Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unapata Faida Kabisa Katika Chakula cha Kiroho Chenye Yehova Anatupatia?

Unapata Faida Kabisa Katika Chakula cha Kiroho Chenye Yehova Anatupatia?

“Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi [upate faida] mwenyewe.”ISAYA 48:17.

NYIMBO: 117, 114

1, 2. (a) Namna gani Mashahidi wa Yehova wanaona Biblia? (b) Unapenda vitabu gani vya Biblia?

SISI Mashahidi wa Yehova tunapenda Biblia. Inatupatia kitulizo, tumaini, na mafundisho yenye tunaweza kutumainia. (Waroma 15:4) Kitabu hicho hakina mawazo ya wanadamu lakini ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

2 Inawezekana sisi wote tuko na vitabu fulani vya Biblia vyenye tunapenda sana. Watu fulani wanapenda vitabu vya Injili kwa sababu vinazungumuzia sifa za muzuri sana za Yehova zenye Yesu alionyesha. (Yohana 14:9) Wengine wanafurahia vitabu vya unabii kama vile kitabu cha Ufunuo, chenye kutuonyesha “mambo ambayo lazima yatendeke upesi.” (Ufunuo 1:1) Watu fulani wanapata kitulizo wakati wanasoma Zaburi, na wengine wanafurahia mashauri ya muzuri yenye kupatikana katika kitabu cha Methali. Kwa kweli, Biblia ni kitabu kwa ajili ya watu wote.

3, 4. (a) Namna gani tunaona vichapo vyetu? (b) Ni vichapo gani tunapata vyenye kuandikwa kwa ajili ya vikundi fulani vya watu?

3 Kwa kuwa tunapenda Biblia, tunapenda pia vichapo vyetu kwa sababu vinazungumuzia Neno la Mungu. Vitabu, broshua, magazeti, na vichapo vingine vyote vyenye tunapata ni chakula cha kiroho chenye Yehova anatupatia. Vinatusaidia tumukaribie Yehova na kutia nguvu imani yetu.—Tito 2:2.

4 Vichapo vyetu vingi vinaandikwa kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova wote. Lakini, kuko vichapo fulani vyenye kuandikwa kwa ajili ya kikundi fulani cha watu, kama vile vijana ao wazazi. Habari na video nyingi zenye kuwa kwenye adresi yetu ya Internete zinatayarishwa zaidi sana kwa ajili ya watu wenye hawako Mashahidi wa Yehova. Habari hizo za namna mbalimbali zinaonyesha kama Yehova ametimiza ahadi yake ya kupatia watu wote mafundisho mengi.—Isaya 25:6.

5. Tunaweza kuwa hakika kama Yehova anafurahi kuona nini?

5 Wengi kati yetu wanaweza kupenda kupata wakati mwingi wa kusoma Biblia na vichapo vyetu. Lakini, hatuwezi kupitisha kila mara wakati uleule ili kujifunza kila kichapo chenye tunapata. Tunaweza kuwa hakika kama Yehova anafurahi wakati anaona tunatumia wakati wetu kwa hekima ili kusoma na kujifunza Biblia na vichapo vyetu. (Waefeso 5:15, 16) Lakini, tunapaswa kuwa waangalifu ili tuepuke hatari fulani. Ni hatari gani?

6. Ni nini inaweza kutuzuia kupata faida katika chakula cha kiroho chenye Yehova anatupatia?

6 Ikiwa hatuko waangalifu, tunaweza kufikiri kama vitabu fulani vya Biblia ao vichapo fulani havituhusu ao havituangalie. Kwa mufano, tutafanya nini ikiwa kitabu fulani cha Biblia kinaonekana kuwa hakina mafaa kwetu? Ao tutafanya nini ikiwa kichapo fulani hakikuandikwa kabisa kwa ajili yetu? Tunasoma tu mbiombio habari hizo ao tunaepuka kabisa kuzisoma? Ikiwa tunafanya hivyo, tunaweza kukosa habari za maana zenye zinaweza kutuletea faida. Namna gani tunaweza kuepuka hatari hiyo? Tunapaswa kukumbuka kama habari zote zenye tunapata zinatoka kwa Yehova. Biblia inasema hivi: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.” (Isaya 48:17) Katika habari hii, tutazungumuzia mashauri tatu ya kutusaidia tupate faida katika chakula chote cha kiroho chenye Yehova anatupatia.

MASHAURI YA KUKUSAIDIA UPATE FAIDA KATIKA USOMAJI WA BIBLIA

7. Sababu gani tunapaswa kuwa na mawazo ya muzuri wakati tunasoma Biblia?

7 Ukuwe na mawazo ya muzuri wakati unasoma. Ni kweli kama vitabu fulani vya Biblia viliandikwa kwa ajili ya mutu ao kikundi fulani cha watu. Lakini, Biblia inasema wazi kama “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” (2 Timotheo 3:16) Ndiyo sababu tunapaswa kuwa na mawazo ya muzuri wakati tunasoma Biblia. Ndugu mumoja anakumbuka kama anaweza kujifunza mambo mengi katika habari moja tu ya Biblia. Jambo hilo linamusaidia avumbue mambo yenye hayaonyeshwe waziwazi. Kwa hiyo, mbele ya kusoma Biblia, tunapaswa kumuomba Yehova atusaidie tukuwe na hekima na mawazo ya muzuri ili tuelewe mambo yenye anapenda tujifunze.—Ezra 7:10; soma Yakobo 1:5.

Unajikaza kupata faida kabisa katika usomaji wako wa Biblia? (Picha hii inapatana na fungu la 7)

8, 9. (a) Tunaweza kujiuliza maulizo gani wakati tunasoma Biblia? (b) Mambo yenye Yehova anaomba wazee Wakristo watimize yanatufundisha nini juu yake?

8 Ujiulize maulizo. Wakati unasoma Biblia, usimamishe kwanza usomaji na ujiulize maulizo haya: ‘Habari hii inanifundisha nini juu ya Yehova? Namna gani ninaweza kutumikisha habari hii katika maisha yangu? Namna gani ninaweza kutumikisha habari hii ili kusaidia wengine?’ Wakati tunafikiri sana juu ya maulizo hayo, tutapata faida nyingi katika usomaji wetu wa Biblia. Tuzungumuzie mufano moja. Biblia inataja mambo fulani yenye wazee Wakristo wanapaswa kutimiza. (Soma 1 Timotheo 3:2-7.) Lakini wengi kati yetu hawako wazee wa kutaniko; kwa hiyo, tunaweza kuwaza kama habari hiyo haiwezi kutusaidia katika njia fulani. Hata hivyo, tutumie maulizo tatu yenye tumetaja hapo juu ili tuone namna mambo hayo yenye wazee wanapaswa kutimiza yanaweza kutusaidia sisi wote.

9 “Habari hii inanifundisha nini juu ya Yehova?” Yehova ametuonyesha mambo yenye anaomba wazee wa kutaniko watimize. Anaweka kanuni za juu kwa ajili ya wanaume wenye kuchunga kutaniko. Hilo linaonyesha kama kutaniko ni la maana sana kwa Yehova. Biblia inasema kama aliuza kutaniko “kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Matendo 20:28) Kwa hiyo, Yehova anaomba wazee wa kutaniko wakuwe mifano ya muzuri, na watatoa hesabu kwake juu ya namna wanatendea ndugu na dada katika kutaniko. Yehova anataka tujisikie salama chini ya ulinzi wao. (Isaya 32:1, 2) Wakati tunasoma mambo hayo, tunaona kabisa kama Yehova anatuhangaikia sana.

Yehova anataka kila mumoja wetu akuwe na usawaziko na atumikishe utambuzi

10, 11. (a) Wakati tunasoma mambo yenye wazee wanaombwa kutimiza, namna gani tunaweza kutumikisha habari hiyo katika maisha yetu? (b) Namna gani tunaweza kutumikisha habari hiyo ili kusaidia wengine?

10 “Namna gani ninaweza kutumikisha habari hii katika maisha yangu?” Ikiwa tayari uko muzee wa kutaniko, unapaswa kujikumbusha kwa ukawaida mambo hayo na kujikaza kufanya maendeleo. Ikiwa ‘unajitahidi [unajikaza] kufikia cheo cha mwangalizi [muzee],’ unapaswa kujikaza ili kutimiza mambo hayo kulingana na uwezo wako. (1 Timotheo 3:1) Lakini Wakristo wote wanaweza kujifunza jambo fulani kwa kuchunguza mambo yenye wazee wanaombwa kutimiza. Kwa mufano, Yehova anataka kila mumoja wetu akuwe na usawaziko na atumikishe utambuzi. (Wafilipi 4:5; 1 Petro 4:7) Wakati wazee wanakuwa “vielelezo [mifano] kwa kundi,” tunaweza kuiga mufano wao na ‘imani yao.’—1 Petro 5:3; Waebrania 13:7.

11 “Namna gani ninaweza kutumikisha habari hii ili kusaidia wengine?” Tunaweza kutumikisha mambo hayo yote ili kusaidia wanafunzi wa Biblia na watu wengine wenye kupendezwa na kweli waelewe kama wazee hawako kama viongozi wa dini zingine. Mambo hayo yanaweza pia kutusaidia kukumbuka kazi ngumu yenye wazee wanafanya katika kutaniko. Na kukumbuka kazi yao ngumu kutatuchochea tuheshimie ndugu hao. (1 Wathesalonike 5:12) Kama tunawaheshimia sana, watakuwa na furaha nyingi katika kazi yao.—Waebrania 13:17.

12, 13. (a) Wakati tunatumikisha vyombo vyenye tuko navyo, tunaweza kutafuta habari gani? (b) Toa mufano ili kuonyesha namna habari zenye kuzungumuziwa katika andiko fulani zinaweza kutusaidia kujifunza mambo yenye hayaonyeshwe waziwazi.

12 Utafute habari. Wakati tunajifunza Biblia, tunaweza kutafuta majibu ya maulizo yenye kufuata:

  • Ni nani aliandika kitabu hiki cha Biblia?

  • Kiliandikwa wapi na wakati gani?

  • Ni mambo gani ya maana yalikuwa yanatokea wakati kiliandikwa?

Majibu ya maulizo kama hayo yanaweza kutusaidia tujifunze mambo yenye hayaonyeshwe waziwazi katika habari yenye tunajifunza.

13 Kwa mufano, andiko la Ezekieli 14:13, 14 linasema hivi: “Ikiwa [inchi] itanitendea zambi kwa kutenda kwa kukosa uaminifu, pia nitanyoosha mukono wangu juu yake na kuivunjia fimbo ambazo mikate ya muviringo unaninginizwa, nami nitaleta njaa juu yake na kumukatilia mbali mutu wa udongo na munyama wa kufugwa kutoka ndani yake. ‘Na kama watu hawa watatu wangekuwa katikati yake, Noa, Danieli na Ayubu, wao wenyewe kwa sababu ya uadilifu wao wangeikomboa nafsi yao,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu [Mamlaka Makubwa Zaidi] Yehova.” Ikiwa tunatafuta habari, tutaona kama Ezekieli aliandika maneno hayo miaka karibu 612 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. Noa na Ayubu walikuwa wamekwisha kufa kumepita miaka mingi sana, lakini Yehova aliendelea kukumbuka uaminifu wao. Danieli yeye alikuwa angali muzima. Inawezekana alikuwa na miaka 20 hivi wakati Yehova alisema kwamba alikuwa muaminifu kama vile Noa na Ayubu. Habari hiyo inatufundisha nini? Yehova anaona watumishi wake wote, na wote ni wa maana sana kwake, hata vijana.—Zaburi 148:12-14.

PATA FAIDA KATIKA VICHAPO MBALIMBALI

14. Habari nyingi zenye kuchapishwa kwa ajili ya vijana zinawasaidia namna gani, na namna gani wengine wanaweza kupata faida katika habari hizo? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

14 Vichapo kwa ajili ya vijana. Tumejifunza kama tunaweza kupata faida katika vitabu vyote vya Biblia. Vilevile, tunaweza kupata faida katika vichapo vyetu vyote. Tuzungumuzie mifano fulani. Katika miaka ya hivi karibuni, Yehova ametolea vijana habari nyingi sana. [1] (Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.) Habari hizo zinawasaidia kupambana na mikazo kwenye masomo na magumu yenye wanapata wakati wanaendelea kukomaa. Lakini, namna gani sisi wote tunaweza kupata faida kwa kusoma habari na vitabu vyenye kuandikwa kwa ajili ya vijana? Wakati tunasoma habari hizo, tunajua magumu yenye vijana wanapambana nayo na tunaweza kujua namna ya kuwasaidia na kuwatia moyo.

Wakristo wenye kukomaa hawapaswe kuacha kiburi kiwazuie kusoma habari zenye kuandikwa kwa ajili ya vijana

15. Sababu gani Wakristo wenye kukomaa wanapaswa kupendezwa na habari zenye kuandikwa kwa ajili ya vijana?

15 Wakristo wenye kukomaa hawapaswe kuacha kiburi kiwazuie kusoma habari zenye kuandikwa kwa ajili ya vijana. Magumu mengi yenye kuzungumuziwa katika habari hizo yanapata Wakristo wote. Kwa mufano, sisi wote tunapaswa kutetea mambo yenye tunaamini, kuzuia hasira yetu, kupambana na mikazo kutoka kwa watu wengine na kuepuka marafiki wabaya na mambo mabaya ya kujifurahisha. Kwa hiyo, hata kama vichapo hivyo viliandikwa kwa ajili ya vijana, habari zenye kuwa ndani zinatoka katika Biblia, na Wakristo wote wanaweza kupata faida kwa kusoma habari hizo.

16. Vichapo vyetu vinasaidia pia vijana kufanya nini?

16 Vichapo vyenye kuandikwa kwa ajili ya vijana vinaweza pia kuwasaidia kutia nguvu urafiki wao pamoja na Yehova. (Soma Mhubiri 12:1, 13.) Na watu wenye kukomaa wanaweza pia kupata faida katika vichapo hivyo. Kwa mufano, gazeti Amuka! la Mwezi wa 4, 2009 lilikuwa na habari yenye kichwa “Vijana Huuliza . . . Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kusoma Biblia?” Habari hiyo ilikuwa na mashauri mengi ya muzuri na kisanduku chenye kingeweza kukatwa, kuchungwa, na kutumiwa kwa ajili ya funzo. Watu wenye kukomaa walipata faida katika habari hiyo? Mwanamuke mumoja mwenye kuwa na watoto alisema kama sikuzote kusoma Biblia lilikuwa jambo ngumu kwake. Lakini alitumikisha mashauri yenye kupatikana katika habari hiyo na leo anangojea kwa hamu usomaji wake wa Biblia. Anasema kama anafurahia kuona namna vitabu vya Biblia vinapatana na vinafanyiza picha ya muzuri. Aliongezea hivi: “Sasa, ninafurahia sana kusoma Biblia kuliko wakati mwingine wowote.”

17, 18. Namna gani tunaweza kupata faida kwa kusoma habari zenye kuandikwa kwa ajili ya watu wote? Toa mufano.

17 Vichapo kwa ajili ya watu wote. Tangu mwaka wa 2008, tulifurahi kupata Munara wa Mulinzi gazeti la funzo. Gazeti hilo linaandikwa zaidi sana kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova, lakini tuko pia na magazeti yenye kuandikwa zaidi sana kwa ajili ya watu wote. Namna gani tunaweza kupata faida katika magazeti hayo pia? Tukamate mufano moja. Wakati unaalika mutu fulani kwenye Jumba la Ufalme na mutu huyo anakuja, jambo hilo linakufurahisha. Wakati musemaji anatoa hotuba, unafikiria mutu mwenye ulialika. Unafikiria namna mutu huyo anajisikia juu ya habari yenye kufundishwa na namna inaweza kumusaidia afanye mabadiliko katika maisha yake. Kwa hiyo, habari hiyo inakugusa moyo na inakufanya ukuwe mwenye shukrani hata zaidi.

18 Tunaweza pia kujisikia hivyo wakati tunasoma vichapo vyenye kuandikwa kwa ajili ya watu wote. Kwa mufano, Munara wa Mulinzi gazeti la watu wote na habari zenye kupatikana kwenye adresi yetu ya Internete jw.org vinatumia maneno mepesi ili kufasiria mafundisho ya Biblia. Wakati tunasoma habari hizo, tunaelewa na kupenda zaidi mafundisho ya Biblia yenye tumekwisha kujua muzuri. Pia, tunaweza kujifunza njia za mupya za kuelezea wengine mambo yenye tunaamini. Vilevile, gazeti Amuka! linatusaidia kuamini kabisa kama kuko Muumbaji. Linatusaidia pia kujua namna ya kufasiria wengine mambo yenye tunaamini.—Soma 1 Petro 3:15.

19. Namna gani tunaweza kumuonyesha Yehova shukrani kwa ajili ya chakula cha kiroho chenye anatupatia?

19 Kwa kweli, Yehova ametupatia mashauri na mafundisho mengi kwa faida yetu. (Mathayo 5:3) Tuendelee basi kusoma na kutumikisha habari zote zenye ametupatia. Ikiwa tunafanya hivyo, tutapata faida na tutaonyesha Yehova kama tuko wenye shukrani kwa ajili ya chakula chote cha kiroho chenye anatupatia.—Isaya 48:17.

^ [1] (fungu la 14) Kati ya habari hizo, kuna kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1 na la 2, na habari zenye kichwa “Vijana Huuliza,” zenye sasa zinapatikana tu kwenye Internete.