Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

‘Yehova Ametutendea kwa Fazili’

‘Yehova Ametutendea kwa Fazili’

MIMI na bibi yangu, Danièle, tulikuwa tu tumeingia mu hoteli wakati mutu mwenye kupokea wageni aliniambia hivi: “Papa, tafazali, unaweza kuita polisi wenye kutumika kwenye mipaka?” Kulikuwa kumepita saa kidogo kisha sisi kufika mu Gabon, inchi moja ya Afrika, kwenye kazi yetu ilikuwa imekatazwa mu miaka ya 1970.

Kwa sababu Danièle alikuwa anatambua mambo haraka, aliniambia kwa sauti ya chini hivi: “Usijisumbue kuita polisi, tayari wako hapa!” Nyuma yetu, motokari ilisimama mbele ya hoteli. Kisha dakika kidogo, maaskari walitufunga. Lakini kwa sababu Danièle alinionya, nilipata wakati wa kupatia ndugu mwingine vikaratasi fulani.

Wakati tulikuwa tunapelekwa kwenye kituo cha polisi, nilifikiria namna nilibarikiwa kuwa na bibi mwenye uhodari na wa kiroho. Hiyo ni mara moja tu kati ya mara nyingi zenye mimi na Danièle tulifanya kazi pamoja. Acha nifasirie ni nini ilifanya tutembelee inchi mbalimbali kwenye kazi yetu ilikuwa imewekewa vizuizi.

KWA UPENDO, YEHOVA ALIFUNGUA MACHO YANGU

Nilizaliwa mu mwaka wa 1930 mu familia yenye ilikuwa na bidii mu dini ya Katoliki, katika muji mudogo wenye kuitwa Croix, kaskazini mwa inchi ya Ufaransa. Familia yetu ilikuwa inaenda ku Misa kila juma, na baba yangu alijiingiza sana mu mambo ya kanisa. Lakini, wakati nilikuwa na miaka karibu 14, tukio fulani ilinifungua macho juu ya unafiki wa kanisa.

Inchi ya Ufaransa ilikuwa mu mikono ya jeshi ya Ujerumani wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Mu mafundisho yake, padri wetu alitutia moyo kwa ukawaida tuunge mukono serikali ya Vichy yenye iliunga mukono Wanazi. Hotuba zake zilituogopesha sana. Kama watu wengine wengi mu inchi ya Ufaransa, tulikuwa tunasikiliza kwa siri habari ku radio BBC, yenye ilikuwa inatangaza habari juu ya majeshi ya Muungano. Kisha padri alibadilisha mara moja musimamo wake na kuanza kuunga mukono upande mwingine na alifanya mipango ili misa ya shukrani ifanyike kwa sababu majeshi ya Muungano ilikuwa inasonga mbele katika Mwezi wa 9, 1944. Unafiki huo ulinivunja moyo. Sikutumainia tena viongozi wa dini.

Muda mufupi kisha vita, baba yangu alikufa. Dada yangu mukubwa alikuwa amekwisha kuolewa na alikuwa anaishi mu inchi ya Ubelgiji (Belgique), kwa hiyo nilipaswa kuhangaikia mama yangu. Nilipata kazi mu kiwanda cha kutengeneza manguo. Mukubwa wangu wa kazi na watoto wake wawili wanaume walikuwa Wakatoliki wenye bidii. Hata kama mu kompanyi yao nilikuwa ninatazamia kama mambo itakuwa muzuri wakati wenye kuja, ningepambana na jaribu bila kukawia.

Mu mwaka wa 1953, dada yangu Simone, mwenye alikuwa tayari Shahidi, alikuja kututembelea. Kwa kutumia Biblia yake, alifunua kwa ufundi mafundisho ya uongo ya Kanisa Katoliki juu ya moto wa mateso, Utatu, na kutokufa kwa nafsi. Kwanza, nilibisha kwa sababu hakukuwa anatumia Biblia ya Katoliki, lakini, bila kukawia nilisadiki kama alikuwa anasema kweli. Kisha wakati fulani, aliniletea magazeti ya zamani ya Munara wa Mulinzi. Nilisoma ile magazeti kwa bidii usiku mu chumba changu cha kulala. Bila kukawia, nilielewa kama nilikuwa nimepata kweli; lakini, niliogopa kama nitapoteza kazi yangu ikiwa ningejiunga na Mashahidi wa Yehova.

Kwa miezi fulani, niliendelea kujifunza Biblia na habari za Munara wa Mulinzi mimi mwenyewe. Mwishowe, niliamua kuenda ku Jumba la Ufalme. Upendo wenye niliona katika kutaniko ulinigusa moyo kabisa. Kisha kujifunza Biblia kwa miezi sita pamoja na ndugu fulani mwenye alikuwa na uzoefu, nilibatizwa mu Mwezi wa 9, 1954. Bila kukawia, nilifurahi wakati mama yangu na dada yangu mudogo walifikia kuwa Mashahidi.

TULIMUTEGEMEA YEHOVA KATIKA UTUMISHI WA WAKATI WOTE

Jambo ya kuhuzunisha ni hili: mama yangu alikufa majuma fulani mbele ya mukusanyiko wa kimataifa wa New York wenye ulifanywa mu mwaka wa 1958, wenye nilipata pendeleo la kuhuzuria. Wakati nilirudia, sikukuwa tena na madaraka ya kuhangaikia mutu yeyote wa familia, kwa hiyo, niliacha kazi yangu ya kimwili na nikakuwa painia. Wakati huo nilianza kuchumbia Danièle Delie, dada mumoja painia mwenye bidii, mwenye nilioa mu Mwezi wa 5, 1959.

Danièle alikuwa ameanza utumishi wa wakati wote mu sehemu za vijiji vya Bretagne, mbali sana na kwao. Alikuwa na lazima ya uhodari ili kuhubiri mu eneo ya Wakatoliki na kusafiri kwa kinga ili kuenda mu maeneo ya vijiji. Kama mimi, alikuwa anaona kuwa ni jambo ya maana kutenda kwa haraka; tulikuwa tunaona kama mwisho ulikuwa karibu sana. (Mt. 25:13) Roho yake ya kujitoa ilitusaidia kuvumilia mu utumishi wa wakati wote.

Siku kidogo kisha kuoana, tulipewa mugao wa kutumikia mu muzunguko. Tulijifunza kuishi maisha mepesi. Kutaniko la kwanza lenye tulitembelea lilikuwa na wahubiri 14, na ndugu hawakukuwa na uwezo wa kutupangisha. Kwa hiyo, tulikuwa tunalala ku matela kwenye jukwaa mu Jumba la Ufalme. Kulala vile haikukuwa jambo yenye kufaa kabisa, lakini ilikuwa muzuri kwa ajili ya mugongo!

Tulitembelea makutaniko kwa kutumia motokari yetu ya kidogo

Hata kama tulikuwa na mambo mingi ya kufanya, Danièle alizoea kazi ya kusafiri. Mara nyingi, aliningojea mu motokari yetu ya kidogo wakati tulifanya mukutano wa wazee wenye haukupangwa, lakini hakunungunika hata siku moja. Tulifanya miaka mbili tu mu kazi ya muzunguko na katika miaka hiyo, tulijifunza kama ni jambo ya maana sana kwa bibi na bwana kuzungumuza kutoka moyoni na kutumika pamoja.​—Muh. 4:9.

TULIPEWA MIGAO YA MUPYA YA UTUMISHI

Mu mwaka wa 1962, tulialikwa kuhuzuria darasa la 37 la Masomo ya Gileadi, katika Brooklyn, New York; mazoezi ilifanya miezi kumi. Kati ya wanafunzi 100, kulikuwa watu 26 wenye kuoana, kwa hiyo, tuliona kama tulipata pendeleo la kuhuzuria pamoja ile masomo. Ninaendelea kukumbuka mambo mingi ya muzuri yenye tulipata kwa kushirikiana na ndugu wenye walikuwa kama nguzo za imani, kama vile Frederick Franz, Ulysses Glass, na Alexander Macmillan.

Tulifurahi sana kusoma Masomo ya Gileadi pamoja!

Wakati wa masomo, tulitiwa moyo tukomalishe uwezo wetu wa kutazama. Siku za posho fulani kisha masomo, mazoezi yetu ilitia ndani kutembelea maeneo fulani mu muji wa New York. Tulijua kama Siku ya Kwanza tulipaswa kujikumbusha kwa kuandika mambo yenye tuliona. Mara nyingi, kila Siku ya Posho tulirudia wenye kuchoka, lakini Mwanabeteli mwenye alituongoza kufanya matembezi, alikuwa anatuuliza maulizo fulani ili kutusaidia kukumbuka mambo makubwa yenye tungepaswa kuandika. Siku moja ya Posho, tulitembea mu muji kipindi chote cha kisha midi. Tulitembelea kituo kimoja cha kuchunguza anga kwenye tulijifunza juu ya meteori na meteoriti. * Kwenye Jumba la Makumbusho la Amerika la Historia ya Asili, tulijifunza juu ya aina mbalimbali za mamba. Wakati tulirudia ku Beteli, mwenye alituongoza alituuliza hivi: “Sasa, kuko tofauti gani kati ya meteori na meteoriti?” Danièle alikuwa mwenye kuchoka na akajibu hivi: “Meteoriti ziko na meno ya murefu!”

Tulifurahia kutembelea ndugu na dada zetu waaminifu mu Afrika

Tulishangaa sana wakati tulipewa mugao wa kutumikia ku tawi ya Ufaransa, kwenye tulitumikia pamoja kwa miaka zaidi ya 53. Mu mwaka wa 1976, niliwekwa kuwa muratibu wa Halmashauri ya Tawi na nilipewa pia mugao wa kutembelea inchi za Afrika na za Asia ya Kati kwenye kazi yetu ya kuhubiri ilikuwa imekatazwa ao kuwekewa vizuizi. Ni hilo lilifanya tutembelee inchi ya Gabon, kwenye tulikutana na jambo lenye kuzungumuziwa ku mwanzo wa habari hii. Kusema kweli, sikuzote sikujisikia kuwa nilistahili kabisa kutimiza migao hiyo yenye sikutazamia. Lakini, Danièle, alinitegemeza sana, na hilo lilinisaidia kushugulikia mugao wowote wenye nilipewa.

Ninatafsiri hotuba ya Ndugu Theodore Jaracz kwenye Mukusanyiko “Haki ya Kimungu” wenye ulifanywa mu muji wa Paris, mwaka wa 1988

TULIVUMILIA JARIBU KALI PAMOJA

Tangu tu mwanzo, tulifurahia maisha ya Beteli. Danièle, mwenye alikuwa amejifunza Kiingereza kwa miezi tano mbele tuende ku Masomo ya Gileadi, alifikia kuwa mutafsiri mwenye ufundi wa vichapo vyetu. Tulipata furaha sana mu kazi yetu ku Beteli, lakini kuwa wenye bidii mu kazi za kutaniko kulituletea furaha zaidi. Ninakumbuka kwa furaha wakati nilikuwa ninapanda usiku sana mu treni ya Paris ya chini ya udongo pamoja na Danièle; tulikuwa wenye kuchoka lakini tulifurahi sana kwa sababu tuliongoza pamoja mafunzo ya Biblia yenye kufanya maendeleo. Jambo la kuhuzunisha ni kuwa, afya ya Danièle ilibadilika bila kutazamia na hilo lilimuzuia asifanye mengi kama vile alipenda.

Mu mwaka wa 1993, wanganga walivumbua kama alikuwa na ugonjwa wa kansere ya maziba. Matunzo ilikuwa ya nguvu sana, ilitia ndani upasuaji na matunzo ya kemikali (chimiothérapie). Miaka kumi na tano kisha pale, alivumbuliwa tena na kansere, mara hiyo ilikuwa kansere ya nguvu sana. Lakini, alipenda sana mugao wake wa kutafsiri, kwa hiyo alikuwa anajikaza kurudilia kazi yake kila wakati kama hali yake inakuwa muzuri.

Hata kama Danièle alikuwa na ugonjwa hatari, hatukufikiria hata siku moja kutoka ku Beteli. Hata hivyo, kuwa mugonjwa kwenye Beteli kuko na magumu yake, zaidi sana ikiwa wengine hawajue uzito wa hali yako. (Mez. 14:13) Hata wakati Danièle alikuwa na miaka karibu 80, hakuonekana kuwa mugonjwa kwa sababu alikuwa mwenye sura ya muzuri na umbo ya muzuri. Hakukuwa anajisikilia huruma juu ya hali yake. Lakini, alikaza akili juu ya kusaidia wengine. Alijua kama kusikiliza wengine kunaweza kuwasaidia sana. (Mez. 17:17) Danièle hakujiita mushauri hata siku moja, lakini alitumia uzoefu wake ili kusaidia dada wengi wasiogope kansere.

Tulipaswa pia kuvumilia magumu ya mupya. Wakati Danièle hakukuwa tena na uwezo wa kutumika wakati wote, alijikaza sana kunitegemeza mu njia nyingi zaidi. Alifanya mambo mingi sana ili kufanya maisha yangu ikuwe mwepesi, na hilo lilinisaidia niendelee kuwa muratibu wa Halmashauri ya Tawi kwa miaka 37. Kwa mufano, alikuwa anatayarisha kila kitu ili tukule chakula cha midi mu chumba chetu na kupumuzika kidogo pamoja kila siku.​—Mez. 18:22.

KUPAMBANA NA MAHANGAIKO YA KILA SIKU

Sikuzote, Danièle alikuwa na mawazo ya muzuri na alipenda kuishi. Kisha akavumbuliwa na kansere kwa mara ya tatu. Tulijisikia kuwa tumeishiwa kabisa. Matunzo ya kutumia kemikali (chimiothérapie) na matunzo ya kutumia miali (radiothérapie) ilimumaliza nguvu kabisa, wakati fulani hakuweza kabisa kutembea. Nilihuzunika sana mu moyo wakati bibi yangu mupendwa, mwenye alikuwa mutafsiri mwenye uzoefu, alianza kuwa na magumu ya kupata maneno ya kusema.

Hata kama tulijisikia kuwa tuliishiwa, tuliendelea kusali; tulikuwa hakika kama Yehova hangetuacha tuteseke kupita vile tungeweza kuvumilia. (1 Ko. 10:13) Sikuzote, tulijikaza sana ili tuendelee kuwa wenye shukrani juu ya musaada wenye Yehova alitupatia kupitia Neno lake, wanganga kwenye Beteli, na kupitia ndugu na dada zetu wa kiroho wenye walitutegemeza kwa upendo.

Mara mingi, tulimuomba Yehova atuongoze ili tujue matunzo yenye tulipaswa kukubali. Wakati fulani, tulibakia bila matunzo yoyote. Munganga mwenye alikuwa amemusaidia Danièle kwa miaka 23 hakuweza kufasiria juu ya nini alikuwa anapoteza ufahamu kisha kila matunzo ya kemikali. Hakuweza kupendekeza matunzo ingine yoyote. Tulijisikia kama tumeachwa peke yetu na tulijiuliza ikiwa mambo itakuwa namna gani. Kisha munganga mwingine wa kansere alikubali kumutunza Danièle. Ni kama vile Yehova alitufanyia njia ya kutokea ili kutusaidia kupambana na mahangaiko yetu.

Tulijifunza kupiganisha mahangaiko kwa kuepuka kuhangaika juu ya kesho. Kama vile Yesu alisema, “kila siku iko na matatizo yake yenye yanaeneana na siku hiyo.” (Mt. 6:34) Kuwa na mawazo ya muzuri na kuwa wenye kuchekesha kulitusaidia pia. Kwa mufano, wakati Danièle alifanya miezi mbili bila matunzo yoyote ya kemikali, aliniambia hivi kwa sura yake ya kicheko: “Unajua, hakuna siku nimejisikia muzuri hivi!” (Mez. 17:22) Hata kama alikuwa anateseka, alikuwa anafurahia kujizoeza kuimba nyimbo za mupya za Ufalme kwa sauti kubwa na yenye nguvu.

Hali yake ya kuwa na mawazo ya muzuri ilinisaidia kuvumilia uzaifu wangu mwenyewe. Kusema kweli, mu miaka 57 yenye tulifanya mu ndoa, alihangaikia mahitaji yangu mbalimbali. Hakupenda hata kunionyesha namna ya kukaanga mayai! Kwa hiyo, wakati alifikia kuwa muzaifu sana, nilipaswa kujifunza namna ya kusafisha masahani, kufua manguo, na kupika chakula cha mwepesi. Tangu wakati huo, nimepasua bilauri fulani, lakini nilifurahia sana kufanya mambo yenye itamupendeza. *

NIKO MWENYE SHUKRANI JUU YA FAZILI ZENYE UPENDO ZA YEHOVA

Wakati ninafikiria maisha yetu, ninaona kama nimejifunza mambo mingi kupitia uzaifu wenye tumekuwa nao kwa sababu ya matatizo ya afya na uzee. Kwanza, kuwa na mambo mingi ya kufanya hakupaswe kutuzuia kumuonyesha upendo bibi ao bwana yetu mupendwa. Tunapaswa kutumia muzuri miaka yenye tungali na nguvu ili kuhangaikia wapendwa wetu. (Muh. 9:9) Pili, hatupaswe kuhangaika sana juu ya mambo ya kidogo-kidogo, kwa sababu hilo linaweza kufanya tusahau baraka nyingi zenye tunapata kila siku.​—Mez. 15:15.

Wakati ninafikiria maisha yetu mu utumishi wa wakati wote, ninajisikia kabisa kuwa Yehova alitubariki sana kupita namna tuliwazia. Ninajisikia kama muandikaji mumoja wa zaburi mwenye alisema hivi: “Yehova amenitendea kwa fazili.”​—Zb. 116:7.

^ fu. 20 Meteori ni kipande cha jiwe ao cha metali chenye kuwaka sana wakati kinaingia mu angahewa ya dunia. Na meteoriti ni kipande kikubwa cha jiwe ao metali chenye kutoka mu anga na kuanguka ku dunia.

^ fu. 32 Dada Danièle Bockaert alikufa wakati habari hii ilikuwa inatayarishwa. Alikuwa na miaka 78.