Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 46

Nyie Wenye Mumetoka tu Kuoana​—Mutie kazi ya Yehova pa Nafasi ya Kwanza

Nyie Wenye Mumetoka tu Kuoana​—Mutie kazi ya Yehova pa Nafasi ya Kwanza

“Yehova ni nguvu zangu . . . Moyo wangu unamutegemea yeye.”​—ZB. 28:7.

WIMBO 131 “Kile Chenye Mungu Ameunganisha”

KIFUPI YA HABARI *

1-2. (a) Juu ya nini wale wenye wametoka tu kuoana wanapaswa kumutegemea Yehova? (Zaburi 37:3, 4) (b) Tutazungumuzia nini mu hii habari?

 UKO napanga kuoa ao kuolewa hivi karibuni, ao mumetoka tu kuoana? Kama ni vile, weye na ule mwenye unapenda sana, munatazamia kuwa na furaha sana mu ndoa yenu. Kusema kweli, ndoa iko na magumu yake. Na wale wenye wametoka tu kuoana, wako na maamuzi ya maana ya kukamata. Vile munafanyaka wakati munakuwa na magumu, na maamuzi yenye munakamataka, inaweza kufanya mukuwe na furaha ao hapana mu ndoa yenu. Kama munamutegemea Yehova, mutakamata maamuzi ya muzuri, ndoa yenu itakuwa nguvu na mutakuwa na furaha sana miaka yote yenye mutaishi pamoja. Kama hamufuate mashauri ya Mungu, mutakuwa na magumu mu ndoa yenu; na ile itafanya musikuwe na furaha.​—Soma Zaburi 37:3, 4.

2 Hata kama hii habari inazungumuzia zaidi sana wenye wametoka tu kuoana, inazungumuzia pia magumu yenye wale wote wenye kuoana wanaweza kukutana nayo. Tutazungumuzia mifano ya wanaume na wanamuke waaminifu wa zamani na mambo yenye ile mifano inaweza kutufundisha. Mifano yao itatufundisha mambo fulani yenye tunaweza kutumikisha mu sehemu mbalimbali za maisha yetu, kutia ndani mu ndoa. Tutazungumuzia pia mifano ya watu fulani wa mu siku zetu wenye walishakaoana, na mambo yenye wanaweza kutufundisha.

NI MAGUMU GANI YENYE WALE WENYE WAMETOKA TU KUOANA WANAWEZA KUPATA?

Ni maamuzi gani yenye inaweza kufanya wale wenye wemetoka tu kuoana wasifanye mambo mingi mu kazi ya Yehova? (Ona fungu ya 3-4)

3-4. Ni magumu gani yenye wale wenye wametoka tu kuoana wanaweza kupata?

3 Watu fulani wanaweza kutia moyo wale wenye wametoka tu kuoana wakuwe na maisha sawa ya watu wengi leo. Kwa mufano, wazazi na watu wengine wa familia, wanaweza kuanza kusukuma wenye wemetoka tu kuoana wazale haraka. Ao, inawezekana marafiki na watu fulani wa familia, wenye hawana na nia ya mubaya, wanaanza kuwaambia wauze nyumba ya muzuri na wakuwe na vitu mingi.

4 Kama hawako waangalifu, bibi na bwana wanaweza kukamata maamuzi yenye itafanya waingie mu madeni mingi. Na ile inaweza kufanya wakuwe natumika saa mingi juu wapate namna ya kulipa ile madeni. Kazi ya kimwili inaweza kufanya wasikuwe napata wakati ya kufanya funzo ya kipekee, ibada ya familia na kuhubiri. Juu wapate makuta ya mingi ao juu wasiwafukuze ku kazi, wanaweza kuanza kutumika saa mingi zaidi. Matokeo? Ile inaweza kufanya waanze kukosa mikutano, na kuwazuia kupata furaha yenye inatokana na kupanua utumishi wao kwa Yehova.

5. Mufano wa Klaus na Marisa, unakufundisha nini?

5 Kuko mifano fulani yenye kuonyesha kama kutafuta sana vitu vya kimwili hakuletake furaha. Ona mambo yenye Klaus na Marisa, bibi yake, walijifunza juu ya ile. * Kisha tu kuoana, wote wawili walikuwa wanatumika wakati wote juu wapate vitu na makuta mingi. Ni kweli walivipata, lakini, hawakukuwa na furaha. Klaus anasema: “Tulikuwa na vitu mingi sana lakini, hatukukuwa na miradi ya kiroho. Kusema kweli, maisha yetu ilikuwa tu ya mahangaiko na ya kuchokesha.” Pengine na weye ulishakajionea kama kuwa na vitu mingi vya kimwili haikukuleteaka furaha. Kama ni vile, usivunjike moyo. Kufikiria mifano ya muzuri ya watu wengine, inaweza kukusaidia ufanye mabadiliko fulani. Tuzungumuzie kwanza, mambo yenye bwana wanaweza kujifunza kupitia mufano wa Mufalme Yehoshafati.

KAMA VILE MUFALME YEHOSHAFATI UMUTEGEMEE YEHOVA

6. Kulingana na Mezali 3:5, 6, Yehoshafati alifanya nini wakati maaskari wengi walikuja kupigana naye?

6 Bwana, wakati fulani munaonaka madaraka inawalemea? Kama ni vile, mufano wa Mufalme Yehoshafati itawasaidia sana. Juu alikuwa Mufalme, Yehoshafati alikuwa na daraka ya kuhangaikia usalama wa taifa yote! Alifanya nini juu ya kushugulikia ile daraka yake nzito sana? Alifanya yote yenye aliweza, ili kulinda taifa yote. Alitia nguvu miji ya Yuda, na kukusanya maaskari wenye nguvu, zaidi ya 1 160 000. (2 Ny. 17:12-19) Kisha pale Yehoshafati alipambana na tatizo kubwa sana. Maaskari wengi Waamoni, Wamoabu, na wanaume wa eneo ya milima ya Seiri, walimuogopesha, waliogopesha familia yake, na hata watu wake. (2 Ny. 20:1, 2) Yehoshafati alifanya nini? Alimuomba Yehova amusaidie na amupatie nguvu. Ile ilipatana na shauri ya hekima, yenye kuwa mu Mezali 3:5, 6. (Soma.) Sala ya unyenyekevu yenye Yehoshafati alimutolea Yehova, yenye inapatikana mu 2 Mambo ya Nyakati 20:5-12, inaonyesha namna Yehoshafati alimutegemea kabisa baba yake wa mbinguni mwenye upendo, Yehova. Yehova alijibia namna gani sala ya Yehoshafati?

7. Yehova alijibia namna gani sala ya Yehoshafati?

7 Yehova alisema na Yehoshafati kupitia Mulawi mwenye kuitwa Yahazieli. Yehova alisema hivi: “Musimame mahali penu, musimame bila kutikisika, na muone wokovu wa Yehova kwa ajili yenu.” (2 Ny. 20:13-17) Kwa kawaida, haiko vile njo watu wanapiganaka vita! Lakini, ile maagizo haikutolewa na mwanadamu; ni Yehova njo aliitoa. Juu Yehoshafati alimutegemea sana Mungu, alitii ile maagizo. Wakati walienda ili kukutana na maadui, Yehoshafati aliweka mbele waimbaji wenye hawakukuwa na silaha, hapana maaskari wenye walikuwa na uzoefu sana. Yehova hakuachilia Yehoshafati. Alimusaidia kwa kupiga maadui wake.​—2 Ny. 20:18-23.

Wale wenye wametoka tu kuoana, wanaweza kutia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza kwa kusali na kujifunza Biblia (Ona fungu ya 8, 10)

8. Mufano wa Yehoshafati, unaweza kufundisha nini bwana?

8 Nyie bwana, mufano wa Yehoshafati unaweza kuwafundisha mambo fulani. Muko na daraka ya kuhangaikia familia yenu; kwa hiyo, munapaswa kutumika sana juu mulinde na kutegemeza watu wa familia yenu. Wakati munapata magumu, munaweza kuwaza kama mutaimaliza nyie wenyewe. Lakini ni muzuri mukumbuke kama, haiko muzuri kutegemea nguvu yenu. Jambo ya lazima yenye munaweza kufanya, ni kumuomba Yehova awasaidie. Zaidi ya ile, sali kwa moyo wote pamoja na bibi yako. Juu mupate muongozo wa Yehova, mujifunze Biblia na vichapo vya tengenezo, na mutumikishe mashauri yenye munapata ndani. Wakati munakamata maamuzi yenye kutegemea Biblia, inawezekana wengine wasikubaliane nayo, na wanaweza kusema kama akili yenu haitumike tena muzuri. Wanaweza kusema kama njia muzuri zaidi ya kulinda familia yenu, ni kuwa na makuta na kuuza vitu mingi. Lakini mukumbuke mufano wa Yehoshafati. Alimutegemea Yehova na matendo yake ilionyesha vile, tena alikuwa mushikamanifu. Yehova hakumutupa, na nyie pia hawezi kuwatupa. (Zb. 37:28; Ebr. 13:5) Ni nini ingine yenye bibi na bwana wanapaswa kufanya juu wakuwe na furaha?

KAMA VILE NABII ISAYA NA BIBI YAKE MUTIE KAZI YA YEHOVA PA NAFASI YA KWANZA

9. Tunajua nini juu ya Nabii Isaya na bibi yake?

9 Nabii Isaya na bibi yake, walitia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza mu maisha yao. Isaya alikuwa nabii, na pengine bibi yake alikuwa na migao fulani ya kiunabii, juu mu Biblia anaitwa “ule nabii mwanamuke.” (Isa. 8:1-4) Kwa kweli, Isaya na bibi yake, walitia ibada ya Yehova pa nafasi ya kwanza mu maisha yao. Ni mufano ya muzuri sana kwa bibi na bwana leo!

10. Juu ya nini kujifunza maunabii yenye kuwa mu Biblia kunaweza kusaidia bibi na bwana waazimie kabisa kufanya mambo mingi mu kazi ya Yehova?

10 Leo, bibi na bwana wanaweza kuiga nabii Isaya na bibi yake kwa kufanya yote yenye wanaweza mu kazi ya Yehova. Jambo yenye inaweza kuwasaidia wafikie kumutegemea Yehova zaidi, ni kujifunza pamoja maunabii yenye kuwa mu Biblia na kuona namna haikosake kutimia. * (Tit. 1:2) Wanaweza kufikiri juu ya mambo fulani yenye wanaweza kufanya ili kusaidia maunabii fulani yenye kuwa mu Biblia itimie. Kwa mufano, wanaweza kusaidia kutimiza unabii wa Yesu wa kuhubiri habari njema mu dunia yote mbele ule mwisho ufike. (Mt. 24:14) Kadiri bibi na bwana wanaamini kabisa kama maunabii yenye kuwa mu Biblia iko natimia, ni vile wataazimia kabisa kufanya mambo mingi mu kazi ya Yehova.

KAMA VILE PRISILA NA AKILA MUTIE FAIDA ZA UFALME PA NAFASI YA KWANZA

11. Prisila na Akila waliweza kufanya nini, na juu ya nini?

11 Prisila na Akila bwana yake, ni Wayahudi wenye waliishi mu muji wa Roma. Mufano wao unaweza kufundisha mambo fulani wale wenye wemetoka tu kuoana. Walisikiaka habari njema kuhusu Yesu na wakakuwa Wakristo. Kusema kweli, walizoea maisha yao na waliifurahia. Lakini, maisha yao ilibadilika mu njia yenye hawakutazamia, wakati mutawala Claudio alitoa amri ya kufukuza Wayahudi wote mu Roma. Wazia mabadiliko yenye Akila na Prisila walipaswa kufanya. Walipaswa kutoka mu eneo yenye walizoea, kutafuta nyumba ingine, na kuanza tena kazi ya kushona mahema mu eneo ingine yenye hawazoee. Hata vile, juu walizoea kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza, mu nyumba yao ya mupya yenye walipata Korinto, Akila na Prisila waliweza kusaidiana na Paulo ili kutia nguvu imani ya ndugu wenye walikuwa mu kutaniko ya Korinto. Kisha walienda mu miji ingine, mwenye mulikuwa lazima kubwa ya wahubiri. (Mdo. 18:18-21; Ro. 16:3-5) Ile ilifanya wakuwe na furaha sana!

12. Juu ya nini bibi na bwana wanapaswa kujiwekea miradi ya kiroho?

12 Leo, bibi na bwana wanaweza kuiga Prisila na Akila kwa kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza. Wakati ya muzuri zaidi ya kuzungumuzia miradi yao, ni mbele waoane. Wakati bibi na bwana wanakamata maamuzi pamoja, na wanajikaza kufikia miradi yao ya kiroho, watajionea namna roho ya Yehova itafanya kazi mu maisha yao. (Muh. 4:9, 12) Tufikirie mufano wa Russell na Elizabeth. Russell anasema hivi: “Mbele tuoane, tulizungumuziaka miradi yetu ya kiroho.” Elizabeth anasema hivi: “Tulikuwaka na ile mazungumuzo, juu kama mu maisha yetu munakuwa maamuzi ingine ya kukamata, tuikamate mu njia yenye haitatuzuia kufikia ile miradi yetu ya kiroho.” Hali ya Russell na Elizabeth iliwaruhusu kuenda kutumikia Mikronesia, fasi kwenye kulikuwa lazima kubwa ya wahubiri.

Wale wenye wametoka tu kuoana, wanaweza kutia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza kwa kujiwekea miradi ya kiroho (Ona fungu ya 13)

13. Kulingana na andiko ya Zaburi 28:7, tutapata faida gani kama tunamutegemea Yehova?

13 Sawa vile Russell na Elizabeth, kuko bibi na bwana wengi, wenye walishakaamua kufanya maisha yao ikuwe ya mwepesi, juu wafanye mingi zaidi mu kazi ya kuhubiri na kufundisha. Kama bibi na bwana wanajiwekea miradi ya kiroho, na wanatumika pamoja juu ya kuifikia, matokeo itakuwa ya muzuri. Watajionea namna Yehova anawahagaikia, watamutegemea zaidi na watapata furaha ya kweli.​—Soma Zaburi 28:7.

KAMA VILE MUTUME PETRO NA BIBI YAKE MUTUMAINIE AHADI ZA YEHOVA

14. Ni nini inaonyesha kama Petro na bibi yake walitumainia kabisa ahadi yenye kuwa mu andiko ya Matayo 6:25, 31-34?

14 Mufano wa mutume Petro na bibi yake unaweza pia kufundisha wale wenye kuoana mambo fulani. Kisha miezi sita kufika karibu mwaka moja hivi, tangu aonane na Yesu kwa mara ya kwanza, Petro alipaswa kukamata uamuzi fulani muzito. Alikuwa nafanya kazi ya kuvua samaki juu ya kuhangaikia familia yake. Kwa hiyo, wakati Yesu alimualika akuwe mufuasi wake wa wakati wote, Petro alipaswa kufikiria pia hali ya familia yake. (Lu. 5:1-11) Petro aliamua kumufuata Yesu mu kazi ya kuhubiri. Uamuzi wake ulikuwa muzuri kabisa! Na hatukosee kama tunasema bibi yake alitegemeza ile uamuzi. Biblia inaonyesha kama kisha Yesu kufufuliwa, kuko wakati Petro alisindikizwa na bibi yake mu safari. (1 Ko. 9:5) Bila shaka, bibi yake alikuwa Mukristo mwenye alikuwa mufano muzuri. Na ile ilimupatia Petro uhuru wa kutoa mashauri kwa bibi na bwana Wakristo. (1 Pe. 3:1-7) Kusema kweli, Petro na bibi yake walitumainia kama Yehova atatimiza ahadi yake ya kuwapatia mambo yenye wako nayo lazima, kama wanatia Ufalme wake pa nafasi ya kwanza mu maisha yao.​—Soma Matayo 6:25, 31-34.

15. Habari ya Tiago na Esther inakufundisha nini?

15 Kama kumepita tu miaka fulani tangu muoane, munaweza kufanya nini juu mukuwe na tamaa zaidi ya kufanya mambo mingi mu kazi ya Yehova? Njia moja ya kufanya vile, ni kujifunza kupitia mifano ya bibi na bwana wengine. Kwa mufano, munaweza kusoma habari “Walijitoa kwa Kujipendea.” Zile habari zilisaidia Tiago na Esther, bibi na bwana wa Inchi ya Brazili, wapende sana kutumikia fasi kwenye kuwa lazima kubwa. Tiago anasema hivi : “Wakati tulisoma mambo yenye kuonyesha namna Yehova iko nahangaikia watumishi wake leo, na siye tulipenda kujionea mukono wa Yehova na namna atatuhangaikia.” Ku mwisho, walihamia Paraguay. Ni kule walianza kutumikia tangu 2014 mu eneo ya watu wenye kusema luga ya Kireno (Portugais). Esther anasema hivi: “Andiko yenye tunapendaka sana ni Waefeso 3:20. Mu utumishi wetu kwa Yehova tumejionea mara mingi namna ile maneno iko natimia.” Mu ile barua kwa Waefeso, Paulo anaonyesha kama Yehova iko tayari kutupatia mambo mingi zaidi kupita yote yenye tunaomba. Watu wengi walishajionea utimizo wa ile ahadi mara mingi!

Wale wenye wametoka tu kuoana, wanaweza kutia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza kwa kuomba mashauri kwa bibi na bwana wenye kukomala (Ona fungu ya 16)

16. Wale wenye wametoka tu kuoana, wanaweza kuomba nani mashauri juu wafikie miradi yao?

16 Kuchunguza habari fulani ya watu wenye walimutegemea Yehova, kunaweza kusaidia wale wenye wametoka tu kuoana. Kuko bibi na bwana fulani wenye walishakafanya miaka mingi mu utumishi wa wakati wote. Muwaombe mashauri kama munapenda kufikia miradi yenu. Ile ni njia ingine ya kuonyesha kama munamutumainia Yehova. (Mez. 22:17, 19) Wazee pia, wanaweza kusaidia wale wenye wametoka tu kuoana, wajiwekee miradi ya kiroho na kuifikia.

17. Ni mambo gani ilifikia Klaus na Marisa, na mufano wao unatufundisha nini?

17 Tunaweza kuwa na miradi ya kupanua utumishi wetu mu njia fulani, lakini wakati fulani, Yehova anaweza amua tumutumikie mu njia ingine. Tufikirie mufano wa Klaus na Marisa, wenye tulizungumuzia ku mwanzo wa hii habari. Kisha kufanya miaka tatu mu ndoa, walitoka mu inchi yao, na kuhamia mu eneo ya tawi ya Finlandi ili kusaidia mu kazi ya ujenzi. Lakini, waliambiwa kama hawangefanya zaidi ya miezi sita kule. Ku mwanzo, walivunjika moyo. Lakini kisha ile kutokea, walialikwa ili wajifunze luga ya Kiarabu; na sasa wako na furaha ya kutumikia mu eneo ya luga ya Kiarabu, mu inchi ingine. Wakati Marisa anawaza juu ya ile mambo yote yenye ilitokea, anasema hivi: “Niliogopa kufanya mambo yenye siyafanyaka mu maisha yangu, na iliomba nimutegemee Yehova kabisa. Lakini nilijionea namna Yehova alikuwa anatusaidia kila mara mu njia yenye hatukuwazia. Ile yote, ilifanya nimutegemee Yehova zaidi.” Vile hii mufano inaonyesha, mukuwe hakika kama Yehova ataendelea kuwabariki kama munaendelea kumutumainia kabisa.

18. Wale wenye kuoana, wanapaswa kufanya nini ili waendelee kumutumainia Yehova?

18 Ndoa ni zawadi kutoka kwa Yehova. (Mt. 19:5, 6) Anapenda wale wenye kuoana wafurahie ile zawadi. (Mez. 5:18) Nyie wenye mumetoka tu kuoana, muchunguze miradi yenye muko nayo mu maisha. Muko munafanya yenu yote, ili kuonyesha kama munamushukuru Yehova kwa zawadi zenye amewapatia? Muzungumuze na Yehova katika sala. Muchunguze kanuni zenye kuwa mu Biblia, zenye zinaweza kuwasaidia mu hali yenu. Kisha mufuate mashauri yenye Yehova anawapatia. Mukuwe hakika kama maisha yenu itakuwa muzuri na mutakuwa na furaha mu ndoa yenu, kama munatia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza!

WIMBO 132 Sasa Tunakuwa Mwili Mumoja

^ Maamuzi fulani yenye tunakamata inaweza kuonyesha namna tunatumia wakati na nguvu yenye inatubakilia ili kumutumikia Yehova. Nyie wenye mumetoka tu kuoana, muko na maamuzi fulani ya pekee ya kukamata; na ile maamuzi njo inaweza kuonyesha namna maisha yenu itakuwa. Hii habari itawasaidia kujua namna ya kukamata maamuzi ya muzuri yenye inaweza kufanya mukuwe na furaha mu maisha yenu.

^ Majina fulani imebadilishwa.

^ Kwa mufano, munaweza kufikiria masomo yenye kuwa mu sura ya 6, ya 7, na ya 19 ya kitabu Ibada Safi ya Yehova​—Inarudishwa Tena!