Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Namna Nilipata Furaha ya Kutoa

Namna Nilipata Furaha ya Kutoa

NILIKUWA na miaka 12 wakati nilitambua kama nilikuwa na kitu fulani cha maana sana cha kutoa. Kwenye mukusanyiko fulani, ndugu mumoja aliniuliza ikiwa ningependa kuhubiri. Hata kama nilikuwa sijahubiri hata siku moja, nilisema ndiyo. Tulienda katika eneo, na alinipatia vijitabu fulani vyenye kuzungumuzia Ufalme wa Mungu. Kisha alisema hivi: “Wewe uende kuhubiria watu wenye kuwa ile ngambo ya barabara, na mimi nitaenda ngambo ingine.” Niliogopa, lakini nilianza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Nilishangaa wakati nilitolea watu vijitabu vyote kwa wakati kidogo tu. Kwa kweli, watu wengi walipenda habari yenye niliwatolea.

Nilizaliwa katika mwaka wa 1923, katika muji wa Chatham, eneo la Kent, Uingereza. Katika miaka hiyo, kisha Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, watu walikuwa na tumaini kama dunia itakuwa nafasi ya muzuri sana. Lakini, wakati watu wengi waliona kama jambo hilo halikutokea, walivunjika moyo, na hata wazazi wangu. Pia, walivunjika moyo kwa sababu ya viongozi wa dini ya Baptiste wenye walikuwa wanahangaikia sana kupata cheo cha juu katika kanisa. Wakati nilikuwa na miaka karibu 9, mama yangu alianza kuenda kwenye jumba la Shirika la Kimataifa la Wanafunzi wa Biblia, nafasi kwenye Mashahidi wa Yehova walikuwa wanafanyia “madarasa,” ao mikutano yao. Dada mumoja alitupatia vichapo vya watoto vyenye kuwa na mafundisho yenye kutoka katika Biblia na katika kitabu La Harpe de Dieu. Nilipenda mambo yenye nilikuwa ninajifunza.

NINAJIFUNZA MAMBO MENGI KWA NDUGU WENYE KUKOMAA

Wakati nilikuwa na miaka kati ya 13 na 19, nilifurahia kutolea watu tumaini kupitia Neno la Mungu. Mara nyingi nilihubiri nyumba kwa nyumba mimi mwenyewe, lakini wakati nilihubiri na wengine, nilijifunza mambo mengi. Kwa mufano, siku moja tulikuwa tunaenda katika eneo pamoja na ndugu fulani mwenye kukomaa, tuliona kiongozi fulani wa dini na nikasema hivi: “Ona ule mbuzi.” Ndugu huyo alisimamisha kinga yake na aliniomba tukae pamoja kwenye kipande cha muti. Aliniuliza hivi: “Ni nani mwenye alikupatia mamlaka ya kuhukumu kama mutu fulani ni mbuzi ao hapana? Sisi tuhubirie tu watu habari njema na tumuachie Yehova kazi ya kuhukumu.” Wakati huo, nilijifunza mambo mengi juu ya furaha yenye mutu anapata wakati anatoa.—Mathayo 25:31-33; Matendo 20:35.

Ndugu mwengine mwenye kukomaa alinifundisha kama ili kupata furaha katika kutoa, tunapaswa kuvumilia wakati fulani. Bibi yake hakupenda Mashahidi wa Yehova. Siku moja alinialika nyumbani kwake ili kula chakula. Bibi huyo alikasirika sana kwa sababu bwana yake alienda katika mahubiri, na akaanza kututupia paketi za chai. Kuliko kukasirikia bibi yake, ndugu huyo aliokota paketi hizo za chai kwa furaha na kuzitia kwenye nafasi yenye kufaa. Kisha miaka fulani, ndugu huyo alipata matokeo ya muzuri kwa sababu ya uvumilivu wake; bibi yake alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

Katika Mwezi wa 9, mwaka wa 1939, wakati nilikuwa na miaka 16, inchi ya Uingereza ilianza kupigana vita na Ujerumani. Katika Mwezi wa 3, mwaka wa 1940, mimi na mama yangu tulibatizwa huko Dover. Katika Mwezi wa 6, mwaka wa 1940, niliangalia kupitia mulango wa mbele wa nyumba yetu na kuona namna askari wengi sana walikuwa wanapita katika motokari kubwa-kubwa. Askari hao waliokoka Vita ya Dunkirk. Walikuwa wenye kuvurugika na hawakukuwa na tumaini. Nilitaka kabisa kuwahubiria juu ya Ufalme wa Mungu na kuwapatia tumaini la wakati unaokuja. Mwishoni mwa mwaka huo, askari wa Ujerumani walianza kuangusha bombe huko Uingereza. Kila usiku, ndege (avion) za vita za Ujerumani zilikuwa zinapita-pita katika eneo letu. Tuliogopa sana kusikia makelele yenye bombe zilikuwa zinafanya wakati zilikuwa zinaanguka. Asubui, nyumba zilikuwa zimeharibiwa katika maeneo yote. Mambo hayo yalinisaidia kutambua hata zaidi kama Ufalme wa Mungu ndio ulikuwa tu tumaini langu kwa ajili ya wakati unaokuja.

NINAANZA MAISHA YA KUTOA

Katika mwaka wa 1941, nilianza kazi ya utumishi wa wakati wote, na hilo lilikuwa mwanzo wa maisha yenye imeniletea furaha kubwa. Nilikuwa ninatumika katika kompanyi ya Royal Dockyard, huko Chatham, nilikuwa ninajifunza kutengeneza mashua. Watu wengi walipenda kupata kazi hiyo, na ilikuwa kazi ya muzuri sana. Lakini, watumishi wa Yehova walikuwa wamekwisha kujua kama Wakristo hawapaswe kupigana vita na taifa lingine. Na katika mwaka wa 1941, tulielewa pia kama tunapaswa kuepuka kutegemeza kazi yoyote ya kutengeneza silaha. (Yohana 18:36) Kompanyi hiyo ilikuwa inatengeneza mashua za vita za kupita chini ya maji. Kwa hiyo, niliona kuwa huo ulikuwa wakati wa kuacha kazi yangu na kuanza kazi ya utumishi wa wakati wote. Mugao wangu wa kwanza ulikuwa katika Cirencester, muji muzuri sana katika eneo la Cotswolds.

Wakati nilikuwa na miaka 18, nilifungwa katika gereza kwa miezi kenda kwa sababu nilikataa kuingia katika kazi ya jeshi. Niliogopa sana wakati mulango wa chumba changu cha gereza ulifungwa nguvu na nikabakia peke yangu. Lakini kisha tu wakati kidogo, walinzi wa gereza na wafungwa wengine walianza kuniuliza sababu gani nilifungwa, na nilifurahi kuwaelezea mambo yenye ninaamini.

Kisha kufunguliwa, nilijiunga na Leonard Smith, * na tulihubiri katika miji mbalimbali ya eneo la Kent, kwenye tulikuwa tunaishi. Ndege za Wanazi zilipaswa kupita katika anga ya eneo la Kent ili kuangusha bombe katika muji wa Londres. Kuanzia mwaka wa 1944, bombe nyingi zenye kuitwa doodlebugs zilianguka katika eneo la Kent. Bombe hizo zilikuwa kabisa ndege zenye hazikukuwa na mutu wa kuziongoza na zenye zilijaa vitu vya kulipuka. Wakati tulikuwa tunasikia motere unazimika, tulijua kama kisha segonde kidogo ndege itaanguka na kulipuka. Watu wote waliogopa sana. Wakati huo, tulikuwa tunajifunza Biblia pamoja na familia ya watu tano. Wakati fulani tulipaswa kukaa chini ya meza ya chuma ili itulinde ikiwa nyumba ingeanguka. Kisha, watu wote wa familia hiyo walibatizwa.

KUHUBIRI HABARI NJEMA KATIKA INCHI ZINGINE

Tunatangaza mukusanyiko wakati nilikuwa painia katika Irelandi (chini)

Kisha vita, nilikuwa painia kwa miaka mbili katika eneo la kusini la inchi ya Irelandi. Tulienda nyumba kwa nyumba na kusema kama tulikuwa wamisionere na tulikuwa tunatafuta nafasi ya kukaa. Tulitolea watu magazeti katika barabara. Lakini inchi ya Irelandi ilikuwa tofauti sana na inchi ya Uingereza. Watu wengi waliona kama tuko wapumbavu kuwaza kama watu wangepokea muzuri ujumbe wetu katika inchi hiyo ya dini ya Katoliki! Wakati mutu fulani alisema kama atatutendea mubaya, niliambia polisi fulani, lakini alinijibu hivi: “Sasa, unapenda nifanye nini?” Hatukujua kama mapadri walikuwa na mamlaka makubwa katika inchi hiyo. Watu wangepoteza kazi yao ikiwa wangekamata vitabu vyetu. Na tulilazimishwa kutoka nafasi kwenye tulikuwa tunaishi.

Kisha wakati fulani tulitambua kama wakati tunafika katika eneo mupya, ilikuwa muzuri zaidi tuhubiri mahali kwenye mapadri hawatujue. Kwa hiyo, tulipaswa kuenda mbali sana na mahali kwenye tulikuwa tunaishi na kutembelea watu katika maeneo hayo. Kisha hapo, tulihubiria watu katika maeneo ya karibu. Katika eneo la Kilkenny, tulijifunza na kijana mumoja mwanaume mara tatu katika juma hata kama vikundi vya watu wenye jeuri ao wakali walituogopesha. Kwa sababu nilipenda kabisa kufundisha watu Biblia, nilipenda kupata mazoezi ya kuwa misionere. Kwa hiyo, niliamua kujaza fomu ya Masomo ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower.

Mashua Sibia ilikuwa nyumba yetu ya wamisionere kuanzia mwaka wa 1948 mupaka 1953 (kuume)

Kisha kusoma masomo hayo kwa miezi tano katika muji wa New York, nilikuwa kati ya watu ine kwenye masomo ya Gileadi, wenye walipewa mugao wa kuenda katika visiwa kidogo-vidogo sana vya Bahari ya Karibea. Katika Mwezi wa 11, 1948, tuliondoka New York City na kusafiri katika mashua (bateau) yenye kuwa na urefu wa metre 18 yenye kuitwa Sibia. Ilikuwa mara yangu ya kwanza kusafiri katika mashua kama hiyo, kwa hiyo, nilifurahi sana. Gust Maki, mumoja kati ya wale wenye tulisoma nao masomo ya Gileadi, alikuwa na uzoefu sana wa kutembeza mashua. Alitufundisha ufundi wa musingi juu ya namna ya kutembeza mashua, kama vile namna ya kupandisha na kushusha tanga (kitambaa kikubwa chenye kuingiza upepo ili kufanya mashua iende), namna ya kusafiri katika bahari kwa kutumia dira (boussole), namna ya kutembeza katika zoruba. Gust alitembeza mashua yetu kwa ufundi kwa siku 30 katika zoruba yenye hatari mupaka wakati tulifika katika visiwa vya Bahamas.

‘ULITANGAZE KATI YA VISIWA’

Kisha kuhubiri kwa miezi kidogo katika visiwa vidogo-vidogo vya Bahamas, tulisafiri kwa mashua mupaka visiwa vya Leeward (Les îles Sous-le-Vent) na Windward (Les îles du Vent). Visiwa hivyo vidogo-vidogo vinaenea katika eneo la kilometre karibu 800 kati ya visiwa vya Îles Vierges na vya Trinité. Kwa miaka tano, tulihubiri zaidi sana katika visiwa vya mbali kwenye hakukuwa Mashahidi. Wakati fulani, hatukukuwa na namna ya kutuma ao kupokea barua kwa majuma fulani. Lakini, tulifurahi sana kuhubiria watu juu ya Yehova “kati ya visiwa”!—Yeremia 31:10.

Kikundi cha wamisionere katika Sibia (kushoto mupaka kuume): Ron Parkin, Dick Ryde, Gust Maki, na Stanley Carter

Wakati tulisimamisha mashua kwenye inchi kavu, wakaaji wa vijiji walikuwa wanafurahi sana na walikuwa wanajikusanya pembeni ya mashua ili kuona kama tulikuwa watu gani. Wengine walikuwa hawajaonaka mashua kama ile yenye tulikuwa nayo ao muzungu. Wakaaji wa visiwa walikuwa watu wenye urafiki na wenye kujua Biblia muzuri. Mara nyingi, walitupatia samaki za mubichi, avocats, na kalanga. Hata kama mashua yetu haikukuwa na nafasi nyingi, tulikuwa tunapika, tunalala, na kufua manguo yetu humo.

Tulikuwa tunaenda inchi kavu na kutembelea watu muchana wote. Tuliwaambia kama kutakuwa hotuba yenye kuzungumuzia Biblia. Kisha, mangaribi tulipiga kengele ya mashua. Tulifurahi sana kuona watu wanakuja. Taa zao za mafuta zilionekana kama nyota zenye kungaa zenye zilikuwa zinatokea ngambo ya milima. Wakati fulani watu mia moja hivi walikuja, na waliuliza maulizo mupaka usiku sana. Walifurahia kuimba, kwa hiyo, tuliwaandikia nyimbo fulani za Ufalme kwa kutumia mashini. Sisi wote ine tulifanya yetu yote ili kuimba nyimbo hizo. Kisha watu walianza kuimba pamoja na sisi, na walikuwa wanaimba na sauti za muzuri sana. Huo ulikuwa wakati wenye kufurahisha sana!

Kisha funzo la Biblia, wanafunzi fulani walikuwa wanaenda pamoja na sisi kwenye familia ingine yenye tulikuwa tunatembelea ili wakuwe pia kwenye funzo hilo. Kisha kupitisha majuma mahali fulani, tuliondoka. Lakini, mara nyingi tulikuwa tunaomba wale wenye kupendezwa sana waendelee kujifunza na wengine mupaka wakati tungerudia. Tulifurahi sana kuona namna watu fulani kati yao walikamata mugao wao kwa uzito.

Leo, visiwa vingi kati ya visiwa hivyo vinajaa watembeaji (touristes) wengi sana, lakini zamani vilikuwa mahali pa kimya penye kuwa tu nyangwa (maji yenye haina urefu pembeni ya bahari) za maji yenye rangi ya samawati (rangi ya bleu yenye kuchangana na ya kijani), sehemu za pembeni ya bahari zenye muchanga, na miti ya mingazi. Mara nyingi, tulikuwa tunasafiri usiku ili kutoka kwenye kisiwa kimoja na kuenda kwenye kisiwa kingine. Samaki wenye kuitwa dolfini walikuwa wanacheza-cheza pembeni yetu, na tulikuwa tunasikia tu mulio wa mashua yetu yenye kutembea juu ya maji. Mwangaza wa mwezi kwenye bahari ulionekana kama njia yenye rangi ya feza yenye kuongoza mbali sana.

Kisha kuhubiri miaka tano katika visiwa, tulisafiri katika mashua na kuenda Porto Rico ili kuuza mashua ya mupya, yenye kuwa na motere. Wakati tulifika huko, nilikutana na Maxine Boyd, dada mumoja misionere mwenye sura ya muzuri sana na nikamupenda. Alikuwa muhubiri mwenye bidii wa habari njema tangu utoto wake. Kisha, alikuwa misionere katika Jamhuri ya Dominika kuanzia mwaka wa 1950, wakati serikali ya Wakatoliki ilimulazimisha aondoke. Kwa sababu nilikuwa mumoja wa watu wenye kutumika ndani ya mashua, niliruhusiwa kubakia katika inchi ya Porto Rico mwezi moja tu. Kisha hapo, nilipaswa kusafiri ili kuenda katika visiwa na kuwa mbali kwa miaka mingine kidogo. Kwa hiyo, nilijiambia mimi mwenyewe hivi: ‘Ronald, ikiwa unapenda mwanamuke huyu, unapaswa kutenda haraka.’ Kisha majuma tatu nilimuomba mukono, na kisha majuma sita tulioana. Mimi na Maxine tulipata mugao wa kufanya kazi ya umisionere katika inchi ya Porto Rico, kwa hiyo, sikupanda tena hata kidogo katika mashua hiyo ya mupya.

Katika mwaka wa 1956, tulianza kazi ya muzunguko, na tulifurahia kutembelea ndugu na dada. Wengi kati yao walikuwa masikini. Kwa mufano, katika kijiji cha Potala Pastillo, kulikuwa familia mbili za Mashahidi zenye zilikuwa na watoto wengi, na nilizoea kucheza nao filimbi. Niliuliza Hilda, mumoja kati ya watoto wanawake, ikiwa alipenda kuja na kuhubiri pamoja na sisi. Alisema hivi: “Ninapenda kuhubiri, lakini siwezi. Sina viatu.” Tulimuuzia viatu, na alikuja kuhubiri pamoja na sisi. Kisha miaka fulani, wakati mimi na Maxine tulienda Brooklyn katika mwaka wa 1972, dada mumoja mwenye alikuwa anatokea tu kumaliza Masomo ya Gileadi alikuja kuzungumuza na sisi. Alikuwa karibu kuenda katika mugao wake katika inchi ya Ekwado (Équateur), na alisema hivi: “Hamunikumbuke tena? Mimi ni yule mutoto mwanamuke wa kijiji cha Pastillo mwenye hakukuwa na viatu.” Kumbe alikuwa Hilda! Tulilia kwa sababu ya furaha!

Katika mwaka wa 1960, tulianza kutumika kwenye biro ya tawi ya Porto Rico, yenye ilikuwa katika nyumba ndogo katika muji wa Santurce, San Juan. Mwanzoni, mimi na Lennart Johnson ndio tulikuwa tunafanya kazi nyingi zaidi. Lennart Johnson na bibi yake walikuwa Mashahidi wa kwanza katika Jamhuri ya Dominika, na katika mwaka wa 1957, walihamia Porto Rico. Kisha, Maxine alifanya kazi ya kutuma magazeti kwa watu wenye walikuwa wamejiandikisha. Kila juma, alikuwa anatuma magazeti zaidi ya elfu moja. Alifurahia kufanya kazi hiyo kwa sababu alikuwa anafikiria watu wote hao wenye walikuwa wanajifunza juu wa Yehova.

Nimefurahia kutumika kwenye Beteli kwa sababu kazi hiyo inanisaidia nitumie nguvu zangu katika kazi ya Yehova. Lakini, haiko mwepesi sikuzote. Kwa mufano, kwenye mukusanyiko wa kwanza wa kimataifa katika inchi ya Porto Rico, mwaka wa 1967, nilikuwa na mambo mengi sana yenye nilipaswa kupanga. Nathan Knorr, mwenye alikuwa anaongoza kazi ya Mashahidi wa Yehova, alikuja huko Porto Rico. Aliwaza kama sikupanga kazi ya kusafirisha wamisionere wageni, lakini nilikuwa nimeipanga. Kisha, alinipatia mashauri makali juu ya kuwa mwenye kupanga mambo muzuri na alisema kama nilimuvunja moyo. Sikupenda kubishana naye, lakini niliona kama hakunitendea kwa haki, na jambo hilo lilinivunja moyo kwa wakati fulani. Lakini, wakati mwingine mimi na Maxine tulikutana na ndugu Knorr. Alituita katika chumba chake na kutupikia chakula.

Tulitembelea mara nyingi watu wa familia yangu katika inchi ya Uingereza. Baba yangu hakukubali kweli wakati mimi na Mama tuliikubali. Lakini wakati ndugu wenye kutumika kwenye Beteli walikuwa wanatembelea eneo lao, mara nyingi mama yangu aliwakaribisha nyumbani kwetu. Baba yangu aliona kama ndugu hao wenye kusimamia kazi mbalimbali kwenye Beteli walikuwa wanyenyekevu. Walikuwa tofauti na viongozi wa dini wenye walikuwa wamemuchukiza kwa miaka mingi. Mwishowe, katika mwaka wa 1962, alibatizwa na kuwa Shahidi ya Yehova.

Mimi na Maxine katika Porto Rico kisha tu kufunga ndoa na tunakumbuka miaka 50 ya ndoa yetu katika mwaka wa 2003

Maxine, bibi yangu mupendwa, alikufa katika mwaka wa 2011. Ninangojea kabisa kwa hamu kumuona tena wakati wa ufufuo. Tumaini hilo linanifurahisha sana! Katika miaka 58 yenye tuliishi pamoja, tuliona hesabu ya Mashahidi wa Yehova katika inchi ya Porto Rico inaongezeka kutoka 650 hivi mupaka 26000! Kisha, katika mwaka wa 2013, Beteli ya Porto Rico ilitiwa pamoja na Beteli ya inchi ya Amerika, na niliombwa kutumika huko Wallkill, New York. Kisha miaka 60 kwenye kisiwa hicho, nilijisikia kama coqui, chura mudogo wa Porto Rico mwenye kujulikana sana. Chura huyo anaishi katika miti na anaimba ko-kee, ko-kee wakati wa mangaribi. Nilikuwa mwenye furaha sana katika inchi ya Porto Rico, lakini sasa nilipaswa kuhama.

‘MUNGU ANAPENDA MUTOAJI MUCHANGAMUFU’

Ningali ninafurahia kutumikia Mungu kwenye Beteli. Niko sasa na miaka zaidi ya 90, na kazi yangu ni kutia Wanabeteli moyo. Tangu wakati nilifika Wallkill, nimetembelea ndugu na dada zaidi ya 600. Ndugu na dada fulani wenye wanakuja kuniona wanapenda kuzungumuzia magumu yao ya pekee ao ya familia. Wengine wanapenda kupata mashauri juu ya namna wanaweza kufanya kwa furaha kazi yao kwenye Beteli. Lakini wengine wako na lazima ya mashauri kwa sababu wameoa hivi karibuni ao wamepata mugao mupya wa kuwa mapainia. Ninasikiliza kila mutu mwenye kuzungumuza na mimi, na ikiwa inafaa, mara nyingi ninawaambia hivi: “‘Mungu anapenda mutoaji muchangamufu.’ Kwa hiyo, fanya kazi yako kwa furaha. Ni kazi ya Yehova.”—2 Wakorintho 9:7.

Ikiwa unapenda kuwa na furaha kwenye Beteli ao mahali pengine, unapaswa kukumbuka sikuzote sababu gani kazi yako ni ya maana. Kazi yote yenye tunafanya kwenye Beteli ni utumishi mutakatifu. Inasaidia “mutumwa mwaminifu na mwenye busara” atolee ndugu na dada chakula cha kiroho katika dunia yote. (Mathayo 24:45) Kila mahali kwenye tunamutumikia Yehova, tuko na nafasi nyingi za kumusifu. Tufurahie basi kazi yenye anatuomba tufanye, kwa sababu ‘Mungu anapenda mutoaji muchangamufu.’

^ fu. 13 Habari juu ya maisha ya Leonard Smith inapatikana katika gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 15 Mwezi wa 4, 2012.