Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Ninaacha Vitu Nyuma ili Kumufuata Bwana

Ninaacha Vitu Nyuma ili Kumufuata Bwana

“Ikiwa unaenda kuhubiri usirudie hapa. Ikiwa unarudia, nitavunja miguu yako.” Kwa sababu ya maneno hayo yenye kuogopesha ya Baba yangu, niliamua kuondoka nyumbani. Hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kuacha vitu nyuma ili kumufuata Bwana. Nilikuwa na miaka 16 tu.

NAMNA gani nilifikia kuwa katika hali hiyo? Acha niwaelezee. Nilizaliwa tarehe 29 Mwezi wa 7, 1929, na nilikomalia katika kijiji kimoja cha jimbo la Bulacan katika Ufilipino. Maisha yalikuwa ya hali ya chini huko kwa sababu kulikuwa magumu ya kupata feza. Wakati nilikuwa kijana, vita ilitokea. Jeshi la Japani lilishambulia Ufilipino. Lakini, kijiji chetu kilikuwa mbali sana, kwa hiyo hatukusumbuliwa moja kwa moja na vita hiyo. Hatukukuwa na radio, televizyo, na magazeti ya kutangaza habari; kwa hiyo, tulipata habari za vita kupitia vinywa vya watu.

Nilikuwa wa pili kati ya watoto munane na wazazi wa mama yangu walikuwa wamenichukua ili niishi pamoja nao wakati nilikuwa na miaka munane. Hata kama tulikuwa katika dini ya Katoliki tate yangu mwanaume alikuwa tayari kusikiliza mafundisho ya dini zingine na alikuwa anakusanya vichapo vyenye kuzungumuzia mambo ya dini vyenye rafiki zake walimupatia. Ninakumbuka kuwa alinionyesha vijitabu Protection, Sécurité, na Dévoilées katika luga ya Tagalog, * pamoja na Biblia. Nilifurahia kusoma Biblia, zaidi sana vitabu ine vya Injili. Kufanya hivyo kulinichochea nipende kuiga mufano wa Yesu.​—Yoh. 10:27.

NINAJIFUNZA KUMUFUATA BWANA

Jeshi la Japani liliondoka katika mwaka wa 1945. Wakati huo, wazazi wangu waliniomba nirudie nyumbani. Tate yangu mwanaume alinitia moyo niende. Kwa hiyo, nilienda.

Muda mufupi kisha hapo, katika Mwezi wa 12, 1945, kikundi cha Mashahidi wa Yehova kutoka katika muji wa Angat kilikuja kuhubiri katika kijiji chetu. Shahidi mumoja mwenye kuzeeka alifika kwenye nyumba yetu na akatuelezea mambo yenye Biblia inasema juu ya “siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1-5) Akatualika kuhuzuria funzo la Biblia katika kijiji chenye kuwa karibu. Wazazi wangu hawakuenda, lakini mimi nilienda. Watu 20 hivi walikusanyika hapo, na wamoja kati yao waliuliza maulizo ya Biblia.

Kwa sababu sikuelewa kabisa mambo yote yenye walikuwa wanazungumuzia, niliamua kuondoka. Lakini, wakati huo, walianza kuimba wimbo wa Ufalme. Wimbo huo ulinipendeza sana, kwa hiyo nilibakia. Kisha wimbo na sala, sisi wote tulialikwa kuhuzuria mukutano katika Angat Siku ya Yenga yenye kufuata.

Wengi kati yetu tulitembea kilometre 8 hivi ili kuhuzuria mukutano katika nyumba ya familia ya Cruz. Nilishangaa sana kwa sababu hata watoto wadogo wenye walikuwa kati ya watu 50 wenye walikuwa hapo walikuwa wanatoa maelezo juu ya mafundisho mazito ya Biblia. Kisha kuhuzuria mikutano mingi, Ndugu Damian Santos, painia mumoja mwenye kukomaa mwenye zamani alikuwa meya ao mukubwa wa muji alinialika nilale kwake. Tulipitisha karibu usiku wote katika mazungumuzo ya Biblia.

Katika siku hizo, wengi kati yetu waliamini bila kukawia mafundisho ya musingi ya Biblia. Kisha tu kuhuzuria mikutano fulani, ndugu waliniuliza pamoja na wengine hivi: “Munapenda kubatizwa?” Nilijibia hivi: “Ndiyo ninapenda.” Nilijua kuwa nilipenda ‘kutumikia Bwana, Kristo.’ (Kol. 3:24) Tulienda kwenye mutoni wenye ulikuwa karibu, na wawili kati yetu tulibatizwa tarehe 15 Mwezi wa 2, 1946.

Tulielewa kuwa kwa sababu tuko Wakristo wenye kubatizwa, tunapaswa kuhubiri kwa ukawaida kwa kuiga mufano wa Yesu. Kufanya hivyo hakukumupendeza baba yangu. Alisema hivi: “Ungali mutoto sana hauwezi kuhubiri. Zaidi ya hilo, kutumbukizwa katika mutoni hakukufanye ukuwe muhubiri.” Nilimuelezea kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba tuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Niliongeza hivi: “Ninapaswa kutimiza naziri yangu kwa Mungu.” Huo ndio wakati baba yangu alisema maneno yenye kuogopesha yenye nilieleza kwenye mwanzo wa habari hii. Ndiyo, alikuwa na kusudi la kunizuia kuhubiri. Na hiyo ndiyo ilikuwa mwanzo wa maisha yangu ya kuacha vitu nyuma ili kufuatilia miradi ya kiroho.

Watu wa familia ya Cruz walinialika niishi pamoja nao katika Angat. Pia walinitia moyo mimi na Nora mutoto wao mwanamuke wa mwisho, tuanze kazi ya upainia. Sisi wawili tulianza kufanya kazi ya upainia tarehe 1 Mwezi wa 11, 1947. Nora alitumikia katika muji mwingine, na mimi niliendelea kutegemeza kazi ya kuhubiri katika Angat.

NAFASI INGINE YA KUACHA VITU NYUMA

Katika mwaka wangu wa tatu katika kazi ya upainia, Earl Stewart, ndugu mwenye alikuwa anatumika kwenye biro ya tawi, alitolea hotuba watu zaidi ya 500 katika nafasi moja ya watu wengi katika Angat. Aliitoa katika Kiingereza, na kisha nilitoa kifupi cha hotuba yake katika luga ya Tagalog. Nilifanya tu miaka saba kwenye masomo, lakini walimu wetu walikuwa wanatumia kwa ukawaida luga ya Kiingereza. Jambo lingine lenye lilinisaidia kufanya maendeleo katika luga Kiingereza ilikuwa kwa sababu tulikuwa na vichapo vidogo vyenye kutegemea Biblia katika luga ya Tagalog. Kwa hiyo, nilijifunza vichapo vingi katika Kiingereza. Na nilikuwa nimejua Kiingereza cha kutosha ili kutafsiri hotuba hiyo na kisha hotuba zingine.

Siku moja nilitafsiri hotuba ya Ndugu Stewart; aliambia kutaniko la eneo hilo kuwa biro ya tawi inapenda kualika ndugu mumoja ao wawili wenye kuwa mapainia ili wakuje kwenye Beteli. Wangeenda kusaidia kazi huko wakati wamisionere wangeenda kuhuzuria Kusanyiko la Ongezeko la Kitheokrasi la mwaka wa 1950 katika New York, Amerika. Nilikuwa kati ya ndugu wenye walialikwa. Tena niliacha mambo fulani, nafasi yenye nilikuwa ninazoea na ndugu na dada, ili kusaidia katika kazi kwenye Beteli.

Nilifika kwenye Beteli tarehe 19 Mwezi wa 6, 1950, na kuanza mugawo wangu wa mupya. Beteli ilikuwa katika nyumba kubwa ya zamani yenye kuzungukwa na hektare mbili na nusu za miti mikubwa-mikubwa. Ndugu kumi na mbili hivi wenye walikuwa hawajaoa walikuwa wanatumika huko. Asubui sana, nilitumika mahali pa kupikia chakula. Kisha, kuanzia saa tatu hivi, nilitumika nafasi ya kusafisha manguo na kupiga pasi ao kugoma manguo. Nilifanya hivyohivyo kisha midi. Hata wakati wamisionere walirudia kutoka kwenye mukusanyiko wa kimataifa, niliendelea kutumikia kwenye Beteli. Nilikuwa ninafunga magazeti ya kutumia watu, nilishugulikia ombi za watu wenye walijiandikisha ili kupata vichapo, na nilifanya kazi ya kupokea wageni; nilifanya kila kazi yenye niliombwa kufanya.

NINAACHA UFILIPINO ILI KUENDA KWENYE MASOMO YA GILEADI

Katika mwaka wa 1952, pamoja na ndugu wengine sita kutoka Ufilipino, nilifurahi kupata mualiko wa kusoma darasa la 20 la Masomo ya Gileadi. Mambo mengi yenye tulijionea katika Amerika yalikuwa ya mupya kwetu. Kwa kweli, yalikuwa tofauti na mambo yenye nilikuwa ninajua katika kijiji chetu kidogo.

Niko na wanafunzi wenzangu kwenye Gileadi

Kwa mufano, tulijifunza kutumikisha mashine za nyumbani na vyombo fulani vya kupikia chakula vyenye hatukukuwa tunajua. Na kusema kweli, hali ya hewa ilikuwa tofauti sana! Asubui moja nilitoka inje na kuona kuwa kila mahali kulikuwa mweupe. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kuona teluji. Kisha nikatambua kuwa kulikuwa baridi, baridi sana!

Hata hivyo, mabadiliko hayo hayakunisumbua kwa sababu nilikuwa ninapata mazoezi ya muzuri sana kwenye Gileadi. Walimu walitumia ufundi mbalimbali muzuri wa kufundisha. Tulijifunza namna ya kutafuta habari na kujifunza muzuri. Mazoezi ya Gileadi yalinisaidia sana kufanya hali yangu ya kiroho ikuwe muzuri zaidi.

Kisha kumaliza masomo, nilitumwa kwa muda kuwa painia wa pekee katika eneo la Bronx katika Muji wa New York. Kwa hiyo katika Mwezi wa 7, 1953, nilihuzuria Mkusanyiko wa Jamii ya Ulimwengu Mpya, wenye ulifanyika katika eneo hilohilo la muji huo. Kisha mukusanyiko, nilirudia katika mugawo fulani katika Ufilipino.

NINAACHA UZURI WA MUJI

Ndugu wa biro ya tawi waliniambia hivi: “Sasa utaenda katika kazi ya muzunguko.” Hilo lingenipatia nafasi ya kufuata moja kwa moja hatua za Bwana, mwenye alisafiri katika miji na vijiji vya mbali ili kusaidia kondoo za Yehova. (1 Pet. 2:21) Nilitumwa katika muzunguko wenye ulifanyizwa na eneo kubwa la Luzon ya kati, kisiwa kikubwa zaidi katika Ufilipino. Eneo hilo lilifanyizwa na majimbo kama vile Bulacan, Nueva Ecija, Tarlac, na Zambales. Ili kutembelea miji fulani, nilipaswa kupita katika eneo lenye majiwe-majiwe la Milima ya Sierra Madre. Motokari za kusafirisha watu hazikukuwa zinafika katika maeneo hayo. Kwa hiyo, nilipaswa kuomba watu wenye kutembeza motokari kubwa-kubwa ikiwa ningekaa juu ya vipande vikubwa vya miti vyenye walikuwa wanabeba katika motokari zao. Mara nyingi waliniruhusu, lakini haikukuwa namna ya kusafiri ya muzuri.

Makutaniko mengi yalikuwa na hesabu kidogo ya watu na yalikuwa ya mupya. Kwa hiyo, ndugu walishukuru wakati niliwasaidia kupanga muzuri zaidi mikutano na kazi ya kuhubiri.

Kisha nilitumwa katika muzunguko wenye ulifanyizwa na eneo lote la Bicol. Lilifanyizwa zaidi sana na vikundi vidogo-vidogo vyenye kuwa mbali kwenye mapainia wa pekee walikuwa wanahubiria maeneo yenye yalikuwa hayajahubiriwa. Kwenye nyumba moja, choo ao WC moja yenye walikuwa nayo ilikuwa shimo na miti mbili yenye kuwekwa juu ya shimo hilo. Wakati nilisimama kwenye miti hiyo, nikaangukia katika shimo hilo pamoja na miti hiyo. Iliniomba wakati fulani ili kujisafisha na kuwa tayari kula chakula cha asubui!

Ilikuwa wakati nilikuwa katika mugawo huo ndio nilianza kufikiri juu ya Nora, mwenye alianza kufanya kazi ya upainia katika Bulacan. Wakati huu, alikuwa painia wa pekee katika Muji wa Dumaguete, na nilienda kumutembelea. Kisha hapo, tulianza kuandikiana kwa muda fulani, na katika mwaka wa 1956, tulifunga ndoa. Tulipitisha juma la kwanza la ndoa yetu kwa kutembelea kutaniko katika Kisiwa cha Rapu Rapu. Huko tulipaswa kupanda milima na kutembea sana, lakini ilikuwa furaha sana kutumikia ndugu katika maeneo ya mbali pamoja!

NINAALIKWA TENA KUTUMIKIA KWENYE BETELI

Kisha kufanya miaka ine hivi katika kazi ya muzunguko, tulipata mualiko wa kutumikia kwenye biro ya tawi. Kwa hiyo, katika Mwezi wa 1, 1960 tulianza kufanya kazi kwenye Beteli. Kwa miaka mingi yenye tumekuwa kwenye Beteli, nimejifunza mengi kwa kutumika pamoja na ndugu wenye kuwa na madaraka mazito, na Nora ametumikia migawo mbalimbali kwenye Beteli.

Ninatoa hotuba kwenye mukusanyiko na ndugu mumoja anaitafsiri katika luga ya Cebuano

Kwa kutumikia kwenye Beteli, nimebarikiwa kuona ongezeko kubwa la kiroho katika Ufilipino. Wakati niliingia kwenye Beteli kwa mara ya kwanza wakati nilikuwa kijana mwenye hajaoa, kulikuwa wahubiri 10000 hivi katika inchi yote. Sasa kuko wahubiri zaidi ya 200000 katika Ufilipino, na mamia ya Wanabeteli wenye kutegemeza kazi kubwa ya kuhubiri.

Kadiri miaka ilipita, kazi iliendelea kuongezeka, kwa hiyo, majengo ya Beteli yakakuwa kidogo sana. Kisha Baraza Lenye Kuongoza lilituomba tutafute nafasi kwenye tunaweza kujenga majengo mapya makubwa. Mimi na mwangalizi wa kazi ya kuchapisha tulienda nyumba kwa nyumba karibu na tawi ili kuuliza ikiwa kulikuwa mutu mwenye angependa kuuzisha kwake. Hakuna mwenye alipenda kuuzisha; mutu mumoja mwenye alikuwa na kiwanja chake alituambia hata hivi: “Wachina hawauzishake nafasi zao. Tunauzaka.”

Ninatafsiri hotuba ya Ndugu Albert Schroeder

Hata hivyo, bila kutazamia mutu mumoja mwenye alikuwa na kiwanja chake alituuliza ikiwa tunapenda kuuza kiwanja hicho; alikuwa anajitayarisha kuhamia Amerika. Hilo lilikuwa mwanzo ya matukio yenye kushangaza. Jirani mwingine aliamua kuuzisha kiwanja chake, na alitia wengine moyo wafanye hivyo. Tuliweza hata kuuza kiwanja kutoka kwa mutu mwenye alikuwa amesema kuwa “Wachina hawauzishake nafasi zao.” Kwa muda mufupi, ukubwa wa kiwanja cha tawi uliongezeka zaidi ya mara tatu. Niko hakika kuwa Yehova Mungu alipenda mambo yakuwe hivyo.

Katika mwaka wa 1950, mimi ndiye nilikuwa kijana sana katika familia ya Beteli. Sasa mimi na bibi yangu, sisi ndiyo watu wenye kukomaa zaidi katika familia ya Beteli. Sijute kabisa kwa sababu nimefuata Bwana nafasi yoyote kwenye ameniongoza. Kwa kweli, wazazi wangu walinifukuza katika nyumba yao, lakini Yehova amenipatia familia kubwa ya Wakristo wenzangu. Sina mashaka hata kidogo kuwa Yehova anatupatia kila kitu chenye tuko nacho lazima, hata tupewe mugawo gani. Mimi na Nora tuko wenye shukrani sana kwa Yehova kwa mambo yote ya muzuri yenye ametupatia, na tunatia wengine moyo wamujaribu Yehova.​—Mal. 3:10.

Siku moja Yesu alialika mukusanya-kodi mwenye aliitwa Mathayo Lawi, kwa kusema hivi: ‘Ukuwe mufuasi wangu.’ Alitenda namna gani? ‘Akaacha kila kitu akaondoka akaanza kumufuata [Yesu].’ (Lu. 5:27, 28) Mimi pia nimepata nafasi yakufanya hivyo, na ninatia wengine moyo kwa furaha wafanye hivyo ili wapate baraka nyingi.

Ninafurahi kuendelea kuchangia katika ongezeko katika Ufilipino

^ fu. 6 Vilichapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa havichapishwe tena.