Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sifa Yenye Kumupendeza Mungu ya Maana Sana Kupita Alimasi

Sifa Yenye Kumupendeza Mungu ya Maana Sana Kupita Alimasi

Watu wanaona alimasi (diamant) kuwa majiwe ya bei sana. Alimasi fulani ziko na bei ya mamilioni ya dola. Lakini, kuko jambo fulani lenye Mungu anaona kuwa la maana sana kupita alimasi ao majiwe mengine ya bei?

Haykanush, muhubiri mwenye hajabatizwa wa inchi ya Armenia, aliokota pasipoti (passeport) karibu na nyumba yake. Ndani ya pasipoti hiyo mulikuwa karte za banki na feza nyingi. Alimuambia bwana yake, ambaye pia alikuwa muhubiri mwenye hajabatizwa, kama aliokota pasipoti hiyo.

Bibi na bwana hao walikuwa na magumu sana ya kupata feza na walikuwa na deni. Lakini waliamua kupeleka feza hizo kwenye adresi yenye ilikuwa katika pasipoti hiyo. Mwanaume mwenye alipoteza feza hizo, yeye na familia yake walishangaa. Haykanush na bwana yake walieleza kama mambo yenye walikuwa wanajifunza katika Biblia ndiyo yaliwachochea watende kwa uaminifu. Kisha, walitumia nafasi hiyo ili kuzungumuza juu ya Mashahidi wa Yehova na kutolea familia hiyo vichapo fulani.

Familia hiyo ilitaka kumupatia Haykanush zawadi ya feza fulani, lakini hakupenda kukamata feza hizo. Siku yenye ilifuata, mwanamuke huyo alitembelea Haykanush na bwana yake nyumbani kwao, na kuonyesha kama alikuwa mwenye shukrani sana, na alimukaza Haykanush akamate pete ya alimasi.

Kama familia hiyo, watu wengi wanaweza kushangaa juu ya uaminifu wenye Haykanush na bwana yake walionyesha. Lakini Yehova naye alishangaa? Namna gani Yehova aliona uaminifu wao? Uaminifu wao ulikuwa na faida yoyote?

SIFA ZENYE MAANA SANA KUPITA VITU VYA KIMWILI

Majibu ya maulizo hayo hayako magumu. Sababu gani? Kwa sababu watumishi wa Mungu wanajua kama kuiga sifa za Yehova ni jambo la maana sana kwake kuliko alimasi, zahabu, ao vitu vingine vya kimwili. Ndiyo, vitu vyenye Yehova anaona kuwa vya maana sana ni tofauti na vitu vyenye watu wengi wanaona kuwa vya maana sana. (Isaya 55:8, 9) Na watumishi wake wanaona kuwa bidii yenye wanafanya ili kuiga sifa za Yehova ni ya maana sana.

Mambo yenye Biblia inasema juu ya utambuzi na hekima yanaweza kutusaidia kuelewa jambo hilo. Methali 3:13-15 inasema hivi: ‘Mwenye furaha ni mutu ambaye amepata hekima, na mutu anayepata utambuzi; kwa maana kuwa nayo kama mapato ni bora kuliko kuwa na mapato ya feza na kuwa nayo kama mazao ni bora kuliko zahabu yenyewe. Ina samani kuliko marijani, na mapendezi yako mengine yote hayawezi kulinganishwa nayo.’ Kwa kweli, Yehova anapendezwa na sifa hizo kupita vitu vyote vya kimwili vya maana sana.

Tuseme nini juu ya sifa ya uaminifu?

Yehova mwenyewe ni muaminifu. ‘Hawezi kusema uongo.’ (Tito 1:2) Na wakati wa mitume, alimuongoza mutume Paulo kupitia roho yake ili aandikie Wakristo Waebrania hivi: ‘Muendelee kusali kwa ajili yetu, kwa maana sisi tuna uhakika kwamba tuna zamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu [kwa uaminifu] katika mambo yote.’—Waebrania 13:18.

Yesu alituachia mufano muzuri wa uaminifu. Kwa mufano, wakati Kuhani Mukubwa Kayafa alisema hivi: “Kwa Mungu aliye hai [mwenye kuishi] ninakuweka chini ya kiapo utuambie kama wewe ndiye Kristo Mwana wa Mungu!,” Yesu alikuwa muaminifu na alijitambulisha kuwa yeye ni Masiya. Alisema kweli hata kama alijua kwamba Sanhedrini ingemushitaki kuwa mukufuru (muasi) na kwamba hilo lingemufanya auawe.—Mathayo 26:63-67.

Halafu sisi? Ikiwa hali fulani inatuomba tusiseme kweli yote ao kubadilisha kweli ili tupate faida fulani ya kimwili, tutabakia waaminifu?

MAGUMU YA KUBAKIA MUAMINIFU

Inaweza kuwa vigumu kuwa muaminifu katika siku hizi za mwisho kwa sababu watu wengi ni “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa [feza].” (2 Timotheo 3:2) Wakati kunakuwa magumu ya kupata feza ao wakati inakuwa vigumu kupata kazi, watu wengi hawaone kuwa ni mubaya kuiba, ao kutenda kwa udanganyifu. Mawazo hayo yanaenea sana, na kwa hiyo, watu wengi wanaona kuwa njia moja tu ya kupata vitu vya kimwili ni kutenda kwa udanganyifu. Hata Wakristo fulani wamekamata maamuzi ya mubaya na kwa sababu ya “pato lisilo la haki” wamepoteza sifa yao muzuri katika kutaniko.—1 Timotheo 3:8; Tito 1:7.

Lakini, Wakristo wengi wanaiga mufano wa Yesu. Wanaelewa kama kuiga sifa za Mungu ndilo jambo la maana sana kupita utajiri ao faida yoyote. Ndiyo sababu vijana Wakristo hawaibe majibu ili waweze kwenye masomo. (Methali 20:23) Sikuzote, hatuwezi kupata zawadi kwa sababu ya uaminifu wetu kama vile Haykanush. Hata hivyo, Mungu anasema kama ni muzuri kuwa waaminifu, na sifa hiyo inatusaidia tukuwe na kitu cha maana sana, ni kusema, zamiri safi.

Mufano wa Gagik unaonyesha hilo. Anasema hivi: “Mbele nikuwe Mukristo, nilikuwa ninatumika katika kompanyi fulani. Mwenye kompanyi hiyo alikuwa anaepuka kulipa kodi (taxe) kwa kuonyesha faida kidogo tu ya kompanyi hiyo. Kwa sababu nilikuwa musimamizi wa kompanyi hiyo, niliombwa kufanya ‘makubaliano’ na mutu mwenye kulipisha kodi kwa kumupatia rushwa (kata-midomo) ili asiangalie mambo ya udanganyifu ya kompanyi yetu. Kwa hiyo, nilijulikana kuwa mutu mwenye kutenda kwa udanganyifu. Wakati nilijifunza kweli, nilikataa kuendelea kufanya hivyo, hata kama nilikuwa ninapata mushahara wa muzuri. Lakini, nilianzisha kompanyi yangu mwenyewe. Na siku tu ya kwanza, niliandikisha kisheria kompanyi yangu na nililipa kodi zote.”—2 Wakorintho 8:21.

Gagik anasema hivi: “Nilianza kupata nusu ya feza zenye nilikuwa ninapata mbele, kwa hiyo, ilikuwa vigumu kutimiza mambo ya lazima ya familia yangu. Lakini, leo niko na furaha zaidi. Niko na zamiri safi mbele ya Yehova. Ninaonyesha watoto wangu wawili wanaume mufano muzuri, na nimepata mapendeleo fulani katika kutaniko. Watu wenye kuchunguza mambo ya kodi na wengine wenye ninatumika pamoja nao wananijua sasa kuwa mutu muaminifu.”

YEHOVA ANATUSAIDIA

Yehova anapenda watu wenye kumuletea sifa kwa kuiga sifa zake zenye kupendeza sana, na pia sifa ya uaminifu. (Tito 2:10) Na wakati tunafanya hivyo, anaahidi kama atatusaidia. Alimuongoza Mufalme Daudi kusema hivi: ‘Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamuona mutu yeyote muadilifu [mwenye haki] akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mukate.’—Zaburi 37:25.

Mufano wa Ruthu, mwanamuke muaminifu, unaonyesha hivyo. Alishikamana na mama mukwe wake, Naomi, kuliko kumuacha kwa sababu alikuwa amezeeka. Ruthu alihamia Israeli, kwenye angeweza kumuabudu Mungu wa kweli. (Ruthu 1:16, 17) Alikuwa muaminifu na alitumika sana ili kukusanya masalio, kulingana na mupango wa Sheria juu ya watu masikini. Yehova hakuacha hata kidogo Ruthu na Naomi, kisha wakati fulani, Daudi naye alijionea kama Yehova haache watu wake. (Ruthu 2:2-18) Alimufanyia Ruthu mambo mengi zaidi kuliko kumupatia tu vitu vya kimwili. Alimuchagua ili akuwe kati ya watu wa kizazi cha Daudi na hata kizazi cha Masiya mwenye aliahidiwa!—Ruthu 4:13-17; Mathayo 1:5, 16.

Inaweza kuwa vigumu kwa watumishi fulani wa Yehova kupata feza za kutimiza mambo yao yote ya lazima. Lakini, kuliko kujikaza kutafuta njia nyepesi na ya udanganyifu, wanatumika sana na kwa bidii. Kwa kufanya hivyo, wanaonyesha kama sifa za Mungu zenye kupendeza sana, hata sifa ya uaminifu, ni za maana sana kuliko vitu vingine vyote vya kimwili.—Methali 12:24; Waefeso 4:28.

Kama vile Ruthu, Wakristo katika dunia yote wameonyesha imani kama Yehova ana nguvu za kuwasaidia. Wanatumainia kabisa Ule mwenye ametoa ahadi hii: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Waebrania 13:5) Yehova ameonyesha mara nyingi kama ana uwezo wa kusaidia wale wenye kuwa waaminifu sikuzote na atafanya hivyo. Ametimiza sikuzote ahadi yake ya kupatia watumishi wake mambo ya lazima.—Mathayo 6:33.

Ndiyo, wanadamu wanaweza kuona alimasi na vitu vingine vya kimwili kuwa vya maana sana. Lakini tunaweza kuwa hakika kama Baba yetu wa mbinguni anaona uaminifu na sifa zingine za muzuri kuwa za maana zaidi kupita majiwe yoyote ya bei!

Wakati tuko waaminifu, tunaweza kuwa na zamiri safi wakati tunazungumuza na watu katika mahubiri