Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Ukuwe Hodari . . . na Utende’

‘Ukuwe Hodari . . . na Utende’

‘Ukuwe hodari na mwenye nguvu nawe utende. Usiogope wala usikuwe na hofu [woga], kwa maana Yehova . . . yuko pamoja nawe.’​—1 NYA. 28:20.

NYIMBO: 60, 29

1, 2. (a) Sulemani alipewa mugawo gani wa maana? (b) Sababu gani Daudi alimuogopea Sulemani?

SULEMANI aliombwa kusimamia kazi moja ya maana sana ya ujenzi kuliko zote, ni kusema, kazi ya kujenga hekalu la Yerusalemu. Nyumba hiyo ilipaswa ‘kuwa yenye utukufu zaidi kwa ajili ya uzuri wenye heshima kwa inchi zote.’ Jambo la maana zaidi, hekalu hilo lingekuwa “nyumba ya Yehova Mungu wa kweli.” Yehova alitoa muongozo kuwa Sulemani ndiye asimamie kazi hiyo.​—1 Nya. 22:1, 5, 9-11.

2 Mufalme Daudi alikuwa hakika kuwa Mungu angemusaidia, lakini Sulemani alikuwa ‘muchanga na mwororo [mwenye hana uzoefu].’ Angekuwa na uhodari, ni kusema, angetenda bila kuogopa ili kutimiza kazi ya kujenga hekalu? Angeshindwa kutimiza kazi hiyo kwa sababu alikuwa kijana na hakukuwa na uzoefu? Ili kuweza, Sulemani alipaswa kuwa na uhodari na kutenda.

3. Inawezekana Sulemani alijua nini juu ya uhodari wa baba yake?

3 Inawezekana Sulemani alijua mambo mengi juu ya uhodari wa baba yake. Wakati alikuwa kijana, Daudi alipigana na wanyama wa pori wenye walibeba kondoo za baba yake. (1 Sam. 17:34, 35) Alionyesha uhodari mukubwa wakati alipigana na mutu munene na murefu sana mwenye alikuwa na uzoefu wa vita. Kwa kweli, kwa musaada wa Mungu na jiwe ndogo, Daudi alipata ushindi juu ya Goliathi.​—1 Sam. 17:45, 49, 50.

4. Sababu gani Sulemani alipaswa kuwa na uhodari?

4 Daudi alikuwa na sababu kabisa ya kuambia Sulemani akuwe hodari na ajenge hekalu! (Soma 1 Mambo ya Nyakati 28:20.) Ikiwa Sulemani hangeonyesha uhodari, woga ungemufanya asitende, na hilo lingekuwa mubaya zaidi kuliko kushindwa kutimiza mugawo wake.

5. Sababu gani tuko na lazima ya uhodari?

5 Kama Sulemani, tuko na lazima ya musaada kutoka kwa Yehova ili kuwa na uhodari na kumaliza kazi. Ili kufanya hivyo, tunapaswa kufikiri sana juu ya mifano ya watu fulani wa zamani wenye walionyesha uhodari. Na tunaweza kufikiria namna gani tunaweza kuonyesha uhodari na kutimiza kazi yetu.

MIFANO YA WATU WENYE WALIONYESHA UHODARI

6. Ni jambo gani lenye linakupendeza juu ya uhodari wa Yosefu?

6 Fikiria uhodari wenye Yosefu alionyesha wakati bibi ya Potifa alimushawishi afanye uasherati. Bila shaka alijua kuwa angepata matokeo ya mubaya sana ikiwa angemukatalia. Lakini kuliko kukubali kulala naye, alionyesha uhodari na kukimbia mara moja.​—Mwa. 39:10, 12.

7. Eleza namna Rahabu alionyesha uhodari. (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

7 Rahabu alionyesha pia uhodari. Wakati wapelelezi Waisraeli waliingia katika nyumba yake katika muji wa Yeriko, angeogopa na kuwafukuza kabisa. Lakini kwa sababu alimutegemea Yehova, alionyesha uhodari kwa kuficha wanaume hao wawili na kuwasaidia waondoke kwa usalama. (Yos. 2:4, 5, 9, 12-16) Rahabu alikubali kuwa Yehova ni Mungu wa kweli, na alikuwa hakika kuwa angepatia Waisraeli inchi hiyo. Hakuruhusu kuogopa watu, kutia ndani mufalme wa Yeriko na wanaume wake, kumuzuie kutenda. Lakini, alitenda kwa njia yenye ilifikia kumuokoa yeye na familia yake.​—Yos. 6:22, 23.

8. Namna gani uhodari wa Yesu ulisaidia mitume wake?

8 Mitume waaminifu wa Yesu walituachia mufano muzuri wa kuonyesha uhodari. Walikuwa wameona namna Yesu alionyesha uhodari. (Mt. 8:28-32; Yoh. 2:13-17; 18:3-5) Mufano huo uliwasaidia kuwa na uhodari. Wakati walipingwa na Masadukayo, mitume hawakuacha kufundisha juu ya musingi wa jina la Yesu.​—Mdo. 5:17, 18, 27-29.

9. Namna gani 2 Timotheo 1:7 inatusaidia tujue chanzo kikubwa cha uhodari?

9 Yosefu, Rahabu, Yesu, na mitume waliazimia kufanya matendo ya muzuri. Walikuwa hodari, haiko kwa sababu walijitumainia. Ni kwa sababu walimutegemea Yehova. Sisi pia tunapambana na hali zenye kutuomba tuonyeshe uhodari. Kuliko kujitegemea sisi wenyewe, tunapaswa kumutegemea Yehova. (Soma 2 Timotheo 1:7.) Tuzungumuzie basi hali mbili za maisha zenye kutuomba tuonyeshe uhodari: katika familia yetu na katika kutaniko letu.

HALI ZENYE KUOMBA UHODARI

10. Sababu gani vijana Wakristo wanapaswa kuonyesha uhodari?

10 Vijana Wakristo wanapambana na hali zenye kuomba waonyeshe uhodari ili wamutumikie Yehova. Wanaweza kujifunza na kufuata mufano wa Sulemani juu ya namna alionyesha uhodari katika kufanya maamuzi yenye hekima ili kumaliza ujenzi wa hekalu. Hata kama vijana Wakristo wanaweza na wanapaswa kupata muongozo kutoka kwa wazazi wao, vijana wenyewe wanapaswa kukamata maamuzi fulani ya maana. (Met. 27:11) Wanapaswa kuwa na uhodari ili kukamata maamuzi ya hekima juu ya marafiki, mambo ya muzuri ya kujifurahisha, kuwa na mwenendo wa muzuri, na kubatizwa. Wako na lazima ya uhodari kwa sababu hawatende kupatana na mapenzi ya Shetani, mwenye kumuchokoza Mungu.

11, 12. (a) Namna gani Musa alionyesha mufano muzuri wa uhodari? (b) Namna gani vijana wanaweza kuiga mufano wa Musa?

11 Uamuzi wa maana wenye vijana wanapaswa kukamata unahusu miradi yao. Katika inchi fulani, vijana wanachochewa sana wajiwekee miradi yenye kukazia sana masomo ya juu na kupata kazi yenye mushahara muzuri. Katika inchi zingine, hali ya kukosa feza inaweza kuwafanya vijana wafikiri kuwa wanapaswa kukaza akili yao juu ya kutimizia familia zao mahitaji ya kimwili. Ikiwa uko katika hali moja kati ya hizo, fikiria mufano wa Musa. Kwa sababu alilelewa na binti ya Farao, angejiwekea muradi wa kuwa tajiri ao kuwa mutu mwenye kujulikana sana. Alipaswa kuchochewa sana na familia yake ya Wamisri, walimu wake, na washauri wake! Lakini, kuliko kufuatilia mambo hayo, Musa alionyesha uhodari kwa kuunga mukono ibada ya kweli. Kisha kuacha utajiri wa Misri, Musa alimutumainia Yehova. (Ebr. 11:24-26) Hilo lilimusaidia kupata baraka za Yehova wakati huo, na kwa kweli, Musa atapata baraka zingine wakati wenye kuja.

12 Vilevile, Yehova atabariki vijana wenye kuonyesha uhodari kwa kujiwekea miradi ya kiroho na kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza katika maisha yao. Atawasaidia kutimiza mahitaji ya familia zao. Wakati wa mitume, kijana Timotheo alikaza akili yake juu ya miradi ya kiroho, na wewe pia unaweza kufanya hivyo. *​—Soma Wafilipi 2:19-22.

Unaazimia kuonyesha uhodari katika hali zote za maisha yako?

(Picha hizi zinapatana na fungu la 13-17)

13. Namna gani uhodari ulimusaidia dada mumoja kijana afikie miradi yake?

13 Dada mumoja wa Alabama, Amerika, alipaswa kuwa na uhodari ili kujiwekea miradi ya kiroho. Anaandika hivi: “Nilikuwa mwenye haya sana wakati nilikuwa ninakomaa. Ilikuwa vigumu kwangu kuzungumuza na watu kwenye jumba la Ufalme, na ilikuwa vigumu zaidi kugonga kwenye mulango wa mutu mwenye sijue kabisa.” Kwa musaada wa wazazi wake na wengine katika kutaniko, dada huyo kijana alifikia muradi wake wa kuwa painia wa kawaida. Anasema hivi: “Ulimwengu wa Shetani unakazia kuwa ni muzuri kujiwekea miradi ya kufuatia masomo ya juu, kujulikana sana, kutafuta feza, na kutafuta vitu vingi vya kimwili. Mara nyingi watu hawafikie kupata mambo hayo na hilo linaleta mahangaiko na maumivu ya moyoni. Lakini, kumutumikia Yehova kumeniletea furaha kubwa na ninajisikia kuwa nimetimiza jambo fulani.”

14. Ni katika hali gani fulani wazazi Wakristo wako na lazima ya kuonyesha uhodari?

14 Wazazi Wakristo pia wako na lazima ya kuonyesha uhodari. Kwa mufano, mukubwa wako wa kazi anaweza kukuomba mara kwa mara utumike mangaribi kisha saa za kazi na katika mwisho wa juma, wakati wenye umepanga kufanya ibada ya familia, kuhubiri, na kuenda kwenye mikutano ya Kikristo. Inaomba kuwa na uhodari ili kukataa ombi hilo la mara kwa mara na kuwekea watoto wako mufano muzuri. Ao pengine wazazi fulani katika kutaniko wanaruhusu watoto wao wafanye mambo yenye wewe haupendi mutoto wako afanye. Wazazi hao wanaweza kukuuliza sababu gani mutoto wako hafanye mambo kama hayo. Utaonyesha uhodari na kuwaelezea kwa upole sababu gani ulikamata uamuzi huo?

15. Namna gani maandiko ya Zaburi 37:25 na Waebrania 13:5 yanaweza kusaidia wazazi?

15 Tunaonyesha uhodari wakati tunasaidia watoto wetu wajiwekee na kufikia miradi ya kiroho. Kwa mufano, wazazi fulani wanaweza kusita kutia mutoto wao moyo afanye kazi ya upainia, atumikie mahali kwenye kuwa lazima kubwa ya wahubiri, atumikie kwenye Beteli, ao kutumika katika kazi za ujenzi wa kiteokrasi. Wazazi wanaweza kuogopa kuwa mutoto wao hataweza kuwatunza wakati watazeeka. Hata hivyo, wazazi wenye kuwa na hekima wanaonyesha uhodari na imani katika ahadi za Yehova. (Soma Zaburi 37:25; Waebrania 13:5.) Na pia njia ingine ya kuonyesha kuwa uko hodari na unamutegemea Yehova, ni kwa kumusaidia mutoto wako afanye hivyo pia.​—1 Sam. 1:27, 28; 2 Tim. 3:14, 15.

16. Namna gani wazazi fulani wamesaidia watoto wao wajiwekee miradi ya kiroho, na namna gani jambo hilo limewaletea faida?

16 Bibi na bwana fulani wa Amerika, walisaidia watoto wao wajiwekee miradi ya kiroho. Bwana anasema hivi: “Mbele watoto wetu waanze kutembea na kusema, tuliwaelezea furaha ya kuwa painia na kutumikia kutaniko. Sasa wamejiwekea muradi huo. Kuwa na miradi ya kiroho na kuitimiza kunasaidia watoto wetu washinde vishawishi vya ulimwengu wa Shetani na wakaze akili yao juu ya kazi ya Yehova.” Ndugu mumoja mwenye kuwa na watoto wawili, aliandika hivi: “Wazazi wengi wanatumia nguvu nyingi na mali ili kusaidia watoto wao wafikie miradi yao katika mambo kama vile michezo, mambo ya kujifurahisha, na masomo. Ni jambo la maana zaidi kutumia nguvu nyingi na mali ili kusaidia watoto wetu wafikie miradi yenye itawasaidia waendelee kuwa na urafiki muzuri pamoja na Yehova. Tumepata furaha kubwa kuona watoto wetu wanafikia miradi yao ya kiroho, lakini pia kwa sababu tumewasaidia kufanya hivyo.” Unaweza kuwa hakika kuwa Mungu atabariki wazazi wenye kusaidia watoto wao wajiwekee na kufikia miradi ya kiroho.

KUONYESHA UHODARI KATIKA KUTANIKO

17. Toa mifano ya watu wenye wako na lazima ya kuonyesha uhodari katika kutaniko.

17 Tunapaswa pia kuonyesha uhodari katika kutaniko. Kwa mufano, wazee wako na lazima ya kuonyesha uhodari wakati wanafanya mambo ya hukumu ao wakati wanasaidia wale wenye kuwa na matatizo makubwa ya afya yenye yanaomba kuhangaikiwa haraka. Wazee fulani wanatembelea magereza ili kutimiza mahitaji ya kiroho ya wafungwa. Tuseme nini juu ya dada wenye hawajaolewa? Wako sasa na nafasi nyingi za kupanua utumishi wao kwa kufanya kazi ya upainia, kuhamia mahali kwenye kuwa lazima kubwa ya wahubiri, kutumika katika programu ya Ujenzi wa Mahali, na kusoma Masomo kwa Ajili ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Hata wamoja wanaweza kusoma Masomo ya Gileadi.

18. Namna gani dada wenye kukomaa wanaweza kuonyesha uhodari?

18 Wanawake wenye kukomaa ni baraka kwa kutaniko. Tunawapenda sana dada hao wapendwa! Wamoja hawawezi kufanya tena mengi katika kazi ya Mungu kama vile zamani, lakini wangali wanaweza kuonyesha uhodari na kutenda. (Soma Tito 2:3-5.) Kwa mufano, dada mwenye kukomaa anapaswa kuonyesha ujasiri ikiwa anaombwa kuzungumuza na dada kijana juu ya kuvaa kwa kiasi. Hatamufokea dada huyo juu ya namna yake ya kuchagua nguo za kuvaa, lakini anaweza kumutia moyo afikirie namna manguo yenye anachagua yanaweza kuwa na matokeo juu ya wengine. (1 Tim. 2:9, 10) Kuonyesha upendo katika njia hiyo kunaweza kuleta matokeo ya muzuri.

19. (a) Namna gani ndugu wenye kubatizwa wanaweza kuonyesha uhodari? (b) Namna gani andiko la Wafilipi 2:13 na 4:13 linaweza kusaidia ndugu wakuwe na uhodari?

19 Wengine wenye wanapaswa kuonyesha uhodari na kutenda ni ndugu wenye kubatizwa. Wanaume wenye kuwa na uhodari wenye kuwa tayari kutimiza madaraka zaidi ni baraka kwa kutaniko. (1 Tim. 3:1) Hata hivyo, wamoja wanaweza kusita kujikaza kufikia madaraka. Pengine ndugu alifanya makosa zamani, na sasa anajisikia kuwa hastahili kuwa mutumishi wa huduma ao muzee. Ndugu mwingine anaweza kujisikia kuwa hana uwezo wa kutimiza mugawo fulani. Ikiwa unajisikia hivyo, Yehova anaweza kukusaidia kuwa na uhodari. (Soma Wafilipi 2:13; 4:13.) Kumbuka kuwa, wakati fulani, Musa aliona kuwa hawezi kutimiza mugawo fulani. (Kut. 3:11) Lakini, Yehova alimusaidia, na kisha wakati fulani, Musa alikuwa na uhodari wa kutimiza kazi yake. Ndugu mwenye kubatizwa anaweza kuonyesha uhodari kama huo kwa kumuomba Mungu musaada katika sala na kwa kusoma Biblia kila siku. Kutafakari juu ya mifano ya watu wenye walionyesha uhodari kunaweza kumusaidia pia. Kwa unyenyekevu, anaweza kuomba wazee wamuzoeze na kuwa tayari kusaidia katika njia yoyote yenye kuhitajiwa. Tunatia moyo ndugu wote wenye kubatizwa waonyeshe uhodari na kutumika kwa bidii kwa ajili ya kutaniko!

“YEHOVA . . . YUKO PAMOJA NAWE”

20, 21. (a) Daudi alimutolea Sulemani uhakika gani? (b) Tunaweza kuwa hakika juu ya jambo gani?

20 Mufalme Daudi alimukumbusha Sulemani kuwa Yehova angekuwa pamoja naye mupaka kazi ya kujenga hekalu imalizike. (1 Nya. 28:20) Sulemani aliweka maneno hayo ya baba yake katika moyo na akili yake, kwa hiyo, hata kama alikuwa kijana na hakukuwa na uzoefu, hakuacha mambo hayo yamuzuie kufanya kazi. Alionyesha uhodari mukubwa, akatenda, na kwa musaada wa Yehova alimaliza kazi ya kujenga hekalu la muzuri sana katika miaka saba na nusu.

21 Kama vile Yehova alimusaidia Sulemani, anaweza kutusaidia tuonyeshe uhodari na tutimize kazi yetu, katika familia yetu na katika kutaniko. (Isa. 41:10, 13) Wakati tunaonyesha uhodari katika ibada yetu kwa Yehova, tunaweza kuwa hakika kuwa atatubariki sasa na wakati wenye kuja. Kwa hiyo, ‘ukuwe hodari . . . na utende.’

^ fu. 12 Unaweza kupata mashauri fulani ya maana ya kukusaidia kujiwekea miradi ya kiroho katika habari yenye kichwa “Tumia Miradi ya Kiroho ili Kumtukuza Muumba Wako,” katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 7, 2004.