Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 15

Maneno ya Mwisho ya Yesu Inaweza Kutufundisha Nini?

Maneno ya Mwisho ya Yesu Inaweza Kutufundisha Nini?

“Huyu ni Mwana wangu, mupendwa, mwenye nimekubali. Mumusikilize.”​—MT. 17:5.

WIMBO 17 “Ninataka”

KIFUPI CHA HABARI *

1-2. Yesu alikuwa mu hali gani wakati alisema maneno yake ya mwisho mbele akufe?

TUKO tarehe 14, Mwezi wa Nisani, mwaka wa 33 K.K.Y. Yesu anashitakiwa mambo ya uongo, na anahukumiwa juu ya mambo yenye hakufanya. Sasa, Yesu anaanza kuchekelewa, anapigwa mubaya, na ku mwisho, anatundikwa ku muti wa mateso. Misumari inaingia mu mikono na mu miguu yake. Wakati anapumua na wakati anasema, ni maumivu tu. Lakini, anapaswa tu kusema tena, juu mambo yenye atasema sasa ni ya maana sana.

2 Tuzungumuzie basi maneno yenye Yesu alisema wakati alikuwa ku muti wa mateso, mbele tu akufe, na tuone ni mambo gani ile maneno inaweza kutufundisha. Sasa, muache ‘tumusikilize.’​—Mt. 17:5.

“BABA, UWASAMEHE”

3. Wakati Yesu alisema: “Baba, uwasamehe,” alikuwa anazungumuzia nani?

3 Yesu alisema nini? Wakati alikuwa ku muti wa mateso, Yesu alisali hivi: “Baba, uwasamehe.” Asamehe nani? Maneno yenye kufuata inatupatia wazo: “Hawajue jambo lenye wanafanya.” (Lu. 23:33, 34) Pengine Yesu alikuwa anazungumuzia maaskari Waroma wenye walimupigilia misumari ku mikono na ku miguu. Hawakujua kabisa yeye ni nani. Inawezekana alikuwa anazungumuzia pia watu fulani wenye waliomba auawe, lakini wenye kisha wakati fulani, walifikia kumuamini. (Mdo. 2:36-38) Hakuna kitu ya mubaya yenye Yesu alifanya juu astahili kifo, lakini ile haikufanya akasirikie ao akatae kusamehe wale wenye walimutesa. (1 Pe. 2:23) Kuliko kufanya vile, alimuomba Yehova awasamehe.

4. Yesu alikuwa tayari kusamehe wapinzani wake. Ile inaweza kutufundisha nini?

4 Maneno ya Yesu inaweza kutufundisha nini? Kama Yesu, tunapaswa kuwa tayari kusamehe wengine. (Kol. 3:13) Watu fulani, hata watu wa familia yetu, pengine wanaweza kutupinga juu hawaelewe mambo yenye tunaamini na namna yetu ya kuishi. Pengine wanaweza kutusemea mambo ya uongo, kutupatisha haya mbele ya watu, kuharibu vichapo vyetu, ao hata kutuogopesha kama watatutendea mubaya. Kuliko kuendelea kukasirika, tumuombe Yehova asaidie wale wenye kutupinga wakubali kweli. (Mt. 5:44, 45) Wakati fulani, pengine tunaweza kuona kama ni nguvu kusamehe, zaidi sana kama wametutendea mubaya sana. Lakini, kama tunaendelea kukasirika na kuweka kinyongo, tunajiumiza siye wenyewe. Dada mumoja anafasiria hivi: “Natambua kama wakati nasamehe wengine, ile haionyeshe kama walikuwa na haki ya kunitendea mubaya, ao nilipenda wanitendee vile. Ile inaonyesha tu kama siwawekee tena kinyongo.” (Zb. 37:8) Wakati tunasamehe wengine, tunaonyesha kama hatupende kuacha makosa yenye walitutendea iendelee kutuhuzunisha ao kutukasirisha.​—Efe. 4:31, 32.

“UTAKUWA PAMOJA NA MIMI KATIKA PARADISO”

5. Yesu alimuahidi nini ule mutenda-mabaya mwenye alitundikwa pembeni yake, na juu ya nini alifanya vile?

5 Yesu alisema nini? Wakati Yesu alitundikwa, watenda-mabaya wawili pia walitundikwa pembeni yake. Ku mwanzo, wote wawili walikuwa wanamuchekelea. (Mt. 27:44) Kisha mumoja kati yao akaacha kufanya vile. Alifikia kutambua kama Yesu hakufanya “jambo lolote la mubaya.” (Lu. 23:40, 41) Zaidi ya ile, alionyesha kama anaamini kuwa Yesu atafufuliwa na kama siku moja atakuwa Mufalme. Ule mutenda-mabaya alimuambia hivi: “Yesu, unikumbuke wakati utaingia katika Ufalme wako.” (Lu. 23:42) Ile ni imani kubwa kabisa! Yesu alimujibia hivi: “Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja na mimi [hapana katika Ufalme, lakini] katika Paradiso.” (Lu. 23:43) Maneno “ninakuambia,” “utakuwa,” na “mimi” inaonyesha kama Yesu hakukuwa anaahidi watu wote, lakini alikuwa anamuahidi tu ule mutenda-mabaya. Juu Yesu alijua kama Baba yake ni mwenye rehema, njo maana, alimupatia tumaini ule mutenda-mabaya.​—Zb. 103:8.

6. Maneno yenye Yesu aliambia ule mutenda-mabaya inatufundisha nini?

6 Maneno ya Yesu inaweza kutufundisha nini? Yesu anaiga sifa za baba yake kwa ukamilifu. (Ebr. 1:3) Yehova anapenda kutusamehe na anapenda kutuonyesha rehema. Lakini, atafanya vile, kama tu tunahuzunika sana juu ya zambi zenye tulifanyaka zamani, na kama tunaonyesha imani katika zabihu ya Yesu Kristo. (1 Yo. 1:7) Watu fulani wanawaza kama Yehova hawezi kusamehe makosa yenye walifanyaka zamani. Wakati fulani, kama unajisikia vile, fikiria hii jambo: Wakati kidogo mbele akufe, Yesu alionyesha rehema mutenda-mabaya mwenye alikuwa alishahukumiwa, lakini mwenye alikuwa tu ameanza kuonyesha imani. Sasa unawaza ni kwa kiasi gani Yehova ataonyesha rehema waabudu wake waaminifu wenye tayari wako wanafanya yao yote ili kutii amri zake? ​—Zb. 51:1; 1 Yo. 2:1, 2.

“ONA! MWANA WAKO! . . . ONA! MAMA YAKO!”

7. Kulingana na Yohana 19:26, 27, ni mambo gani Yesu aliambia Maria na Yohana, na juu ya nini alisema vile?

7 Yesu alisema nini? (Soma Yohana 19:26, 27.) Yesu alihangaikia mama yake, mwenye inawezekana ile wakati alikuwa mujane. Pengine ndugu wa familia ya Yesu wangemutimizia mama yao mahitaji yake ya kimwili. Lakini, ni nani angemutimizia mahitaji yake ya kiroho? Hakuna kitu inaonyesha kama ile wakati, tayari ndugu za Yesu walikuwa wanafunzi wake. Hata vile, Yohana alikuwa mutume muaminifu, na alikuwa mumoja kati ya marafiki wa karibu sana wa Yesu. Yesu aliona wale wenye walimuabudu Yehova pamoja naye kuwa njo familia yake ya kiroho. (Mt. 12:46-50) Njo maana, kwa sababu alimupenda na alimuhangaikia sana mama yake Maria, Yesu alimuacha mu mikono ya Yohana, juu alijua kama Yohana angehangaikia mahitaji yake ya kiroho. Aliambia mama yake hivi: “Ona! Mwana wako!” Na kisha, aliambia Yohana hivi: “Ona! Mama yako!” Na kuanzia ile siku, Yohana akakuwa kama vile mwana wa Maria na alimuhangaikia sawa vile mama yake. Yesu alionyesha kama anamupenda sana mama yake mwenye alimuhangaikia kwa upendo, tangu azaliwe mupaka siku alikufa!

8. Maneno yenye Yesu aliambia Maria na Yohana inaweza kutufundisha nini?

8 Maneno ya Yesu inaweza kutufundisha nini? Uhusiano wetu pamoja na ndugu na dada zetu wa Kikristo unaweza kuwa nguvu zaidi kuliko uhusiano wenye tuko nao pamoja na watu wa familia yetu. Watu wa familia yetu wanaweza kutupinga ao hata kutuacha, lakini sawa vile Yesu aliahidi, kama tunabakia karibu kabisa na Yehova na tengenezo Lake, tutapata “mara mia moja (100)” zaidi kuliko mambo yenye tulipoteza. Wengi watakuwa kwetu sawa vile, mwana mupendwa, binti mupendwa, mama mupendwa, ao baba mupendwa. (Mk. 10:29, 30) Unajisikia namna gani vile uko mu familia ya kiroho ya ndugu na dada wenye kuwa mu umoja, juu wako na imani na juu wanamupenda Yehova na wanapendana kati yao? ​—Kol. 3:14; 1 Pe. 2:17.

“MUNGU WANGU, SABABU GANI UMENIACHA?”

9. Maneno ya Yesu yenye kuwa mu Matayo 27:46 inaweza kutufundisha nini?

9 Yesu alisema nini? Wakati kidogo mbele akufe, Yesu alisema hivi kwa sauti kubwa: “Mungu wangu, Mungu wangu, sababu gani umeniacha?” (Mt. 27:46) Biblia haionyeshe waziwazi juu ya nini Yesu alisema vile. Lakini, ona mambo yenye ile maneno inaweza kutufundisha. Jambo la kwanza lenye tunajifunza ni hili: Kwa kusema ile maneno, Yesu alikuwa anatimiza unabii wa Zaburi 22:1. * Tena, ile maneno inaonyesha waziwazi kama, Yehova hakutia “ukuta wa ulinzi kumuzunguka” Mwana wake. (Yob. 1:10) Yesu alielewa kama Baba yake aliruhusu wale wenye walikuwa wanamuchukia wajaribu imani yake kabisa mupaka kufikia kifo. Hakuna mwanadamu mwenye alishakajaribiwa sawa vile Yesu. Zaidi ya ile, ile maneno ilihakikisha kama Yesu hakufanya kitu fulani yenye ingefanya astahili kifo.

10. Maneno yenye Yesu aliambia Baba yake, inaweza kutufundisha nini?

10 Maneno ya Yesu inaweza kutufundisha nini? Jambo moja lenye tunajifunza ni hili: Hatupaswe kutazamia kama Yehova atatulinda ili tusipatwe na magumu yenye inajaribu imani yetu. Sawa vile Yesu mwenye alijaribiwa mupaka kifo, siye pia tunapaswa kujitayarisha ili kubakia waaminifu mupaka kifo, kama inaomba ikuwe vile. (Mt. 16:24, 25) Hata vile, tuko hakika kama Mungu, hataacha tujaribiwe kupita vile tunaweza kuvumilia. (1 Ko. 10:13) Tunajifunza pia kama, sawa vile Yesu, tunaweza kuteseka juu ya mambo yenye hatukufanya. (1 Pe. 2:19, 20) Wale wenye kutupinga wanatutesa, haiko juu tulifanya jambo fulani la mubaya, lakini juu hatuko sehemu ya ulimwengu na juu tunatoa ushahidi kuhusu ile kweli. (Yoh. 17:14; 1 Pe. 4:15, 16) Yesu alielewa juu ya nini Yehova aliruhusu apate mateso. Lakini, tofauti na yeye, waabudu fulani waaminifu wenye walikuwa mu majaribu walijiuliza wakati fulani juu ya nini Yehova aliruhusu mambo fulani itokee. (Hab. 1:3) Mungu wetu mwenye rehema na muvumilivu anaelewa kama wale waabudu hawakose imani, wako njo na lazima ya faraja yenye yeye tu njo anaweza kutoa.​—2 Ko. 1:3, 4.

“NINASIKIA KIU”

11. Juu ya nini Yesu alisema maneno yenye tunapata mu Yohana 19:28?

11 Yesu alisema nini? (Soma Yohana 19:28.) Juu ya nini Yesu alisema: “Ninasikia kiu”? Alisema vile “ili kutimiza andiko,” ni kusema unabii wenye kuwa mu Zaburi 22:15, yenye inasema: “Nguvu zangu zimekauka kama kipande cha chombo cha udongo; ulimi wangu unashikamana na fizi zangu.” Tena, kisha mateso yote yenye alipata, bila kusahau maumivu yenye alisikia wakati alikuwa ku muti wa mateso, Yesu alipaswa kabisa kusikia kiu ya maji. Alikuwa na lazima ya kumaliza kiu yenye alikuwa nayo.

12. Maneno “ninasikia kiu,” yenye Yesu alisemaka, inaweza kutufundisha nini?

12 Maneno ya Yesu inaweza kutufundisha nini? Yesu hakuwaza kama ni mubaya kusema namna alijisikia. Na siye pia tunapaswa kusema namna tunajisikia. Wamoja kati yetu hawapendake kuomba musaada kwa watu wengine, lakini kama tuko na lazima ya musaada, tusijizuie kuambia wengine. Kwa mufano, kama tuko wenye kuzeeka kimwili, ao tuko na ulemavu fulani, tunaweza kuomba rafiki moja atusindikize kuuza kitu fulani ao kuenda kuona munganga. Ikiwa tumevunjika moyo, tunaweza kumuomba muzee ao rafiki Mukristo mwenye kukomaa kiroho atusikilize ao atuambie “neno la muzuri” lenye litatutia moyo. (Mez. 12:25) Tusisahau kama ndugu na dada zetu wanatupenda, na wako tayari kutusaidia katika “nyakati za taabu.” (Mez. 17:17) Lakini, hawawezi kujua mambo yenye iko mu moyo wetu. Kama hauseme, hawatajua kama uko na lazima ya musaada.

“IMETIMIZWA!”

13. Yesu alitimiza nini juu alibakia muaminifu-mushikamanifu mupaka kifo?

13 Yesu alisema nini? Karibu saa kenda ya muchana (ao, 15:00) mu siku ya 14, Mwezi wa Nisani, Yesu akasema hivi kwa sauti kubwa: “Imetimizwa!” (Yoh. 19:30) Wakati kidogo tu mbele akufe, Yesu alijua kama alikuwa ametimiza mambo yote yenye Baba yake alipenda afanye. Yesu alikuwa ametimiza mambo mingi juu aliendelea kuwa muaminifu-mushikamanifu mupaka kifo. Kwanza, alionyesha kama Shetani ni muongo. Kwa kweli, alionyesha kama mwanadamu mukamilifu anaweza kuendelea kuwa muaminifu-mushikamanifu, hata kama Shetani anafanya nini. Pili, Yesu alitoa uzima wake kuwa bei ya ukombozi. Ile imewezesha wanadamu wenye hawakamilike wakuwe na uhusiano pamoja na Mungu na pia wakuwe na tumaini la kuishi milele. Tatu, Yesu alionyesha kama Yehova njo iko na haki ya kutawala. Na pia alisaidia kutakasa jina la Baba yake.

14. Tunapaswa kuazimia kuishi namna gani kila siku? Fasiria.

14 Maneno ya Yesu inaweza kutufundisha nini? Tunapaswa kufanya yetu yote ili kuendelea kuwa waaminifu-washikamanifu kila siku. Fikiria maelezo ya Ndugu Maxwell Friend, mwenye alikuwaka mwalimu ku masomo ya Gileadi. Ku mukusanyiko moja wa kimataifa, mu hotuba yake yenye ilikuwa inazungumuzia uaminifu, Ndugu Friend alisema hivi: “Usichunge kesho juu useme ao ufanye mambo yenye unaweza kufanya leo. Nani anakuambia kama kesho utakuwa ungali muzima? Kila siku, uishi sawa vile njo siku yako ya mwisho ya kufanya mambo yenye itaonyesha kama unastahili kuishi milele.” Tuishi basi kila siku sawa vile njo siku yetu ya mwisho ya kuonyesha uaminifu wetu mushikamanifu! Hata kama tunaona kifo mbele yetu, tutaweza kusema, “Yehova, umejionea namna nimebakia muaminifu-mushikamanifu kwako, namna nimeonyesha kama Shetani ni muongo, na namna nimetetea jina lako na haki yako ya kutawala!”

“NINAWEKA ROHO YANGU KATIKA MIKONO YAKO”

15. Kulingana na Luka 23:46, Yesu alikuwa hakika na jambo gani?

15 Yesu alisema nini? (Soma Luka 23:46.) Kwa uhakika wote, Yesu alisema hivi: “Baba, ninaweka roho yangu katika mikono yako.” Yesu alijua kama wakati wake wenye kuja ulitegemea Yehova, na alikuwa hakika kama Baba yake hangemusahau.

16. Mufano wa Shahidi mumoja kijana wa miaka 15 unakufundisha nini?

16 Maneno ya Yesu inaweza kutufundisha nini? Endelea kuwa mushikamanifu kwa Yehova hata kama uzima wako uko mu hatari. Juu ufikie kufanya vile, unapaswa ‘kumutegemea Yehova kwa moyo wako wote.’ (Mez. 3:5) Fikiria mufano wa Joshua, kijana Shahidi wa Yehova wa miaka 15 mwenye alikuwa na ugonjwa hatari sana. Alikataa matunzo yenye inapinga Sheria ya Mungu. Wakati kidogo tu mbele akufe, aliambiaka mama yake hivi: “Mama, niko mu mikono ya Yehova. . . . Acha nikuambie mama, sina mashaka: Niko hakika kabisa kama Yehova atanifufua, anajua mambo iko mu moyo wangu, na ninamupenda kabisa.” * Ni muzuri kila mumoja wetu ajiulize hivi, ‘Kama najikuta mu hali yenye inajaribu imani yangu, nitakuwa tayari kutia uzima wangu mu mikono ya Yehova na kuwa hakika kama atanikumbuka?’

17-18. Ni mambo gani tumejifunza? (Ona kisanduku “ Mambo Tunajifunza mu Maneno ya Mwisho ya Yesu.”)

17 Maneno ya mwisho yenye Yesu alisema mbele akufe inatufundisha mambo ya maana sana! Tunaelewa kama ni jambo la maana kusamehe wengine na kuwa hakika kama Yehova atatusamehe. Tumeona pia kama ni pendeleo kuwa mu familia ya kiroho ya ndugu na dada wenye wako tayari kutusaidia. Lakini, wakati tuko na lazima ya musaada, tusijizuie kuambia wengine. Tunajua kama Yehova atatusaidia kuvumilia jaribu lolote lenye linaweza kutupata. Na tumeona kama ni jambo la maana kuishi kila siku sawa vile njo siku yetu ya mwisho ya kuonyesha kama tuko waaminifu-washikamanifu, na kuendelea kuwa hakika kama Yehova atatufufua kama tunakufa.

18 Kusema kweli, maneno yenye Yesu alisema wakati alikuwa ku muti wa mateso, inatufundisha mambo mingi ya muzuri! Wakati tunatumikisha mambo yenye tumejifunza, tutaonyesha kama tunatii hii maneno yenye Yehova alisema kuhusu Mwana wake: “Mumusikilize.”​—Mt. 17:5.

WIMBO 126 Ukuwe Macho, Usimame Imara, Ukuwe na Nguvu

^ fu. 5 Kama vile Matayo 17:5 inasema, Yehova anapenda tusikilize Mwana wake. Mu hii habari, tutaona mambo yenye tunaweza kujifunza mu maneno yenye Yesu alisema mbele akufe, wakati alikuwa ku muti wa mateso.

^ fu. 9 Ili kujua sababu zenye pengine zilifanya Yesu ataje maneno ya Zaburi 22:1, ona sehemu “Maulizo ya Wasomaji Wetu” yenye kuwa mu hii gazeti.

^ fu. 16 Ona habari, “Imani ya Joshua, Ushindi kwa Haki za Watoto” yenye kuwa mu Amuka ya tarehe 22, Mwezi wa 1, Mwaka wa 1995.