Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 16

Usikilize Wengine, Uwajue Muzuri, na Uwasikilie Huruma

Usikilize Wengine, Uwajue Muzuri, na Uwasikilie Huruma

“Muache kuhukumu kulingana na namna mutu anaonekana kwa inje, lakini muhukumu kwa hukumu ya haki.”​—YOH. 7:24.

WIMBO 101 Kufanya Kazi Pamoja kwa Umoja

KIFUPI CHA HABARI *

1. Ni jambo gani lenye kutia moyo lenye Biblia inazungumuzia juu ya Yehova?

UNAWEZA kupenda watu wakuhukumu juu ya rangi yako ya ngozi, sura yako, ao mwili wako? Inawezekana hapana. Inatia moyo sana kujua kama Yehova yeye hatuhukumu kulingana na namna tunaonekana kwa inje! Kwa mufano, wakati Samweli alikuwa anaangalia watoto wanaume wa Yese, hakuona mambo yenye Yehova alikuwa anaona. Yehova alikuwa amemuambia Samweli kama mumoja kati ya watoto wanaume wa Yese angekuwa mufalme wa Israeli. Lakini nani? Wakati Samweli aliona Eliabu, mutoto mwanaume wa kwanza wa Yese, alisema hivi: “Hakika mutiwa-mafuta wa Yehova amesimama hapa mbele yake.” Eliabu alionekana kama mufalme. “Lakini Yehova akamuambia Samweli: ‘Usiangalie sura yake wala urefu wake, kwa sababu nimemukataa.’” Tunajifunza somo gani? Yehova aliongeza hivi: ‘Mwanadamu anaona kile chenye kinaonekana kwa macho, lakini Yehova anaona ndani ya moyo.’​—1 Sa. 16:1, 6, 7.

2. Kulingana na Yohana 7:24, juu ya nini hatupaswe kuhukumu mutu kulingana na namna anaonekana kwa inje? Leta mufano.

2 Kwa sababu tuko wanadamu wenye hawakamilike, sisi wote tuko na muelekeo wa kuhukumu wengine kulingana na namna wanaonekana kwa inje. (Soma Yohana 7:24.) Lakini hatuwezi kujua mambo mingi juu ya mutu fulani kwa kumuangalia tu kwa inje. Kwa mufano, hata munganga mwenye kuwa na uzoefu sana hawezi kujua mambo mingi juu ya mugonjwa kwa kumuangalia tu. Anapaswa kumusikiliza mugonjwa kwa uangalifu kama anapenda kujua matatizo ya afya yenye amekuwa nayo zamani, namna anajisikia, na alama zenye kuonyesha ugonjwa. Munganga anaweza hata kumuomba mugonjwa afanye radio ili kujua mambo yenye kuwa ndani ya mwili wa mugonjwa. Kama munganga hafanye vile, anaweza kupatia mugonjwa matunzo yenye haifae. Vilevile, hatuwezi kuelewa muzuri kabisa ndugu na dada zetu kwa kuangalia tu namna wanaonekana kwa inje. Tunapaswa kujikaza kuelewa utu wao wa ndani. Kwa kweli, hatuwezi kusoma katika moyo, kwa hiyo hatuwezi kabisa kuelewa wengine namna Yehova anawaelewa. Lakini tunaweza kujikaza sana ili kumuiga Yehova. Namna gani?

3. Namna gani habari za Biblia zenye tutazungumuzia katika habari hii zitatusaidia kumuiga Yehova?

3 Namna gani Yehova anatendea waabudu wake? Anawasikiliza. Anafikiria hali zao na mambo yote yenye kuwachochea. Na anawasikilia huruma. Wakati tunazungumuzia namna Yehova alitendea Yona, Eliya, Hagari na Loti, tutaona namna tunaweza kumuiga katika namna tunatendea ndugu na dada zetu.

SIKILIZA KWA UANGALIFU

4. Juu ya nini tunaweza kuwa na mawazo ya mubaya juu ya Yona?

4 Kwa sababu hatujue mambo yote, tunaweza kumuhukumu Yona kuwa mutu mwenye hakukuwa mwenye kutegemeka ao mwenye alikosa uaminifu. Yehova alimupatia amri yenye ilikuwa wazi ya kutangaza ujumbe wa hukumu katika Ninawi. Lakini, kuliko kutii, Yona aliingia katika mashua yenye ilikuwa inaenda ngambo ingine, “mbali na Yehova.” (Yon. 1:1-3) Ingekuwa wewe, ungemutuma tena Yona aende kutimiza mugao huo? Inawezekana hapana. Lakini, Yehova aliona kama inafaa amutume tena Ninawi.​—Yon. 3:1, 2.

5. Maneno ya Yona yenye kupatikana katika Yona 2:1, 2, 9 inakufundisha nini juu yake?

5 Katika sala yake, Yona alionyesha kama alikuwa mutu wa namna gani kabisa. (Soma Yona 2:1, 2, 9.) Kwa kweli, Yona alisali mara mingi kwa Yehova. Moja kati ya sala zake, ni kusema, ile yenye alitoa na iko mu tumbo la samaki, inatusaidia tusimuone tu kuwa mutu mwenye alikimbia mugao wake. Maneno yake inaonyesha kama alikuwa munyenyekevu, mwenye shukrani, na aliazimia kumutii Yehova. Njo maana Yehova hakukaza akili juu ya makosa ya Yona, lakini alijibu sala yake, na aliendelea kumutumia kuwa nabii!

Kama tunaelewa ukweli wa mambo, tunaweza kuonyesha zaidi sifa ya huruma (Ona fungu la 6) *

6. Juu ya nini ni jambo la maana kusikiliza kwa uangalifu?

6 Ili tusikilize wengine kwa uangalifu, tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wavumilivu. Ni jambo la maana kufanya vile kwa sababu tatu hivi. Sababu ya kwanza, inawezekana hatutakuwa haraka kuhukumu watu. Sababu ya pili, tutatambua namna ndugu ao dada yetu anajisikia na nia yake, na hilo litatusaidia tumuelewe. Na sababu ya tatu, wakati tunaacha ndugu ao dada yetu ajieleze, anaweza hata kuelewa jambo fulani juu yake mwenyewe. Wakati fulani, hatuelewe kabisa namna sisi wenyewe tunajisikia mupaka tuseme namna tunajisikia. (Mez. 20:5) Muzee mumoja wa Asia anasema hivi: “Ninakumbuka wakati fulani nilifanya kosa la kusema mbele ya kusikiliza. Niliambia dada mumoja kama anapaswa kujikaza kutoa majibu ya muzuri ku mikutano. Kisha, nilitambua kama alikuwa na magumu ya kusoma na alikuwa anajikaza sana kutoa majibu.” Ni jambo la maana sana kila muzee ‘asikie ukweli wa mambo’ mbele ya kutoa mashauri!​—Mez. 18:13.

7. Namna Yehova alimutendea Eliya inakufundisha nini?

7 Ndugu na dada zetu fulani wanashindwa kusema namna wanajisikia kwa sababu ya mambo yenye iliwafikia zamani, desturi yao, ao kwa sababu ya utu wao. Tunaweza kufanya nini ili tuwasaidie wakuwe tayari kutuambia namna wanajisikia? Ukumbuke namna Yehova alimutendea Eliya wakati alikuwa anamukimbia Yezebeli. Kulipita siku mingi mbele Eliya aelezee Baba yake wa mbinguni namna alikuwa anajisikia. Yehova alimusikiliza kwa uangalifu. Kisha akamutia Eliya moyo na kumupatia kazi ya muzuri ya kufanya. (1 Fa. 19:1-18) Inaweza kuomba wakati mbele ndugu na dada wajisikie huru kuzungumuza na sisi, lakini kama tu wanafanya vile, hilo litatusaidia kuelewa muzuri namna wanajisikia kabisa. Kama tunamuiga Yehova kwa kuwa wavumilivu, wanaweza kufikia kututumainia. Kisha, wakati wanakuwa tayari kutuambia namna wanajisikia, tunapaswa kusikiliza kwa uangalifu.

UJIKAZE KUJUA MUZURI NDUGU NA DADA ZAKO

8. Kulingana na Mwanzo 16:7-13, namna gani Yehova alimusaidia Hagari?

8 Hagari, mutumishi mwanamuke wa Sarai, alitenda kwa upumbavu kisha kuwa bibi ya Abramu. Wakati Hagari alipata mimba, akaanza kumuzarau Sarai, mwenye hakukuwa na mutoto. Hali ikakuwa mubaya zaidi mupaka Sarai akamufukuza Hagari. (Mwa. 16:4-6) Kwa sababu hatukamilike, tunaweza kumuona Hagari kuwa mwanamuke mwenye kiburi na mwenye alistahili malipizi yenye alipata. Lakini Yehova hakumuona Hagari vile. Alimutumia malaika. Wakati malaika alikutana naye, alimusaidia kubadilisha mawazo yake na akamubariki. Hagari alielewa kama Yehova alikuwa anamuona na alikuwa anajua mambo yote juu ya hali yake. Alishangaa sana mupaka akamuita Yehova kuwa “Mungu mwenye kuona, . . . yeye mwenye kuniona.”​—Soma Mwanzo 16:7-13.

9. Ni mambo gani yenye Mungu alifikiria wakati alishugulika na Hagari?

9 Yehova alijua nini juu ya Hagari? Alijua muzuri maisha yake ya zamani na mambo yenye ilikuwa imemupata. (Mez. 15:3) Hagari alikuwa mwanamuke Mumisri mwenye alikuwa anaishi katika familia ya Waebrania. Je, wakati fulani alijisikia kuwa mugeni? Alikuwa anakumbuka watu wa familia yake na inchi yake? Haiko yeye tu njo alikuwa bibi ya Abramu. Kwa wakati fulani, wanaume fulani waaminifu walikuwa na bibi wengi. Lakini Yehova hakukusudia vile tangu mwanzo. (Mt. 19:4-6) Kwa hiyo, hatuwezi kushangaa kuona kama mara mingi hali hiyo ilitokeza matatizo makubwa kama vile wivu na chuki katika familia. Yehova alijua kama Hagari alifanya mubaya kwa kumukosea Sarai heshima. Lakini alifikiria namna Hagari alikuwa anajisikia na hali yake na kwa hiyo, akamutendea kwa wema.

Ujikaze kujua muzuri ndugu na dada zako (Ona fungu la 10-12) *

10. Tunaweza kufanya nini ili tufikie kujua muzuri ndugu na dada zetu?

10 Tunaweza kumuiga Yehova kwa kujikaza kuelewa ndugu na dada zetu. Ujikaze kujua muzuri ndugu na dada zako. Uzungumuze nao mbele na kisha mikutano, uhubiri pamoja nao, na kama inawezekana uwaalike ili mukule pamoja nao. Wakati unafanya vile, unaweza kujua kama dada mwenye anaonekana kuwa mwenye kujitenga na wengine kwa kweli iko mwenye haya, ndugu mwenye pengine unawazia kuwa anapenda vitu vya kimwili ni mwenye kuonyesha ukaribishaji-wageni, ao watu wa familia fulani wenye wanafika nyuma kila mara ku mikutano wanavumilia upinzani. (Yob. 6:29) Kwa kweli, hatupaswe ‘kujiingiza katika mambo ya watu wengine.’ (1 Ti. 5:13) Lakini, ni muzuri kujua jambo fulani juu ya ndugu na dada zetu na hali zenye kuwafanya wakuwe na utu fulani.

11. Juu ya nini ni jambo la maana wazee wajue muzuri kondoo?

11 Zaidi sana wazee wanapaswa kujua muzuri ndugu na dada zao wenye wanahangaikia. Fikiria mufano wa ndugu mumoja mwenye kuitwa Artur mwenye alikuwa mwangalizi wa muzunguko. Yeye na muzee mwingine walienda kutembelea dada mumoja mwenye haya na mwenye kuogopa kukaribia wengine. Artur anasema hivi: “Tulifikia kujua kama bwana yake alikufaka muda mufupi kisha wao kuoana. Hata kama alikuwa anapambana na magumu, alisaidia watoto wake wawili wanamuke wamupende Yehova na wamutumikie kwa uaminifu. Lakini sasa, alikuwa haone tena muzuri, na alikuwa na ugonjwa wa kushuka moyo. Hata hivyo, aliendelea kumupenda Yehova sana na aliendelea kuwa na imani yenye nguvu. Tulielewa kama mufano muzuri wa dada huyo ulipaswa kutufundisha mambo mingi.” (Flp. 2:3) Mwangalizi huyo wa muzunguko alikuwa anaiga mufano wa Yehova. Yehova anajua kondoo wake na maumivu yenye wako nayo. (Kut. 3:7) Wazee wenye wanajua kondoo wanaweza kuwasaidia muzuri.

12. Namna gani dada Yip Yee alifikia kujua muzuri dada mumoja katika kutaniko lao?

12 Wakati unajua muzuri ndugu ao dada yako mwenye unaonaka kama anakukwazaka, inawezekana kabisa kama utamuelewa. Fikiria mufano moja. Dada mumoja mwenye kuitwa Yip Yee, mwenye kuishi Asia, anasema hivi: “Dada mumoja katika kutaniko letu alikuwa anasema kwa sauti ya juu sana. Nilikuwa ninawaza kama hakukuwa na adabu. Lakini wakati nilihubiri pamoja naye, nilijua kama alikuwa anasaidia wazazi wake kuuzisha samaki mu soko. Kwa hiyo, alipaswa kusema kwa sauti ya juu ili kuita watu wauze samaki.” Yip Yee anaongeza hivi: “Nilijifunza kama ili kuelewa ndugu na dada zangu, ninapaswa kuwajua muzuri.” Inaomba kujikaza sana ili kufikia kujua muzuri ndugu na dada zako. Lakini, wakati unatii shauri la Biblia lenye linakuomba ufungue moyo wako wazi, unamuiga Yehova mwenye anapenda “watu wa namna zote.”​—1 Ti. 2:3, 4; 2 Ko. 6:11-13.

UWASIKILIE HURUMA

13. Kulingana na Mwanzo 19:15, 16, malaika walifanya nini wakati Loti aliendelea kukawia, na juu ya nini walifanya vile?

13 Wakati fulani wa maana katika maisha yake, Loti alikawia kutii maagizo ya Yehova. Malaika wawili walimutembelea Loti na kumuambia atoshe familia yake katika muji wa Sodoma. Juu ya nini? Walimuambia hivi: “Tutaharibu mahali hapa.” (Mwa. 19:12, 13) Asubui yenye ilifuata, Loti na familia yake walikuwa wangali mu nyumba. Kwa hiyo, malaika walimuonya tena Loti. Lakini “aliendelea kukawia.” Tunaweza kuwaza kama Loti hakuhangaikia mambo yenye Yehova alimuambia afanye, ao hata kuwaza kama alikosa kutii. Lakini, Yehova hakumuacha. “Kwa sababu Yehova alimusikilia huruma,” malaika walikamata watu wa familia hiyo ku mikono na kuwapeleka inje ya muji.​—Soma Mwanzo 19:15, 16.

14. Pengine ni juu ya nini Yehova alimusikilia Loti huruma?

14 Pengine Yehova alimusikilia Loti huruma kwa sababu mbalimbali. Inawezekana Loti alikawia kutoka katika nyumba yake kwa sababu aliogopa watu wenye walikuwa inje ya muji. Kulikuwa pia hatari zingine. Inawezekana Loti alijua habari juu ya wafalme wawili wenye waliangukia mu mashimo ya kabulimbo, katika bonde lenye lilikuwa karibu na muji. (Mwa. 14:8-12) Kwa sababu alikuwa bwana na muzazi, pengine alikuwa na mahangaiko juu ya familia yake. Zaidi ya ile, Loti alikuwa tajiri, kwa hiyo, pengine alikuwa na nyumba ya muzuri sana katika Sodoma. (Mwa. 13:5, 6) Kwa kweli, hakuna jambo moja kati ya ile mambo yote lenye lingemufanya akose kumutii Yehova bila kukawia. Lakini, Yehova hakukaza akili juu ya makosa ya Loti, lakini alimuona kuwa mutu “mwenye haki.”​—2 Pe. 2:7, 8.

Wakati tunasikiliza wengine, tunaweza kuelewa namna ya kuwasikilia huruma (Ona fungu la 15-16) *

15. Kuliko kuhukumu matendo ya mutu fulani, tunapaswa kufanya nini?

15 Kuliko kuhukumu matendo ya mutu mwingine, ujikaze kuelewa namna anajisikia. Veronica, dada mumoja wa Ulaya, alijikaza kufanya vile. Anasema hivi: “Sikuzote, dada mumoja alikuwa anaonekana kuwa hana furaha. Aliendelea kujitenga na wengine. Wakati fulani, niliogopa kumukaribia. Lakini niliwaza hivi: ‘Kama ningekuwa katika hali yake, ningekuwa na lazima ya rafiki.’ Kwa hiyo, niliamua kumuuliza namna alikuwa anajisikia. Na alianza kuniambia namna alikuwa anajisikia! Sasa ninaelewa mambo mingi juu yake.”

16. Juu ya nini tunapaswa kumuomba Yehova musaada katika sala ili tuelewe ndugu na dada zetu?

16 Mutu mumoja mwenye anatuelewa muzuri kabisa ni Yehova. (Mez. 15:11) Kwa hiyo, umuombe akusaidie kuona wengine namna anawaona na kuelewa namna ya kuwasikilia huruma. Sala ilisaidia dada mumoja mwenye kuitwa Anzhela akuwe mwenye kuelewa zaidi wengine. Alikuwa ameshindwa kuelewana na dada mumoja katika kutaniko lao. Anzhela anasema hivi: “Ingekuwa mwepesi sana kuangukia katika mutego wa kuchambua-chambua dada huyo na kumuepuka. Lakini nilimuomba Yehova anisaidie kuelewa dada huyo.” Je, Yehova alijibu sala ya dada Anzhela? Anaendelea kusema hivi: “Tulienda katika mahubiri pamoja naye na kisha tuliongea kwa saa mingi. Nilimusikiliza kwa huruma. Sasa ninamupenda zaidi, na ninaazimia kumusaidia.”

17. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Tutendee ndugu na dada wote kwa huruma yenye upole, bila ubaguzi. Wote wanapambana na magumu kama vile Yona, Eliya, Hagari, na Loti. Katika hali fulani, wamejiletea magumu wao wenyewe. Kwa kweli, sisi wote tumekwisha kujiletea magumu sisi wenyewe wakati fulani. Njo maana Yehova anatuomba tujitie pa nafasi ya wengine. (1 Pe. 3:8) Wakati tunamutii Yehova, tunatia nguvu umoja wa familia yetu ya mu dunia yote, yenye kuwa ya pekee na yenye kufanyizwa na watu mbalimbali. Kwa hiyo, katika uhusiano wetu pamoja na ndugu na dada, tuazimie kuwasikiliza, kuwajua muzuri, na kuwasikilia huruma.

WIMBO 87 Njooni! Mburudishwe

^ fu. 5 Kwa sababu tuko wanadamu wenye hawakamilike, tuko haraka kuwa na mawazo ya mubaya juu watu na nia zao. Lakini Yehova yeye “anaona ndani ya moyo.” (1 Sa. 16:7) Habari hii itazungumuzia namna Yehova alisaidia kwa upendo Yona, Eliya, Hagari, na Loti. Na itatusaidia tumuige Yehova katika namna tunatendea ndugu na dada zetu.

^ fu. 52 MAFASIRIO YA PICHA: Ndugu mumoja mwenye kuzeeka anakasirikia kijana mwanaume mwenye anafika nyuma ku mukutano, lakini kisha, anafikia kujua kama kijana huyo alichelewa kwa sababu gari lake liligongwa.

^ fu. 54 MAFASIRIO YA PICHA: Hata kama mwangalizi wa kikundi cha mahubiri aliwaza kwanza kama dada alikuwa mwenye kujitenga na wengine, alifikia kujua kama alikuwa tu mwenye haya na wasiwasi wakati iko pamoja na watu wenye hajue muzuri.

^ fu. 56 MAFASIRIO YA PICHA: Dada mumoja anafikia kumuelewa muzuri dada mwingine wakati wanapitisha wakati pamoja; anaelewa kama dada huyo hakukuwa mwenye huzuni-huzuni na mwenye hahangaikie wengine, kama vile aliwaza wakati alikutana naye kwa mara ya kwanza kwenye Jumba la Ufalme.