Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Iga Huruma ya Yehova

Iga Huruma ya Yehova

“Yehova, aliwahurumia watu wake.”​—2 NYA. 36:15.

NYIMBO: 142, 12

1. Ni katika njia gani ya pekee Yehova alijifunua kwa Musa, na sababu gani jambo hilo ni la maana?

WAKATI fulani, Mungu alijifunua kwa Musa kwa kutangaza jina lake na sifa zake. Sifa za kwanza zenye alitaja zilikuwa rehema na neema ao huruma. (Soma Kutoka 34:5-7.) Yehova angekazia nguvu yake ao hekima yake. Lakini, kwa sababu Musa alikuwa anatafuta jambo lenye kumuhakikishia kuwa Mungu angemusaidia, Yehova alikazia sifa zenye zilionyesha kuwa iko tayari kusaidia watumishi wake. (Kut. 33:13) Hauone kuwa ni jambo lenye kufurahisha kuona namna Mungu alitaja kwanza sifa hizo zenye kupendeza mbele ya kutaja sifa zingine zote? Habari hii itazungumuzia zaidi sifa ya huruma, yenye kumaanisha kutambua mateso ao taabu ya mutu mwingine, kujitia pa nafasi yake, na kupenda kumusaidia.

2, 3. (a) Ni nini inaonyesha kuwa wanadamu wako na uwezo wa kuonyesha sifa ya huruma? (b) Sababu gani tunapaswa kupendezwa na mambo yenye Biblia inafundisha juu ya sifa ya huruma?

2 Wanadamu waliumbwa kwa mufano wa Mungu. Kwa kweli, kwa sababu Yehova iko na sifa ya huruma, wanadamu wako pia na tamaa ya kusaidia wengine wajisikie muzuri. Hata wale wenye hawajue Mungu wa kweli mara nyingi wanaonyesha huruma. (Mwa. 1:27) Biblia iko na habari nyingi zenye kuzungumuzia namna sifa ya huruma ilionyeshwa. Kumbuka mufano wa makahaba wawili wenye walibishana mbele ya Sulemani juu ya nani kati yao alikuwa mama wa kweli kabisa wa mutoto. Wakati Sulemani aliwajaribu kwa kusema kuwa mutoto huyo akatwe vipande viwili, mwanamuke mwenye alikuwa kabisa mama ya mutoto huyo alisikia huruma sana. Sifa hiyo ilimuchochea atende, alikuwa hata tayari kuachia ule mwanamuke mwingine mutoto huyo. (1 Fal. 3:23-27) Pia, kumbuka binti ya Farao mwenye aliokoa maisha ya Musa wakati alikuwa angali mutoto. Hata kama alivumbua kuwa mutoto huyo alikuwa Mwebrania na alipaswa kufa, ‘alimuonea huruma’ na akaamua kumulea kama mutoto wake.​—Kut. 2:5, 6.

3 Sababu gani tunapaswa kuzungumuzia sifa ya huruma? Kwa sababu Biblia inatutia moyo tumuige Yehova. (Efe. 5:1) Wanadamu waliumbwa na uwezo wa kuonyesha sifa ya huruma, lakini kwa sababu tuko wazao wa Adamu wenye hawakamilike, tunachochewa kutafuta faida zetu wenyewe. Wakati fulani tunaweza kuona kuwa ni vigumu kuamua ikiwa tutasaidia wengine ao tutajifikiria tu sisi wenyewe. Kwa watu fulani, hilo ni pigano la kuendelea, ao wanapaswa kujikaza sana ili kuwa na usawaziko. Ni nini inaweza kukusaidia ukuwe mwenye kuhangaikia wengine na uendelee kufanya hivyo? Kwanza, ukamate wakati wa kuchunguza namna Yehova ameonyesha sifa ya huruma na namna wengine wameonyesha sifa hiyo. Pili, fikiria namna unaweza kuiga mufano wa Mungu na namna kufanya hivyo kunaweza kukuletea faida kabisa.

YEHOVA NI MUFANO MUKAMILIFU WA KUONYESHA HURUMA

4. (a) Sababu gani Yehova alituma malaika Sodoma? (b) Habari ya Loti na binti zake inatufundisha nini?

4 Katika Biblia kuko mifano mingi yenye kuonyesha namna Yehova alionyesha sifa ya huruma. Fikiria namna Mungu alimutendea Loti. Mutu huyo muadilifu “alitaabishwa [alihuzunishwa] sana” na mwenendo mubaya sana wa bila haya wa wakaaji wa Sodoma na Gomora. Kwa kweli, Mungu aliamua kuwa watu hao wenye mwenendo mubaya wa bila haya walipaswa kufa. (2 Pet. 2:7, 8) Mungu alituma malaika ili wamuokoe Loti. Walimuomba yeye na familia yake wakimbie kutoka katika miji yenye ilipaswa kuharibiwa. ‘Alipoendelea kukawia, ndipo kwa huruma za Yehova kwake, wale wanaume wakaushika mukono wake na mukono wa muke wake na mikono ya binti zake wawili. Wakamutoa inje na kumuweka inje ya jiji.’ (Mwa. 19:16) Kwa kweli, mufano huo unaonyesha kuwa Yehova anajua muzuri kabisa hali ngumu zenye watumishi wake waaminifu wanapata wakati fulani.​—Isa. 63:7-9; Yak. 5:11; 2 Pet. 2:9.

5. Namna gani andiko la 1 Yohana 3:17 linatufundisha kuonyesha sifa ya huruma?

5 Yehova ameonyesha sifa ya huruma, lakini pia amefundisha watu wake kuwa ni jambo la lazima waonyeshe sifa hiyo. Fikiria sheria yenye Waisraeli walipewa kuhusu mutu kubeba nguo ya mutu mwenye kuwa na deni lake ili ikuwe uhakikisho kuwa atamulipa. (Soma Kutoka 22:26, 27.) Mutu mwenye hana huruma mwenye alipatia mwenzake deni angejaribu kukamata nguo ya mwenzake, na kumuacha bila kitu cha kujifunika wakati atalala. Lakini, Yehova alifundisha watu wake waepuke mawazo na tabia hiyo yenye haina huruma. Watu wake walipaswa kuonyesha sifa ya huruma. Kwa kweli, kanuni yenye kupatikana katika sheria hiyo inatuchochea kutenda. Tunaweza kuacha ndugu zetu katika baridi ya mufano, ikiwa tunaweza kufanya jambo fulani ili kuwasaidia katika magumu yao?​— Kol. 3:12; Yak. 2:15, 16; soma 1 Yohana 3:17.

6. Namna Yehova alitendea Waisraeli watenda-zambi, inatufundisha nini?

6 Yehova alisikilia huruma watu wake, taifa la Israeli hata wakati walitenda zambi. Biblia inasema hivi: “Yehova Mungu wa mababu zao akaendelea kutuma juu yao kupitia kwa wajumbe wake, akatuma tena na tena, kwa sababu aliwahurumia watu wake na makao yake.” (2 Nya. 36:15) Kwa kweli, sisi pia tunapaswa kusikilia huruma watu wenye wanaweza kufikia kutubu na kuacha matendo ya zambi na kisha wakubaliwe na Mungu. Yehova hapendi mutu yeyote aharibiwa wakati wa hukumu yenye kuja. (2 Pet. 3:9) Kwa hiyo, mbele Mungu aharibu watu wabaya, tuendelee basi kutangaza ujumbe wake wenye kuonya na wenye kuonyesha sifa ya huruma.

7, 8. Sababu gani watu wa familia fulani waliamini kuwa Yehova aliwaonyesha huruma?

7 Kuko mifano mingi yenye kuonyesha namna Mungu alitenda kwa huruma. Fikiria jambo lenye lilipata familia moja ya mutoto mumoja mwanaume wa miaka 12 mwenye tunaweza kuita Milan. Ilikuwa wakati wa mapigano ya kikabila mwanzoni mwa miaka ya 1990. Milan, ndugu yake, wazazi wake, na Mashahidi wengine walikuwa katika bisi ya kutoka Bosnia ili kuenda Serbia. Walikuwa wanaenda kwenye mukusanyiko mumoja kwenye wazazi wa Milan walipaswa kubatizwa. Lakini kwenye mupaka wa inchi, maaskari walitosha familia hiyo katika bisi kwa sababu ya kabila yao; hata hivyo, waliacha ndugu wengine waendelee na safari. Kisha kubakia na familia hiyo kwa siku mbili, ofisa mwenye alikuwa amewakamata aliita mukubwa wake na kumuuliza ikiwa wawafanye nini. Ofisa huyo alikuwa anasimama mbele ya familia hiyo, kwa hiyo, wote walisikia jibu la mukubwa huyo, alisema hivi: “Muwakamate na kuwapiga masasi!”

8 Wakati ofisa huyo alikuwa anazungumuza na watu wake, watu wawili walikaribia familia hiyo na waliwaambia polepole kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova. Wengine wenye walikuwa katika bisi hiyo walikuwa wamewaambia juu ya tatizo hilo. Watu hao wawili waliambia Milan na ndugu yake waingie katika motokari yao ili wavuke mupaka, kwa sababu vikaratasi vya watoto havikukuwa vinachunguzwa. Kisha wanaume hao waliambia wazazi wazunguke nyuma ya mipaka na wawakutane upande mwingine. Wakati Milan alisikia hivyo, hakujua ikiwa alie ao acheke. Wazazi wake waliuliza hivi: “Munafikiri kuwa watatuacha tu tuende?” Lakini, wakati walikuwa wanaondoka, ilionekana kuwa maaskari walikuwa wanawaangalia. Wazazi na watoto walikutana kwenye upande mwengine wa mupaka. Wakaendelea na safari yao ya kuenda kwenye mukusanyiko, na walikuwa hakika kuwa Yehova alisikia sala zao za kumuomba musaada. Biblia inatuonyesha kama wakati fulani Yehova hakutenda moja kwa moja ili kulinda watumishi wake. (Mdo. 7:58-60) Lakini, Milan alisema namna alijisikia. Anasema hivi: “Mimi niliona kuwa malaika walifunga maaskari hao macho na kwamba Yehova alituokoa.”​—Zab. 97:10.

9. Namna gani Yesu alitendea kikundi cha watu wenye walikuwa wanamufuata? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

9 Mufano wa Yesu unaweza kutufundisha jambo fulani. Alisikilia huruma kikundi cha watu wenye alikutana nao kwa sababu ‘walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na muchungaji.’ Alitenda namna gani juu ya hali yao yenye kuhuzunisha? ‘Alianza kuwafundisha mambo mengi.’ (Mt. 9:36; soma Marko 6:34.) Alitenda tofauti kabisa na Mafarisayo wenye hawakupenda kusaidia watu wa hali ya chini. (Mt. 12:9-14; 23:4; Yoh. 7:49) Kwa kweli, kama Yesu, wewe pia unatamani sana kufundisha watu wenye kuwa na njaa ya kiroho. Sivyo?

10, 11. Ni muzuri kuonyesha huruma kila mara? Eleza.

10 Hilo halimaanishe kuwa tunapaswa kuonyesha huruma katika kila hali. Katika mifano ya Biblia yenye tumezungumuzia, Mungu alionyesha huruma yenye kufaa. Lakini, Mufalme Sauli alikosa kumutii Mungu wakati alifanya jambo lenye pengine alifikiri kuwa ni huruma. Hakumuua Agagi, adui wa watu wa Mungu, na hakuua pia wanyama wazuri zaidi wa kundi na mifugo. Kwa hiyo, Yehova alimukataa Sauli ili asikuwe tena mufalme juu ya Israeli. (1 Sam. 15:3, 9, 15) Kwa kweli, Yehova ni Muamuzi mwenye haki. Anaweza kusoma mioyo ya watu na anajua ni wakati gani haifae kuonyesha huruma. (Omb. 2:17; Eze. 5:11) Hivi karibuni atahukumu wale wote wenye kukataa kumutii. (2 Tes. 1:6-10) Huo hautakuwa wakati wa kuonyesha huruma kwa wale wenye amehukumu kuwa wabaya. Lakini, kuwaua itakuwa njia yenye kufaa ya kuonyesha huruma yake kwa watu wenye haki, wenye ataokoa.

11 Ni wazi kwamba, haiko daraka letu kuhukumu ikiwa watu wanapaswa kuharibiwa ao kuokolewa. Lakini, tunapaswa kufanya yetu yote leo ili kusaidia watu. Kwa hiyo, ni katika njia gani tunaweza kuonyesha huruma kwa wanadamu wenzetu? Fikiria njia hizi mbalimbali.

KUKOMALISHA NA KUONYESHA HURUMA YENYE KUFAA

12. Namna gani unaweza kuonyesha wengine huruma?

12 Saidia wengine katika maisha ya kila siku. Kuonyesha majirani wetu huruma na ndugu na dada zetu Wakristo ni jambo la maana lenye wale wote wenye wanajikaza kumuiga Yesu wanapaswa kufanya. (Yoh. 13:34, 35; 1 Pet. 3:8) Maana moja ya sifa ya huruma ni “kuteseka pamoja na wengine.” Mutu mwenye kuonyesha huruma anachochewa kutuliza wengine wakati wanateseka, pengine kwa kuwasaidia wakati wa magumu yao. Utafute nafasi za kufanya hivyo! Kwa mufano, unaweza kumusaidia mutu kwa kumufanyia kazi za maana za nyumbani, pengine kwa kuenda kumuuzia vitu fulani?​—Mt. 7:12.

Onyesha wengine huruma kwa kuwatolea musaada wenye wako nao lazima (Picha hii inapatana na fungu la 12)

13. Watu wa Mungu wanaonyesha sifa gani ya pekee kisha misiba ya asili kutokea?

13 Saidia katika kazi ya kutoa misaada. Mateso ya wale wenye wamepigwa na misiba ya asili yamechochea wengi waonyeshe huruma. Watu wa Yehova wanajulikana kuwa wanajitolea ili kusaidia wengine katika wakati kama huo. (1 Pet. 2:17) Dada mumoja wa Japani aliishi katika eneo lenye liliharibiwa sana na tetemeko la inchi na tsunami katika mwaka wa 2011. Alisema kuwa “alitiwa moyo na kufarijiwa sana” na namna wajitoleaji wengi wenye kutoka sehemu zingine za Japani na wenye kutoka katika inchi zingine, walijikaza ili kutengeneza nyumba zenye kuharibika. Aliandika hivi: “Tukio hilo lilinisaidia kutambua kuwa Yehova anatuhangaikia. Na Mashahidi wenzangu wanahangaikiana. Ndugu na dada katika dunia yote wanasali kwa ajili yetu.”

14. Namna gani unaweza kusaidia wagonjwa na wale wenye kuzeeka?

14 Saidia wagonjwa na wale wenye kuzeeka. Wakati tunaona wengine wanapatwa na matokeo ya zambi ya Adamu, tunachochewa kabisa kuonyesha sifa ya huruma. Tunatamani sana kuona magonjwa na uzee vinaisha. Kwa hiyo, tunasali Ufalme wa Mungu ukuje. Wakati huohuo, tunafanya yote yenye tunaweza ili kusaidia wale wenye kuwa na lazima ya musaada. Fikiria mambo yenye mwandishi mumoja aliandika juu ya mama yake mwenye kuzeeka na mwenye alikuwa na ugonjwa wa kupoteza akili wenye kuitwa Alzheimer. Siku moja alichafua nguo zake. Wakati alikuwa anajikaza kuzisafisha, kengele ya mulango ililia. Wageni hao walikuwa Mashahidi wawili wenye walitembelea mwanamuke huyo kwa ukawaida. Dada hao walimuuliza ikiwa kuko jambo fulani lenye wangemusaidia kufanya. Mwanamuke huyo alijibia hivi: “Inaleta haya, lakini ndiyo.” Wageni hao walimusaidia kufanya usafi. Kisha wakamupikia chai na wakabakia ili kuzungumuza naye. Mutoto wake mwanaume alikuwa mwenye shukrani sana. Aliandika hivi: “Mashahidi hao wanastahili pongezi. Wanatenda kulingana na mambo yenye wanahubiri.” Kuonea huruma wagonjwa na wenye kuzeeka kunakuchochea ufanye yote yenye unaweza ili kuwasaidia katika magumu yao?​—Flp. 2:3, 4.

15. Kazi yetu ya kuhubiri inatutolea nafasi ya kufanya jambo gani?

15 Saidia watu kiroho. Magumu na mahangaiko yenye watu wanapambana nayo yanatuchochea tuwasaidie kiroho. Njia ya muzuri zaidi ya kufanya hivyo ni kuwafundisha juu ya Mungu na juu ya mambo yenye Ufalme wake utafanyia wanadamu. Njia ingine ya kufanya hivyo ni kuwasaidia waone kuwa ni jambo la hekima kutumikisha kanuni za Mungu katika maisha yao. (Isa. 48:17, 18) Unaweza kuongeza bidii yako katika kazi ya kuhubiri, kazi yenye kumutukuza Yehova na yenye kuonyesha huruma yako kwa wengine?​—1 Tim. 2:3, 4.

SIFA YA HURUMA INAKULETEA WEWE PIA FAIDA!

16. Namna gani kuonyesha sifa ya huruma kunaweza kuletea mutu faida?

16 Watu wenye kujifunza mambo ya afya wanasema kuwa kuonyesha sifa ya huruma kunaweza kukusaidia ukuwe na afya ya muzuri zaidi, ujisikie muzuri, na ukuwe na urafiki muzuri pamoja na wengine. Wakati unasaidia wengine katika magumu yao, utapata furaha zaidi, utakuwa na mawazo ya muzuri zaidi, hautajisikia kuwa pekee yako, na mara nyingi hautakuwa na mawazo ya mubaya. Kwa kweli, utapata faida ikiwa unaonyesha sifa ya huruma. (Efe. 4:31, 32) Wakristo wenye wanajikaza kusaidia wengine kwa upendo, wanapata baraka ya kuwa na zamiri safi, kwa sababu wanajua kuwa wanatenda kulingana na kanuni za Mungu. Kuonyesha huruma kunafanya mutu akuwe muzazi mwenye kuhangaikia watoto wake, akuwe bibi ao bwana muzuri zaidi, na rafiki muzuri zaidi. Wale wenye kuwa tayari kuonyesha sifa ya huruma, mara nyingi wao pia wanapata musaada na kutegemezwa wakati wako katika uhitaji.​—Soma Mathayo 5:7; Luka 6:38.

17. Sababu gani unapenda kukomalisha na kuonyesha sifa ya huruma?

17 Kujua kuwa kuonyesha sifa ya huruma kutakuletea faida haipaswe kuwa sababu kubwa ya kukuchochea kukomalisha sifa hiyo. Sababu kubwa inapaswa kuwa tamaa yako ya kumuiga na kumutukuza Yehova Mungu, Chanzo cha upendo na huruma. (Met. 14:31) Anatuonyesha mufano mukamilifu. Basi, tufanye yetu yote ili kumuiga; tuendelee kuonyesha upendo kati ya ndugu na dada zetu na kuwa na uhusiano wa muzuri pamoja na majirani wetu kwa kuwaonyesha huruma.​—Gal. 6:10; 1 Yoh. 4:16.