Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 5

Kuhuzuria Mikutano Kunaonyesha Nini Juu Yetu?

Kuhuzuria Mikutano Kunaonyesha Nini Juu Yetu?

‘Muendelee kutangaza kifo cha Bwana, mupaka wakati atakuja.’​—1 KO. 11:26.

WIMBO 18 Tunathamini Fidia

KIFUPI CHA HABARI *

1-2. (a) Yehova anaona nini wakati mamilioni ya watu wanakusanyika kwa ajili ya Chakula cha Mangaribi cha Bwana? (Ona picha ku jalada ya gazeti hii.) (b) Tutazungumuzia nini mu habari hii?

FIKIRIA jambo lenye Yehova anaona wakati mamilioni ya watu mu dunia yote wanakusanyika kwa ajili ya Chakula cha Mangaribi cha Bwana. Haangalie tu hesabu kubwa ya watu; lakini anaona kila mutu mwenye kuwa pale. Kwa mufano, anaona wale wenye wanahuzuria Ukumbusho kwa uaminifu kila mwaka. Kati yao kunaweza kuwa watu wenye wanakuja hata kama wanapambana na mateso makali. Wengine hawakuje ku mikutano yetu kwa ukawaida, lakini wanaona kuwa kuhuzuria ukumbusho ni jambo la maana lenye wanapaswa kufanya. Yehova anaona pia wale wenye pengine wamekuja ku Ukumbusho kwa mara ya kwanza, pengine kwa sababu wanapenda tu kujua ni nini inafanyika ku mukutano huo.

2 Kwa kweli, Yehova anapendezwa wakati anaona watu wengi sana wanakuja ku Ukumbusho. (Lu. 22:19) Lakini, jambo la maana zaidi lenye Yehova anahangaikia, haiko hesabu ya watu wenye wanakuja. Yehova anahangaikia zaidi sababu yenye kufanya watu wakuje; nia yao ni ya maana kwa Yehova. Mu habari hii, tutazungumuzia ulizo moja la maana sana: Juu ya nini hatuhuzurie tu Ukumbusho wa kila mwaka lakini pia tunahuzuria mikutano ya kila juma yenye Yehova anatayarisha kwa ajili ya watu wenye wanamupenda?

(Picha hizi zinapatana na fungu la 1-2) *

UNYENYEKEVU UNATUCHOCHEA KUHUZURIA MIKUTANO

3-4. (a) Juu ya nini tunahuzuria mikutano? (b) Wakati tunahuzuria mikutano, hilo linaonyesha nini juu yetu? (c) Kulingana na 1 Wakorinto 11:23-26, juu ya nini hatupaswe kukosa kuhuzuria Ukumbusho?

3 Sababu kubwa yenye kutuchochea tuhuzurie mikutano yetu ni juu iko sehemu ya ibada yetu. Pia, tunahuzuria kwa sababu tunafundishwa na Yehova ku mikutano. Watu wenye kiburi hawaamini kama wako na lazima ya kufundishwa jambo fulani. (3 Yo. 9) Lakini, sisi tuko na hamu ya kufundishwa na Yehova na tengenezo lenye anatumia.​—Isa. 30:20; Yoh. 6:45.

4 Wakati tunahuzuria mikutano, hilo linaonyesha kama tuko wanyenyekevu, na tuko tayari kufundishwa. Usiku wa kufanya Ukumbusho wa kifo cha Yesu, tunahuzuria tukio hilo la maana haiko kwa sababu tu tunaona kama tunapaswa kufanya vile, lakini pia kwa sababu tunatii kwa unyenyekevu amri hii ya Yesu: “Muendelee kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Soma 1 Wakorinto 11:23-26.) Mukutano huo unatia nguvu tumaini letu kwa ajili ya wakati wenye kuja na unatukumbusha namna Yehova anatupenda kabisa. Lakini, Yehova anajua kama tuko na lazima ya kutiwa moyo na kutiwa nguvu haiko tu mara moja mu mwaka. Kwa hiyo, anatutolea mikutano kila juma na anatutia moyo tuhuzurie ile mikutano. Unyenyekevu unatuchochea kutii. Tunatumia saa fulani kila juma ili kutayarisha na kuhuzuria ile mikutano.

5. Juu ya nini watu wanyenyekevu wanakubali mualiko wa Yehova?

5 Kila mwaka, Yehova anaalika watu ili awafundishe, na watu wengi wanyenyekevu wanakubali mualiko wake. (Isa. 50:4) Wanafurahia kuja ku Ukumbusho, na wanaanza kuja ku mikutano ingine. (Zek. 8:20-23) Sisi wote pamoja, tunafurahia kufundishwa na kuongozwa na Yehova, “musaidizi [wetu] na mwokozi [wetu].” (Zb. 40:17) Kwa kweli, hakuna jambo lenye kufurahisha zaidi, ao la maana zaidi, kuliko kukubali mualiko wa kufundishwa na Yehova na Yesu, Mwana wake mwenye anapenda sana.​—Mt. 17:5; 18:20; 28:20.

6. Namna gani unyenyekevu ulisaidia mwanaume mumoja ahuzurie Ukumbusho?

6 Kila mwaka, tunajikaza kualika watu wengi kabisa ili wahuzurie Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Watu wengi wanyenyekevu wamepata faida kwa kukubali mualiko wetu. Fikiria mufano moja. Miaka fulani yenye imepita, mwanaume fulani alikubali kikaratasi cha mualiko wa Ukumbusho, lakini aliambia ndugu mwenye alimupatia ule mualiko kama hataweza kuja. Hata hivyo, usiku wa Ukumbusho ndugu huyo alishangaa kuona ule mwanaume anaingia mu Jumba la Ufalme. Mwanaume huyo alishangaa sana kuona namna ndugu walimukaribisha kwa furaha, kwa hiyo, akaanza kuja ku mikutano yetu ya kila juma. Kwa kweli, alikosa mikutano tatu tu mu mwaka muzima. Ni nini ilimusaidia aamue kuhuzuria mikutano yote? Alibadilisha mawazo yake kwa sababu alikuwa munyenyekevu sana. Ndugu mwenye alimualika alifikia kusema hivi: “Ni mwanaume munyenyekevu sana.” Kwa kweli, Yehova alivuta ule mwanaume ili amuabudu, na sasa ni ndugu mwenye kubatizwa.​—2 Sa. 22:28; Yoh. 6:44.

7. Namna gani mambo yenye tunajifunza ku mikutano na mambo yenye tunasoma mu Biblia inaweza kutusaidia tukuwe wanyenyekevu?

7 Mambo yenye tunajifunza ku mikutano na mambo yenye tunasoma mu Biblia inaweza kutusaidia tukuwe wanyenyekevu. Mu majuma fulani mbele ya Ukumbusho, mara nyingi mikutano yetu inakazia sana mufano wa Yesu na unyenyekevu wenye alionyesha kwa kutoa uzima wake kuwa bei ya ukombozi. Na siku fulani mbele ya Ukumbusho, tunatiwa moyo kusoma habari za Biblia zenye kuzungumuzia mambo yenye ilitokea muda mufupi mbele ya kifo cha Yesu na muda mufupi kisha kufufuliwa kwake. Mambo yenye tunajifunza ku ile mikutano, na mambo yenye tunajifunza mu habari hizo za Biblia inafanya tukuwe wenye shukrani zaidi juu ya zabihu yenye Yesu alitoa kwa ajili yetu. Tunachochewa kuiga unyenyekevu wake na kufanya mapenzi ya Yehova hata wakati haiko mwepesi kwetu kufanya vile.​—Lu. 22:41, 42.

UHODARI UNATUSAIDIA KUHUZURIA MIKUTANO

8. Namna gani Yesu alionyesha uhodari?

8 Pia, tunajikaza kumuiga Yesu kwa kuonyesha uhodari. Fikiria uhodari wenye alionyesha siku fulani mbele ya kifo chake. Alijua muzuri sana kama maadui wake walikuwa karibu kumutendea kwa zarau, kumupiga, na kumuua. (Mt. 20:17-19) Lakini, alikuwa tayari kufa. Wakati muda ulifika, aliambia hivi mitume wake waaminifu wenye walikuwa naye katika Getsemane: “Musimame tuende. Muangalie! Musaliti wangu amekaribia.” (Mt. 26:36, 46) Na wakati kikundi cha watu wenye walikuwa na silaha walikuja kumukamata, alienda mbele, akajitambulisha, na kuamuru maaskari waache mitume wake waende. (Yoh. 18:3-8) Kwa kweli, Yesu alionyesha uhodari mukubwa sana! Leo, Wakristo watiwa-mafuta na kondoo wengine wanajikaza kumuiga Yesu kwa kuonyesha uhodari. Namna gani?

Uhodari wenye unaonyesha kwa kuhuzuria mikutano ya Kikristo unatia wengine nguvu (Picha hizi zinapatana na fungu la 9) *

9. (a) Sababu gani tunaweza kuwa na lazima ya uhodari ili kuhuzuria mikutano kwa ukawaida? (b) Namna gani mufano wetu unaweza kusaidia ndugu na dada zetu wenye wamefungwa kwa sababu ya imani yao?

9 Ili kuhuzuria mikutano kwa ukawaida, tunaweza kuwa na lazima ya kuonyesha uhodari wakati tunapambana na hali zenye kuwa nguvu. Ndugu na dada zetu fulani wanahuzuria mikutano hata kama wanateseka kwa sababu ya huzuni, kuvunjika moyo, ao matatizo ya afya. Wengine wanaonyesha uhodari ili kuhuzuria mikutano hata kama wanapingwa sana na watu wa familia yao ao wakubwa wa serikali. Fikiria kidogo namna mufano wetu unasaidia ndugu zetu wenye wamefungwa kwa sababu ya imani yao. (Ebr. 13:3) Wakati wanasikia kama tunaendelea kumutumikia Yehova hata kama tunapambana na magumu, hilo linawatia nguvu waendelee kuwa na imani, uhodari, na uaminifu-mushikamanifu. Jambo hilo lilimufikia mutume Paulo. Wakati alikuwa mu gereza katika Roma, alifurahi kila mara wakati alisikia kama ndugu zake walikuwa wanamutumikia Mungu kwa uaminifu. (Flp. 1:3-5, 12-14) Muda mufupi mbele ya Paulo kufunguliwa ao kisha tu kufunguliwa kwake, aliandikia Wakristo Waebrania barua. Mu ile barua alitia moyo Wakristo hao waaminifu waache ‘upendo wao wa kindugu uendelee’ na wasiache hata kidogo kukutana pamoja.​—Ebr. 10:24, 25; 13:1.

10-11. (a) Ni nani tunapaswa kualika ili wakuje ku Ukumbusho? (b) Andiko la Waefeso 1:7 linatoa sababu gani ya kufanya vile?

10 Tunaonyesha uhodari wakati tunaalika watu wa familia yetu, wafanyakazi wenzetu, na majirani wetu ili wakuje ku Ukumbusho. Juu ya nini tunawaalika? Tuko wenye shukrani sana juu ya mambo yenye Yehova na Yesu wametufanyia; kwa hiyo, tuko na hamu sana ya kualika wengine ili wakuje ku Ukumbusho. Tunapenda wajifunze namna wao pia wanaweza kupata faida kutokana na “fazili [za Yehova] zenye hazistahiliwe” kupitia bei ya ukombozi.​—Soma Waefeso 1:7; Ufu. 22:17.

11 Wakati tunaonyesha uhodari kwa kukusanyika pamoja, tunaonyesha pia sifa ingine ya maana, yenye Mungu na Mwana wake wanaonyesha kwa njia za pekee.

UPENDO UNATULAZIMISHA KUHUZURIA MIKUTANO

12. (a) Namna gani mikutano yetu inatia nguvu upendo wetu kwa Yehova na kwa Yesu? (b) Andiko la 2 Wakorinto 5:14, 15 linatutia moyo tufanye nini kwa kumuiga Yesu?

12 Upendo wetu kwa Yehova na kwa Yesu, unatulazimisha kuhuzuria mikutano. Kisha, mambo yenye tunajifunza ku mikutano inafanya tumupende zaidi Yehova na Mwana wake. Ku mikutano, tunakumbushwa kwa ukawaida mambo yenye wametufanyia. (Ro. 5:8) Ukumbusho njo unatukumbusha zaidi sana kama Yehova na Yesu wako na upendo mwingi sana, na wanapenda hata wale wenye hawajaelewa kama bei ya ukombozi ni ya maana sana. Kwa sababu tuko wenye shukrani sana, tunajikaza kila siku kumuiga Yesu katika maisha yetu ya kila siku. (Soma 2 Wakorinto 5:14, 15.) Zaidi ya ile, moyo wetu unatuchochea tumusifu Yehova kwa sababu alitutolea bei ya ukombozi. Njia moja ya kumusifu ni kutoa majibu yenye kutoka mu moyo wakati tuko ku mikutano yetu.

13. Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kama tunamupenda sana Yehova na Mwana wake? Fasiria.

13 Tunaweza kuonyesha kama tunamupenda sana Yehova na Mwana wake kwa kuwa tayari kujiima mambo fulani kwa ajili yao. Mara mingi, tunapaswa kujiima mambo mbalimbali ili kuhuzuria mikutano yetu. Makutaniko mingi inafanyaka mukutano moja mangaribi kisha kazi, wakati pengine wengi kati yetu ni wenye kuchoka. Na mukutano ingine inafanywa ku mwisho wa juma wakati watu wengine wako wanapumuzika. Je, Yehova anaona wakati tunahuzuria mikutano yetu hata kama tunachoka? Kwa kweli, anaona! Yehova anaona na anapendezwa sana na bidii yenye tunafanya ili kuhuzuria mikutano.​—Mk. 12:41-44.

14. Namna gani Yesu alituachia mufano muzuri sana wa kuonyesha upendo wa kujitoa?

14 Yesu alituachia mufano muzuri sana wa kuonyesha upendo wa kujitoa. Alikuwa tayari kufa kwa ajili ya wanafunzi wake na kila siku alikuwa tayari kuishi maisha yenye kutia faida zao pa nafasi ya kwanza kuliko faida zake mwenyewe. Kwa mufano, alizungumuza na wanafunzi wake hata wakati alikuwa mwenye kuchoka kimwili ao mwenye huzuni. (Lu. 22:39-46) Na alikaza akili juu ya mambo yenye angeweza kutolea wengine, kuliko mambo yenye wengine wangeweza kumutolea. (Mt. 20:28) Kama tunapenda sana Yehova na ndugu na dada zetu kama vile Yesu alipenda wanafunzi wake, tutafanya nguvu yetu yote ili kuhuzuria tukio la Chakula cha Mangaribi cha Bwana na mikutano ingine yote ya kutaniko.

15. Tunapenda kusaidia zaidi sana nani?

15 Tuko mu familia moja tu ya Wakristo wa kweli, na tunafurahia kutumia wakati mwingi kulingana na uwezo wetu ili kualika wapya wajiunge na sisi. Hata hivyo, tunapenda kusaidia zaidi sana wale wenye “kuwa wa jamaa yetu katika imani” lakini wenye wameacha kuhubiri na kukusanyika. (Gal. 6:10) Tunaonyesha kama tunawapenda kwa kuwatia moyo wahuzurie mikutano yetu, zaidi sana Ukumbusho. Kama Yehova na Yesu, tunafurahi sana wakati mutu mwenye ameacha kuhubiri na kukusanyika anamurudilia Yehova, Baba na Muchungaji wetu mwenye upendo.​—Mt. 18:14.

16. (a) Tunaweza kufanya nini ili kutiana moyo, na mikutano yetu itatusaidia namna gani? (b) Juu ya nini huu ni wakati muzuri wa mwaka wa kukumbuka maneno ya Yesu yenye kuwa katika Yohana 3:16?

16 Katika majuma yenye kuja, ujikaze ili kualika watu wengi kadiri inawezekana ili wahuzurie Ukumbusho siku ya Tano mangaribi, tarehe 19 Mwezi wa 4, 2019. (Ona kisanduku “ Utawaalika?”) Mu mwaka huu wote, tufanye nguvu yetu yote ili kutiana moyo kwa kuhuzuria kwa ukawaida mikutano yote yenye Yehova anatutolea. Kadiri mwisho wa ulimwengu huu unakaribia, tuko na lazima ya mikutano yetu ili itusaidie kuendelea kuwa wanyenyekevu, wenye uhodari, na wenye upendo. (1 Te. 5:8-11) Tuonyeshe basi kwa moyo wetu wote, namna tuko wenye shukrani sana kwa Yehova na Mwana wake kwa sababu wanatupenda sana!​—Soma Yohana 3:16.

WIMBO 126 Uwe Macho, Simama Imara, Uwe na Nguvu

^ fu. 5 Ukumbusho wa kifo cha Kristo utafanywa mangaribi ya Siku ya Tano, tarehe 19 Mwezi wa 4, 2019. Huo utakuwa mukutano wa maana zaidi mu mwaka muzima. Ni nini inatuchochea tuhuzurie tukio hilo? Kwa kweli, ni juu tunapenda kumupendeza Yehova. Mu habari hii, tutaona ikiwa kuhuzuria Ukumbusho na mikutano yetu ya kila juma kunaonyesha nini juu yetu.

^ fu. 50 PICHA KWENYE JALADA: Mu dunia yote mamilioni ya watu wanakaribishwa kwenye Chakula cha Mangaribi cha Bwana

^ fu. 52 MAFASIRIO YA PICHA: Ndugu mwenye amefungwa mu gereza kwa sababu ya imani yake, anatiwa moyo wakati anasoma barua yenye watu wa familia yake wamemutumia. Anajua kama hawajamusahau, kwa hiyo, anafurahi sana kupata habari kama watu wa familia yake wanaendelea pia kuwa waaminifu kwa Yehova hata kama kuko muvurugo mu eneo lao.