Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Endelea Kupigana ili Upate Baraka za Yehova

Endelea Kupigana ili Upate Baraka za Yehova

“Umeshindana [umepigana] na Mungu na wanadamu hata ukashinda [ukapata ushindi] mwishowe.”—MWANZO 32:28.

NYIMBO: 60, 38

1, 2. Watumishi wa Yehova wanapigana na nini?

 WATUMISHI wote waaminifu wa Mungu wamepigana kwa ajili ya imani yao, tangu Abeli mupaka watumishi washikamanifu wa leo. Mutume Paulo aliambia Wakristo Waebrania kama ‘walivumilia shindano [pambano] kubwa chini ya mateso’ kwa sababu walijikaza ili wakubaliwe na Yehova na wapate baraka zake. (Waebrania 10:32-34) Mutume Paulo alilinganisha mapambano (ao vita) ya Wakristo na mapambano ya wachezaji wenye walikuwa wanapambana katika michezo ya Wagiriki, kama vile muchezo wa kukimbia, kupigana mweleka (muchezo wa kuangushana), na muchezo wa kupigana ngumi (boxe). (Waebrania 12:1, 4) Leo, tuko katika shindano la mbio kwa ajili ya uzima, na tuko na maadui wenye wanapenda kutukengeusha na kutufanya tupoteze furaha yetu leo na tukose baraka zetu za wakati unaokuja.

2 Pigano la nguvu sana lenye tuko nalo, ao “kushindana mweleka,” ni kupigana na Shetani na ulimwengu wake. (Waefeso 6:12) Ni jambo la maana sana tuepuke kuchochewa na mafundisho ya ulimwengu huu, filozofia, na matendo ya mubaya, kama vile kufanya uasherati, kuvuta tumbako, kunywa pombe sana na kutumia dawa za kulewesha. Pia, tunapaswa kuendelea kupiganisha mambo yenye yanaweza kutuvunja moyo na kupiganisha uzaifu wetu wenyewe.—2 Wakorintho 10:3-6; Wakolosai 3:5-9.

3. Namna gani Yehova anatuzoeza ili tupigane na maadui wetu?

3 Tunaweza kabisa kupata ushindi juu ya maadui hao wenye nguvu? Ndiyo, lakini haiko vyepesi! Paulo alijilinganisha na mutu mwenye kupigana ngumi. Alisema hivi: ‘Jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisikuwe ninapiga hewa.’ (1 Wakorintho 9:26) Kama vile mutu mwenye kupigana ngumi anapigana na mwenzake, sisi pia tunapaswa kupigana na maadui wetu. Yehova anatusaidia na anatuzoeza ili tupigane na maadui hao. Anafanya hivyo kupitia Biblia. Pia, anatusaidia kupitia vichapo vyetu vyenye kuzungumuzia Biblia, mikutano yetu ya Kikristo, na mikusanyiko yetu. Unatumia mazoezi yote yenye unapata? Kama haufanye vile, inaweza kuwa haupigane kabisa na adui yako, utakuwa kama vile mutu mwenye kupiga ngumi katika hewa.

4. Tunapaswa kufanya nini ili tuepuke kushindwa na mambo maovu?

4 Tunapaswa kuwa macho kila wakati. Sababu gani? Maadui wetu wanaweza kutupiganisha wakati hatuwazie ao wakati tuko wazaifu. Biblia inatuonya na inatutia moyo hivi: “Usiache ushindwe na uovu, bali [lakini] endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Waroma 12:21) Ikiwa tunaendelea kupigana na Shetani, tunaweza kupata ushindi! Lakini, ikiwa hatuko tena waangalifu na tunaacha kupigana, hatuwezi kupata ushindi juu ya Shetani, ulimwengu wake, na juu ya uzaifu wetu. Kwa hiyo, usichoke hata kidogo. Usivunjike moyo na usiache mikono yako iregee!—1 Petro 5:9.

5. (a) Tunapaswa kukumbuka nini ili tukubaliwe na Mungu na tupate baraka zake? (b) Tutazungumuzia watu gani wenye kutajwa katika Biblia?

5 Ili tupate ushindi, tunapaswa kukumbuka sababu gani tunapigana. Ni kwa sababu tunataka tukubaliwe na Mungu na tupate baraka zake. Andiko la Waebrania 11:6 linasema hivi: ‘Yule anayemukaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye iko na kwamba yeye anakuwa musawabishaji [mwenye kulipa] wale wanaomutafuta kwa bidii.’ Kumutafuta Yehova kwa bidii kunamaanisha kuwa tunapaswa kujikaza sana ikiwa tunataka tukubaliwe naye. (Matendo 15:17) Biblia inazungumuzia mifano mingi ya muzuri ya wanaume na wanawake wenye walifanya hivyo. Yakobo, Raheli, Yosefu, na Paulo walipiganisha magumu mengi ya kimwili na ya moyoni, lakini walipata ushindi. Mifano yao inaonyesha kama ikiwa tunajikaza sana, sisi pia tunaweza kupata baraka za Yehova. Acha tuone namna gani.

UTAPATA BARAKA IKIWA UNAVUMILIA

6. Ni nini ilimusaidia Yakobo avumilie, na alipata baraka gani? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

6 Yakobo, mwanaume muaminifu, alipigana sana na alivumilia kwa sababu alimupenda Yehova na aliona urafiki wake pamoja naye kuwa wa maana sana. Alikuwa na imani kabisa katika ahadi ya Yehova ya kubariki uzao wake. (Mwanzo 28:3, 4) Wakati Yakobo alikuwa na miaka karibu 100, alipigana hata na malaika ili apate baraka za Mungu. (Soma Mwanzo 32:24-28.) Je, Yakobo alikuwa kabisa na uwezo wa kupigana na malaika huyo mwenye nguvu? Hapana! Lakini aliazimia kabisa kupigana, na alionyesha kama alikuwa tayari kujikaza sana ili apate baraka za Yehova! Yehova alibariki Yakobo kwa sababu ya uvumilivu wake, na alimupatia jina Israeli, lenye kumaanisha “Mwenye Kushindana, ao Kuvumilia, Pamoja na Mungu.” Yakobo alipata zawadi yenye sisi pia tunatafuta, ni kusema, kukubaliwa na Yehova na kupata baraka zake.

7. (a) Raheli alikuwa katika hali gani yenye kuvunja moyo? (b) Raheli alifanya nini, na alipata baraka gani?

7 Pia, Raheli, bibi mupendwa wa Yakobo, alikuwa na hamu ya kuona namna Yehova angetimiza ahadi yenye alipatia bwana yake. Lakini alikuwa na tatizo fulani. Raheli alikuwa hajakuwa na watoto, na kukosa watoto kuliletea wanawake huzuni nyingi wakati wa zamani. Namna gani Raheli aliendelea kupigana hata kama alikuwa katika hali yenye kuvunja moyo? Hakupoteza hata kidogo tumaini lake. Lakini, aliendelea kupigana kwa kusali sana kwa Yehova. Yehova alisikia sala ya Raheli, na aliona kuwa anabarikiwa wakati alifikia kuwa na watoto. Ndiyo sababu alisema hivi: ‘Nimepigana mieleka yenye nguvu . . . Na mimi nimekuwa mushindi!’—Mwanzo 30:8, 20-24.

8. Yosefu alipata magumu gani, na alituachia mufano gani muzuri?

8 Inawezekana mufano wa uaminifu wa Yakobo na Raheli ulichochea mutoto wao Yosefu na kumusaidia wakati alipata magumu katika maisha yake. Wakati Yosefu alikuwa na miaka 17, maisha yake yalibadilika kabisa. Ndugu zake walimusikilia wivu, na walimuuzisha katika utumwa. Kisha, alifanya miaka mingi katika gereza huko Misri, hata kama hakufanya kosa lolote. (Mwanzo 37:23-28; 39:7-9, 20, 21) Lakini Yosefu hakuvunjika moyo ao kukasirika, na hakujaribu kulipiza kisasi. Sababu gani? Kwa sababu aliona urafiki wake pamoja na Yehova kuwa wa maana sana na alikazia jambo hilo katika moyo wake. (Mambo ya Walawi 19:18; Waroma 12:17-21) Mufano wa Yosefu unaweza kutusaidia. Hata kama tulikuwa na maisha ya mubaya wakati tulikuwa watoto ao ikiwa leo tunaona kuwa hatuna tumaini katika maisha yetu, tunapaswa kuendelea kupigana kwa uvumilivu. Ikiwa tunafanya hivyo, tunaweza kuwa hakika kama Yehova atatubariki.—Soma Mwanzo 39:21-23.

9. Namna gani tunaweza kuiga mufano wa Yakobo, Raheli, na Yosefu?

9 Leo, sisi pia tunaweza kuwa na lazima ya kuvumilia magumu makali. Pengine unateseka kwa sababu ya ukosefu wa haki, ubaguzi, ao kwa sababu mutu fulani anakusikilia wivu. Kuliko kuvunjika moyo, ukumbuke mambo yenye yalisaidia Yakobo, Raheli, na Yosefu waendelee kumutumikia Yehova kwa furaha. Mungu aliwatia nguvu na kuwabariki kwa sababu waliona urafiki wao pamoja naye kuwa wa maana sana. Waliendelea kushinda, ao kupigana, na kutenda kulingana na sala zao. Kwa sababu tunaishi katika siku za mwisho, ni jambo la maana tuendelee kuwa na tumaini lenye nguvu kwa ajili ya wakati unaokuja! Uko tayari kupigana, ni kusema, kujikaza sana, ili ukubaliwe na Yehova?

UKUWE TAYARI KUPIGANA ILI UPATE BARAKA

10, 11. (a) Sababu gani tunaweza kuwa na lazima ya kupigana ili tupate baraka za Mungu? (b) Ni nini itatusaidia tukamate maamuzi ya muzuri?

10 Sababu gani tunaweza kuwa na lazima ya kupigana ili tupate baraka za Mungu? Sababu moja ni kwamba hatukamilike, tunaweza kupiganisha tamaa fulani za mubaya. Wamoja wanapigana ili wakuwe na mawazo ya muzuri juu ya kazi ya kuhubiri, na wengine wanapigana kwa sababu ya matatizo ya afya ao kujisikia kuwa peke yao. Na kuko wengine wenye wanaona kuwa ni vigumu kusamehe mutu fulani mwenye aliwakosea. Hata kama tumetumikia Yehova kwa muda murefu ao hapana, sisi wote tuko na lazima ya kupiganisha mambo yenye yanaweza kutuzuia kutumikia Mungu, mwenye kubariki watu waaminifu.

Unaendelea kupigana ili upate baraka za Mungu? (Picha hii inapatana na fungu la 10, 11)

11 Kwa kweli, inaweza kuwa vigumu sana kuendelea kuwa Mukristo na kukamata maamuzi ya muzuri, zaidi sana wakati tunapiganisha tamaa za mubaya. (Yeremia 17:9) Ikiwa unajisikia hivyo, usali kwa Yehova na umuombe roho yake takatifu. Sala na roho takatifu vinaweza kukusaidia upate nguvu ya kufanya mambo ya muzuri, na kwa hiyo unaweza kupata baraka za Mungu. Uazimie kutenda kulingana na sala zako. Ujikaze kusoma Biblia kila siku, na upange wakati wa kufanya funzo la pekee na ibada ya familia.—Soma Zaburi 119:32.

12, 13. Ni nini ilisaidia Wakristo wawili waachane na tamaa ya mubaya?

12 Kuko mifano mingi yenye kuonyesha namna Neno la Mungu, roho yake, na vichapo vyetu vya Kikristo vimesaidia ndugu na dada zetu waachane na tamaa za mubaya. Kijana mumoja wa miaka kati ya 13 na 19 alisoma habari yenye kichwa “Unawezaje Kushinda Tamaa Mbaya?” katika gazeti Amuka! la tarehe 8 Mwezi wa 12, 2003. Alisema hivi: “Ninaendelea kupigana ili nizuie mawazo ya mubaya. Wakati nilisoma katika habari hiyo kama ‘kwa watu wengi pambano la kuachana na tamaa za mubaya ni kali zaidi,’ hilo lilinifanya nijisikie kuwa katika familia ya ndugu na dada. Niliona kama sikukuwa peke yangu.” Kijana huyo alipata pia faida kwa kusoma habari yenye kichwa “Je, Mungu Anakubali Ngono Isiyo ya Asili?” katika Amuka! ya tarehe 8 Mwezi wa 10, 2003. Katika habari hiyo, alitambua kama watu fulani wanapiganisha tamaa hizo kila siku, kama vile “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) Lakini, wakati wanapigana ili waendelee kuwa na mwenendo muzuri, wanakuwa na tumaini hakika juu ya wakati unaokuja. Kijana huyo alisema tena hivi: “Kwa sababu hiyo, ninafikiri kwamba ninaweza kuendelea kuwa muaminifu kila siku. Niko mwenye shukrani sana kwa Yehova kwa sababu anatumia tengenezo lake ili kutusaidia tupate ushindi kila siku katika ulimwengu huu muovu.”

13 Fikiria pia mufano wa dada mumoja katika inchi ya Amerika. Aliandika hivi: “Ninapenda kuwashukuru kwa sababu munaendelea kutupatia chakula cha kiroho chenye tuko nacho lazima na kwa wakati wenye kufaa. Mara nyingi ninaona kuwa habari hizo zimeandikwa tu kwa ajili yangu. Kwa miaka mingi, ninaendelea kupiganisha tamaa ya nguvu ili kuachana na tabia fulani yenye Yehova anachukia. Wakati fulani, ninataka kuregeza mikono yangu na kuacha kupigana. Ninajua kama Yehova ni mwenye rehema na mwenye kusamehe, lakini kwa sababu niko na tamaa hiyo ya mubaya na iko kabisa ndani ya moyo wangu na siichukie, nilijisikia kuwa Yehova hawezi kabisa kunisaidia. Pigano hilo la kila siku limekuwa na matokeo katika kila hali ya maisha yangu. . . . Kisha kusoma habari ‘Je, Una ‘Moyo wa Kumujua’ Yehova?’ katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 3, 2013, niliona kabisa kama Yehova anapenda kunisaidia.”

14. (a) Paulo aliona namna gani pigano lake? (b) Tunaweza kufanya nini ili tupate ushindi katika pigano juu ya uzaifu wetu?

14 Soma Waroma 7:21-25. Paulo alijionea kama ni vigumu sana kupiganisha tamaa za mubaya na uzaifu wetu. Hata hivyo, alikuwa hakika kama angepata ushindi katika pigano hilo ikiwa angesali kwa Yehova, kutegemea musaada wake, na kuonyesha imani katika zabihu ya Yesu ya ukombozi. Halafu sisi? Tunaweza kupata ushindi katika pigano juu ya uzaifu wetu? Ndiyo, ikiwa tuko na imani katika zabihu ya Yesu, tunaiga mufano wa Paulo na kumutegemea Yehova kabisa, kuliko kutegemea nguvu zetu wenyewe.

15. Namna gani Yehova anaweza kutusaidia tuendelee kuwa waaminifu na kuvumilia majaribu?

15 Wakati fulani Mungu anaweza kuacha tuonyeshe ikiwa tunahangaikia kabisa jambo fulani. Kwa mufano, utafanya nini ikiwa wewe ao mutu fulani wa familia yako anagonjwa sana ao anatendewa bila haki? Ikiwa unamutumainia Yehova kabisa, utamuomba akupatie nguvu yenye uko nayo lazima ili ubakie muaminifu na uendelee kuwa na furaha na urafiki wenye nguvu pamoja naye. (Wafilipi 4:13) Mifano ya Wakristo wengi waaminifu, wa zamani na wa leo, imeonyesha kama sala inaweza kututia nguvu na kutupatia ujasiri wenye tuko nao lazima ili tuendelee kuvumilia.

ENDELEA KUPIGANA ILI UPATE BARAKA ZA YEHOVA

16, 17. Unaazimia kufanya nini?

16 Shetani anapenda uvunjike moyo, uache kupigana na uregeze mikono yako. Kwa hiyo, uazimie ‘kushika sana yaliyo mazuri.’ (1 Wathesalonike 5:21) Unaweza kupata ushindi katika pigano lako juu ya Shetani, ulimwengu wake muovu, na kila tamaa ya mubaya! Unaweza kupata ushindi ikiwa unatumaini kabisa kama Mungu atakutia nguvu na kukusaidia.—2 Wakorintho 4:7-9; Wagalatia 6:9.

17 Kwa hiyo, endelea kupigana. Endelea kushindana. Endelea kupambana. Endelea kuvumilia. Unaweza kuwa hakika kabisa kama Yehova ‘atakumwangia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’—Malaki 3:10.