Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Onésime na Géraldine

Yehova Anabariki Wale Wenye Wanarudia Katika Inchi Zao

Yehova Anabariki Wale Wenye Wanarudia Katika Inchi Zao

NDUGU na dada wengi wenye walihamia mu inchi zingine ili kutafuta feza, wamerudia katika inchi zao. Kwa sababu wanamupenda Yehova na wanadamu wenzao, walihamia mahali kwenye kuwa lazima kubwa ya wahubiri. (Mt. 22:37-39) Walijiima mambo gani na wamepata baraka gani? Ili kupata jibu tuzungumuzie ndugu na dada wa inchi ya Kameruni katika Afrika ya mangaribi.

“NAFASI YENYE KUFAA KWA AJILI YA ‘KUVUA’”

Mu mwaka wa 1998, ndugu mumoja mwenye kuitwa Onésime alitoka kwao mu inchi ya Kameruni na akahamia mu inchi ingine. Alifanya miaka 14 mu ile inchi. Siku moja kwenye mukutano alisikia mufano wenye kuhusu kazi ya kuhubiri. Musemaji alisema hivi: “Kama marafiki wawili wako wanavua samaki kwenye nafasi mbili mbalimbali, unawaza ule mwenye iko anakamata samaki kidogo hataenda nafasi kwenye ule mwenye iko anakamata samaki wengi iko?”

Ule mufano ulimusaidia Onésime afikirie kurudia mu inchi ya Kameruni, kwenye watu wengi walikuwa wanapenda kujifunza Biblia. Lakini alikuwa na wasiwasi. Alikuwa anajiuliza kama angezoea maisha ya kule kisha kuishi miaka mingi mu inchi ingine. Ili kujua kama angeweza, Onésime alienda Kameruni kwa miezi sita. Kisha mu mwaka wa 2012, alihamia Kameruni ili kuishi kule.

Onésime anasema hivi: “Nilipaswa kujipatanisha na hali ya maisha ya kule, na pia hali ya hewa yenye joto. Na mu Jumba la Ufalme nilipaswa kuzoea tena kukaa kwenye viti vya mbao.” Anasema tena hivi kwa furaha: “Lakini, kadiri nilikuwa nakaza akili kwenye programu ya mikutano, ni vile nilikuwa ninasahau viti vya muzuri vyenye kuwa mu Majumba ingine ya Ufalme.”

Mu mwaka wa 2013, Onésime alioa Géraldine, mwenye naye alirudia Kameruni kisha kuishi miaka kenda katika inchi ya Ufaransa. Walipata baraka gani kwa sababu walitia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza mu maisha yao? Onésime anasema hivi: “Tulisoma Masomo kwa Ajili ya Waeneza-Injili wa Ufalme na tulianza kutumikia ku Beteli. Mu mwaka moja tu, watu 20 wenye walikuwa wanajifunza Biblia mu kutaniko letu, walibatizwa. Sasa, nawaza kama niko kwenye nafasi yenye kufaa kwa ajili ya ‘kuvua.’” (Mk. 1:17, 18) Géraldine anaongeza hivi: “Nimepata baraka mingi kuliko vile ningewazia.”

NINAFURAHI KUPATA WATOTO WA KIROHO

Judith na Sam-Castel

Judith alikuwa amehamia katika Inchi ya Amerika na alikuwa anapenda sana kufanya mambo mingi mu kazi ya Yehova. Anasema hivi: “Kila mara wakati nilikuwa natembelea familia yangu katika Kameruni, mbele nirudie nilikuwa nalia kwa sababu nilipaswa kuacha watu wenye nilikuwa nimeanza kujifunza nao Biblia.” Lakini, Judith alikuwa anasita kuhamia Kameruni. Alikuwa na kazi ya muzuri na alikuwa anapata feza mingi, zenye zilimusaidia akuwe analipa matunzo ya baba yake mwenye alikuwa Kameruni. Hata vile, alimutumainia Yehova na akahamia Kameruni. Anakubali kama alikuwa anakumbuka mambo fulani yenye alikuwa anafurahia wakati alikuwa katika Inchi ya Amerika. Alimuomba Yehova amusaidie ili ajipatanishe na hali ya maisha ya Kameruni. Na alipata musaada wa Yehova kupitia mwangalizi wa muzunguko na bibi yake wenye walimutia moyo.

Judith anakumbuka hivi: “Mu miaka tatu nilifurahi kupata watoto ine wa kiroho.” Judith alifikia kuwa painia wa pekee. Leo iko anatumika pamoja na bwana yake Sam-Castel, mu kazi ya muzunguko. Lakini mambo ilikuwa namna gani juu ya baba ya Judith? Judith na familia yake waliweza kupata hospitali mu inchi ingine yenye ilikuwa tayari kulipia upasuaji wa baba yake. Inafurahisha kujua kama upasuaji wa baba yake ulipita muzuri.

YEHOVA ALITUTEGEMEZA

Caroline na Victor

Ndugu mwenye kuitwa Victor alihamia katika inchi ya Kanada. Kisha kusoma habari fulani mu Munara wa Mulinzi, yenye ilikuwa inazungumuzia masomo ya juu, alifikiri kuhusu masomo yenye alikuwa anasoma. Aliacha masomo ya juu na akajifunza ufundi fulani wenye haungemukamata wakati mingi. Anasema hivi: “Ile ilinisaidia nipate kazi bila kukawia na nifanye jambo lenye nilikuwa napenda sana, ni kusema, kazi ya upainia.” Kisha Victor alioa Caroline, na walitembelea Kameruni. Wakati walikuwa kule, walitembelea biro ya tawi na walitiwa moyo wafikiri ikiwa wanaweza kutumikia katika Kameruni. Victor anasema hivi: “Hatukukuwa na sababu ya kukataa. Na kwa sababu tulikuwa tumefanya maisha yetu ikuwe mwepesi, tulikubali kutumikia Kameruni.” Hata kama Caroline alikuwa na matatizo fulani ya afya walikubali tu kuhamia Kameruni.

Victor na Caroline walianza kutumikia katika Kameruni wakiwa mapainia wa kawaida, ili kusaidia watu wenye walikuwa wanafurahia kujifunza Biblia. Kwa wakati fulani walitumia feza zote zenye walikuwa wamechunga. Kisha walienda kutumika katika Kanada kwa miezi fulani na walipata feza zenye ziliwasaidia warudie Kameruni ili waendelee kufanya kazi ya upainia. Walipata baraka gani? Walisoma Masomo kwa Ajili ya Waeneza-Injili wa Ufalme, walifikia kuwa mapainia wa pekee, na sasa wako mu kazi ya ujenzi. Victor anasema hivi: “Kwa sababu tuliacha maisha yenye tulikuwa nayo, tulipaswa kumutegemea Yehova, na Yehova alitutegemeza.”

FURAHA YA KUSAIDIA WATU WAJITOE KWA YEHOVA

Stéphanie na Alain

Mu mwaka wa 2002, Alain, mwenye alikuwa nasoma masomo ya juu mu inchi ya Ujerumani, alisoma trakte Vijana​—Mtatumiaje Maisha Yenu? Mambo yenye alisoma ilimuchochea ajiwekee miradi ingine. Mu mwaka wa 2006, alisoma Shule ya Mazoezi ya Kihuduma na alipewa mugao wa kutumikia katika Kameruni, kwenye alizaliwa.

Wakati alikuwa Kameruni, Alain alipata kazi yenye haikumukamata wakati mingi. Kisha alipata kazi yenye ilimusaidia apate feza mingi, lakini alikuwa na wasiwasi kuwa ile kazi ingefanya asikuwe anahubiri sana sawa zamani. Kwa hiyo, wakati aliombwa kuwa painia wa pekee, alikubali bila kusita. Mukubwa wake wa kazi alimuahidi kama atamuongezea mushahara, lakini Alain alikataa na akakuwa painia wa pekee. Kisha, Alain alioa Stéphanie, mwenye naye aliishi miaka fulani katika inchi ya Ufaransa. Stéphanie alipata magumu gani wakati alihamia Kameruni?

Stéphanie anasema hivi: “Nilianza kuwa na matatizo kidogo-kidogo ya afya. Lakini nilikuwa ninapata matunzo kwa ukawaida na nilijisikia muzuri.” Yehova alibariki Stéphanie na bwana yake kwa sababu walivumilia. Alain anasema hivi: “Wakati tulienda kuhubiri mu kijiji cha Katé, kijiji chenye kuwa mbali sana, tulipata watu wengi wenye walipenda kujifunza Biblia. Kisha tulianza kujifunza nao kupitia telefone. Kati ya watu wenye tulikuwa tunajifunza nao, watu wawili walifikia kubatizwa, na kikundi cha wahubiri kilianzishwa.” Stéphanie anaongeza hivi: “Hakuna furaha yenye inashinda furaha ya kusaidia watu wafikie kujitoa kwa Yehova. Kwa sababu tulijitoa ili kutumikia hapa, tumejionea furaha kama hiyo mara mingi.” Leo Alain na Stéphanie wako mu kazi ya muzunguko.

“TULIFANYA JAMBO LENYE TULIPASWA KUFANYA”

Léonce na Gisèle

Gisèle alibatizwa wakati alikuwa anasoma masomo ya kinganga mu inchi ya Italia. Kwa sababu bibi na bwana mapainia wenye walikuwa wanajifunza naye Biblia walikuwa na maisha mepesi, ile ilimufurahisha sana. Alipenda kufanya mengi mu kazi ya Yehova. Kwa hiyo, wakati alikaribia kumaliza masomo akakuwa painia wa kawaida.

Gisèle alipenda kurudia Kameruni ili kufanya mengi zaidi mu kazi ya Yehova. Lakini alikuwa na wasiwasi, anasema hivi: “Ningepoteza haki yangu ya kuishi mu inchi ya Italia, na ningeachana na marafiki na watu wa familia yangu wenye walikuwa Italia.” Hata vile, mu Mwezi wa 5, 2016, Gisèle alihamia mu inchi ya Kameruni. Kisha wakati fulani, Gisèle aliolewa na Léonce, na biro ya tawi ya Kameruni iliwaomba waende watumikie mu muji wa Ayos, kwenye kulikuwa lazima kubwa ya wahubiri.

Maisha ilikuwa namna gani mu muji wa Ayos? Gisèle anasema hivi: “Mara mingi hatukuwa na umeme. Kwa hiyo, mara mingi hatukuweza kutumikisha telefone zetu juu zilikuwa zinakosa moto. Nilijifunza kupikia ku moto wa kuni. Na tulikuwa tunabeba brouette na torshe ili kuenda kushota maji usiku wakati ku mutoni hakukuwa watu wengi.” Nini njo iliwasaidia kuvumilia? Gisèle anasema hivi: “Roho ya Yehova ilitusaidia, tulikuwa tunategemezana, na watu wa familia na marafiki walikuwa wanatutia moyo na kutupatia feza. Ile mambo yote ilitusaidia tuvumilie.”

Gisèle anafurahi kwa sababu alirudia mu inchi yake? Anajibia hivi: “Ndiyo kabisa! Ku mwanzo, tulikuwa na matatizo fulani, na wakati fulani tulijisikia kuwa wenye kuvunjika moyo. Lakini kisha kushinda ile magumu yote, mimi na bwana yangu tuliona kama tulifanya jambo lenye tulipaswa kufanya. Tunamutegemea Yehova, na tunajisikia kuwa tumemukaribia zaidi.” Léonce na Gisèle walisoma Masomo kwa Ajili ya Waeneza-Injili wa Ufalme, na sasa wako mapainia wa pekee wa muda.

Kama vile wavuvi wako tayari kupambana na hali ya nguvu ili kukamata samaki wengi, wale wenye wanarudia mu inchi zao wako tayari kujiima mambo mbalimbali ili kusaidia wale wenye wanapendezwa na ujumbe wa Ufalme. Bila shaka Yehova hatasahau kazi yao na atawabariki kwa sababu ya upendo wenye wameonyesha kwa ajili ya jina lake. (Ne. 5:19; Ebr. 6:10) Kama unaishi mu inchi ingine na mu inchi yenu muko lazima kubwa ya wahubiri, unaweza kurudia mu inchi yenu? Kama unafanya vile Yehova atakubariki.​—Mez. 10:22.