Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 3

Unaweza Kufanya Nini ili Kulinda Moyo Wako?

Unaweza Kufanya Nini ili Kulinda Moyo Wako?

“Linda moyo wako kuliko vitu vyote vyenye unalinda.”​—MEZ. 4:23.

WIMBO 36 Tuulinde Moyo Wetu

KIFUPI CHA HABARI *

1-3. (a) Juu ya nini Yehova alimupenda Sulemani, na Sulemani alipata baraka gani? (b) Tutajibu maulizo gani mu habari hii?

SULEMANI aliwekwa kuwa mufalme wa Israeli wakati alikuwa tu kijana. Ku mwanzo wa utawala wake, Yehova alimutokea mu ndoto na kumuambia hivi: “Omba kile unataka nikupatie.” Sulemani alijibu hivi: “Mimi ni kijana tu na sina uzoefu. . . . Basi patia mutumishi wako moyo mutiifu ili kuhukumu watu wako.” (1 Fa. 3:5-10) Sulemani aliomba “moyo mutiifu.” Ombi hilo linaonyesha kama alikuwa mwenye kiasi ao mwenye kutambua mipaka yake! Tunaelewa juu ya nini Yehova alimupenda Sulemani! (2 Sa. 12:24) Mungu wetu alipendezwa sana na jibu la Sulemani, mufalme huyo kijana, na akamupatia “moyo wenye hekima na uelewaji.”​—1 Fa. 3:12.

2 Wakati Sulemani aliendelea kuwa muaminifu, alipata baraka mingi. Alipata pendeleo la kujenga hekalu “kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli.” (1 Fa. 8:20) Akajulikana sana kwa sababu ya hekima yenye Mungu alimupatia. Na mambo yenye alisema wakati aliongozwa na roho ya Mungu, inaandikwa mu vitabu tatu vya Biblia. Kitabu cha Mezali kiko kati ya vile vitabu.

3 Moyo unatajwa karibu mara 90 mu kitabu cha Mezali. Kwa mufano, Mezali 4:23, inasema hivi: “Linda moyo wako kuliko vitu vyote vyenye unalinda.” Katika andiko hili neno “moyo,” maana yake nini? Tutajibu ulizo hilo mu habari hii. Tutajibu pia maulizo ingine mbili: Shetani anatumia njia gani ili kujaribu kuchafua ao kuharibu moyo wetu? Na tunaweza kufanya nini ili kulinda moyo wetu? Ili kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu, tunapaswa kuelewa majibu ya ile maulizo ya maana.

“MOYO WAKO,” MAANA YAKE NINI?

4-5. (a) Namna gani Zaburi 51:6 inatusaidia kuelewa neno “moyo” maana yake nini? (b) Namna gani kuhangaikia afya yetu ya kimwili kunatusaidia kuelewa lazima ya kuhangaikia moyo wetu wa mufano?

4 Mu Mezali 4:23, neno “moyo” linatumiwa ili kumaanisha “mutu wa ndani” ao “mutu mwenye kuwa katika siri.” (Soma Zaburi 51:6 na maelezo ya chini.) Katika maneno ingine, neno “moyo” maana yake, mawazo yetu ya siri, namna tunajisikia, nia zetu, na tamaa zetu. Ni namna tuko kabisa ndani yetu, haiko tu namna tunaonekana kwa inje.

5 Fikiria namna afya yetu ya kimwili inatusaidia kuelewa kama tunapaswa kuhangaikia moyo wetu wa mufano. Kwanza, ili tuendelee kuwa na afya ya muzuri ya kimwili, tunapaswa kula chakula chenye kujenga mwili na kufanya mazoezi kwa ukawaida. Vilevile, ili tuendelee kuwa na hali ya muzuri ya kiroho, tunapaswa kula chakula cha kiroho chenye kujenga na kufanya kwa ukawaida mazoezi ya imani yetu katika Yehova. Ile mazoezi inatia ndani, kutumia mambo yenye tunajifunza na kuzungumuza juu ya imani yetu. (Ro. 10:8-10; Yak. 2:26) Pili, kwa kuangalia namna tunaonekana kwa inje, tunaweza kuwaza kama tuko na afya ya muzuri hata kama kwa kweli ndani tuko wagonjwa. Vilevile, tunaweza kuwaza kama imani yetu iko nguvu, kwa sababu tu tunafanya mambo ya kiroho kwa ukawaida, lakini pengine tamaa za mubaya zinakomaa ndani yetu. (1 Ko. 10:12; Yak. 1:14, 15) Tunapaswa kukumbuka kama Shetani anapenda kutuambukiza mawazo yake. Anaweza kutumia zaidi sana njia gani ili kujaribu kufanya vile? Na tunaweza kufanya nini ili kujilinda?

NAMNA SHETANI ANAJARIBU KUCHAFUA MOYO WETU

6. Shetani iko na muradi gani, na anafanya nini ili kujaribu kufikia muradi huo?

6 Shetani anapenda tukuwe kama yeye, ni kusema, mupinzani mwenye kukataa kanuni za Yehova na mwenye kuchochewa na roho ya kujipenda mwenyewe. Shetani hawezi kutukaza tuwaze na kutenda kama yeye. Kwa hiyo, anajaribu kufikia muradi wake kwa kutumia njia zingine. Kwa mufano, anafanya tuzungukwe na watu wenye amekwisha kupotosha. (1 Yo. 5:19) Anatumaini kama tutachagua kupitisha wakati pamoja nao, hata kama tunajua kuwa mashirika ya mubaya ‘yataharibisha’ ao kupotosha namna yetu ya kufikiri na kutenda. (1 Ko. 15:33) Alitumia ile njia ili kumudanganya Mufalme Sulemani na alipata matokeo ya muzuri. Sulemani alioa wanamuke wengi wapagani, na mwishowe “walikuwa na uvutano mukubwa juu yake” na ‘pole kwa pole waligeuza moyo wake’ mbali na Yehova.​—1 Fa. 11:3; maelezo ya chini.

Unaweza kufanya nini ili kulinda moyo wako ili Shetani asiuchafue na mawazo yake? (Picha hii inapatana na fungu la 7) *

7. Ni njia gani ingine yenye Shetani anatumia ili kueneza mawazo yake, na juu ya nini tunapaswa kuwa waangalifu juu ya ile njia?

7 Shetani anatumia filme mbalimbali na programu ao vipindi vya televizyo ili kueneza mawazo yake. Anajua kama zaidi ya kutufurahisha, habari zenye kuelezwa zinatufundisha pia namna ya kufikiri, namna ya kujisikia, na namna ya kutenda. Yesu alitumia muzuri ufundi huo wa kufundisha. Kwa mufano, fikiria mufano wake wa Musamaria mwema na mutoto mwanaume mwenye alitoka kwao na kutumia mubaya uriti wake. (Mt. 13:34; Lu. 10:29-37; 15:11-32) Kwa hiyo, wale wenye wamechafuliwa na mawazo ya Shetani wanaweza kutumia habari zenye kuelezwa ili kutupotosha. Tunapaswa kuwa na usawaziko. Filme na programu za televizyo zinaweza kutufurahisha na kutufundisha bila kuambukiza akili yetu mambo ya mubaya. Lakini tunapaswa kuwa waangalifu. Wakati tunachagua mambo ya kujifurahisha, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Filme hii ao programu hii ya televizyo inanifundisha kama ni sawa kutimiza tamaa zangu za kimwili?’ (Gal. 5:19-21; Efe. 2:1-3) Unapaswa kufanya nini kama unatambua kama programu fulani inachochea mawazo ya Shetani? Uepuke ile programu kama vile unaweza kuepuka ugonjwa wenye kuambukiza!

8. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kusaidia watoto wao walinde moyo wao?

8 Wazazi, muko na daraka kubwa la kulinda watoto wenu ili Shetani asichafue moyo wao. Kwa kweli, munafanya nguvu yenu yote juu ya kulinda watoto wenu ili wasipatwe na magonjwa. Munasafisha nyumba yenu, munatupa kila kitu chenye kinaweza kuwaletea magonjwa ninyi ao watoto wenu. Vilevile, munapaswa kulinda watoto wenu juu ya filme, vipindi vya televizyo, michezo ya video, na site za Enternete zenye zinaweza kuwaambukiza mawazo ya Shetani. Yehova amewapatia daraka la kuhangaikia mahitaji ya kiroho ya watoto wenu. (Mez. 1:8; Efe. 6:1, 4) Kwa hiyo, musiogope kuweka katika familia sheria zenye kutegemea kanuni za Biblia. Muambie watoto wenu wadogo mambo yenye wanaweza kuangalia na mambo yenye hawawezi kuangalia, na muwasaidie waelewe sababu gani mumekamata ile maamuzi. (Mt. 5:37) Kadiri watoto wenu wanaendelea kukomaa, muwazoeze ili wajue kutambua wao wenyewe mambo yenye kuwa sawa na yenye kuwa makosa kulingana na kanuni za Yehova. (Ebr. 5:14) Na mukumbuke kama watoto wenu watajifunza mambo mingi kupitia mambo yenye munasema, lakini watajifunza mambo mingi zaidi kupitia mambo yenye munafanya.​—Kum. 6:6, 7; Ro. 2:21.

9. Shetani anachochea wazo gani, na juu ya nini wazo hilo liko hatari?

9 Tena, Shetani anajaribu kuchafua moyo wetu kwa kutufanya tutegemee hekima ya wanadamu kuliko kutegemea mawazo ya Yehova. (Kol. 2:8) Fikiria wazo moja lenye Shetani anachochea; anaonyesha kama kuwa tajiri njo inapaswa kuwa muradi wa kwanza mu maisha. Watu wenye kuwa na ile mawazo wanaweza kufikia kuwa matajiri ao hapana. Ikuwe wanakuwa matajiri ao hapana wako katika hatari. Sababu gani? Kwa sababu wanaweza kukaza sana akili yao juu ya kutafuta feza mupaka wanaacha hata kuhangaikia afya yao, uhusiano wao pamoja na watu wa familia, na hata urafiki wao pamoja na Mungu kusudi tu wafikie muradi wao. (1 Ti. 6:10) Tunaweza kuwa wenye shukrani kwa sababu Baba yetu wa mbinguni mwenye hekima anatusaidia kuwa na mawazo yenye usawaziko juu ya feza.​—Muh. 7:12; Lu. 12:15.

TUNAWEZA KUFANYA NINI ILI KULINDA MOYO WETU?

Kama walinzi na walinzi wa milango mikubwa wa wakati wa zamani, ukuwe muangalifu na kutenda ili mambo ya mubaya isiingie mu moyo wako (Picha hii inapatana na fungu la 10-11) *

10-11. (a) Tunapaswa kufanya nini ili kujilinda? (b) Walinzi walikuwa wanafanya nini wakati wa zamani, na namna gani zamiri yetu inaweza kutenda kama mulinzi wetu?

10 Ili tuweze kulinda moyo wetu, tunapaswa kuwa na uwezo wa kutambua hatari na kutenda haraka ili kujilinda. Neno lenye kutafsiriwa “linda” mu Mezali 4:23, linatukumbusha kazi ya mulinzi. Mu siku za Mufalme Sulemani, walinzi walikuwa wanasimama kwenye ukuta wa muji ili kulinda muji na wangetumia chombo fulani ili kutoa mulio ikiwa wangeona hatari inakaribia. Kuona picha ya jambo hilo mu akili yetu kunatusaidia kuelewa mambo yenye tunapaswa kufanya ili kumuzuia Shetani asipotoshe mawazo yetu.

11 Wakati wa zamani, walinzi walitumika pamoja na walinzi wa milango mikubwa ya muji. (2 Sa. 18:24-26) Walitumika pamoja ili kusaidia kulinda muji kwa kuhakikisha kama milango mikubwa ilifungwa kila mara wakati adui alikaribia. (Ne. 7:1-3) Zamiri yetu yenye kuzoezwa na Biblia * inaweza kutenda kama mulinzi wetu na kutuonya wakati Shetani anajaribu kushambulia moyo wetu, ni kusema, wakati anajaribu kuchochea mawazo yetu, namna yetu ya kujisikia, nia zetu, na tamaa zetu. Kila wakati zamiri yetu inatoa sauti ya kutuonya tunapaswa kuisikiliza na kufunga mulango, ni kusema, kufanya nguvu yetu yote ili kuepuka hatari.

12-13. Tunaweza kushawishiwa kufanya nini, lakini tunapaswa kutenda namna gani?

12 Fikiria mufano wenye kuonyesha namna tunaweza kujilinda ili mawazo ya Shetani isituchochee. Yehova ametufundisha kama “uasherati na kila namna ya ukosefu wa usafi ao pupa visitajwe hata kidogo katikati [yetu].” (Efe. 5:3) Lakini, tutafanya nini ikiwa wenzetu kwenye masomo ao kwenye kazi wanaanza kuzungumuzia mambo ya uasherati? Tunajua kama tunapaswa “kukataa matendo ya kukosa kumuogopa Mungu na tamaa za ulimwengu.” (Tit. 2:12) Mulinzi, ni kusema, zamiri yetu, anaweza kutoa sauti, maana yake, kutuonya juu ya hatari. (Ro. 2:15) Lakini, tutasikiliza sauti hiyo? Tunaweza kushawishiwa kusikiliza wanafunzi ao wafanyakazi wenzetu ao kuangalia picha zenye pengine wanatumiana. Lakini huo njo wakati wa kufunga mulango mukubwa wa muji kwa njia ya mufano, kwa kubadilisha mazungumuzo ao kuondoka.

13 Inaomba uhodari ili kupinga mikazo ya wanafunzi ao wafanyakazi wenzetu ya kuwaza ao kufanya mambo ya mubaya. Tunapaswa kuwa hakika kama Yehova anaona namna tunajikaza sana, na atatupatia nguvu na hekima yenye tuko nayo lazima ili kupinga mawazo ya Shetani. (2 Ny. 16:9; Isa. 40:29; Yak. 1:5) Lakini, tunaweza kufanya nini ingine ili kuendelea kulinda moyo wetu?

ENDELEA KULINDA MOYO WAKO

14-15. (a) Tunapaswa kufungua moyo wetu ili nini iingie ndani, na namna gani tunaweza kufanya vile? (b) Namna gani Mezali 4:20-22 inatusaidia kupata faida kabisa wakati tunasoma Biblia? (Ona pia kisanduku “ Namna ya Kufikiri Sana.”)

14 Ili kulinda moyo wetu, tunapaswa kuufunga ili mambo ya mubaya isiingie ndani, lakini pia tunapaswa kuufungua ili mambo ya muzuri iingie ndani. Fikiria tena mufano wa muji wenye kuzungukwa na ukuta. Mulinzi wa mulango mukubwa alikuwa anafunga milango mikubwa ya muji ili kuzuia adui asiingie ndani, lakini wakati mwingine alikuwa anafungua milango mikubwa ili kuruhusu chakula na mambo ingine ya lazima viingizwe ndani ya muji. Kama milango mikubwa haingefunguliwa hata siku moja, wakaaji wa muji wangekufa na njaa. Vilevile tunapaswa kufungua moyo wetu kwa ukawaida ili mawazo ya Mungu iingie ndani.

15 Biblia iko na mawazo ya Yehova, kwa hiyo, kila wakati tunasoma Biblia, tunaruhusu mawazo ya Yehova ichochee namna yetu ya kuwaza, namna tunajisikia, na namna tunatenda. Tunaweza kufanya nini ili tupate faida wakati tunasoma Biblia? Kusali ni jambo la maana sana. Dada mumoja alisema hivi: “Mbele ya kusoma Biblia, ninasali kwa Yehova na kumuomba anisaidie ‘nione waziwazi mambo ya ajabu’ yenye kuwa mu Neno lake.” (Zb. 119:18) Pia, tunapaswa kufikiri sana juu ya mambo yenye tunasoma. Wakati tunasali, na tunafikiri sana, Neno la Mungu linaingia “ndani kabisa ya moyo [wetu],” na tunafikia kupenda mawazo ya Yehova.​—Soma Mezali 4:20-22; Zb. 119:97.

16. Kuangalia JW Télédiffusion kumeletea watu wengi faida gani?

16 Njia ingine ya kuruhusu mawazo ya Mungu ituchochee ni kuangalia mambo mbalimbali yenye kuwa ku JW Télédiffusion. Bibi na bwana fulani wanasema hivi: “Programu za kila mwezi zimekuwa kabisa jibu kwa sala zetu! Zimetutia nguvu na kututia moyo wakati tuko na huzuni ao wakati tunajisikia kuwa peke yetu. Na mu nyumba yetu mara nyingi tunasikiliza nyimbo zetu zenye zilitungwa. Tunasikiliza nyimbo hizo wakati tuko tunapika chakula, wakati tuko tunafanya usafi, ao wakati tuko tu tunakunywa chai.” Programu hizo zinatusaidia kulinda moyo wetu. Zinatufundisha kuwa na mawazo ya Yehova na kupinga mukazo wa kuwa na mawazo ya Shetani.

17-18. (a) Kulingana na 1 Wafalme 8:61, tunaonyesha nini wakati tunatumia mambo yenye Yehova anatufundisha? (b) Mufano wa Mufalme Hezekia unaweza kutufundisha nini? (c) Kulingana na sala ya Daudi yenye kupatikana katika Zaburi 139:23, 24, tunaweza kusali juu ya jambo gani?

17 Kila wakati tunaona faida ya kufanya mambo yenye kuwa sawa, imani yetu inakuwa yenye nguvu zaidi. (Yak. 1:2, 3) Tunajisikia muzuri juu tumemufanya Yehova ajivunie kutuita watoto wake, na tamaa yetu ya kumufurahisha inakuwa nguvu zaidi. (Mez. 27:11) Kila jaribu linatupatia nafasi ya kuonyesha kama hatumutumikie kwa moyo nusu-nusu Baba yetu mwenye kutuhangaikia. (Zb. 119:113) Lakini, tunaonyesha kama tunamupenda Yehova kwa moyo kamili, moyo wenye kuazimia kabisa kutii amri zake na kufanya mapenzi yake.​—Soma 1 Wafalme 8:61.

18 Tutafanya makosa? Ndiyo; kwa sababu hatuko wakamilifu. Kama tunajikwaa, tukumbuke mufano wa Mufalme Hezekia. Alifanya makosa. Lakini, alitubu, na akaendelea kumutumikia Yehova “kwa moyo kamili.” (Isa. 38:3-6; 2 Ny. 29:1, 2; 32:25, 26) Tuendelee basi kupinga vishawishi vya Shetani vya kupenda kutuambukiza mawazo yake. Tumuombe Yehova atusaidie kuwa na “moyo mutiifu.” (1 Fa. 3:9; soma Zaburi 139:23, 24.) Tunaweza kuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, ikiwa tunalinda moyo wetu kuliko vitu vingine vyote.

WIMBO 54 “Hii Ndiyo Njia”

^ fu. 5 Tutaendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, ao tutaacha Shetani atudanganye kwa werevu ili tuache kumutumikia Mungu? Jibu la ulizo hilo halitegemee ikiwa tunapata majaribu makali ao hapana, lakini linategemea namna tunalinda muzuri moyo wetu. Neno “moyo,” maana yake nini? Shetani anatumia njia gani ili kujaribu kupotosha ao kuharibu moyo wetu? Na tunaweza kufanya nini ili kulinda moyo wetu? Habari hii itajibu ile maulizo.

^ fu. 11 MAFASIRIO YA MANENO FULANI: Yehova alitupatia uwezo wa kuchunguza mawazo yetu, namna tunajisikia, na matendo yetu na kisha kujihukumu. Biblia inaita uwezo huo zamiri. (Ro. 2:15; 9:1) Zamiri yenye kuzoezwa na Biblia ni zamiri yenye inatumia kanuni za Yehova zenye kuwa mu Biblia, ili kuhukumu ikiwa mambo yenye tunawaza, tunafanya, ao kusema ni ya muzuri ao ni ya mubaya.

^ fu. 56 MAFASIRIO YA PICHA: Ndugu mwenye kubatizwa anaangalia televizyo kisha picha chafu inatokea. Anapaswa kuamua jambo lenye atafanya.

^ fu. 58 MAFASIRIO YA PICHA: Mulinzi wa wakati wa zamani anaona hatari inje ya muji. Anajulisha walinzi wa milango mikubwa wenye kuwa chini na wanatenda palepale kwa kufunga milango mikubwa ya muji na kuifunga nguvu sana kwa ndani.