Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tumainia Kiongozi Wetu—Kristo

Tumainia Kiongozi Wetu—Kristo

“Kiongozi wenu ni mumoja, Kristo.”​—MT. 23:10.

NYIMBO: 16, 14

1, 2. Yoshua alikuwa na kazi gani kubwa kisha Musa kufa?

YEHOVA alimuambia Yoshua hivi: “Musa mutumishi wangu amekufa. Sasa simama, vuka Muto Yordani, wewe na watu hawa wote, na muingie katika inchi yenye ninapatia watu wa Israeli.” (Yos. 1:1, 2) Hayo yalikuwa mabadiliko makubwa kwa Yoshua, mwenye alikuwa musaidizi wa Musa kwa miaka karibu 40!

2 Musa alikuwa ameongoza Waisraeli kwa muda murefu, lakini sasa Yoshua ndiye angewaongoza. Kwa hiyo, pengine alijiuliza ikiwa watu wangemukubali akuwe kiongozi wao. (Kum. 34:8, 10-12) Juu ya andiko la Yoshua 1:1, 2, kitabu kimoja chenye kufasiria Biblia kinasema kama kipindi kimoja kati ya vipindi vya magumu zaidi na vyenye kuwa hatari kwa taifa, ikuwe zamani ao leo, ni wakati kiongozi fulani anakamata nafasi ya kiongozi mwingine.

3, 4. Namna gani Mungu alimubariki Yoshua juu alimutumainia, na tunaweza kujiuliza ulizo gani?

3 Yoshua alikuwa na sababu ya kuogopa. Lakini alimutumainia Yehova na alifuata maagizo yake bila kukawia. (Yos. 1:9-11) Mungu alimubariki Yoshua kwa sababu alimutumainia na alitumia malaika wake ili kuongoza Yoshua na Waisraeli. Inawezekana kabisa kuwa malaika huyo alikuwa Neno, ni kusema, Mwana-muzaliwa wa kwanza wa Mungu.​—Kut. 23:20-23; Yoh. 1:1.

4 Yehova alisaidia taifa la Israeli lijipatanishe na mabadiliko wakati Yoshua aliwekwa kuwa kiongozi wao mupya. Katika siku zetu, kuko pia mabadiliko mengi makubwa yenye kutokea. Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Wakati tengenezo la Mungu linaendelea kusonga mbele, tuko na sababu ya kutumainia Kiongozi wetu mwenye amewekwa, ni kusema, Yesu?’ (Soma Matayo 23:10.) Ili kujibu ulizo hilo, tutachunguza namna Yehova aliongoza watu wake zamani wakati wa mabadiliko.

KUONGOZA WATU WA MUNGU ILI KUINGIA MU INCHI YA AHADI

5. Yoshua alikutana na jambo gani fulani lenye halikukuwa la kawaida karibu na muji wa Yeriko? (Ona picha ku mwanzo wa habari hii.)

5 Kisha tu Waisraeli kuvuka Yordani, Yoshua alikutana na jambo fulani lenye halikukuwa la kawaida. Karibu na muji wa Yeriko, alikutana na mwanaume mwenye alikuwa na upanga. Yoshua alimuuliza mwanaume huyo hivi: “Uko upande wetu ao upande wa maadui wetu?” Yoshua alishangaa wakati mwanaume huyo alisema kama alikuwa “mukubwa wa jeshi la Yehova,” malaika mwenye alikuwa tayari ili kupigania watu wa Mungu. (Soma Yoshua 5:13-15, maelezo ya chini.) Hata kama mahali pengine habari hii inasema kama ni Yehova alikuwa anasema na Yoshua moja kwa moja, inaonekana kama Mungu alikuwa anatumia malaika ili kuzungumuza pa nafasi yake, kama vile alifanya mara mingi mbele ya pale.​—Kut. 3:2-4; Yos. 4:1, 15; 5:2, 9; Mdo. 7:38; Gal. 3:19.

6-8. (a) Juu ya nini maagizo fulani ya malaika yangeonekana kuwa hayafae? (b) Ni nini inaonyesha kama maagizo hayo yalikuwa yenye hekima na yalitolewa kwa wakati wenye kufaa? (Ona pia maelezo ya chini.)

6 Malaika huyo aliambia Yoshua jambo lenye alipaswa kufanya ili apate ushindi juu ya muji wa Yeriko. Mwanzoni, pengine maagizo fulani yalionekana kuwa hayafae. Kwa mufano, malaika aliambia Yoshua atahiri maaskari wote. Hilo lilimaanisha kama hawangeweza kupigana kwa siku fulani. Je, huo ulikuwa wakati muzuri kabisa wa kutahiri wanaume hao?​—Mwa. 34:24, 25; Yos. 5:2, 8.

7 Pengine maaskari walijiuliza hivi: ‘Namna gani tutalinda familia zetu kama maadui wanashambulia kambi letu?’ Lakini kisha jambo fulani lenye hawakutazamia lilitokea! Kuliko kushambulia Waisraeli, wanaume wa Yeriko waliwaogopa. Biblia inasema hivi: “Yeriko ilikuwa imefungwa kabisa kwa sababu ya Waisraeli; hakuna mutu alikuwa anatoka wala kuingia.” (Yos. 6:1) Habari hiyo ilipaswa kuchochea Waisraeli watumainie hata zaidi muongozo wa Mungu!

8 Malaika aliambia Yoshua kama Waisraeli hawakupaswa kushambulia Yeriko. Lakini, walipaswa kutembea ili kuzunguka muji mara moja kila siku kwa siku sita na kisha mara saba siku ya saba. Pengine maaskari waliwaza hivi: ‘Kufanya vile ni kupoteza wakati na nguvu kabisa!’ Lakini, Yehova, Kiongozi wa Israeli mwenye hakukuwa anaonekana alijua kabisa jambo lenye alikuwa anafanya! Kufuata maagizo yake kulitia nguvu zaidi imani ya Waisraeli, na hawakulazimika kupigana na maaskari wa Yeriko.​—Yos. 6:2-5; Ebr. 11:30. * (Ona maelezo ya chini.)

9. Juu ya nini tunapaswa kufuata maagizo yote yenye tengenezo la Mungu linatutolea? Leta mufano.

9 Habari hii inaweza kutufundisha nini? Wakati fulani tengenezo la Yehova linafanya mambo kwa njia ya mupya, na pengine sikuzote hatuwezi kuelewa sababu. Kwa mufano, pengine zamani hatukuwazia kama ni wazo la muzuri kutumia vyombo vya kielektroniki mu mahubiri, ku mikutano, ao ili kufanya funzo la pekee. Lakini sasa pengine tunaona faida za kutumia vyombo hivyo ikiwa inawezekana. Wakati tunaona matokeo ya muzuri ya mabadiliko kama hayo, imani yetu inakuwa yenye nguvu zaidi na tunakuwa na umoja zaidi pamoja na ndugu na dada zetu.

NAMNA GANI KRISTO ALIONGOZA WAKRISTO WA KWANZA-KWANZA?

10. Ni nani kabisa alifanya mipango ili baraza lenye kuongoza lifanye mukutano wa maana mu muji wa Yerusalemu?

10 Miaka 13 hivi kisha Kornelio, Mutu wa Mataifa mwenye hakukuwa anatahiriwa, kuwa Mukristo, Wakristo fulani Wayahudi walikuwa wanaendelea kusema kama kutahiriwa kulikuwa kwa lazima. (Mdo. 15:1, 2) Katika muji wa Antiokia, ndugu walikuwa wanabishana juu ya jambo hilo. Kwa hiyo, wazee walifanya mipango ili Paulo aende Yerusalemu na kuuliza baraza lenye kuongoza juu ya jambo hilo. Lakini ni nani mwenye alikuwa anafanya mipango kabisa ili Paulo aende kule? Paulo alisema hivi: “Nilipanda kuenda kule kwa sababu nilipewa ufunuo.” Kwa kweli, ni Kristo ndiye aliongoza mambo ili baraza lenye kuongoza lishugulikie jambo hilo.​—Gal. 2:1-3.

Kristo alikuwa Kiongozi wa kutaniko la Kikristo la kwanza-kwanza (Picha hii inapatana na fungu la 10, 11)

11. (a) Wakristo fulani Wayahudi waliendelea kuamini nini juu ya kutahiriwa? (b) Namna gani Paulo alionyesha kama aliunga mukono kwa unyenyekevu wazee katika Yerusalemu? (Ona pia maelezo ya chini.)

11 Kristo aliongoza baraza lenye kuongoza ili lionyeshe wazi kama haikukuwa lazima Wakristo wenye hawakukuwa Wayahudi watahiriwe. (Mdo. 15:19, 20) Lakini, miaka fulani kisha pale, Wakristo wengi Wayahudi waliendelea kutahiri watoto wao wanaume. Kisha, wazee katika Yerusalemu walisikia habari fulani yenye ilikuwa inaenezwa kwamba Paulo hakukuwa anaheshimia Sheria ya Musa. Basi, wazee walimuomba Paulo afanye jambo fulani lenye lingeonyesha kama anaheshimia Sheria hiyo. * (Ona maelezo ya chini.) (Mdo. 21:20-26) Walimuambia achukue wanaume ine aende nao mu hekalu ili watu waone kama alikuwa anaheshimia Sheria. Paulo angesema hivi: ‘Haina maana kufanya vile! Juu ya nini munaniomba nifanye vile? Wakristo Wayahudi wenye hawaelewe jambo la kutahiriwa ndio wenye kuwa na shida.’ Lakini Paulo alielewa kama wazee walipenda Wakristo wote wakuwe na umoja, kwa hiyo alifuata maagizo yao kwa unyenyekevu. Lakini, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Juu ya nini Yesu aliacha jambo la kutahiriwa liendelee kuwa tatizo kwa muda murefu, hata kama Sheria ya Musa ilikuwa imefikia mwisho wakati Yesu alikufa?’​—Kol. 2:13, 14.

12. Pengine ni juu ya nini Kristo aliacha wakati upite mbele amalize kabisa tatizo juu ya kutahiriwa?

12 Inaweza kuomba wakati ili tukubali mafasirio fulani ya mupya. Wakristo fulani Wayahudi walikuwa na lazima ya wakati ili wakubali kama hawakukuwa tena wanaongozwa na Sheria ya Musa. (Yoh. 16:12) Kwa muda murefu, walikuwa wanawaza kama kutahiriwa ilikuwa alama yenye ilionyesha kama mutu iko na uhusiano wa pekee pamoja na Mungu. (Mwa. 17:9-12) Wengine waliogopa kama Wayahudi wenzao wa eneo lao wangewatesa ikiwa wangekuwa tofauti nao. (Gal. 6:12) Lakini kisha wakati fulani, Kristo aliwapatia muongozo zaidi kupitia barua mbalimbali zenye Paulo aliwaandikia.​—Ro. 2:28, 29; Gal. 3:23-25.

KRISTO ANGALI ANAONGOZA KUTANIKO LAKE

13. Ni nini inaweza kutusaidia tuunge mukono namna Kristo anatuongoza leo?

13 Kristo angali Kiongozi wa kutaniko la Kikristo leo. Kwa hiyo, kama tengenezo linafanya mabadiliko fulani yenye hauelewe, fikiria namna Kristo aliongoza watu wa Mungu zamani. Ikuwe mu siku za Yoshua ao mu siku za mitume, sikuzote Kristo ametoa muongozo wenye hekima ili kulinda watu wa Mungu, kufanya imani yao ikuwe yenye nguvu zaidi, na kuwasaidia waendelee kuwa na umoja.​—Ebr. 13:8.

14-16. Muongozo wenye “mutumwa muaminifu na mwenye busara” anatoa unaonyesha kama Kristo anapenda kutusaidia ili tuendelee kuwa na imani yenye nguvu. Namna gani?

14 Leo, “mutumwa muaminifu na mwenye busara” anatupatia muongozo wenye tuko nao lazima kwa wakati wenye kufaa kabisa. (Mt. 24:45) Muongozo huo unaonyesha kama Yesu anatuhangaikia. Marc, mwenye kuwa na watoto ine, anasema hivi: “Shetani iko anajaribu kufanya makutaniko yakuwe zaifu kwa kushambulia familia mbalimbali. Sasa kwa sababu tumetiwa moyo kuongoza ibada ya familia kila juma, ujumbe uko wazi kwa vichwa vya familia​—mulinde familia zenu!”

15 Wakati tunaona namna Kristo anatuongoza, tutaelewa kama anapenda kutusaidia tuendelee kuwa na imani yenye nguvu. Kwa mufano, muzee mumoja mwenye kuitwa Patrick anasema hivi: “Ku mwanzo, kukutana ku mwisho wa juma mu vikundi vidogo-vidogo kwa ajili ya mahubiri kulivunja wengine moyo.” Lakini anasema kama badiliko hilo linaonyesha namna Yesu anahangaikia kila mutu mu kutaniko. Kwa mufano, ndugu na dada fulani wenye kuwa na haya ao wenye hawakukuwa wanaenda mu mahubiri kwa ukawaida, wanajisikia kuwa wanahitajiwa sana na wako wa maana zaidi. Hilo limetia nguvu imani yao.

16 Tena, Kristo anatusaidia tuendelee kukaza akili juu ya kazi ya kuhubiri; hiyo ndiyo kazi ya maana zaidi yenye kufanywa mu dunia leo. (Soma Marko 13:10.) André, muzee mupya, amejikaza sikuzote kufuata kila muongozo wenye tengenezo la Yehova linatoa. Anasema hivi: “Kupunguza watu kwenye biro ya tawi kunatukumbusha kama tuko mu wakati wenye unaomba tutende kwa haraka na tunapaswa kutumia nguvu zetu zote mu kazi ya kuhubiri.”

NAMNA GANI TUNAWEZA KUUNGA MUKONO MUONGOZO WA KRISTO?

17, 18. Juu ya nini tunapaswa kufikiria faida zenye tunapata wakati tunajipatanisha na mabadiliko?

17 Muongozo wenye Yesu Kristo, Mufalme wetu mwenye kutawala, anatutolea utatusaidia sasa na wakati wenye kuja. Fikiria faida zenye umepata juu umejipatanisha na mabadiliko ya hivi majuzi. Katika ibada yenu ya familia, munaweza kuzungumuzia namna mabadiliko yenye yamefanywa juu ya mikutano ao juu ya kazi ya kuhubiri yamesaidia familia yenu.

Unasaidia watu wa familia yako na wengine ili wajipatanishe na mabadiliko mu tengenezo la Yehova? (Picha hizi zinapatana na fungu la 17, 18)

18 Kama tunakumbuka kwamba kufuata maagizo ya tengenezo la Yehova kunatuletea matokeo mengi ya muzuri, hilo litafanya ikuwe mwepesi kufuata maagizo hayo na tutakuwa wenye furaha. Kwa mufano, juu hatuchapishe tena vichapo mingi sana kama vile zamani, hilo linatusaidia tusitumie feza nyingi. Na kwa sababu tunatumia teknolojia za sasa, tunahubiria watu wengi zaidi habari njema. Je, tunaweza kutumia zaidi vichapo vya kielektroniki na video ao habari mbalimbali zenye kurekodiwa? Hiyo ni njia moja ya kumuunga Kristo mukono, mwenye anapenda tutumie kwa hekima mali ya tengenezo.

19. Juu ya nini tunapaswa kuunga mukono muongozo wa Kristo?

19 Wakati tunaunga mukono muongozo wa Kristo, tunasaidia ndugu na dada zetu wakuwe na imani yenye nguvu zaidi na wakuwe na umoja zaidi. Kuhusu mabadiliko ya hivi majuzi ya kupunguza watu mu familia ya Beteli ya dunia yote, André anasema hivi: “Roho ya muzuri ya kujipatanisha na mabadiliko kama hayo, yenye ilionyeshwa na wale wenye walikuwa Wanabeteli zamani, inanichochea niwatumainie na kuwaheshimia. Wanasonga mbele pamoja na gari la Yehova kwa kupata furaha katika mugao wowote wenye wanapewa.”

UKUWE NA IMANI NA UMUTUMAINIE KIONGOZI WETU

20, 21. (a) Juu ya nini tunaweza kumutumainia Kristo, Kiongozi wetu? (b) Tutazungumuzia ulizo gani mu habari yenye kufuata?

20 Hivi karibuni, Kiongozi wetu, Yesu Kristo, ‘atakamilisha ushindi wake’ na ‘kutimiza mambo yenye kuogopesha sana.’ (Ufu. 6:2; Zb. 45:4) Lakini hata leo anatutayarisha kwa ajili ya uzima mu dunia mupya na kwa ajili ya kazi yenye tutafanya mule, wakati tutafundisha wale wenye watafufuliwa na kusaidia ili kufanya dunia ikuwe paradiso.

21 Kama tunaendelea kutumainia Kiongozi na Mufalme wetu hata kutokee jambo gani, atatuongoza ili tuingie mu dunia mupya. (Soma Zaburi 46:1-3.) Leo, mabadiliko yanaweza kuwa nguvu, zaidi sana wakati yanatufikia mu njia zenye hatukuwazia. Wakati jambo hilo linatokea, tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuwa na amani ya akili na imani yenye nguvu katika Yehova? Tutazungumuzia ulizo hilo mu habari yenye kufuata.

^ fu. 8 Watu wenye kuchimbua vitu vya zamani walipata nafaka ao mbegu nyingi sana zenye watu walivuna lakini hawakuzikula. Hilo linaunga mukono habari ya Biblia yenye kusema kama Waisraeli walizunguka muji wa Yeriko kwa muda mufupi na hawakuruhusiwa kula nafaka zenye walikuta mu muji huo. Kwa sababu huo ulikuwa wakati wa mavuno, ulikuwa wakati muzuri kwa Waisraeli kukamata inchi hiyo kwa sababu kulikuwa chakula mingi katika mashamba.​—Yos. 5:10-12.

^ fu. 11 Ona kisanduku “Paulo Akabili Jaribu kwa Unyenyekevu” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 3, 2003, ukurasa wa 24.