Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ndoa—Ilianza Namna Gani na Iko na Kusudi Gani?

Ndoa—Ilianza Namna Gani na Iko na Kusudi Gani?

“Yehova Mungu akaendelea kusema: ‘Si vema [haiko muzuri] huyo mwanaume aendelee kuwa peke yake. Nitamufanyia musaidizi, akuwe kikamilisho chake.’”MWANZO 2:18.

NYIMBO: 36, 11

1, 2. (a) Ndoa ilianza namna gani? (b) Bibi na bwana wa kwanza walipaswa kutambua nini juu ya ndoa? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

NI JAMBO la kawaida kuoa ao kuolewa. Lakini, ndoa ilianza namna gani, na iko na kusudi gani? Kujua hilo kutatusaidia tukuwe na mawazo ya muzuri juu ya ndoa na baraka zake. Mungu aliumba Adamu, mwanaume wa kwanza, na akamupatia kazi ya kupanga wanyama majina. Adamu aliona kama wanyama wote walikuwa wawili-wawili, ‘lakini kwa ajili ya huyo mwanaume hakupatikana musaidizi wa kuwa kikamilisho chake.’ Kwa hiyo, Mungu alimulalisha Adamu usingizi muzito, na kisha akakamata ubavu wake na akafanya mwanamuke. Yehova alimuletea Adamu mwanamuke huyo, na akakuwa bibi yake. (Soma Mwanzo 2:20-24.) Hilo linaonyesha kama ndoa ni zawadi kutoka kwa Yehova.

2 Kisha miaka mingi, Yesu alirudilia maneno haya yenye Yehova alikuwa amesema katika shamba la Edeni: ‘Mwanaume atamuacha baba yake na mama yake naye atashikamana na muke [bibi] wake, na hao wawili watakuwa mwili mumoja.’ (Mathayo 19:4, 5) Kwa sababu Mungu alitumia ubavu wa Adamu ili kuumba mwanamuke, bibi na bwana hao walipaswa kutambua kama kila mumoja alifanywa kwa ajili ya mwengine. Yehova hakupenda hata kidogo bibi na bwana wavunje ndoa yao ao mutu akuwe na bibi ao bwana wengi.

NDOA NI SEHEMU YA KUSUDI LA YEHOVA

3. Ni nini lilikuwa kusudi kubwa la ndoa?

3 Adamu alifurahia bibi yake, na kisha alimupatia jina la Eva. Alikuwa musaidizi na kikamilisho chake. Adamu na Eva wangefurahia kuishi pamoja wakiwa bibi na bwana. (Mwanzo 2:18) Kusudi kubwa la ndoa lilikuwa kuzaa watoto ili kujaza dunia. (Mwanzo 1:28) Watoto wanaume na wanawake wangependa wazazi wao, lakini kisha wangewaacha ili kuoa ao kuolewa na kuanzisha familia zao wenyewe. Wanadamu wangejaza dunia na kuifanya yote ikuwe paradiso.

4. Ni nini ilifikia ndoa ya kwanza?

4 Ndoa ya kwanza iliharibika wakati Adamu na Eva walikosa kumutii Yehova. “Nyoka wa zamani,” ni kusema, Shetani Ibilisi, alidanganya Eva na kumuambia kama, akikula tunda la ‘muti wa ujuzi wa mema na mabaya’ angekuwa na ujuzi wa pekee. Shetani alisema kama ikiwa Eva anakula tunda la muti huo, hilo lingefanya ajue mema na mabaya. Eva hakuheshimia Adamu mwenye alikuwa kichwa cha familia wakati aliamua kula tunda hilo mbele ya kuzungumuza kwanza na bwana yake. Na Adamu naye alikosa kutii Mungu wakati alikubali tunda lenye bibi yake alimupatia.—Ufunuo 12:9; Mwanzo 2:9, 16, 17; 3:1-6.

Ili ndoa ikuwe ya muzuri, bibi na bwana wanapaswa kutii Yehova na kukubali matokeo ya matendo yao

5. Majibu yenye Adamu na Eva walimupatia Yehova yanatufundisha nini?

5 Wakati Yehova aliwauliza, Adamu alisema kama ni kosa la bibi yake. Alisema hivi: ‘Mwanamuke uliyenipa akuwe pamoja na mimi, alinipa tunda kutoka katika ule muti na mimi nikakula.’ Eva naye alisema kama ni kosa la nyoka kwa sababu nyoka ndiye alimudanganya. (Mwanzo 3:12, 13) Adamu na Eva walitoa sababu zenye hazikukuwa na musingi juu ya tendo lao la kukosa kutii, na Yehova aliwahukumu waasi hao. Kwa kweli, mufano wao ni angalisho kwetu! Ili ndoa ikuwe ya muzuri, bibi na bwana wanapaswa kutii Yehova na kukubali matokeo ya matendo yao.

6. Namna gani unaweza kufasiria andiko la Mwanzo 3:15?

6 Hata kama Shetani aliharibisha mambo katika Edeni, Yehova alitolea wanadamu tumaini juu ya wakati unaokuja. Tumaini hilo linaonyeshwa katika unabii wa kwanza wa Biblia. (Soma Mwanzo 3:15.) Unabii huo ulionyesha kama “uzao” wa ‘mwanamuke’ utaponda Shetani. Viumbe wengi wa roho waaminifu wenye kumutumikia Yehova mbinguni wako na urafiki wa sana pamoja naye. Wako kama vile mwanamuke wa Yehova. Angetuma mutu mumoja kati ya viumbe hao wa roho ili ‘kuponda’ Ibilisi. Uzao huo ungewezesha wanadamu wenye kutii wapate tena mambo yenye bibi na bwana wa kwanza walipoteza. Wanadamu wenye kutii watakuwa na nafasi ya kuishi milele duniani, kama vile Yehova alikusudia.—Yohana 3:16.

7. (a) Ndoa imepatwa na nini kuanzia wakati Adamu na Eva walimuasi Mungu? (b) Biblia inaomba bibi na bwana wafanye nini?

7 Kwa sababu Adamu na Eva walimuasi Mungu, hilo lilikuwa na matokeo ya mubaya sana juu ya ndoa yao na ndoa zingine zote. Kwa mufano, Eva na watoto wote wanawake wenye angezaa wangepata maumivu makali wakati wa kuzaa. Wanawake wangetamani sana bwana zao wawapende na kuwahangaikia, lakini bwana zao wangewatawala, na hata kuwatendea mubaya wakati fulani kama vile tunaona leo. (Mwanzo 3:16) Yehova anaomba bwana watumie ukichwa wao kwa upendo katika familia, na anaomba bibi wajitiishe kwa bwana zao. (Waefeso 5:33) Ikiwa bibi na bwana Wakristo wanatumika pamoja, wanaweza kumaliza magumu mengi.

HISTORIA YA NDOA KUANZIA WAKATI WA ADAMU MUPAKA WAKATI WA GARIKA

8. Eleza historia ya ndoa kuanzia wakati wa Adamu mupaka wakati wa Garika.

8 Mbele Adamu na Eva wakufe, walizaa watoto wengi wanaume na wanawake. (Mwanzo 5:4) Kaini, mutoto wao wa kwanza, alioa mwanamuke mumoja wa jamaa yao. Lameki, wa kizazi cha Kaini ndiye mwanaume wa kwanza mwenye Biblia inaonyesha kama alikuwa na bibi wawili. (Mwanzo 4:17, 19) Kuanzia wakati wa Adamu mupaka wakati wa Noa, ni watu kidogo tu ndio walikuwa wanamuabudu Yehova. Kati ya watu waaminifu hao kulikuwa Abeli, Enoko, Noa na watu wa familia yake. Biblia inasema kama wakati wa Noa, ‘wana wa Mungu wa kweli walianza kuwaona mabinti [watoto wanawake] wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza. Nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.’ Lakini jambo hilo halikukuwa la kawaida, na malaika walizaa pamoja na wanawake hao watoto wenye jeuri ambao walikuwa warefu na wanene sana. Watoto hao waliitwa Wanefili. Wakati huo, “ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani” na ‘kila mwelekeo wa fikira [mawazo] za moyo wake ulikuwa mubaya tu wakati wote.’—Mwanzo 6:1-5.

9. Yehova alifanya nini juu ya watu waovu katika siku za Noa, na tunaweza kujifunza nini juu ya mambo yenye yalitokea wakati huo?

9 Yehova alisema kama angeleta garika kubwa katika dunia ili kuharibu watu wote waovu. ‘Noa, muhubiri wa uadilifu [haki],’ aliambia watu hao juu ya Garika yenye ilikuwa inakuja. (2 Petro 2:5) Lakini hawakusikiliza Noa kwa sababu walikuwa na mambo mengi ya kufanya katika maisha yao ya kila siku, kama vile kuoa ao kuolewa. Yesu alifananisha wakati wa Noa na wakati wetu. (Soma Mathayo 24:37-39.) Leo, watu wengi hawasikilize habari njema ya Ufalme wa Mungu yenye tunahubiri. Tunahubiri habari hiyo mbele ulimwengu huu muovu uharibiwe. Mambo yenye yalitokea wakati wa Garika yanaweza kutufundisha nini? Hatupaswe kuacha mambo kama vile ndoa na kuwa na watoto yakuwe ya maana sana katika maisha yetu na kutufanya tusahau kama siku ya Yehova iko karibu.

HISTORIA YA NDOA KUANZIA WAKATI WA GARIKA MUPAKA WAKATI WA YESU

10. (a) Ni tabia gani yenye ilienea katika desturi nyingi? (b) Namna gani Abrahamu na Sara walionyesha mufano muzuri katika ndoa yao?

10 Noa na watoto wake watatu walikuwa na bibi mumoja tu kila mutu. Lakini, kisha Garika, wanaume wengi walioa bibi wengi. Katika desturi nyingi, mambo ya uasherati yalienea sana na yalikuwa hata katika mambo ya dini. Wakati Abrahamu na Sara walihamia Kanaani, walikuwa wanaishi kati ya watu wenye kufanya mambo ya uasherati, watu hao hawakuheshimia ndoa. Yehova aliharibu muji wa Sodoma na Gomora kwa sababu ya mambo hayo. Abrahamu alikuwa tofauti na watu hao. Alitumia muzuri ukichwa wake katika familia, na Sara alionyesha mufano muzuri kwa sababu alikuwa mwanamuke mwenye kujitiisha. (Soma 1 Petro 3:3-6.) Abrahamu alifanya mipango ili mutoto wake Isaka aoe bibi mwenye alikuwa anaabudu Yehova. Na Isaka alifanya hivyo juu ya mutoto wake Yakobo, na watoto wa Yakobo wakakuwa mababu wa makabila 12 ya Israeli.

11. Namna gani Sheria ya Musa ililinda Waisraeli?

11 Kisha, Yehova alifanya agano, ao mapatano, pamoja na taifa la Israeli. Aliwapatia Sheria ya Musa, yenye ililinda bibi na bwana katika ibada yao kwa Yehova. Kwa mufano, kulikuwa sheria juu ya mambo ya ndoa, sheria fulani zilihusu wale wenye walioa wanawake wengi. Pia Waisraeli walikatazwa kuoa ao kuolewa na watu wenye hawakuabudu Yehova. (Soma Kumbukumbu la Torati 7:3, 4.) Wakati matatizo mazito yalitokea katika ndoa, wazee walikuwa wanasaidia. Kulikuwa pia sheria zenye zilikataza kukosa uaminifu katika ndoa, kuwa na wivu, na kuwa na mashaka juu ya bibi ao bwana. Kuvunja ndoa kuliruhusiwa, lakini kulikuwa sheria zenye zililinda bibi na bwana. Kwa mufano, mwanaume angevunja ndoa na bibi yake kwa sababu ya “kitu fulani kisichofaa.” (Kumbukumbu la Torati 24:1) Biblia haieleze ikiwa kitu hicho “kisichofaa” kilikuwa kitu gani, lakini bwana hakupaswa kutumia makosa ya kidogo-kidogo kuwa sababu ya kuvunja ndoa na bibi yake.—Mambo ya Walawi 19:18.

ENDELEA KUWA MUSHIKAMANIFU KWA BIBI AO BWANA YAKO

12, 13. (a) Namna gani wanaume fulani walikuwa wanatendea bibi zao wakati wa nabii Malaki? (b) Leo, ni nini inaweza kufikia mutu mwenye kubatizwa ikiwa anakimbia na bibi ao bwana mwenye haiko wake?

12 Wakati wa nabii Malaki, bwana wengi Wayahudi walitumia kila sababu ili kuvunja ndoa na bibi zao. Wanaume hao walivunja ndoa na bibi zao ili waoe wanawake vijana ao wanawake wenye hawakutumikia Yehova. Wakati wa Yesu, wanaume hao Wayahudi walikuwa wangali wanatumia “kila sababu” ili kuvunja ndoa na bibi zao. (Mathayo 19:3) Yehova alichukia tabia hizo za kuvunja ndoa bila sababu yenye kupatana na sheria.—Soma Malaki 2:13-16.

13 Leo, kukosa ushikamanifu katika ndoa hakukubaliwe kati ya watu wa Yehova, na jambo hilo halitokee mara nyingi. Lakini, wazia kuwa mutu mwenye kubatizwa anafanya uzinifu na anavunja ndoa yake ili kuoa ao kuolewa na mutu mwengine. Ikiwa mutu huyo hatubu, anaweza kutengwa ili kutaniko libakie safi. (1 Wakorintho 5:11-13) Mutu huyo anapaswa ‘kuzaa matunda yanayofaa toba’ mbele ya kurudishwa katika kutaniko. (Luka 3:8; 2 Wakorintho 2:5-10) Hakuna wakati fulani wenye kuwekwa ambao unapaswa kupita mbele mutu huyo arudishwe katika kutaniko. Kwa kweli, inaweza kuomba mwaka ao zaidi ili mutu fulani mwenye alitenda zambi aonyeshe kama ametubu kwelikweli na ili arudishwe katika kutaniko. Na hata kisha kurudishwa, mutu huyo angali ‘atasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu’ ili kuonyesha ikiwa toba yake ilikuwa ya kweli ao hapana.—Waroma 14:10-12; soma gazeti Munara wa Mulinzi la tarehe 1 Mwezi wa 4, 1981, ukurasa wa 22-23.

NDOA KATI YA WAKRISTO

14. Sheria ilikuwa na kusudi gani kubwa?

14 Taifa la Israeli liliongozwa na Sheria ya Musa kwa miaka zaidi ya 1500. Sheria hiyo ilisaidia watu wa Mungu katika njia nyingi. Kwa mufano, ilitolea watu kanuni mbalimbali zenye ziliwasaidia kumaliza matatizo katika familia, na iliwaongoza kwenye Masiya. (Wagalatia 3:23, 24) Wakati Yesu alikufa, Sheria ilifikia mwisho wake na Mungu alifanya mupango mupya. (Waebrania 8:6) Lakini, kuko mambo fulani yenye watu waliruhusiwa kufanya katika Sheria ya Musa yenye Wakristo hawakuruhusiwa tena kufanya.

15. (a) Katika kutaniko la Kikristo, ni kanuni gani yenye inapaswa kuongoza ndoa? (b) Mukristo anapaswa kuchunguza mambo gani ikiwa anafikiria kuvunja ndoa yake?

15 Siku moja Mafarisayo waliuliza Yesu ulizo juu ya ndoa. Yesu alijibu kama, katika Sheria ya Musa, Mungu aliruhusu Waisraeli kuvunja ndoa hata kama hakutaka jambo hilo tangu mwanzo. (Mathayo 19:6-8) Jibu la Yesu lilionyesha kama kanuni yenye Mungu aliweka mwanzoni kwa ajili ya ndoa ndiyo ingeongoza sasa Wakristo. (1 Timotheo 3:2, 12) Kwa sababu wamekuwa ‘mwili moja,’ bibi na bwana walipaswa kuendelea kuishi pamoja. Kupenda Mungu na kupendana wao wenyewe kungefanya waendelee kuwa na umoja. Bibi ao bwana mwenye anavunja ndoa yake bila sababu ya uzinifu haruhusiwe kuoa ao kuolewa tena. (Mathayo 19:9) Mutu anaweza kuamua kusamehe bibi ao bwana yake mwenye alifanya uzinifu lakini anatubu. Kwa mufano, nabii Hosea alisamehe Gomeri, bibi yake mwenye alifanya uzinifu, na Yehova alisamehe Waisraeli wenye walitubu. (Hosea 3:1-5) Tena, ikiwa mutu anajua kuwa bibi ao bwana yake alifanya uzinifu na anaamua kufanya tena naye kitendo cha ndoa, hilo linaonyesha kama amemusamehe. Hakuna tena sababu ya Maandiko yenye kumuruhusu avunje ndoa yake.

16. Yesu alisema nini juu ya kubakia bila kuoa ao kuolewa?

16 Yesu alisema kama sababu moja tu yenye inaweza kufanya Mukristo wa kweli avunje ndoa yake ni uzinifu. Kisha alizungumuzia “wale walio na hiyo zawadi” ya kuishi bila kuoa ao kuolewa. Yesu alisema kama mutu mwenye anaweza kufanya hivyo na afanye hivyo. (Mathayo 19:10-12) Wakristo wengi wanaamua kubakia bila kuoa ao kuolewa kwa sababu wanapenda kumutumikia Yehova bila kukengeushwa, na tunapaswa kabisa kuwapongeza kwa sababu ya uamuzi wao!

17. Ni nini inaweza kusaidia Mukristo aamue ikiwa ataoa ao kuolewa?

17 Ni nini inaweza kusaidia mutu aamue ikiwa atabakia bila kuoa ao kuolewa? Mutu anapaswa kuamua ikiwa atafurahia kubakia bila kuoa ao kuolewa. Mutume Paulo alitoa shauri la kubakia bila kuoa ao kuolewa. Lakini alisema tena hivi: ‘Kwa sababu ya kuenea kwa uasherati, kila mwanaume na akuwe na muke wake mwenyewe na kila mwanamuke akuwe na mume [bwana] wake mwenyewe.’ Paulo aliongeza hivi: “Ikiwa hawawezi kujizuia, acheni wafunge ndoa, kwa maana ni bora [muzuri zaidi] kufunga ndoa kuliko kuwaka tamaa.” Kwa hiyo, mutu anaweza kuamua kuoa ao kuolewa ili aepuke tamaa zenye nguvu za ngono zimufanye aangukie katika tabia ya kugusa-gusa viungo vya uzazi ili kuamusha tamaa ya ngono ao katika uasherati. Lakini, vijana wenye hawajaoa ao kuolewa wanapaswa kufikiria ikiwa wamekomaa kabisa ili kufunga ndoa. Paulo alisema hivi: ‘Kama yeyote akiona kwamba anajiendesha isivyofaa kuelekea ubikira wake, ikiwa huo umepita upeo wa ujana, na hivyo ndivyo inavyopaswa kutendeka, acheni afanye lile analotaka; hafanye zambi. Acheni afunge ndoa.’ (1 Wakorintho 7:2, 9, 36; 1 Timotheo 4:1-3) Mutu hapaswe kuchochewa aoe ao kuolewa kwa sababu tu ana tamaa zenye nguvu zenye vijana wengi wanaweza kuwa nazo wakati wa ujana wao. Mutu huyo anaweza kuwa hajakomaa kabisa ili kutimiza madaraka ya ndoa.

18, 19. (a) Katika kutaniko la Kikristo, ni nani wanapaswa kuoana? (b) Tutazungumuzia nini katika habari yenye kufuata?

18 Katika kutaniko la Kikristo, ni mwanaume na mwanamuke wenye kubatizwa na wenye kumupenda Yehova kwa moyo wao wote ndio wanapaswa kuoana. Pia, wanapaswa kupendana sana na kwa hiyo wakuwe tayari kuishi pamoja maisha yao yote. Yehova atawabariki kwa sababu walitii shauri la kuoa ao kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Na ndoa yao itakuwa ya muzuri ikiwa wanaendelea kutii mashauri ya Biblia.

19 Leo, tunaishi katika “siku za mwisho,” na watu wengi hawana sifa zenye kufanya ndoa ikuwe ya muzuri. (2 Timotheo 3:1-5) Katika habari yenye kufuata, tutazungumuzia kanuni za maana sana za Biblia zenye zinaweza kusaidia Wakristo wakuwe na ndoa ya muzuri na yenye furaha hata kama wako na mugumu mengi. Hilo litawasaidia waendelee kutembea katika njia yenye kuongoza kwenye uzima wa milele.—Mathayo 7:13, 14.