Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unaheshimia Kabisa Neno la Yehova?

Unaheshimia Kabisa Neno la Yehova?

‘Mulipolipokea neno la Mungu, . . . mulilikubali . . . kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.’—1 WATHESALONIKE 2:13.

NYIMBO: 114, 113

1-3. Pengine Euodia na Sintike walikuwa na tatizo gani? Namna gani tunaweza kuepuka matatizo kama hayo? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

TUNAONA Biblia kuwa kitabu cha maana sana kwa sababu tunajua kama ni Neno la Mungu. Biblia iko na mashauri yenye yanaweza kutusaidia kuepuka matatizo, na inaweza kutusaidia wakati tunafanya makosa. Kwa hiyo, tunatenda namna gani wakati tunasoma mashauri ya Biblia? Fikiria wanawake wawili watiwa-mafuta wa wakati wa mitume, Euodia na Sintike. Biblia inasema kama walibishana, lakini haituambie sababu gani. Tuwazie basi mambo yenye pengine yalifanyika.

2 Pengine Euodia alialika ndugu na dada fulani kwenye nyumba yake ili wakule chakula pamoja. Lakini hakualika Sintike. Kisha, wakati Sintike alisikia ndugu na dada wanasema kama walifurahia sana chakula, alikasirika sana. Pengine aliwaza hivi: ‘Siwezi kuelewa sababu gani Euodia hakunialika! Nilifikiri kama tuko marafiki wa sana.’ Sintike aliona kama Euodia hamupendi kabisa na kama alikuwa anamuepuka. Kwa hiyo, Sintike alialika ndugu na dada walewale ili wakule chakula pamoja, lakini hakualika Euodia! Pengine hali hiyo haikufurahisha wengine katika kutaniko. Biblia inaonyesha kama Mutume Paulo alisaidia dada hao na aliwatia moyo wafanye amani. Inawezekana walimusikiliza na waliendelea kumutumikia Yehova kwa furaha.—Wafilipi 4:2, 3.

3 Leo, katika makutaniko yetu, wakati fulani sisi pia tunaweza kuwa na tatizo pamoja na ndugu ao dada yetu. Lakini ikiwa tunafuata mashauri yenye kuwa katika Biblia, tunaweza kumaliza matatizo hayo. Tunaweza hata kuyaepuka. Na wakati tunatii mambo yenye Biblia inasema, tunaonyesha kama tunaona Neno la Yehova kuwa la maana sana.—Zaburi 27:11.

BIBLIA INATUFUNDISHA KUJIZUIA

4, 5. Neno la Mungu linatutolea shauri gani juu ya kuzuia hasira yetu?

4 Sikuzote, haiko vyepesi kujizuia. Tunaweza kuhuzunika sana ao kukasirika ikiwa mutu fulani anasema mambo ya mubaya juu yetu ao anatutendea mubaya, pengine kwa sababu ya desturi yetu, rangi yetu ya ngozi, ao kwa sababu ya namna tunaonekana. Na inaweza kutuumiza hata zaidi ikiwa mutu mwenye kusema mambo ya mubaya juu yetu ao mwenye anatutendea mubaya ni ndugu ao dada yetu. Neno la Mungu linatutolea shauri gani lenye linaweza kutusaidia?

5 Yehova anajua jambo lenye linaweza kutokea wakati watu hawajizuie. Wakati tunakasirika ao tuko na hasira, tunaweza kusema ao kufanya mambo yenye tutahuzunikia kisha wakati fulani. Katika Biblia, Yehova anatuomba tuzuie hasira yetu na anatuambia hivi: ‘Usikuwe na haraka kuuzika katika roho yako.’ Tunaepuka magumu mengi sana wakati tunatii shauri hilo na wakati hatukasirike haraka! (Soma Mhubiri 7:9; Methali 16:32.) Pia, Biblia inatuambia tusamehe wengine. Kwa kweli, Yesu alisema kama ikiwa hatusamehe wengine, Yehova naye hatatusamehe. (Mathayo 6:14, 15) Uko na lazima ya kuwa muvumilivu zaidi na kuwa tayari kabisa kusamehe wengine?

6. Nini inaweza kutokea ikiwa hatuzuie hasira yetu?

6 Ikiwa hatujizuie, tunaweza kuendelea kusikia hasira na hata kuanza kuchukia mutu mwenye alitukosea. Ao tunaweza kuchochea wengine katika kutaniko wamuchukie pia. Hata kama tunajikaza kuficha hasira ao chuki yetu, wengine watafikia kutambua namna tunajisikia. Kisha ndugu na dada zetu wanaweza kutuepuka. (Methali 26:24-26) Wazee watatumia Biblia ili kutusaidia kuachana na hasira na chuki yetu na kusamehe wengine. (Mambo ya Walawi 19:17, 18; Waroma 3:11-18) Wakati wanafanya hivyo, tutafuata muongozo wa Neno la Yehova?

YEHOVA ANATUONGOZA

7, 8. (a) Namna gani Yehova anaongoza watu wake? (b) Biblia inatutolea miongozo gani fulani, na sababu gani tunapaswa kutii miongozo hiyo?

7 Leo, Yehova anaongoza watu wenye kuwa katika sehemu ya duniani ya tengenezo lake na anawafundisha. Namna gani? Ameweka Kristo kuwa “kichwa cha kutaniko,” na Yesu ameweka ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara’ ili afundishe na kuongoza watu wa Mungu. (Waefeso 5:23; Mathayo 24:45-47) Kama baraza lenye kuongoza la wakati wa mitume, mutumwa huyo anaona Biblia kuwa kitabu cha maana sana kwa sababu ni Neno la Mungu. (Soma 1 Wathesalonike 2:13.) Tunapata miongozo gani fulani katika Biblia?

8 Biblia inatuomba tukusanyike kwa ukawaida. (Waebrania 10:24, 25) Inatutia moyo sisi wote tuamini mafundisho yaleyale ya Biblia. (1 Wakorintho 1:10) Inatuambia pia tuendelee “kuutafuta kwanza Ufalme.” (Mathayo 6:33) Biblia inatuomba tuhubiri nyumba kwa nyumba, mahali pa watu wengi, na kila mahali watu wanaweza kupatikana. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 5:42; 17:17; 20:20) Inaomba wazee walinde usafi wa kutaniko. (1 Wakorintho 5:1-5, 13; 1 Timotheo 5:19-21) Inatuambia kama tunapaswa kulinda usafi wa mwili wetu na kuepuka mawazo na tabia zenye Yehova anachukia.—2 Wakorintho 7:1.

9. Yesu ameweka nani ili kutusaidia kuelewa Neno la Mungu?

9 Watu fulani wanaweza kufikiri kama hawana lazima ya mutu wa kuwafasiria Biblia. Lakini, tangu mwaka wa 1919, Yesu anatumia ‘mutumwa mwaminifu na mwenye busara’ ili kusaidia watu wa Mungu waelewe mambo yenye Biblia inafundisha na kuyatii. Wakati tunatii mafundisho ya Biblia, tunalinda usafi, amani, na umoja wa kutaniko. Ujiulize hivi: ‘Nitakuwa mushikamanifu kwa Yesu na kufuata muongozo wa mutumwa mwaminifu?’

GARI LA YEHOVA LINAENDA HARAKA!

10. Namna gani kitabu cha Ezekieli kinafasiria sehemu ya mbinguni ya tengenezo la Yehova?

10 Biblia inatufundisha kuwa watumishi wa Yehova wa mbinguni ni wenye kupangwa pia. Kwa mufano, katika maono Ezekieli aliona Yehova anatembeza gari lenye lilikuwa linaenda haraka sana katika upande wowote wenye Yehova alipenda liende. (Ezekieli 1:4-28) Gari hilo linafananisha sehemu ya mbinguni ya tengenezo la Mungu, lenye kufuata haraka muongozo wake. Na hilo linakuwa na matokeo juu ya sehemu ya duniani ya tengenezo lake. Fikiria mabadiliko mengi yenye yamefanyika katika tengenezo la Mungu katika miaka kumi yenye imepita. Ukumbuke kama Yehova ndiye anaongoza mabadiliko hayo. Hivi karibuni, Kristo na malaika wataharibu ulimwengu huu muovu. Hakutakuwa tena mutu mwenye atakosea Yehova na jina lake heshima ao kuchambua namna yake ya kutawala!

Tuko wenye shukrani sana kwa wajenzi wengi wenye kujitolea na kutumika kwa bidii! (Picha hii inapatana na fungu la 11)

11, 12. Tengenezo la Yehova limefanya mambo gani katika siku hizi za mwisho?

11 Fikiria mambo yenye tengenezo la Yehova limefanya katika siku hizi za mwisho. Kazi ya kujenga. Mamia ya ndugu na dada wametumika kwa bidii ili kujenga makao makubwa ya mupya ya Mashahidi wa Yehova katika Warwick, New York, katika Amerika. Maelfu ya ndugu na dada wengine wenye kujitolea katika dunia yote wanajenga Majumba ya Ufalme na biro za tawi. Ndugu na dada hao wenye kujitolea wanaongozwa na Idara ya Ulimwenguni Pote ya Uchoraji wa Majengo na Ujenzi. Tuko wenye shukrani sana kwa wote wenye kufanya kwa bidii kazi hiyo ya kujenga! Na watumishi wa Yehova katika dunia yote wanatoa michango kulingana na uwezo wao ili kutegemeza kazi hiyo ya kujenga. Yehova anabariki watu wake kwa sababu ya unyenyekevu na ushikamanifu wenye wanaonyesha.​—Luka 21:1-4.

12 Kufundisha watu. Yehova anapenda kufundisha watu wake. (Isaya 2:2, 3) Fikiria masomo mbalimbali yenye tuko nayo. Kuko Masomo ya Mapainia, Masomo ya Waeneza-Injili wa Ufalme, Masomo ya Gileadi, Masomo ya Wanabeteli Wapya, Masomo ya Waangalizi wa Muzunguko na Bibi Zao, Masomo ya Wazee wa Kutaniko, Masomo ya Huduma ya Ufalme, na Masomo ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi na Bibi Zao. Na kwenye adresi yetu ya Internete, jw.org, tunaweza kupata Biblia na vichapo vingine katika mamia ya luga. Adresi hiyo iko pia na sehemu za pekee kwa ajili ya watoto na familia na pia sehemu yenye kuwa na habari mbalimbali. Mumekwisha kuanza kutumia jw.org katika mahubiri na katika ibada yenu ya familia?

UKUWE MUSHIKAMANIFU KWA YEHOVA NA UTEGEMEZE TENGENEZO LAKE

13. Watu wa Mungu wanapaswa kufanya nini?

13 Ni pendeleo kubwa sana kuwa katika tengenezo la Yehova na kujua mambo yenye anatuomba tufanye! Kwa kweli, kwa sababu tunajua mambo yenye kupendeza Mungu, tunapaswa kumutii na kufanya mambo yenye kuwa sawa. Na hata kama watu wengi wanapenda kufanya mambo ya mubaya, tunapaswa ‘kuchukia yaliyo mabaya,’ kama vile Yehova anayachukia. (Zaburi 97:10) Hatupaswe hata kidogo kuwa kama watu wenye kufikiri kuwa “wema ni ubaya na ubaya ni wema.” (Isaya 5:20) Tunataka kumupendeza Yehova; kwa hiyo, tunaazimia kuwa safi katika kila njia. (1 Wakorintho 6:9-11) Mambo yenye Yehova anatufundisha katika Biblia ni kwa faida yetu wenyewe. Tunamupenda na tunapenda kuwa washikamanifu kwake. Ndiyo sababu tunafuata muongozo wake katika familia, katika kutaniko, kwenye kazi, kwenye masomo, ao kila mahali kwenye tunaweza kupatikana. (Methali 15:3) Fikiria hali fulani ambamo tunapaswa kuwa washikamanifu kwa Mungu.

14. Namna gani wazazi wanaweza kuwa washikamanifu kwa Yehova?

14 Namna tunazoeza watoto wetu. Katika Biblia, Yehova ametolea wazazi muongozo juu ya namna ya kuzoeza watoto wao. Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu ili wasichochewe kuiga namna ya kufikiri ya watu wengi wa ulimwengu huu. (Waefeso 2:2) Kwa mufano, katika maeneo fulani baba anaweza kuwaza kama ‘Daraka la kufundisha watoto ni la wanawake.’ Lakini Biblia inasema waziwazi kama baba wanapaswa kufundisha watoto wao juu ya Yehova. (Waefeso 6:4) Baba na mama wenye kumupenda Yehova wanataka watoto wao wakuwe na urafiki wa sana pamoja na Yehova, kama vile Samweli alikuwa rafiki ya Yehova wakati alikuwa mutoto.​—1 Samweli 3:19.

15. Namna gani tunaweza kuwa washikamanifu kwa Yehova wakati tunakamata maamuzi mazito?

15 Namna tunakamata maamuzi. Mbele tukamate maamuzi mazito katika maisha, tunapaswa kujua mawazo ya Yehova ili tukuwe washikamanifu kwake. Biblia na tengenezo lake vinaweza kutusaidia. Kwa mufano, leo wakati wazazi fulani wenye wamehamia katika inchi ingine wanazaa mutoto, wanaamua kutuma mutoto huyo katika inchi yao ili aishi pamoja na watu wa jamaa yao. Kwa hiyo, baba na mama wanaendelea kutumika ili kupata feza. Kwa kweli, huo ni uamuzi wa mutu yeye mwenyewe, lakini bibi na bwana wanapaswa kujiuliza hivi: ‘Yehova atawaza nini juu ya uamuzi wetu?’ (Soma Waroma 14:12.) Mbele ya kukamata maamuzi ya maana juu ya familia ao juu ya kazi yetu, itakuwa jambo la hekima kufikiri juu ya mambo yenye Biblia inasema. Tuko na lazima ya musaada wa Baba yetu wa mbinguni kwa sababu hatuwezi kuongoza hatua zetu.—Yeremia 10:23.

16. Wakati mama mumoja alizaa mutoto, alipaswa kukamata uamuzi gani? Ni nini ilimusaidia akamate uamuzi wa muzuri?

16 Kisha bibi na bwana fulani kuhamia katika inchi ingine, walizaa mutoto, na walipanga kumutuma katika inchi yao ili aishi pamoja na wazazi wao. Lakini wakati huo, bibi alianza kujifunza Biblia na Shahidi wa Yehova. Alijifunza kama ni daraka lake kufundisha mutoto wake mwanaume juu ya Yehova. (Zaburi 127:3; Methali 22:6) Kama vile Biblia inatuomba kufanya, mwanamuke huyo alisali kwa Yehova, na kumuomba amusaidie kufanya mambo yenye kuwa sawa. (Zaburi 62:7, 8) Pia, aliambia tatizo lake dada mwenye alikuwa anajifunza naye Biblia na aliambia pia wengine katika kutaniko. Hata kama watu wa jamaa na marafiki wake walikuwa wanamuambia kama anapaswa kutuma mutoto wake kwa wazazi wao, aliamua kama haikukuwa muzuri afanye hivyo. Bwana yake aliona namna ndugu na dada walisaidia sana bibi yake na mutoto wao. Alishangaa sana; kwa hiyo, aliamua kuanza kujifunza Biblia na kuenda kwenye mikutano pamoja na familia yake. Fikiria namna mama huyo alifurahi sana wakati alitambua kama Yehova alikuwa amejibu sala yake!

17. Wakati tunajifunza Biblia pamoja na mutu fulani, ni muongozo gani wenye tunapaswa kufuata?

17 Namna tunafuata muongozo. Ikiwa tuko washikamanifu kwa Yehova, tutafuata muongozo wenye tengenezo lake linatutolea. Kwa mufano, fikiria mambo yenye tunapaswa kufanya kisha tu kuanza kujifunza pamoja na mutu fulani kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? Tumeambiwa kama tunapaswa kutumia dakika kidogo kisha kumaliza kila funzo ili kusaidia mwanafunzi afikie kujua mengi juu ya tengenezo la Yehova. Tunaweza kutumia video Kwa Kawaida, Ni Mambo Gani Tunafanya Kwenye Jumba la Ufalme? na broshua Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo? Kisha kumaliza kitabu Biblia Inafundisha, tunaweza kusaidia mwanafunzi akuwe kabisa ‘imara katika imani’ kwa kujifunza pamoja naye kitabu Mubaki “Katika Upendo wa Mungu, hata kama amekwisha kubatizwa. (Wakolosai 2:7) Unaendelea kufuata muongozo huo wenye tengenezo la Yehova linatutolea?

18, 19. Tuko na sababu gani fulani za kumushukuru Yehova?

18 Tuko na sababu nyingi za kumushukuru Yehova! Sababu moja ni kwamba “kupitia kwake tuna uhai [uzima] na tunaenda na kuwako.” (Matendo 17:27, 28) Pia, ametupatia Neno lake, Biblia. Kama vile Wakristo wa Thesalonike, tunafurahia sana zawadi hiyo kwa sababu ni ujumbe wenye kutoka kwake.​—1 Wathesalonike 2:13.

19 Biblia imetusaidia kumukaribia Yehova, na yeye ametukaribia pia. (Yakobo 4:8) Tuko wenye shukrani sana kwa sababu Baba yetu ametualika tukuwe katika tengenezo lake! Tunajisikia kama vile muandikaji mumoja wa Zaburi mwenye aliandika hivi: ‘Mumushukuru Yehova, kwa maana ni mwema: Kwa maana fazili zake zenye upendo ni za mupaka wakati usio na kipimo.’ (Zaburi 136:1) Katika kila mustari wa Zaburi hiyo ya 136, muandikaji anarudilia maneno ‘fazili zake zenye upendo ni za mupaka wakati usio na kipimo.’ Kwa kweli, ikiwa tuko washikamanifu kwa Yehova na tunafuata muongozo wenye anatutolea kupitia tengenezo lake, atatupatia uzima wa milele na atakuwa mushikamanifu kwetu milele!