Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

1918—Kumepita Sasa Miaka Mia Moja

1918—Kumepita Sasa Miaka Mia Moja

Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 1, 1918, ulianza na maneno haya: “Kutatokea nini mu mwaka wa 1918?” Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilikuwa ingali inapiganwa katika Ulaya, lakini matukio ya miezi ya kwanza-kwanza ya mwaka huo yalionekana kuwa yanatoa tumaini la muzuri kwa Wanafunzi wa Biblia na kwa ulimwengu wote.

ULIMWENGU UNAZUNGUMUZA JUU YA AMANI

Tarehe 8 Mwezi wa 1, 1918, Raisi Woodrow Wilson, mu hotuba yake yenye alitolea Bunge (Parlement) la Amerika, alizungumuzia mawazo 14 yenye aliona kuwa ya lazima ili kupata “amani yenye haki na yenye kuendelea.” Alipendekeza kukuwe uhusiano ao mapatano kati ya mataifa, silaha zipunguzwe, na kuanzishwa kwa “muungano wa mataifa yote” wenye ungeletea faida inchi “kubwa-kubwa na inchi za kidogo-kidogo pia.” “Mawazo Kumi na Ine” yenye alitoa yalifikia kutumiwa ili kuunda Ushirika wa Mataifa na katika mazungumuzo ya kupata Makubaliano ya Versailles, na mambo hayo yalisaidia ili kumaliza Vita ya Kwanza ya Ulimwengu.

WAPINZANI WANASHINDWA

Hata kama kulikuwa muvurugo mwaka wenye ulipita, * Wanafunzi wa Biblia walitumainia pia kupata amani mu siku zenye zilikuwa mbele yao. Mambo yenye yalitokea kwenye mukutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society yalifanya wakuwe na tumaini hilo.

Kwenye mukutano huo, wenye ulifanywa tarehe 5 Mwezi wa 1, 1918, ndugu fulani wenye walikuwa na madaraka katika tengenezo wenye walikuwa wamefukuzwa mu Beteli walijaribu kupata nafasi ya kuongoza tengenezo. Richard Barber, mwangalizi muaminifu mwenye kusafiri, alifungua mukutano huo kwa sala. Kisha kutoa ripoti juu ya kazi ya mwaka wenye ulipita, uchaguzi wa kila mwaka wa wasimamizi ulifanywa. Ndugu Barber alipendekeza Joseph Rutherford na ndugu wengine sita. Kisha mwanasheria mumoja mwenye alikuwa anaunga wapinzani mukono alipendekeza wanaume wengine saba, kutia ndani wale wenye walikuwa wamefukuzwa mu Beteli. Wote walishindwa. Washiriki wengi sana wa Sosaiti walichagua Ndugu Rutherford na ndugu wengine sita waaminifu wakuwe wasimamizi.

Ndugu wengi wenye walikuwa pale waliita mukutano huo “mukusanyiko wenye kubarikiwa zaidi kuliko mikusanyiko yote yenye walikuwa wamehuzuria.” Lakini furaha yao haikuendelea.

NAMNA WATU WALITENDA JUU YA KITABU LE MYSTÈRE DE DIEU ACCOMPLI

Kwa miezi fulani, Wanafunzi wa Biblia walikuwa wanatolea watu kitabu Le mystère de Dieu accompli. Wasomaji wenye moyo muzuri walikubali kweli za Biblia zenye zilikuwa mu kitabu hicho.

Edward Crist, mwangalizi mwenye kusafiri mu inchi ya Kanada, alizungumuzia bibi na bwana fulani wenye walikuwa wamesoma kitabu Le mystère de Dieu accompli na wakakubali kweli katika majuma tano tu! Alisema hivi: “Bibi na bwana, wote wawili wanajitoa kabisa na wanafanya maendeleo ya muzuri.”

Mwanaume mumoja mwenye alipata kitabu hicho alizungumuza bila kukawia na marafiki wake juu ya habari yenye kuwa ndani. “Alipigwa” kitabu chenye kilimupendeza sana. Anasema hivi: “Nilikuwa natembea mu Avenue ya Tatu [na] kitu fulani kilinipiga ku mabega, niliwaza kama ilikuwa tofali lakini, nilishangaa kuona kama ilikuwa kitabu ‘Le mystère de Dieu accompli.’ Nilikibeba ku nyumba na nikakisoma chote. . . . Kisha nilifikia kujua kama ni muhubiri mumoja wa dini . . . ndiye alitupa kitabu hicho kupitia dirisha kwa sababu ya kasirani . . . Ninaamini kabisa kama alisaidia watu wengi wapate tumaini la uzima kupitia tendo hilo moja, kuliko matendo mengine yote ya maisha yake. . . . Kupitia kasirani ya muhubiri huyo sasa tunamusifu Mungu.”

Watu wengine walitenda kama muhubiri huyo. Wenye mamlaka wa inchi ya Kanada walikataza kitabu hicho tarehe 12 Mwezi wa 2, 1918; walisema kama kitabu hicho kilikuwa na maneno yenye kupinga vita na kuchochea watu wapinge serikali. Bila kukawia, wenye mamlaka mu inchi ya Amerika walifanya vilevile. Maofisa wa serikali walichunguza Beteli na biro mbalimbali mu muji wa New York, Pennsylvania, na California, walikuwa wanatafuta ushuhuda ili kushitaki ndugu wenye walikuwa wanaongoza tengenezo. Tarehe 14 Mwezi wa 3, 1918, Idara ya Sheria ya Amerika ilikataza kitabu Le mystère de Dieu accompli kwa kusema kama kuchapisha na kutolea watu kitabu hicho kunazuia bidii za kufanya vita, na ni kuvunja Sheria ya Upelelezi.

NDUGU WANAFUNGWA!

Tarehe 7 Mwezi wa 5, 1918, Idara ya Sheria ilipata ruhusa ya kufunga Giovanni DeCecca, George Fisher, Alexander Macmillan, Robert Martin, Frederick Robison, Joseph Rutherford, William Van Amburgh, na Clayton Woodworth. Walishitakiwa kuwa “walivunja sheria kwa makusudi na kwa hila kwa kuchochea watu wasitii wenye mamlaka, wakose kuwa washikamanifu na wakatae kazi ya jeshi na wakatae kujiunga na majeshi ya mu maji ya inchi ya Amerika.” Walianza kusambishwa tarehe 5 Mwezi wa 6, 1918, lakini walikuwa hakika kama watahukumiwa. Juu ya nini?

Mukubwa wa sheria wa inchi ya Amerika aliita sheria hiyo yenye walishitakiwa kuwa wamevunja, kuwa Sheria ya Upelelezi, “silaha ya muzuri ya kupinga propaganda.” Tarehe 16 Mwezi wa 5, 1918, Bunge lilikataa badiliko kuhusu Sheria hiyo; badiliko hilo lingelinda wale wenye walichapisha “mambo ya kweli, kwa nia ya muzuri, na kwa ajili ya makusudi yenye kufaa.” Katika mazungumuzo yao, walizungumuzia sana kitabu Le mystère de Dieu accompli. Juu ya kitabu hicho, maandishi fulani ya Bunge la inchi ya Amerika yanasema hivi: “Mufano moja wenye kuwa hatari zaidi wa propaganda ya namna hiyo ni kitabu chenye kuitwa ‘Le mystère de Dieu accompli’ . . . Kusudi tu la kitabu hicho ni kuchochea maaskari wakuwe na mashaka juu ya nia yetu na kuchochea . . . watu wakatae kuandikishwa katika kazi ya jeshi.”

Tarehe 20 Mwezi wa 6, 1918, baraza la tribinali lilisema kama ndugu hao munane walikuwa wenye makosa juu ya mambo yote yenye walishitakiwa. Siku yenye ilifuata, muamuzi alitoa hukumu yake. Alisema hivi: “Propaganda ya kidini yenye washitakiwa hawa wametetea kwa bidii na kueneza . . . iko hatari sana kupita kikundi cha jeshi la Ujerumani. . . . Wanapaswa kupewa malipizi makali.” Kisha majuma mbili, ndugu hao munane walifungwa mu Gereza Kubwa la Serikali katika Atlanta, Georgia. Walipewa hukumu ya kufungwa miaka kuanzia 10 mupaka 20.

KAZI YA KUHUBIRI INAENDELEA

Katika kipindi hicho, Wanafunzi wa Biblia walipambana na upinzani mukali. Shirika la Upelelezi (FBI) lilichunguza kwa uangalifu kazi yao, na kutoa maelfu ya documents. Documents hizo zinaonyesha kama ndugu zetu walikuwa wameazimia kuendelea kuhubiri.

Katika barua yenye musimamizi wa biro ya posta ya Orlando, Florida, aliandikia FBI, alisema hivi: “[Wanafunzi wa Biblia] wako wanaenda nyumba kwa nyumba mu muji wote na wanafanya sehemu kubwa ya kazi hiyo usiku. . . . Wanaonekana kuwa wameazimia kuendelea kuhubiri hata kama wanapata upinzani mukubwa.”

Mukubwa mumoja wa maaskari mwenye alikuwa mu Idara ya Vita aliandikia shirika hilo ili kutoa ripoti juu ya kazi ya Frederick Franz, mwenye alifikia kutumikia mu Baraza Lenye Kuongoza. Mukubwa huyo aliandika hivi: “Frederick Franz . . . amefanya kwa bidii kazi ya kuuzisha maelfu ya mabuku ya kitabu ‘Le mystère de Dieu accompli’.”

Charles Fekel, mwenye alifikia pia kutumikia mu Baraza Lenye Kuongoza, alipambana na upinzani mukali. Wenye mamlaka walimufunga juu alikuwa anatolea watu kitabu Le mystère de Dieu accompli na walichunguza barua zake. Alifungwa mu gereza kwa mwezi moja katika Baltimore, Maryland, na alionwa kuwa “Adui mugeni kutoka inchi ya Austria.” Wakati alikuwa anatolea ushahidi bila woga watu wenye walikuwa wanamuuliza maulizo, alikumbuka maneno ya Paulo yenye kuwa mu andiko la 1 Wakorinto 9:16, lenye kusema hivi: “Ole wangu kama sitangaze habari njema!” *

Zaidi ya kuhubiri kwa bidii, Wanafunzi wa Biblia walieneza kwa bidii ombi la kuomba ndugu wenye walikuwa wamefungwa katika Atlanta waachiliwe. Anna Gardner alisema hivi: “Sikuzote tulikuwa tunafanya jambo fulani. Wakati ndugu walikuwa mu gereza, kazi yetu ilikuwa sasa kutafuta watu wa kutia sinyatire. Tulikuwa tunaenda nyumba kwa nyumba. Maelfu ya watu walitia sinyatire zao! Tuliambia watu wenye tulizungumuza nao kama wanaume hao walikuwa Wakristo wa kweli na kama walifungwa bila haki.”

MIKUSANYIKO

Wakati huo wa magumu, mikusanyiko ilifanywa kwa ukawaida ili kutia nguvu ndugu na dada zetu katika hali ya kiroho. Munara wa Mulinzi ulisema hivi: “Mikusanyiko zaidi ya makumi ine . . . imefanywa katika mwaka huu . . . Tumepata ripoti zenye kufurahisha juu ya mikusanyiko hiyo yote. Zamani mikusanyiko ilikuwa inafanywa mu miezi fulani tu (mbili, ao tatu) katika mwaka, lakini sasa inafanywa kila mwezi.”

Watu wenye mioyo ya muzuri waliendelea kukubali habari njema. Ku mukusanyiko moja katika Cleveland, Ohio, watu 1 200 hivi walihuzuria na watu 42 walibatizwa, kutia ndani kijana mudogo mwanaume mwenye “alikuwa anapendezwa na mambo ya Mungu na mwenye kujitoa kwake kungepatisha haya watu wenye kukomaa.”

NI NINI ILITOKEA KISHA?

Wakati mwaka wa 1918 ulikaribia mwisho, Wanafunzi wa Biblia hawakujua ni nini itatokea wakati wenye kuja. Majengo fulani ya Beteli katika Brooklyn yaliuzishwa na makao makubwa yakahamishiwa katika Pittsburgh, Pennsylvania. Wakati wale wenye walikuwa wanaongoza walikuwa mu gereza, mukutano mwingine wa kila mwaka wa washiriki wa Sosaiti ulipangwa kufanywa tarehe 4 Mwezi wa 1, 1919. Ni nini ingetokea?

Ndugu zetu waliendelea kufanya kazi yao. Walikuwa hakika kama matokeo yatakuwa ya muzuri, ndiyo sababu walichagua andiko hili likuwe andiko lao la mwaka wa 1919: “Hakuna silaha yenye itafanywa juu yako yenye itafanikiwa.” (Isa. 54:17) Walikuwa tayari kwa ajili ya badiliko kubwa lenye hawakutazamia lenye lingetia nguvu imani yao na kuwapatia nguvu ya kufanya kazi kubwa yenye ilikuwa inawangojea.

^ fu. 6 Ona habari “Miaka Mia Moja Iliyopita​—1917” mu Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2017, uku. 172-176.

^ fu. 22 Ona habari juu ya maisha ya Charles Fekel, yenye kichwa, “Furaha Yenye Inatokana na Uvumilivu Katika Kila Kazi ya Muzuri,” mu Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 11, 1970 (katika Kifaransa).