Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Uige Marafiki wa Sana wa Yehova

Uige Marafiki wa Sana wa Yehova

‘Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wanaomuogopa.’ZABURI 25:14.

NYIMBO: 106, 118

1-3. (a) Sababu gani tunaweza kuwa hakika kwamba tunaweza kuwa marafiki wa Mungu? (b) Tutazungumuzia watu gani katika habari hii?

BIBLIA inataja wazi-wazi Abrahamu kuwa rafiki ya Mungu. (Isaya 41:8; Yakobo 2:23) Ni yeye tu ndiye anaitwa moja kwa moja rafiki ya Mungu. Je, hilo linamaanisha kwamba ni Abrahamu tu ndiye alikuwa rafiki ya Yehova? Hapana. Biblia inaonyesha kwamba sisi wote tunaweza kuwa na pendeleo hilo.

2 Neno la Mungu linazungumuzia wanaume na wanawake wengi waaminifu wenye walimuogopa Yehova, walionyesha imani, na wakakuwa marafiki wake wa sana. (Soma Zaburi 25:14.) Wako kati ya ‘wingu kubwa la mashahidi’ lenye mutume Paulo alizungumuzia. Watu hao wote walikuwa marafiki wa Mungu.—Waebrania 12:1.

3 Tuzungumuzie basi kwa uangalifu watatu kati ya marafiki wa Yehova wenye Biblia inazungumuzia: (1) Ruthu, kijana mujane muaminifu wa Moabu, (2) Hezekia, mufalme muaminifu wa Yuda, na (3) Maria, mama ya Yesu, mwanamuke munyenyekevu. Namna kila mumoja wao alifikia kuwa rafiki ya Mungu inaweza kutufundisha nini?

ALIONYESHA UPENDO MUSHIKAMANIFU

4, 5. Ruthu alipaswa kuchukua uamuzi gani muzito, na sababu gani uamuzi huo ulikuwa muzito sana? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

4 Naomi, pamoja na Ruthu na Orpa, binti zake wakwe, walikuwa katika safari yao murefu kutoka Moabu kuenda Israeli. Kisha kusafiri kwa muda fulani, Orpa aliamua kurudia Moabu. Lakini Naomi aliendelea na safari yake ya kurudia katika Israeli, inchi yake. Ruthu aliamua kufanya nini? Alipaswa kuchukua uamuzi muzito sana. Je, angerudia kuishi pamoja na watu wa familia yake huko Moabu, ao angebakia pamoja na Naomi, mama mukwe wake, na kusafiri pamoja naye kuenda Bethlehemu?—Ruthu 1:1-8, 14.

5 Watu wa familia ya Ruthu waliishi Moabu. Angerudia kwa watu wa familia yake, na pengine wangeendelea kumusaidia. Alijua watu wa Moabu, luga yao, na namna yao ya kuishi. Naomi hakuahidi Ruthu kwamba angepata mambo hayo huko Bethlehemu. Pia Naomi aliogopa kwamba Ruthu hangepata mwanaume wa kumuoa ao nyumba yenye angeishi ndani. Kwa hiyo, Naomi alimuambia arudie Moabu. Kama vile tuliona, Orpa ‘alirudia kwa watu wake na kwa miungu yake.’ (Ruthu 1:9-15) Lakini Ruthu alikataa kurudia kwa watu wake na miungu yao ya uongo.

6. (a) Ruthu alichukua uamuzi gani wenye hekima? (b) Sababu gani Boazi alisema kwamba Ruthu alitafuta ulinzi chini ya mabawa ya Yehova?

6 Pengine Ruthu alijifunza juu ya Yehova kupitia bwana yake ao kupitia Naomi. Alijifunza kwamba Yehova haiko kama miungu ya Moabu. Alimupenda Yehova na alijua kwamba anapaswa kumupenda na kumuabudu. Kwa hiyo, Ruthu alichukua uamuzi wenye hekima. Alimuambia Naomi hivi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu.” (Ruthu 1:16) Tunaguswa sana moyo wakati tunafikiria namna Ruthu alimupenda Naomi. Lakini jambo lenye kushangaza sana ni namna Ruthu alimupenda Yehova. Jambo hilo lilimushangaza pia Boazi. Kisha wakati fulani, alimusifu Ruthu kwa sababu ‘alitafuta kimbilio chini ya mabawa ya Yehova.’ (Soma Ruthu 2:12.) Maneno yenye Boazi alisema yanatukumbusha namna kitoto cha ndege kinatafuta ulinzi chini ya mabawa ya wazazi wake. (Zaburi 36:7; 91:1-4) Vilevile, Yehova alimulinda Ruthu kwa upendo na alimubariki kwa sababu ya imani yake. Ruthu hakusikitika hata kidogo kwa sababu ya uamuzi wenye alichukua.

7. Ni nini inaweza kusaidia wale wenye kuogopa kutoa maisha yao kwa Yehova?

7 Watu wengi wanajifunza juu ya Yehova lakini hawatafute ulinzi wake. Wanaogopa kutoa maisha yao kwa Yehova na kubatizwa. Ikiwa unajisikia hivyo, ufikirie sababu zenye kukufanya uogope. Kila mutu anatumikia mungu mwenye anapenda. (Yoshua 24:15) Kumutumikia Mungu wa kweli ndiyo uamuzi wenye hekima. Wakati unajitoa kwa Yehova, unaonyesha kwamba unaamini kama atakuwa kimbilio lako. Na atakusaidia uendelee kumutumikia hata kama unaweza kuwa na magumu fulani. Mungu alimusaidia pia Ruthu.

‘ALIENDELEA KUSHIKAMANA NA YEHOVA’

8. Hezekia alikomaa katika hali gani? Eleza.

8 Namna Hezekia alikomaa ilikuwa tofauti sana na namna Ruthu alikomaa. Hezekia alikuwa katika taifa lenye kutolewa kwa Mungu. Lakini Waisraeli wote hawakuendelea kuwa waaminifu. Mufalme Ahazi, baba ya Hezekia, alikuwa mubaya. Alizarau hekalu la Mungu na kuchochea watu waabudu miungu mingine. Ahazi alifikia hata kutoa ndugu fulani za Hezekia ili wachomwe wangali wazima kwa ajili ya mungu wa uongo. Wakati Hezekia alikuwa mutoto, maisha yake ilikuwa katika hatari!—2 Wafalme 16:2-4, 10-17; 2 Mambo ya Nyakati 28:1-3.

9, 10. (a) Sababu gani Hezekia angeweza kukasirika haraka? (b) Sababu gani hatupaswe kumukasirikia Mungu? (c) Sababu gani hatupaswe kufikiri kwamba namna tulikomaa inaweza kufanya tukuwe watu wazuri ao wabaya?

9 Mufano mubaya wa Ahazi ungeweza kumuchochea Hezekia amukasirikie Yehova. Leo, watu fulani wenye wamepata magumu madogo sana kuliko ya Hezekia, wanawaza kwamba wako na haki ya kumukasirikia Yehova ao tengenezo lake. (Methali 19:3) Wengine wanawaza kwamba hali mubaya ya familia yao inaweza kuwafanya wakuwe na maisha mabaya ao wafanye pia makosa kama wazazi wao. (Ezekieli 18:2, 3) Lakini, mawazo hayo ni ya kweli?

10 Maisha ya Hezekia yanaonyesha kwamba jibu la ulizo hilo ni hapana! Hakuna hata jambo moja lenye linaweza kutufanya tumukasirikie Yehova. Haletee watu mateso. (Ayubu 34:10) Ni kweli kwamba wazazi wanaweza kufundisha watoto wao kufanya mambo mazuri ao mabaya. (Methali 22:6; Wakolosai 3:21) Lakini hilo halimaanishe kwamba namna tulikomaa katika familia yetu itaonyesha ikiwa tutakuwa watu wa namna gani. Sababu gani? Kwa sababu Yehova ametupatia zawadi ya uhuru wa kuchagua, ni kusema, uwezo wa kuchagua kati ya mema na mabaya. (Kumbukumbu la Torati 30:19) Namna gani Hezekia alitumia zawadi hiyo ya maana sana?

Vijana wengi wanakubali kweli hata kama walikomalia katika familia zenye kuwa na hali ya mubaya (Picha hii inapatana na fungu la 9, 10)

11. Ni nini ilimufanya Hezekia akuwe kati ya wafalme wazuri zaidi wa Yuda?

11 Baba ya Hezekia alikuwa kati ya wafalme wabaya zaidi wa Yuda; lakini Hezekia alikuwa kati ya wafalme wazuri zaidi. (Soma 2 Wafalme 18:5, 6.) Alikataa kufuata mufano mubaya wa baba yake. Lakini, alichagua kusikiliza kwa uangalifu manabii wa Yehova kama vile Isaya, Mika, na Hosea. Alitii kabisa mashauri na maonyo yenye walimutolea. Hilo lilimuchochea atengeneze mambo mengi yenye baba yake aliharibisha. Alisafisha hekalu, alimuomba Mungu asamehe zambi za watu, na alivunja-vunja sanamu katika inchi yote. (2 Mambo ya Nyakati 29:1-11, 18-24; 31:1) Kisha, wakati Senakeribu, mufalme wa Asiria alitafuta kushambulia Yerusalemu, Hezekia alionyesha imani na hakuogopa hata kidogo. Alitegemea ulinzi wa Yehova na kutia nguvu watu wake. (2 Mambo ya Nyakati 32:7, 8) Wakati fulani Hezekia alikuwa na kiburi, lakini kisha Yehova kumushauria, alijinyenyekeza. (2 Mambo ya Nyakati 32:24-26) Ni wazi kwamba, Hezekia ni mufano muzuri zaidi wenye tunapaswa kuiga. Hakuacha hali ya familia yake iharibishe maisha yake. Lakini alionyesha kwamba alikuwa rafiki ya Yehova.

12. Kama vile Hezekia, namna gani watu wengi leo wamefikia kuwa marafiki wa Yehova?

12 Leo watu wa ulimwengu huu ni wakali na hawana upendo, na watoto wengi wanakomaa bila kuwa na wazazi wenye kuwapenda na kuwahangaikia. (2 Timotheo 3:1-5) Wakristo wengi leo wanatoka katika familia zenye kuwa na hali ya mubaya, lakini wamechagua kuwa marafiki wa Yehova. Kama vile Hezekia, wanaonyesha kwamba hali ya familia zao haiwezi kuchochea maisha yao ya wakati unaokuja. Mungu ametupatia zawadi ya uhuru wa kuchagua, na tunaweza kuchagua kumutumikia na kumutukuza kama vile Hezekia alifanya.

“TAZAMA! KIJAKAZI WA YEHOVA!”

13, 14. Sababu gani mugawo wenye Maria alipewa ulionekana kuwa mugumu sana, lakini alitenda namna gani kisha kusikia maneno ya Gabrieli?

13 Miaka mingi kisha Hezekia, kijana mwanamuke munyenyekevu mwenye kuitwa Maria alikuwa na urafiki wa pekee pamoja na Yehova, na alipewa mugawo wa pekee. Alipata mimba na kuzaa Mutoto wa Mungu na kumukomalisha! Yehova alimupenda Maria na kumutumainia; ndiyo sababu alimupatia pendeleo hilo kubwa sana. Lakini, Maria alitenda namna gani wakati alisikia kwa mara ya kwanza habari juu ya mugawo huo?

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!” (Picha hii inapatana na fungu la 13, 14)

14 Mara nyingi tunazungumuzia pendeleo kubwa lenye Maria alipewa. Lakini, pengine ni mambo gani ilimuogopesha? Kwa mufano, malaika Gabrieli alimuambia kwamba atapata mimba bila kulala na mwanaume. Lakini Gabrieli hakuelezea watu wa familia yake na majirani wake namna angepata mimba hiyo. Wangewaza nini? Namna gani angemuhakikishia Yosefu kwamba angali muaminifu kwake? Zaidi ya hilo, alikuwa na daraka kubwa la kulea Mutoto wa Mungu! Hatujue mambo yote yenye ilimuhangaisha Maria, lakini tunajua mambo yenye alisema kisha Gabrieli kuzungumuza naye. Alisema hivi: “Tazama! Kijakazi [mutumwa mwanamuke] wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako [neno yako].”—Luka 1:26-38.

15. Sababu gani imani ya Maria ni ya pekee?

15 Maria alikuwa na imani kubwa kabisa! Alikuwa tayari kufanya mambo yote yenye aliombwa, kama vile tu mutumwa mwanamuke. Alitumaini kwamba Yehova angemusaidia na kumulinda. Ni nini ilimusaidia Maria akuwe na imani yenye nguvu? Hatuzaliwe na imani. Lakini tunaweza kuipata ikiwa tunaitafuta na kumuomba Mungu abariki bidii yenye tunafanya. (Wagalatia 5:22; Waefeso 2:8) Maria alitumika sana ili kutia nguvu imani yake. Tunajua hilo namna gani? Tuone basi namna gani alisikiliza na mambo yenye alisema.

16. Ni nini inaonyesha kwamba Maria alikuwa musikilizaji muzuri?

16 Namna Maria alisikiliza. Biblia inasema kwamba tunapaswa kuwa wepesi kusikia, lakini tusikuwe wepesi kusema. (Yakobo 1:19) Maria alikuwa musikilizaji muzuri. Biblia inaonyesha kwamba alisikiliza kwa uangalifu mambo yenye alisikia, zaidi sana mambo yenye alijifunza juu ya Yehova. Alichukua wakati wa kufikiri sana juu ya mambo hayo ya maana. Kwa mufano, wakati Yesu alizaliwa, Maria alisikiliza ujumbe wa malaika wenye wachungaji walimuambia. Kisha, wakati Yesu alikuwa na miaka 12, alisikiliza jambo lenye kushangaza sana lenye Yesu alimuambia. Katika hali hizo mbili, Maria alisikiliza, alikumbuka, na alifikiri kwa uangalifu juu ya mambo yenye alikuwa amesikiliza.—Soma Luka 2:16-19, 49, 51.

17. Maneno ya Maria yanaweza kutufundisha nini?

17 Mambo yenye Maria alisema. Biblia haituambie mengi juu ya mambo yote yenye Maria alisema. Maneno yake marefu yanapatikana kwenye Luka 1:46-55. Maneno hayo yanaonyesha kwamba Maria alijua muzuri Maandishi ya Kiebrania. Namna gani? Maneno ya Maria yanafanana na maneno ya sala ya Hana, mama ya Samweli. (1 Samweli 2:1-10) Inaonekana kwamba katika maneno yake, Maria alitaja Maandiko matakatifu mara 20. Ni wazi kwamba alifurahia kuzungumuzia kweli zenye alikuwa amejifunza kutoka kwa Yehova, Rafiki yake mukubwa.

18. Namna gani tunaweza kuiga imani ya Maria?

18 Kama vile Maria, wakati fulani tunaweza kuona kwamba ni vigumu kutimiza migawo fulani yenye Yehova anatupatia. Tuige basi mufano wake, tukubali migawo hiyo kwa unyenyekevu, na tutumaini kwamba Yehova atatusaidia. Tunaweza pia kuiga imani ya Maria ikiwa tunamusikiliza Yehova kwa uangalifu na kufikiri sana juu ya mambo yenye tumejifunza juu yake na mambo yenye amepanga kufanya. Tukifanya hivyo, tunaweza kufurahia kuelezea wengine mambo yenye tumejifunza.—Zaburi 77:11, 12; Luka 8:18; Waroma 10:15.

19. Ikiwa tunaiga imani yenye nguvu ya watu wenye kuzungumuziwa katika Biblia, tunaweza kuwa hakika na jambo gani?

19 Ni wazi kwamba Ruthu, Hezekia, na Maria walikuwa marafiki wa Yehova kama vile tu Abrahamu. Walikuwa kati ya “wingu kubwa la mashahidi” wenye wamepata pia pendeleo la kuwa marafiki wa Mungu. Tuendelee basi kuiga imani yenye nguvu yenye watu hao walionyesha. (Waebrania 6:11, 12) Ikiwa tunafanya hivyo, tunaweza kungojea kwa hamu kupata zawadi ya kuwa marafiki wa Yehova milele!