Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuseme Kweli

Tuseme Kweli

“Museme kweli mumoja na mwingine.”​—ZEK. 8:16.

NYIMBO: 56, 124

1, 2. Ibilisi alifanya nini ili aumize sana wanadamu?

VITU fulani vyenye watu wametengeneza kama vile telefone, taa ya umeme (empoule), na frigo vimefanya maisha yakuwe muzuri. Vitu vingine kama vile bunduki, mabombe yenye kutegwa mu udongo, mabombe ya atomu, vimefanya maisha yakuwe hatari sana. Lakini kuko jambo moja la zamani sana kuliko mambo hayo lenye limeumiza sana wanadamu. Ni jambo gani? Ni uongo! Kusema uongo ni kusema jambo fulani lenye tunajua kama haiko kweli ili tudanganye mutu fulani. Ni nani mwenye alisema uongo wa kwanza? Ni Ibilisi! Yesu Kristo alimuita “baba ya uongo.” (Soma Yohana 8:44.) Ni wakati gani alisema uongo wa kwanza?

2 Alifanya vile mu bustani ya Edeni kumepita maelfu ya miaka. Adamu na Eva walikuwa wanafurahia maisha mu Paradiso yenye Yehova alikuwa umeumba kwa ajili yao. Mungu alikuwa amewaambia kama ikiwa wanakula “matunda ya muti wa ujuzi wa mema na mabaya,” wangekufa. Hata kama Shetani alikuwa anajua jambo hilo, alitumia nyoka ili kumuambia Eva hivi: “Hakika hamutakufa.” Huo ndio ulikuwa uongo wa kwanza. Tena Shetani alisema hivi: “Kwa sababu Mungu anajua kwamba siku ileile yenye mutakula matunda ya muti huo, macho yenu yatafunguliwa na mutakuwa kama Mungu; mukijua mema na mabaya.”​—Mwa. 2:15-17; 3:1-5.

3. Juu ya nini uongo wa Shetani ulikuwa na kusudi la kuumiza sana, na ni mambo gani yalitokea kwa sababu ya uongo huo?

3 Uongo wa Shetani ulikuwa na kusudi la kuumiza sana kwa sababu alijua kama ikiwa Eva anaamini uongo huo na kula tunda hilo, angekufa. Na mambo yalifanyika vile kabisa. Eva alikosa kutii amri ya Mungu na kisha Adamu naye alifanya vile na wote wawili walifikia kufa. (Mwa. 3:6; 5:5) Zaidi ya hilo, juu ya zambi ya Adamu, “kifo kilienea kwa watu wote.” Kwa kweli, “kifo kilitawala kama mufalme . . . , hata juu ya wale wenye hawakukuwa wamefanya zambi kwa njia ileile yenye Adamu alifanya kosa.” (Ro. 5:12, 14) Ndiyo maana hatuko wakamilifu na hatuishi milele kama vile Mungu alikusudia. Lakini tunaishi tu “miaka makumi saba (70), ao makumi munane (80) kama mutu iko na nguvu za pekee,” na maisha yetu ‘yamejaa taabu na huzuni.’ (Zb. 90:10) Mambo hayo yote yanatokea juu ya uongo wa Shetani!

4. (a) Ni maulizo gani yenye tunapaswa kujibu? (b) Kulingana na Zaburi 15:1, 2, ni nani tu mwenye anaweza kuwa rafiki ya Yehova?

4 Yesu alisema hivi juu ya Shetani: “Hakusimama imara katika kweli, kwa sababu kweli haiko ndani yake.” Shetani hajabadilika. Kupitia uongo wake, anaendelea ‘kupotosha [kudanganya] dunia yote yenye kuikaliwa na watu.’ (Ufu. 12:9) Lakini hatupendi Shetani atudanganye. Kwa hiyo, tunapaswa kupata majibu ya maulizo tatu. Namna gani Shetani anadanganya watu leo? Juu ya nini watu wanasemaka uongo? Na namna gani tunaweza kusema kweli kila wakati ili tusipoteze urafiki wetu pamoja na Yehova, kama vile Adamu na Eva walifanya?​—Soma Zaburi 15:1, 2.

NAMNA SHETANI ANADANGANYA WATU LEO

5. Namna gani Shetani anadanganya watu leo?

5 Tunaweza kuepuka kudanganywa na Shetani. Mutume Paulo alisema hivi: “Hatukose kujua nia zake.” (2 Ko. 2:11; maelezo ya chini) Tunajua kama Shetani anatawala ulimwengu wote, kutia ndani dini za uongo, serikali zenye udanganyifu, na biashara yenye pupa. (1 Yo. 5:19) Kwa hiyo, hatushangae kuona kama Shetani na pepo wake wachafu wanasukuma watu wenye mamlaka kusudi waseme uongo. (1 Ti. 4:1, 2) Kwa mufano, wafanyabiashara fulani wanasema uongo mu matangazo yao ya biashara ili wauzishe vitu vyao vyenye kuleta hatari ao ili wadanganye watu na kuiba feza zao.

6, 7. (a) Juu ya nini ni mubaya zaidi wakati viongozi wa dini wanasema uongo? (b) Ni mafundisho gani ya uongo yenye umesikia viongozi wa dini wanafundisha?

6 Ni mubaya zaidi wakati viongozi wa dini wanasema uongo. Juu ya nini? Juu kama mutu fulani anaamini mafundisho ya uongo yenye wanafundisha na anafanya mambo yenye Mungu anachukia, anaweza kupoteza nafasi ya kuishi milele. (Ho. 4:9) Yesu alijua kama viongozi wa dini wa siku zake walikuwa wanadanganya watu. Aliwaambia hivi bila kuogopa: “Ole wenu, waandishi na Wafarisayo, wanafiki! kwa sababu munasafiri katika bahari na kwenye inchi kavu ili kufanya mutu mumoja kuwa mugeuzwa-imani, na wakati amegeuzwa imani, munamufanya astahili Gehena,” maana yake, uharibifu wa milele. (Mt. 23:15; maelezo ya chini) Yesu aliambia viongozi hao wa dini kama walikuwa tu kama baba yao Ibilisi, mwenye kuwa “muuaji.”​—Yoh. 8:44.

7 Leo pia kuko viongozi wengi wa dini. Wanaitwa kwa majina kama vile pastere, padri, ao kwa majina ingine ya cheo. Kama vile Wafarisayo, viongozi hao hawafundishe kweli yenye kuwa katika Neno la Mungu lakini ‘wamebadilisha kweli ya Mungu kwa ajili ya uongo.’ (Ro. 1:18, 25) Kati ya uongo wao kuko mafundisho yenye kusema kama “mutu akiisha kuokolewa, ameokolewa milele,” wanadamu wako na nafsi yenye haiwezi kufa, watu wenye kufa wanazaliwa katika mwili ingine, na kama Mungu anakubali wanaume wenye kulala na wanaume na wanamuke wenye kulala na wanamuke na ndoa kati ya wanaume na wanaume na wanamuke na wanamuke.

8. Ni uongo gani wenye viongozi wa politike watasema hivi karibuni, lakini tunapaswa kutenda namna gani?

8 Viongozi wa politike wametumia pia uongo ili kudanganya watu. Uongo mumoja mukubwa zaidi kati ya uongo wenye watasema hivi karibuni ni kwamba wameleta “amani na usalama” katika ulimwengu. Lakini “uharibifu wa kushitukia utakuja juu yao mara moja.” Kwa hiyo, hatupaswe kuamini viongozi hao wa politike, wenye wanasema kama mambo yanaendelea kuwa muzuri zaidi. Ukweli ni kwamba ‘tunajua muzuri sana kwamba siku ya Yehova inakuja sawasawa kabisa na vile mwizi anakuja usiku.’​—1 Te. 5:1-4.

JUU YA NINI WATU WANASEMAKA UONGO?

9, 10. (a) Juu ya nini watu wanasemaka uongo, na hilo linaleta matokeo gani? (b) Tunapaswa kukumbuka nini juu ya Yehova?

9 Leo, haiko tu watu wenye kuwa na mamlaka ndio wanasemaka uongo. Habari “Juu ya Nini Tunasemaka Uongo,” yenye iliandikwa na Bhattacharjee, inasema kama “tabia ya kusema uongo imefikia kujulikana kuwa tabia ya mwanadamu yenye kuwa na mizizi sana ndani yake.” Maana yake, watu wanawaza kama ni jambo la kawaida kusema uongo. Mara nyingi watu wanasema uongo ili wajilinde, pengine ili wafiche makosa yenye wamefanya ao matendo ya kuvunja sheria yenye wamefanya. Pia wanasema uongo ili wapate feza ao wapate faida katika njia zingine fulani. Habari hiyo inasema tena kama watu fulani hawaone kuwa ni shida kudanganya “wageni, wafanyakazi wenzao, marafiki, na watu wenye wanapenda.”

10 Uongo huo wote umeleta matokeo gani? Watu hawatumainiane tena, na uhusiano kati ya watu umeharibika. Kwa mufano, wazia namna bwana muaminifu anaweza kuhuzunika sana wakati anajua kama bibi yake amefanya uzinifu na kisha anasema uongo juu ya kuficha jambo lenye alifanya. Ao wazia namna inaweza kuhuzunisha sana wakati mwanaume anatendea mubaya bibi yake na watoto wake nyumbani, lakini wakati wako pamoja na watu wengine anaonyesha kama anawapenda na kuwahangaikia. Watu wenye kufanya vile wanaweza kudanganya watu, lakini tunapaswa kukumbuka kama hawawezi kumudanganya Yehova. Biblia inasema kama “vitu vyote viko uchi na vyenye kufunuliwa wazi” mbele yake.​—Ebr. 4:13.

11. Mufano mubaya wa Anania na Safira unatufundisha nini? (Ona picha ku mwanzo wa habari hii.)

11 Katika Biblia, kuko mufano mumoja wa bibi na bwana Wakristo wenye Shetani alisukuma ili wamudanganye Mungu. Anania na Safira walijaribu kudanganya mitume. Waliuzisha shamba lao na wakapelekea mitume sehemu fulani tu ya feza. Anania na Safira walipenda kujionyesha kwa wengine mu kutaniko, kwa hiyo waliambia mitume kama walileta feza yote. Lakini, Yehova alijua kama walikuwa wanasema uongo, na aliwapatia malipizi.​—Mdo. 5:1-10.

12. Watu wenye kusema uongo ili waumize wengine na wenye hawatubu watapatwa na nini, na juu ya nini?

12 Namna gani Yehova anaona watu wenye kusema uongo? Kama vile tu Shetani, watu wote wenye kusema uongo wenye kuumiza na wenye hawatubu watatupwa katika “lile ziwa la moto.” Maana yake, wataharibiwa milele. (Ufu. 20:10; 21:8; Zb. 5:6) Juu ya nini? Juu Yehova anaona watu hao wenye kusema uongo kama vile anaona watu wengine wote “wenye matendo yao yanachukiza mbele ya macho” yake.​—Ufu. 22:15, maelezo ya chini.

13. Tunajua nini juu ya Yehova, na hilo linatuchochea kufanya nini?

13 Tunajua kama Yehova haiko “mwanadamu bure mwenye anasemaka uongo” na kama “haiwezekane Mungu aseme uongo.” (Hes. 23:19; Ebr. 6:18) “Yehova anachukia . . . ulimi wa uongo.” (Mez. 6:16, 17) Kama tunataka kumupendeza, tunapaswa kusema kweli. Kwa hiyo, ‘hatuambiane uongo.’​—Kol. 3:9.

‘TUNASEMA KWELI’

14. (a) Ni nini inafanya Wakristo wa kweli wakuwe tofauti na watu wa dini za uongo? (b) Fasiria kanuni yenye kupatikana katika Luka 6:45.

14 Ni katika njia gani moja Wakristo wa kweli wako tofauti na watu wa dini za uongo? ‘Tunasema kweli.’ (Soma Zekaria 8:16, 17.) Paulo alisema hivi: “Tunajipendekeza sisi wenyewe kuwa watumishi wa Mungu, . . . kwa kusema maneno ya kweli.” (2 Ko. 6:4, 7) Na Yesu alisema kama watu wanasema “mambo yenye kujaa katika moyo.” (Lu. 6:45) Maana yake, mutu munyoofu anasema kweli. Hadanganye wageni, wafanyakazi wenzake, marafiki, na watu wenye anapenda. Sasa, tuzungumuzie mifano fulani juu ya namna tunaweza kuonyesha kama tunasema kweli katika mambo yote.

Unaona shida yenye kuwa katika maisha ya dada huyu kijana? (Picha hii inapatana na fungu la 15, 16)

15. (a) Juu ya nini ni mubaya kuishi maisha ya unafiki? (b) Ni nini inaweza kusaidia vijana wapinge mikazo ya vijana wenzao? (Ona maelezo ya chini.)

15 Kama uko kijana, unaweza kupenda wenzako waone kama uko sawa nao. Juu ya tamaa hiyo, vijana fulani wanaishi maisha ya unafiki. Wanajionyesha kuwa wako na mwenendo muzuri wakati wako pamoja na watu wa familia na ndugu na dada katika kutaniko, lakini wanabadilika kabisa wakati wanatumia adresi za Enternete za kupashana habari na watu wengi ao wakati wako pamoja na watu wenye hawamutumikie Yehova. Wanaweza kutumia maneno machafu, kuvaa nguo zenye kukosa kiasi, kusikiliza miziki yenye kuwa na maneno machafu, kulewa, kutumia dawa za kulewesha, kufanya urafiki wa kimapenzi katika siri, ao kufanya mambo mengine ya mubaya. Wanadanganya wazazi wao, ndugu na dada zao, na Yehova. (Zb. 26:4, 5) Lakini Yehova anajua wakati tunasema kama tunamuheshimia lakini tunafanya mambo yenye anachukia. (Mk. 7:6) Ni jambo la muzuri zaidi kufanya jambo lenye mezali hii inasema: “Moyo wako usisikilie wivu watenda-zambi, lakini umuogope Yehova muchana wote.”​—Mez. 23:17. * (Ona maelezo ya chini.)

16. Namna gani tunapaswa kujibu maulizo yenye kuwa kwenye ombi fulani la utumishi wa wakati wote?

16 Kama unapenda kuwa painia wa kawaida ao kuanza utumishi fulani wa pekee wa wakati wote, kwa mufano kutumikia ku Beteli, unapaswa kujaza ombi fulani. Ni jambo la maana sana kutoa majibu ya kweli juu ya afya yako, mambo ya kujifurahisha yenye unachagua, na juu ya mwenendo wako. (Ebr. 13:18) Halafu kama umefanya jambo lenye Yehova anachukia ao jambo fulani lenye kusumbua zamiri yako na haujaelezea wazee juu ya jambo hilo? Uwaombe musaada kusudi umutumikie Yehova na zamiri yenye kuwa safi.​—Ro. 9:1; Gal. 6:1.

17. Tunapaswa kufanya nini wakati maadui wetu wanatuuliza maulizo juu ya ndugu na dada zetu?

17 Unapaswa kufanya nini kama kazi yetu inakatazwa mahali kwenye unaishi na wenye mamlaka wanakufunga na kukuuliza maulizo juu ya ndugu na dada zako? Unapaswa kuwaambia kila jambo lenye unajua? Yesu alifanya nini wakati gavana Muroma alimuuliza maulizo? Yesu alitumikisha kanuni ya Biblia yenye kusema kama kuko “wakati wa kunyamaza na wakati wa kusema,” na wakati fulani hakusema hata neno moja! (Muh. 3:1, 7; Mt. 27:11-14) Kama tuko mu hali kama hiyo, tunapaswa kuwa na busara na kuwa waangalifu ili tusitie ndugu na dada zetu mu hatari.​—Mez. 10:19; 11:12.

Namna gani unaweza kuamua wakati wa kubakia kimya na wakati wa kusema kweli yote? (Picha hizi zinapatana na fungu la 17, 18)

18. Tuko na daraka gani ikiwa wazee wanatuuliza maulizo juu ya ndugu na dada zetu?

18 Halafu kama mutu fulani mu kutaniko amefanya zambi nzito na unajua jambo hilo? Wazee wako na daraka la kufanya kutaniko liendelee kuwa safi katika mwenendo, kwa hiyo wanaweza kukuuliza maulizo juu ya jambo hilo. Utafanya nini, zaidi sana kama mutu huyo ni rafiki yako wa sana ao mutu wa jamaa yako? Biblia inasema hivi: “Mwenye anatoa ushuhuda kwa uaminifu atasema kweli.” (Mez. 12:17; 21:28) Kwa hiyo, uko na daraka la kuambia wazee kweli yote bila kuficha kitu. Wazee wako na haki ya kujua habari yote kusudi wajue namna ya muzuri zaidi ya kusaidia mutu huyo akuwe tena na urafiki wa muzuri pamoja na Yehova.​—Yak. 5:14, 15.

19. Tutazungumuzia nini katika habari yenye kufuata?

19 Daudi alisali kwa Yehova hivi: “Unapendezwa na kweli katika mutu wa ndani.” (Zb. 51:6) Daudi alijua kama jambo la maana ni namna tuko ndani yetu. Kila wakati, Wakristo wa kweli ‘wanasema kweli mumoja na mwingine.’ Njia ingine ya kuonyesha kama tuko tofauti na watu wa dini za uongo ni kufundisha kweli yenye kuwa mu Biblia. Katika habari yenye kufuata, tutazungumuzia namna tunaweza kufanya vile mu kazi yetu ya kuhubiri.

^ fu. 15 Ona sura ya 15, “Nitashindaje Mkazo Kutoka kwa Vijana Wenzangu?,” na sura ya 16, “Kuwa na Nyuso Mbili​—Kuna Ubaya Gani?,” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2.