Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Vijana, Muumbaji Wenu Anapenda Mukuwe na Furaha

Vijana, Muumbaji Wenu Anapenda Mukuwe na Furaha

“Anakushibisha kwa vitu vya muzuri maisha yako yote.”​—ZB. 103:5.

NYIMBO: 135, 39

1, 2. Juu ya nini ni jambo la hekima kumusikiliza Muumbaji wako wakati unachagua namna utatumia maisha yako? (Ona picha ku mwanzo wa habari hii.)

KAMA uko kijana, inawezekana unapata mashauri mingi juu ya wakati wako wenye kuja. Walimu, watu wenye kutoa mashauri, ao watu wengine wanaweza kukuambia kama unapaswa kusoma masomo ya juu ao kufanya kazi yenye itakusaidia kupata feza mingi. Lakini Yehova anakupatia mashauri yenye kuwa tofauti na ile. Ni kweli kwamba anapenda utumike kwa bidii kwenye masomo ili ukuwe na uwezo wa kujitimizia mahitaji yako na kujitegemeza wewe mwenyewe. (Kol. 3:23) Lakini anajua pia kama wakati uko kijana, unapaswa kukamata maamuzi ya maana yenye itakuwa na matokeo juu ya wakati wako wenye kuja. Kwa hiyo, anatoa kanuni za kukuongoza na kukusaidia kuishi katika njia yenye itamupendeza katika siku hizi za mwisho.​—Mt. 24:14.

2 Ukumbuke kama Yehova anajua kila kitu. Anajua mambo yenye itatokea wakati wenye kuja, na anajua mwisho wa ulimwengu huu unakaribia kwa kadiri gani. (Isa. 46:10; Mt. 24:3, 36) Pia, Yehova anakujua. Anajua mambo yenye itakuletea furaha na yenye itakufanya ukose furaha. Mashauri ya wanadamu inaweza kuonekana kuwa ya muzuri, lakini kama haitegemee Neno la Mungu, haiko ya hekima kabisa.​—Mez. 19:21.

HEKIMA INATOKA TU KWA YEHOVA

3, 4. Kusikiliza mashauri ya mubaya kuliletea Adamu na Eva na watoto wao matokeo gani?

3 Kuko mashauri ya mubaya tangu zamani. Shetani njo mutu wa kwanza mwenye alitolea wanadamu mashauri ya mubaya. Aliambia Eva kama yeye na Adamu wangekuwa na furaha zaidi ikiwa wangejiamulia wenyewe namna wanapenda kuishi. (Mwa. 3:1-6) Lakini Shetani alitafuta faida zake mwenyewe! Alipenda Adamu na Eva, na watoto wao wenye wangezaa wasimuabudu Yehova, lakini wamuabudu yeye. Hata hivyo, Shetani hakukuwa amefanyia wanadamu jambo lolote. Yehova njo alikuwa amewapatia mambo yote yenye walikuwa nayo. Alipatia Adamu bibi na alipatia Eva bwana na uwezo wa kupendana, aliwapatia bustani ya muzuri ili ikuwe makao yao, na miili yao yenye kukamilika yenye ingeweza kuishi milele.

4 Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, Adamu na Eva walikosa kumutii Mungu. Kwa kufanya vile, walijitenga na Ule mwenye aliwapatia uzima. Matokeo ilikuwa ya mubaya sana. Kama vile maua yenye kukatwa kutoka kwenye mumea, Adamu na Eva walifikia kuzeeka na kufa. Pia watoto wao waliteseka, kutia ndani sisi wote. (Ro. 5:12) Watu wengi leo hawafuate mambo yenye Mungu anasema, na wanafanya tu mambo yenye wanapenda. (Efe. 2:1-3) Hilo linaleta matokeo gani? Biblia inasema kama “hakuna hekima” wakati watu wanamupinga Yehova.​—Mez. 21:30.

5. Yehova alikuwa na uhakika gani juu ya wanadamu, na je, alikuwa na sababu ya kuwa na uhakika huo?

5 Yehova alikuwa hakika kama kutakuwa watu, kutia ndani vijana wengi, wenye wangependa kumujua na kumutumikia. (Zb. 103:17, 18; 110:3) Yehova anawaona vijana hao kuwa wa maana sana! Uko kati yao? Kama ni vile, unafurahia “vitu vya muzuri” kutoka kwa Mungu, na hilo linafanya furaha yako iongezeke mu maisha. (Soma Zaburi 103:5; Mez. 10:22) Tutazungumuzia vitu ine kati ya vitu hivyo. Vitu hivyo ni chakula cha kiroho, marafiki wazuri, miradi ya muzuri, na uhuru wa kweli.

YEHOVA ANAKUPATIA CHAKULA CHA KIROHO

6. Juu ya nini unapaswa kuhangaikia uhitaji wako wa kiroho, na Yehova amekutolea nini ili kukusaidia?

6 Wanyama hawana uhitaji wa kiroho, ni kusema, hawajisikie kama wako na lazima ya kujua Muumbaji wao. Lakini sisi tuko na uhitaji wa kiroho. (Mt. 4:4) Wakati tunamusikiliza Mungu, tunapata ufahamu, hekima, na furaha. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wenye wanatambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mt. 5:3) Mungu anatupatia Biblia na anatumia “mutumwa muaminifu na mwenye busara” ili atutolee vichapo vyenye vinatusaidia kutia nguvu imani yetu. (Mt. 24:45) Tunaita vichapo hivyo chakula cha kiroho kwa sababu vinakomalisha imani yetu na vinatia nguvu urafiki wetu pamoja na Yehova. Tunafurahia chakula cha muzuri cha kiroho cha aina mbalimbali!​—Isa. 65:13, 14.

7. Chakula cha kiroho chenye Mungu anatupatia kitakusaidia namna gani?

7 Chakula cha kiroho kinaweza kukupatia hekima na uwezo wa kufikiri muzuri; sifa hizo zinaweza kukulinda mu njia za mingi. (Soma Mezali 2:10-14.) Kwa mufano, sifa hizo zitakusaidia utambue uongo mbalimbali, kama vile fundisho la uongo lenye kusema kama hakuna Muumbaji ao wazo lenye kuonyesha kama feza na vitu vya kimwili vitakufanya ukuwe mwenye furaha. Sifa hizo zitakusaidia pia kuepuka tamaa na tabia zenye zinaweza kukuumiza. Kwa hiyo, fanya nguvu yako yote ili ukuwe na hekima na uwezo wa kufikiri muzuri. Ukifanya vile, utajionea kama Yehova anakupenda na kama anakutakia mambo ya muzuri.​—Zb. 34:8; Isa. 48:17, 18.

8. Juu ya nini unapaswa kumukaribia Mungu leo, na kufanya vile kutakuletea faida gani wakati wenye kuja?

8 Hivi karibuni, kila sehemu ya ulimwengu wa Shetani itaharibiwa. Yehova tu njo mwenye atakuwa na uwezo wa kutulinda na kututolea mambo yenye tutakuwa nayo lazima; ile mambo inaweza kutia ndani chakula chenye tutakuwa nacho lazima. (Hab. 3:2, 12-19) Kwa hiyo, huu njo wakati wa kumukaribia Mungu na kumutegemea zaidi. (2 Pe. 2:9) Kama unafanya vile, hata jambo gani litokee karibu na wewe, utajisikia kama Daudi, mwenye alisema hivi: “Ninamuweka Yehova mbele yangu kila wakati. Kwa sababu iko kwenye mukono wangu wa kuume, sitatikiswa hata kidogo.”​—Zb. 16:8.

YEHOVA ANAKUPATIA MARAFIKI WAZURI SANA

9. (a) Kulingana na Yohana 6:44, Yehova anafanya nini? (b) Ni jambo gani lenye kuwa la pekee wakati unakutana na Mashahidi wenzako?

9 Wakati unakutana kwa mara ya kwanza na mutu fulani mwenye haiko Shahidi, je, unajua mambo mingi kabisa juu ya mutu huyo? Unaweza kujua jina lake na sura yake, lakini pengine haujue mambo mingi zaidi juu yake. Lakini, haiko vile kabisa wakati unakutana kwa mara ya kwanza na mutu fulani mwenye kuwa Shahidi. Unajua kama anamupenda Yehova. Unajua kama Yehova aliona jambo fulani la muzuri ndani yake na alimualika ili akuwe mu familia ya waabudu wake. (Soma Yohana 6:44.) Hata kama mutu huyo anatoka wapi ao alikomaa namna gani, unajua tayari mambo mingi juu yake, na yeye anajua mambo mingi juu yako!

Yehova anapenda ukuwe na marafiki wa muzuri zaidi na ujiwekee miradi ya muzuri (Picha hii inapatana na fungu la 9-12)

10, 11. Watu wa Yehova wanafanana mu mambo gani, na hilo linakuletea faida gani?

10 Wakati tu unakutana na Shahidi mwenzako, unajua tayari kama munafanana mu mambo mingi ya maana sana. Unajua kuwa, hata kama hamuzungumuze luga moja, ninyi wote munazungumuza “luga safi” ya ile kweli. (Sef. 3:9) Maana yake, ninyi wawili munamuamini Mungu, munafuata kanuni zilezile za mwenendo, na muko na tumaini ileile juu ya wakati wenye kuja. Ile mambo inafanya mutumainiane na kufanya urafiki wenye nguvu wenye utaendelea milele.

11 Kwa hiyo, wakati unamuabudu Yehova, unaweza kabisa kusema kama uko na marafiki wazuri sana. Uko na marafiki mu dunia yote, hata kama haujakutana nao! Unaweza kuwazia watu wengine wenye kuwa na zawadi kama hiyo ya maana, isipokuwa watu wa Yehova?

YEHOVA ANAKUSAIDIA KUJIWEKEA MIRADI YA MUZURI

12. Ni miradi gani ya muzuri yenye unaweza kujiwekea?

12 Soma Muhubiri 11:9–12:1. Kuko miradi fulani yenye uko unajikaza kufikia? Pengine umejiwekea muradi wa kusoma Biblia kila siku ao kutoa maelezo ao migao ya muzuri zaidi ku mikutano. Ao pengine unajikaza kutumia Biblia muzuri zaidi mu kazi ya kuhubiri. Unajisikia namna gani wakati unaona kama uko unafanya maendeleo ao wakati wengine wanakuambia vile? Pengine unafurahi sana, na uko na sababu ya kufurahi! Juu ya nini? Juu uko unafanya mambo yenye Yehova anapenda ufanye, kama vile Yesu alifanya.​—Zb. 40:8; Mez. 27:11.

13. Juu ya nini kumutumikia Mungu ni muzuri zaidi kuliko kukaza akili juu ya miradi ya ulimwengu huu?

13 Wakati unakaza akili juu ya utumishi wako kwa Yehova, unafanya kazi yenye itakuletea furaha na kukupatia kusudi mu maisha. Paulo alitoa shauri hili: “Mukuwe imara, bila kutikisika, sikuzote mukiwa na mambo mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mukijua kwamba kazi yenu haiko ya bure kuhusiana na Bwana.” (1 Ko. 15:58) Lakini wakati watu wanakaza akili juu ya miradi ya ulimwengu huu, kama vile kutafuta feza ao kujulikana sana, hawapate furaha kabisa. Hata kama inaonekana kuwa wanapata matokeo ya muzuri, mara nyingi wanajisikia kuwa hawana furaha. (Lu. 9:25) Mufano wa Mufalme Sulemani unatufundisha jambo hilo.​—Ro. 15:4.

14. Mambo yenye Sulemani alijionea inaweza kukufundisha somo gani?

14 Sulemani, mwenye alikuwa kati ya watu matajiri sana na wenye mamlaka zaidi wenye wamepata kuishi, alifanya uchunguzi fulani. Alijiambia hivi: “Nijaribu raha, na nione nitapata mema gani.” (Muh. 2:1-10) Kwa hiyo, Sulemani alijenga nyumba za hali ya juu, alitengeneza mashamba na bustani zenye kupendeza, na alifanya jambo lolote lenye alipenda. Je, alijisikia kuwa mwenye kutosheka na mwenye furaha? Wakati Sulemani aliwaza juu ya mambo yote yenye alikuwa amefanya, alisema hivi: “Niliona kwamba kila kitu ni bure.” Aliongeza hivi: “Sikuona kitu chochote chenye kuwa cha maana kabisa.” (Muh. 2:11) Mambo yenye Sulemani alijionea inakufundisha somo hilo?

15. Juu ya nini uko na lazima ya imani, na kulingana na Zaburi 32:8, imani itakusaidia namna gani?

15 Watu fulani wanajifunza mambo fulani mu maisha kisha tu kufanya makosa na kupatwa na matokeo ya mubaya ya matendo yao. Yehova hapendi jambo hilo likufikie. Anapenda umusikilize na umutii. Inaomba imani ili kufanya vile, lakini hautahuzunika hata kidogo juu ya maamuzi yenye unakamata mu maisha kwa sababu ya imani yako. Na Yehova hatasahau hata kidogo ‘upendo wenye ulionyesha kwa ajili ya jina lake.’ (Ebr. 6:10) Kwa hiyo, fanya nguvu yako yote ili kufanya imani yako ikuwe yenye nguvu. Ukifanya vile, utakamata maamuzi ya muzuri mu maisha na utajionea kama Baba yako wa mbinguni anakutakia mambo ya muzuri sana.​—Soma Zaburi 32:8.

MUNGU ANAKUPATIA UHURU WA KWELI

16. Juu ya nini tunapaswa kuona uhuru kuwa wa maana na kuutumia mu njia ya hekima?

16 Paulo aliandika hivi: “Mahali kwenye kuko roho ya Yehova, kuko uhuru.” (2 Ko. 3:17) Yehova anapenda uhuru, na alikuumba ili ufurahie pia uhuru. Lakini anapenda utumie uhuru wako mu njia ya hekima yenye itakulinda. Pengine vijana fulani wa miaka yako wanaangalia pornografia, wanafanya uasherati, wanatia maisha yao mu hatari kwa kucheza michezo yenye kuwa hatari, ao wanatumia dawa za kulewesha. Ku mwanzo, ile mambo inaweza kuonekana kuwa yenye kufurahisha ao kuvutia, lakini mara nyingi inaleta matokeo ya mubaya, kama vile magonjwa, kufanya mutu kuwa mutumwa, ao hata kifo. (Gal. 6:7, 8) Vijana wenye kujiingiza mu ile mambo wanaweza kuwaza kama wako na uhuru, lakini hawana uhuru.​—Tit. 3:3.

17, 18. (a) Namna gani kumutii Mungu kunatufanya tukuwe na uhuru kabisa? (b) Juu ya nini tunaweza kusema kama Adamu na Eva walikuwa na uhuru zaidi kuliko wanadamu leo?

17 Lakini, kumutii Yehova kunatuletea faida. Kufanya vile kunatusaidia kuwa na afya ya muzuri na kunatufanya kuwa huru kabisa. (Zb. 19:7-11) Na wakati unatumia uhuru wako mu njia ya hekima, ni kusema, wakati unachagua kutii sheria na kanuni kamilifu za Mungu, unaonyesha Mungu na wazazi wako kama uko mutu mwenye kutumainika. Pengine wazazi wako watakutumainia zaidi na kukupatia uhuru zaidi. Na Yehova anaahidi kama hivi karibuni atapatia watumishi wake wote waaminifu uhuru mukamilifu, wenye Biblia inaita “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”​—Ro. 8:21.

18 Huo njo uhuru wenye Adamu na Eva walikuwa nao. Mu bustani ya Edeni, kulikuwa jambo moja tu lenye Mungu aliwakataza kufanya. Hawakupaswa kula matunda ya muti fulani. (Mwa. 2:9, 17) Unawaza kama Mungu hakutenda kwa haki ao aliwaima uhuru kabisa wakati aliwapatia sheria hiyo? Hapana! Fikiria sheria za mingi zenye wanadamu wameunda na kulazimisha watu wazitii. Lakini Yehova alipatia Adamu na Eva sheria moja tu.

19. Yehova na Yesu wanatufundisha mambo gani yenye itatusaidia tukuwe na uhuru?

19 Yehova anaonyesha hekima sana mu namna anatutendea. Kuliko kutupatia sheria za mingi, anatufundisha kwa uvumilivu kutii sheria ya upendo. Anatufundisha kuishi kulingana na kanuni zake na kuchukia mambo ya mubaya. (Ro. 12:9) Mu Mahubiri ya Mulimani, Yesu, Mwana wake, alitusaidia kuelewa juu ya nini watu wanafanyaka mambo ya mubaya. (Mt. 5:27, 28) Na mu ulimwengu mupya, Yesu akiwa Mufalme wa Ufalme wa Mungu, ataendelea kutufundisha kuona mambo ya muzuri na mambo ya mubaya namna yeye anaiona. (Ebr. 1:9) Pia, Yesu atatufanya tukuwe na akili kamilifu na mwili mukamilifu. Wazia namna hali itakuwa wakati hatutashawishiwa hata kidogo kufanya mambo ya mubaya na hatutateseka kwa sababu ya matokeo ya mubaya ya zambi. Kisha, mwishowe, tutafurahia “uhuru wenye utukufu” wenye Yehova anaahidi.

20. (a) Namna gani Yehova anatumia uhuru wake? (b) Namna gani unaweza kumuiga?

20 Katika ulimwengu mupya, uhuru wetu utaendelea kuwa na mipaka. Namna gani? Sikuzote, tutakuwa na lazima ya kumupenda Mungu na kupenda watu wengine. Wakati tunaongozwa na upendo, tunamuiga Yehova. Hata kama Yehova iko na uhuru wenye hauna mipaka, anachagua kuacha upendo uongoze kila kitu chenye anafanya, na hata namna anatutendea. (1 Yo. 4:7, 8) Kwa hiyo, inapatana na akili kusema kama tunaweza kuwa na uhuru kabisa wakati tu tunamuiga Mungu.

21. (a) Namna gani Daudi alijisikia juu ya Yehova? (b) Tutazungumuzia nini mu habari yenye kufuata?

21 Uko mwenye shukrani juu ya vitu vyote vya muzuri vyenye Yehova amekupatia? Amekupatia chakula cha kiroho, marafiki wazuri, miradi ya muzuri, tumaini la kupata uhuru mukamilifu wakati wenye kuja, na zawadi zingine za mingi za muzuri sana. (Zb. 103:5) Pengine unajisikia kama vile Daudi alijisikia wakati alisema katika sala maneno yenye kupatikana mu Zaburi 16:11. Alisema hivi: “Unanijulisha njia ya uzima. Shangwe nyingi iko mbele yako; furaha iko kwenye mukono wako wa kuume milele.” Mu habari yenye kufuata, tutazungumuzia kweli zingine za maana zenye kuwa mu Zaburi ya 16. Kweli hizo zitakusaidia uone namna unaweza kuwa na maisha ya muzuri zaidi!