Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 43

Ushikamane na Yehova Tu

Ushikamane na Yehova Tu

“Yehova ni Mungu mwenye anataka watu washikamane na yeye tu.”​—NAH. 1:2.

WIMBO 51 Tumejiweka Wakfu kwa Mungu!

KIFUPI CHA HABARI *

1. Juu ya nini tunapaswa kushikamana na Yehova tu?

TUNAPASWA kushikamana na Yehova tu juu yeye njo Muumbaji wetu na yeye njo alitupatia uzima. (Ufu. 4:11) Lakini, kuko hatari fulani. Hata kama tunamupenda Yehova na tunamuheshimia, kuko mambo yenye inaweza kutukengeusha ili tusishikamane na yeye tu. Ni muzuri tuelewe namna jambo hilo linaweza kutokea. Lakini, tuzungumuzie kwanza maana ya kushikamana na Yehova tu.

2. Kulingana na Kutoka 34:14, tutafanya nini kama tunashikamana na Yehova tu?

2 Katika Biblia, kushikamana na Mungu maana yake kumupenda sana. Kama tunashikamana na Yehova tu, tutamuabudu yeye tu. Hatutaacha mutu yeyote ao kitu chochote kikamate nafasi yake mu moyo wetu.​—Soma Kutoka 34:14.

3. Juu ya nini tuko na sababu za muzuri za kushikamana na Yehova tu?

3 Tuko na sababu za muzuri za kushikamana na Yehova tu. Juu ya nini tunasema vile? Mambo yenye tumejifunza juu yake njo yenye inafanya tushikamane na yeye tu. Tumefikia kupenda sifa zake za muzuri sana. Tunajua mambo yenye anapenda na mambo yenye anachukia na tuko na mawazo kama yake juu ya ile mambo. Tunaelewa kusudi lake juu ya wanadamu na tunaunga mukono kusudi hilo. Anaturuhusu tukuwe marafiki wake na tunaona hilo kuwa pendeleo kabisa. (Zb. 25:14) Kila jambo lenye tunajifunza juu ya Muumbaji wetu linatufanya tumukaribie zaidi.​—Yak. 4:8.

4. (a) Ibilisi anatumia nini ili kuregeza ushikamanifu wetu kwa Yehova? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?

4 Ibilisi anatawala ulimwengu huu, na anatumia ulimwengu huu ili kuchochea tamaa zetu na uzaifu wetu wa kimwili. (Efe. 2:1-3; 1 Yo. 5:19) Anataka tupende mambo ingine pia ili tusishikamane na Yehova tu. Tuzungumuzie basi njia mbili zenye Ibilisi anatumia ili kufanya vile. Njia ya kwanza, anatuchochea tufuatie utajiri, na njia ya pili, anajaribu kutuchochea tuchague mambo ya mubaya ya kujifurahisha.

UKUWE MUANGALIFU ILI USIANZE KUPENDA FEZA

5. Juu ya nini tunapaswa kuwa waangalifu ili tusianze kupenda feza?

5 Kwa kawaida, tunapenda kuwa na chakula cha kutosha, manguo ya muzuri ya kuvaa, na nafasi ya muzuri ya kuishi. Lakini, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusianze kupenda feza. Watu wengi leo wenye kuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani ni “wenye kupenda feza” na vitu vyenye feza zinaweza kuuza. (2 Ti. 3:2) Yesu alijua kama wanafunzi wake wanaweza kuanza kupenda vitu hivyo. Alisema hivi: “Hakuna mutu mwenye anaweza kutumikia mabwana wawili; kwa maana atachukia mumoja na kupenda mwingine, ao atashikamana na mumoja na kuzarau mwingine. Hamuwezi kuwa watumwa wa Mungu na wa Utajiri.” (Mt. 6:24) Mutu mwenye anamuabudu Yehova na wakati uleule anapitisha wakati mingi na nguvu mingi ili kujikaza kupata utajiri wa ulimwengu huu, kwa njia fulani, ni kama vile anajaribu kutumikia mabwana wawili. Mutu kama huyo hashikamane na Yehova tu.

Namna watu fulani wa Laodikia walijiona . . . na namna Yehova na Yesu waliwaona (Picha hizi zinapatana na fungu la 6)

6. Maneno yenye Yesu aliambia kutaniko la Laodikia inaweza kutufundisha nini?

6 Mbele ya mwaka wa 100 kisha kuzaliwa kwa Yesu (K.K.Y.), ndugu na dada wa kutaniko lenye lilikuwa mu muji wa Laodikia walijivuna hivi: “Mimi ni tajiri, nimejipatia utajiri na sina lazima ya kitu chochote hata kidogo.” Lakini, Yehova na Yesu waliwaona kuwa ‘wenye taabu na wa kusikiliwa huruma na maskini na kipofu na uchi.’ Yesu aliwashauria, haiko juu walikuwa matajiri, lakini ni juu walikuwa wanapenda vitu vya kimwili na upendo huo ulikuwa unaharibu urafiki wao pamoja na Yehova. (Ufu. 3:14-17) Kama tunatambua kwamba tamaa ya kufuatia vitu vya kimwili inaanza kukomaa mu moyo wetu, tunapaswa kutenda haraka ili kurekebisha mawazo yetu. (1 Ti. 6:7, 8) Kama hatufanye vile, moyo wetu utagawanyika na Yehova hatakubali ibada yetu. “Anataka watu washikamane na yeye tu.” (Kum. 4:24) Namna gani mutu anaweza kuanza kutia feza pa nafasi ya kwanza mu maisha yake?

7-9. Mufano wa muzee mumoja mwenye kuitwa David, unaweza kukufundisha nini?

7 Fikiria mufano wa David, muzee wa kutaniko mwenye kutumika kwa bidii mwenye anaishi mu inchi ya Amerika. Anasema kama alikuwa mufanyakazi mwenye bidii. Kompanyi yenye alikuwa anatumikia ilimupatia kazi ya muzuri zaidi na feza zaidi, na alionwa kuwa mumoja kati ya wafanyakazi wazuri zaidi wa ile kazi katika inchi yao. David alisema hivi: “Wakati huo, niliwaza kama ile matokeo ya muzuri yenye nilipata ku kazi yangu ilionyesha kama Yehova alikuwa ananibariki.” Lakini, hiyo ilikuwa baraka ya Yehova kabisa?

8 David alianza kutambua kama kazi yake ilikuwa inaharibu urafiki wake pamoja na Yehova. Anasema hivi: “Ku mikutano ya kutaniko na hata ku mahubiri, nilianza kuwaza juu ya magumu ya kazi. Nilikuwa ninapata feza mingi, lakini niliendelea kuwa na mahangaiko, na nilianza kuwa na magumu mu ndoa yangu.”

9 David alitambua kama alipaswa kuchunguza mambo yenye alikuwa anatia pa nafasi ya kwanza. Anasema hivi: “Nilikamata uamuzi wa kufanya mabadiliko juu ya hali yangu.” David alipenda kubadilisha programu yake ya kazi, na alimuambia mukubwa wake wa kazi mambo yenye alipenda kufanya. Matokeo ilikuwa nini? David alifukuzwa ku kazi! Alitenda namna gani? Alisema hivi: “Siku yenye ilifuata, nilijaza ombi ili nikuwe painia musaidizi wa kuendelea.” Ili kutimiza mahitaji yao, David na bibi yake walianza kufanya kazi ya kusafisha majengo. Kisha wakati fulani, akakuwa painia wa kawaida, na kisha bibi yake naye akakuwa painia. Bwana huyo na bibi yake waliamua kufanya kazi ya kimwili yenye kuzarauliwa na watu wengi, lakini hawaone kama kazi yenye wako wanafanya njo jambo la maana mu maisha yao. Hata kama feza zenye wanapata zimepunguka mara kumi kuliko feza zenye walikuwa wanapata zamani, kila mwezi wako na feza zenye wako nazo lazima ili kutimiza mahitaji yao. Wanapenda kumutia Yehova pa nafasi ya kwanza mu maisha yao, na wamejionea kama anahangaikia wale wenye kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza mu maisha yao.​—Mt. 6:31-33.

10. Namna gani tunaweza kulinda moyo wetu?

10 Ikuwe tuko na vitu kidogo ao vitu mingi vya kimwili, tunapaswa kulinda moyo wetu. Namna gani? Usianze kupenda utajiri. Na usitie kazi yako ya kimwili pa nafasi ya kwanza kuliko kazi ya Yehova. Namna gani unaweza kujua kama uko unatia kazi yako pa nafasi ya kwanza? Ona maulizo fulani yenye unaweza kujiuliza: ‘Mara mingi ninafikiria kazi yangu ya kimwili wakati niko ku mikutano ao katika mahubiri? Ninahangaika kila mara ikiwa nitakuwa na feza za kutosha wakati wenye kuja? Feza na vitu vya kimwili viko vinaleta magumu mu ndoa yangu? Nitakuwa tayari kufanya kazi ya kimwili yenye watu wengi wanazarau kama inaniruhusu nipitishe wakati mingi mu kazi ya Yehova?’ (1 Ti. 6:9-12) Wakati tunajiuliza ile maulizo, tukumbuke kama Yehova anatupenda na anaahidi hivi wale wenye kushikamana naye: “Sitakuacha hata kidogo, na sitakutupa hata kidogo.” Njo maana mutume Paulo aliandika hivi: “Njia yenu ya maisha ikuwe bila upendo wa feza.”​—Ebr. 13:5, 6.

CHAGUA KWA UANGALIFU MAMBO YA KUJIFURAHISHA

11. Mambo ya kujifurahisha inaweza kuwa na matokeo gani juu ya watu?

11 Yehova anapenda tufurahie maisha, na mambo ya kujifurahisha inaweza kutusaidia kufanya vile. Njo maana Neno la Mungu linasema kama “hakuna jambo la muzuri zaidi kwa mutu kuliko kula, kunywa, na kufurahia kazi yake ya nguvu.” (Muh. 2:24) Lakini, mambo mingi ya kujifurahisha ya ulimwengu huu inaweza kuwa na matokeo ya mubaya juu yetu. Inaharibisha mwenendo wa watu, kwa kuwachochea wakubali, ao hata wapende mambo yenye Neno la Mungu linakataza.

Ni nani anatayarisha mambo yako ya kujifurahisha? (Picha hizi zinapatana na fungu la 11-14) *

12. Kulingana na 1 Wakorinto 10:21, 22, juu ya nini tunapaswa kuchagua kwa uangalifu mambo ya kujifurahisha?

12 Tunapenda kushikamana na Yehova tu, kwa hiyo, hatuwezi kula ku “meza ya Yehova” na ku “meza ya pepo wachafu.” (Soma 1 Wakorinto 10:21, 22.) Mara mingi kula chakula pamoja na mutu fulani ni alama ya urafiki. Kama tunachagua mambo ya kujifurahisha yenye inachochea jeuri, kupashana habari na pepo wachafu, uasherati, ao tamaa na mawazo ingine ya kimwili, ni kama vile tunakula chakula chenye maadui wa Mungu walitayarisha. Na kama tunafanya vile, tunajiumiza sisi wenyewe na tunaharibu urafiki wetu pamoja na Yehova.

13-14. Kulingana na Yakobo 1:14, 15, juu ya nini tunapaswa kuwa waangalifu juu ya mambo ya kujifurahisha yenye kuchochea tamaa za mubaya? Leta mufano.

13 Mambo ya kujifurahisha iko kama chakula. Tuone ni katika njia gani fulani. Wakati tunakula, tunaweza kuchagua vitu vyenye tutatia mu kinywa chetu. Lakini kisha kumeza chakula, hatuwezi kuchagua namna chakula hicho kitatumika mu mwili wetu. Chakula cha muzuri kinaweza kutufanya tukuwe na afya ya muzuri, lakini chakula cha mubaya kinaweza kuharibisha afya yetu. Pengine hatutaona palepale matokeo ya chakula juu ya mwili wetu, lakini itaonekana kisha wakati fulani.

14 Vilevile, wakati tunachagua mambo ya kujifurahisha, tunaweza kuamua mambo yenye tutatia mu akili yetu. Lakini kisha, mambo ya kujifurahisha yenye tumechagua itakuwa na matokeo ya muzuri ao ya mubaya juu ya akili na moyo wetu. Mambo ya muzuri ya kujifurahisha inaweza kufanya tujisikie muzuri, lakini mambo ya kujifurahisha yenye haifae inaweza kutuletea matokeo ya mubaya. (Soma Yakobo 1:14, 15.) Pengine matokeo ya mambo ya mubaya ya kujifurahisha haitaonekana palepale, lakini itaonekana kisha wakati fulani. Njo maana Biblia inatuonya hivi: “Musidanganywe: Mungu haiko wa kuchekelewa. Kwa maana kitu chochote chenye mutu anapanda, ni kile atavuna pia; kwa sababu ule mwenye anapanda kwa mwili wake atavuna uharibifu kutokana na mwili wake.” (Gal. 6:7, 8) Ni jambo la maana kabisa tuepuke mambo yote ya kujifurahisha yenye inachochea watu wapende mambo yenye Yehova anachukia!​—Zb. 97:10.

15. Ni zawadi gani ya kufurahisha yenye Yehova ametupatia?

15 Watumishi wengi wa Yehova wanafurahia kuangalia JW Télédiffusion, kituo chetu cha televizyo kwenye Enternete chenye kuwa na programu za muzuri. Dada mumoja mwenye kuitwa Marilyn alisema hivi: “JW Télédiffusion imenisaidia kuwa na mawazo ya muzuri zaidi, na ninaweza kuangalia mambo yote juu yote ni ya muzuri. Wakati ninajisikia kuwa pekee yangu ao mwenye kuvunjika moyo, ninafuata hotuba ao programu fulani ya Ibada ya Familia yenye kutia moyo. Hilo linanisaidia nijisikie kuwa karibu zaidi na Yehova na tengenezo lake. JW Télédiffusion imebadilisha kabisa maisha yangu.” Uko unafaidika na zawadi hiyo yenye Yehova ametupatia? Zaidi ya programu mupya ya kila mwezi, JW Télédiffusion iko na video na programu za mingi za kusikiliza na pia nyimbo zenye kutia moyo zenye unaweza kuangalia ao kusikiliza wakati wowote.

16-17. (a) Juu ya nini tunapaswa kuchunguza kwa uangalifu wakati wenye tunapitisha katika mambo ya kujifurahisha? (b) Tunaweza kufanya nini ili tusipitishe wakati mingi zaidi katika mambo ya kujifurahisha?

16 Tunapaswa kuchagua kwa uangalifu aina ya mambo ya kujifurahisha na pia wakati wenye tunatumia katika ile mambo. Kama hatufanye vile, tunaweza kupitisha wakati mingi zaidi katika kujifurahisha kuliko wakati wenye tunapitisha katika kazi ya Yehova. Watu wengi wanashindwa kuamua wakati wenye watapitisha katika mambo ya kujifurahisha. Dada mumoja mwenye kuwa na miaka 18 mwenye kuitwa Abigail anasema hivi: “Kuangalia televizyo kunanisaidia nijisikie muzuri kisha kutumika sana muchana wote. Lakini, kama siko muangalifu, ninaweza kupitisha saa za mingi mbele ya televizyo.” Ndugu kijana mwenye kuitwa Samuel anasema hivi: “Wakati fulani ninaangalia video mingi za mufupi-mufupi ku Enternete. Ninaangalia kwanza moja, na ninajikuta nimepitisha saa tatu ao ine bila kujua.”

17 Unaweza kufanya nini ili usipitishe wakati mingi zaidi katika mambo ya kujifurahisha? Jambo la kwanza ni kuchunguza wakati wenye unapitisha katika mambo ya kujifurahisha. Unaweza kuandika wakati wenye unapitisha katika mambo ya kujifurahisha kwa juma moja. Andika ku kalendari saa zenye unapitisha ili kuangalia televizyo, kutafuta-tafuta habari ku Enternete, na kucheza michezo ya video ku chombo chako cha kielektroniki kama vile telefone ao tablete. Ukiona kama uko unapitisha wakati mingi sana katika mambo ya kujifurahisha, ujaribu kufanya programu. Kwanza, panga wakati wa kufanya mambo ya maana zaidi, kisha upange wakati wa kupitisha katika mambo ya kujifurahisha. Kisha, umuombe Yehova akusaidie uheshimie programu yako. Ukifanya vile, utakuwa na wakati na nguvu zenye uko nazo lazima ili kufanya funzo la pekee, ibada ya familia, kuenda ku mikutano ya kutaniko, na kumutumikia Yehova katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Pia, inawezekana hautajilaumu juu ya wakati wenye unapitisha katika mambo ya kujifurahisha.

ENDELEA KUSHIKAMANA NA YEHOVA TU

18-19. Namna gani tunaweza kuonyesha kama tunashikamana na Yehova tu?

18 Kisha kuandika juu ya mwisho wa ulimwengu wa Shetani na juu ya ulimwengu mupya wenye utakuja, mutume Petro alisema hivi: “Wapendwa, kwa kuwa munangojea mambo hayo, mufanye nguvu yenu yote ili mwishowe awapate ninyi mukiwa bila doa na uchafu na mukiwa katika amani.” (2 Pe. 3:14) Wakati tunatii shauri hilo na kufanya nguvu yetu yote ili tuendelee kuwa safi kiroho na katika mwenendo wetu, tunaonyesha kama tunashikamana na Yehova tu.

19 Shetani na ulimwengu wake wataendelea kutushawishi ili tusitie mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza. (Lu. 4:13) Lakini, hata tupate majaribu gani, hatutaruhusu kitu chochote ao mutu yeyote akamate nafasi ya Yehova mu moyo wetu. Tunaazimia kumupatia Yehova kile chenye yeye tu njo anastahili, ni kusema, ushikamanifu wetu!

WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu

^ fu. 5 Tunapenda kumutumikia Yehova. Lakini, je, tunashikamana na yeye tu? Maamuzi yenye tunakamata mu maisha njo yenye inaonyesha ikiwa tunashikamana na Yehova tu ao hapana. Tuzungumuzie basi mambo mbili yenye inaweza kutusaidia tuone ikiwa tunashikamana na Yehova tu ao hapana.

^ fu. 53 MAFASIRIO YA PICHA: Hatuwezi kufurahia kula chakula chenye kimepikwa katika mafiga yenye kuwa chafu. Vilevile, hatuwezi kufurahia kuangalia mambo ya kujifurahisha yenye kuchafuliwa na jeuri, mambo ya kupashana habari na pepo wachafu, ao uasherati.