanya tupoteze urafiki wetu pamoja na Yehova na tumaini letu la wakati wenye kuja. Ndugu mumoja mwenye aliangukia katika zambi kwa sababu ya tamaa za mubaya, kisha kurudishwa katika kutaniko, alisema hivi: “Nilichochewa na tamaa yenye nguvu sana hivi kwamba sikurudiwa na ufahamu mupaka wakati ilikuwa nyuma sana.”

5. Namna gani tunaweza kujilinda katika hali zenye kuleta hatari?

5 Ni jambo la lazima zaidi kuwa waangalifu wakati tunapambana na hali zenye zinaweza kutufanya tuvunje kanuni za Yehova za mwenendo. Kwa mufano, ni jambo la hekima, kisha tu kuanzisha uchumba, ndugu na dada wenye kuchumbiana waweke mipaka juu ya mambo kama vile kugusana, kupatiana busu, ao kuwa pamoja wao wenyewe. (Met. 22:3) Pia, hali fulani zenye kutia mwenendo wa Mukristo katika hatari zinaweza kutokea wakati amesafiri kwa ajili ya mambo ya biashara ao wakati anatumika na mutu fulani mwenye haiko bibi ao bwana yake. (Met. 2:10-12, 16) Ikiwa unajikuta katika hali kama hizo, ujitambulishe kuwa wewe ni Shahidi wa Yehova, tenda kwa heshima, na ukumbuke kuwa kuchezea wengine kimapenzi kunaweza kuleta matokeo ya mubaya sana. Pia tunaweza kuwa katika hatari kubwa ikiwa tumeshuka moyo na tuko zaifu. Wakati kama huo, tunaweza kuwa na tamaa ya kuwa na mutu fulani wa kutufanya tujisikie kuwa tuko wa lazima. Tunaweza hata kutamani sana kuwa na mutu wa kututia moyo mupaka tunafikia kuwa tayari kukubali mutu yeyote mwenye kuonyesha kuwa anatuhangaikia. Ikiwa jambo hilo linakufikia, umuombe Yehova na watu wake musaada ili lisikuzuie kupata zawadi.​—Soma Zaburi 34:18; Methali 13:20.

6. Wakati tunachagua mambo ya kujifurahisha, tunapaswa kukumbuka nini?

6 Ili kuua tamaa za mubaya, tunapaswa kuepuka mambo ya mubaya ya kujifurahisha. Mambo mengi ya kujifurahisha leo yanafanana ya mambo yenye yalikuwa yanatendeka katika Sodoma na Gomora ya zamani. (Yuda 7) Wale wenye kufanya mambo hayo ya kujifurahisha wanaonyesha mawazo yao juu ya mwenendo kwa kufanya mambo ya uasherati yaonekane kuwa jambo la kawaida na kuwa hayalete matokeo yoyote ya mubaya. Tunapaswa kuendelea kuwa waangalifu ili tusikubali kila jambo la kujifurahisha lenye tunatolewa. Tunapaswa kuchagua mambo ya kujifurahisha yenye hayatatuzuia kuendelea kukaza macho yetu juu ya zawadi ya uzima.​—Met. 4:23.

‘MUJIVIKE’ UPENDO NA WEMA

7. Ni matatizo gani yenye yanaweza kutokea katika kutaniko la Kikristo?

7 Sisi wote tunakubali kwamba kuwa katika kutaniko la Kikristo ni baraka. Kujifunza Neno la Mungu kwenye mikutano yetu na musaada wenye upendo na wema wenye tunaonyeshana, vinatusaidia kuendelea kukaza macho yetu juu ya zawadi. Hata hivyo, wakati fulani kukosa kuelewana kunaweza kuleta mabishano kati ya ndugu na dada katika kutaniko. Ikiwa tunashindwa kumaliza matatizo hayo, inaweza kuwa mwepesi yafikie kutufanya tukuwe na kinyongo.​—Soma 1 Petro 3:8, 9.

8, 9. (a) Ni sifa gani zenye zinaweza kutusaidia kupata zawadi? (b) Nini inaweza kutusaidia kuendeleza amani ikiwa Mukristo mwenzetu anatukwaza?

8 Tunaweza kufanya nini ili kuweka kinyongo kusituzuie kupata zawadi? Paulo aliwatia moyo Wakolosai hivi: ‘Kama waliochaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, mujivike upendo mwororo wenye huruma, fazili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Muendelee kuvumiliana na kusameheana kwa hiari [kwa kupenda] ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi mufanye vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, mujivike upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.’​—Kol. 3:12-14.

9 Upendo na wema vinaweza kutusaidia kusamehe wengine. Kwa mufano, ikiwa maneno ao matendo ya Mukristo mwenzetu yametukwaza, tunaweza kukumbuka hali fulani ambamo sisi pia tulisema ao kutenda mubaya. Kwa kweli, tunafurahia upendo na wema wa ndugu na dada wenye walitusamehe. (Soma Mhubiri 7:21, 22.) Zaidi sana tuko wenye shukrani sana kwa wema wa Kristo kwa kutukusanya katika ibada ya kweli yenye umoja. (Kol. 3:15) Sisi wote tunapenda Mungu uleule, tunahubiri ujumbe uleule, na tunapatwa na magumu yaleyale. Wakati tunasameheana kwa upendo na wema, tunasaidia kuleta umoja kati ya Wakristo na tunaendelea kukaza macho yetu juu ya zawadi ya uzima.

10, 11. (a) Sababu gani ni hatari kuwa na wivu? (b) Tunaweza kufanya nini ili wivu usituzuie kupata zawadi?

10 Biblia inazungumuzia mifano yenye kuonya na yenye kutukumbusha kwamba kuwa na wivu kunaweza kutuzuia kupata zawadi. Kwa mufano, Kaini alionea Abeli, ndugu yake wivu, na akamuua. Kora, Dathani, na Abiramu walimuonea Musa wivu na wakamupinga. Pia, Mufalme Sauli alimuonea Daudi wivu kwa sababu ya ushindi wenye alipata na kujaribu kumuua. Ndiyo sababu Neno la Mungu linasema hivi: “Mahali ambapo pana wivu na ugomvi, hapo pana machafuko na kila jambo baya.”​—Yak. 3:16.

11 Ikiwa tunakomalisha upendo na wema katika moyo wetu, hatutakuwa wepesi kuonea wengine wivu. Neno la Mungu linasema hivi: ‘Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fazili. Upendo hauna wivu.’ (1 Kor. 13:4) Ili kuepuka wivu kukomaa katika moyo wetu, tunapaswa kujikaza kuona mambo namna Mungu anayaona, ni kusema, kuona ndugu na dada zetu kuwa washiriki wa mwili uleule wa Kristo. Hilo litatusaidia kujitia pa nafasi ya wengine kwa kufuata shauri hili lenye liliongozwa na roho ya Mungu: “Kiungo kimoja kikitukuzwa, vile viungo vingine vyote vinashangilia pamoja nacho.” (1 Kor. 12:16-18, 26) Kwa hiyo, kuliko kuwa na wivu, tutakuwa na furaha wakati wengine wanapata baraka. Fikiria mufano wa Yonathani, mutoto wa Mufalme Sauli. Hakumuonea Daudi wivu wakati alichaguliwa kuwa mufalme kuliko yeye. Lakini, alimutia Daudi moyo. (1 Sam. 23:16-18) Sisi pia tunaweza kuiga wema na upendo wa Yonathani.

FAMILIA YOTE INAWEZA KUPATA ZAWADI

12. Ni mashauri gani yenye kutoka katika Maandiko yenye yanaweza kusaidia familia yote ifikie kupata zawadi?

12 Kutumikisha kanuni za Biblia kunaweza kuleta amani na furaha katika familia na kuwasaidia wapate zawadi. Ni mashauri gani yenye hekima kwa ajili ya familia yenye mutume Paulo alitolea Wakristo katika Kolosai? Alisema hivi: ‘Enyi wake, mujitiishe kwa waume zenu, kwa kuwa inafaa katika Bwana. Enyi waume, muendelee kuwapenda wake zenu nanyi musiwakasirikie kwa uchungu. Enyi watoto, muwatii wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo linapendeza vema katika Bwana. Enyi akina baba, musikuwe mukiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.’ (Kol. 3:18-21) Bila shaka utakubali kuwa kutumia mashauri hayo ya mutume Paulo yenye kuongozwa na roho ya Mungu kutaletea bwana, bibi, na watoto faida.

13. Namna gani dada Mukristo anaweza kusaidia bwana yake mwenye haiko Shahidi?

13 Tuseme nini ikiwa uko bibi na unaona kuwa bwana yako mwenye haiko Shahidi anakutendea mubaya? Utafanya hali ikuwe muzuri kwa kusema-sema juu ya tabia yake? Hata kama unafikia kumuchochea afanye mambo yenye unapenda, utamusaidia afikie kukubali kweli? Pengine hapana. Lakini ikiwa unaheshemia ukichwa wa bwana yako, unaweza kusaidia kuleta amani katika familia, utamuletea Yehova sifa, na unaweza hata kumusaidia bwana yako akubali ibada ya kweli, na ninyi wawili munaweza kupata zawadi.​—Soma 1 Petro 3:1, 2.

14. Bwana Mukristo anapaswa kufanya nini ikiwa bibi yake mwenye haiko Shahidi hamuheshimie?

14 Tuseme nini ikiwa uko bwana na unaona kuwa bibi yako mwenye haiko Shahidi hakuheshimie? Utamuchochea akuheshimie zaidi ikiwa unamutombokea ili kuonyesha kuwa wewe ndiye mukubwa wake? Hapana kabisa! Mungu anakutazamia uonyeshe ukichwa kwa njia ya upendo, kwa kufuata mufano wa Yesu. (Efe. 5:23) Yesu alitumia ukichwa wake juu ya kutaniko lake kwa upendo na uvumilivu. (Lu. 9:46-48) Ikiwa bwana anafuata mufano wa Yesu anaweza kumusaidia bibi yake amutumikie Yehova.

15. Namna gani bwana Mukristo anaonyesha kuwa anapenda bibi yake?

15 Biblia inaambia bwana hivi: ‘Muendelee kuwapenda wake zenu nanyi musiwakasirikie kwa uchungu.’ (Kol. 3:19) Bwana mwenye kuwa na upendo anaheshimia bibi yake kwa kusikiliza mawazo yake na kumuhakikishia kuwa mambo yenye anasema ni ya maana. (1 Pet. 3:7) Hata kama hatafanya siku zote mambo yenye bibi yake anaomba, mara nyingi anafikia kuchukua uamuzi wenye usawaziko zaidi kwa kumuuliza mawazo yake. (Met. 15:22) Bwana mwenye kuwa na upendo anajikaza kufanya bibi yake amuheshimie kwa kupenda kuliko kumukaza afanye hivyo. Bwana mwenye anapenda bibi yake na watoto wake anaweza kufikia kuwa kabisa na familia yenye kumutumikia Yehova katika furaha na yenye itapata zawadi ya uzima.

Tunaweza kufanya nini ili magumu ya familia yasituzuie kupata zawadi? (Picha hizi zinapatana na fungu la 13-15)

VIJANA​—MUSIACHE JAMBO LOLOTE LIWAZUIE KUPATA ZAWADI!

16, 17. Kijana, namna gani unaweza kuepuka kukasirikia sana wazazi wako?

16 Tuseme nini ikiwa uko kijana na unaona kuwa wazazi wako Wakristo hawakuelewe na wamekuwekea vizuizi vingi? Huzuni yako inaweza kukufanya hata ukuwe na mashaka ikiwa kumutumikia Yehova ndilo jambo la maana kabisa katika maisha. Lakini ikiwa unaacha huzuni ikufanye uache kumutumikia Yehova, hautakawia kuona kuwa hakuna mutu mwenye kukuhangaikia kabisa kuliko wazazi wako wenye kumuogopa Mungu na ndugu dada katika kutaniko lako.

17 Ikiwa wazazi wako hawakutolee nizamu hata kidogo, hautajiuliza ikiwa wanakuhangaikia kabisa? (Ebr. 12:8) Lakini pengine ni namna wazazi wako wanakutolea nizamu ndiyo yenye kukukasirisha. Kuliko kukasirika juu ya namna wanakutolea nizamu, ujikaze kuelewa sababu yenye ilifanya wakutolee nizamu katika njia hiyo. Kwa hiyo, ubakie mwenye kutulia na uepuke kabisa kutenda kwa hasira wakati wanasema mambo yenye hayakufurahishe. Neno la Mungu linasema hivi: ‘Yeyote anayezuia maneno yake ana ujuzi, na mutu mwenye utambuzi ana roho ya utulivu.’ (Met. 17:27) Ujiwekee muradi wa kuwa mutu mwenye kukomaa mwenye anaweza kusikiliza mashauri kwa utulivu, na kufaidika nayo bila kuhangaika kupita kiasi juu ya namna yalitolewa. (Met. 1:8) Kuwa na wazazi Mashahidi wenye kumupenda Yehova kabisa ni baraka. Kwa kweli, watakusaidia kupata zawadi ya uzima.

18. Sababu gani umeazimia kuendelea kukaza macho yako juu ya zawadi?

18 Zawadi yenye kuwa mbele yetu, iwe ni uzima wenye hauwezi kufa huko mbinguni ao uzima wa milele katika paradiso duniani, ni jambo la ajabu la kufikiria. Ni tumaini lenye kuwa hakika, lenye Muumbaji yeye mwenyewe ametoa. Kuhusu dunia Paradiso, Mungu anasema hivi: ‘Dunia hakika itajawa na kumujua Yehova.’ (Isa. 11:9) Wakati huo, kila mutu mwenye kuishi duniani atafundishwa na Mungu. Kwa kweli, hiyo ni zawadi yenye tunapaswa kujikaza kufikia. Kwa hiyo, ukaze akili yako juu ya ahadi za Yehova na usiache jambo lolote likuzuie kupata zawadi!