Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Mushukuru kwa Kila Jambo”

“Mushukuru kwa Kila Jambo”

UNAJIONA kuwa mutu mwenye shukrani? Kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza ulizo hilo. Biblia ilitabiri kama wakati wetu, watu wengi wangekuwa “wenye hawana shukrani.” (2 Ti. 3:2) Inawezekana umekwisha kukutana na watu fulani wenye wanapenda wengine wawafanyie mambo yote, ni kama vile wako na haki ya kupewa kila kitu. Inaonekana kuwa wanawaza kama hawana lazima ya kuwa wenye shukrani juu ya mambo yenye wanapewa. Umeona kama haifurahishake kuwa pamoja na watu wa namna hiyo?

Lakini, watumishi wa Yehova wanaambiwa hivi: “Mushukuru kwa kila jambo.” Tunapaswa ‘kushukuru kwa kila jambo.’ (Kol. 3:15; 1 Te. 5:18) Kwa kweli, kuwa wenye shukrani kunatuletea faida. Kuko sababu mingi zenye kuonyesha jambo hilo.

KUWA WENYE SHUKRANI KUNATUSAIDIA TUJISIKIE MUZURI

Sababu moja kubwa ya kutuchochea tukuwe wenye shukrani ni hii: kuwa wenye shukrani kunafanya tujisikie muzuri. Inawezekana kabisa mutu mwenye kuonyesha shukrani anajisikiaka muzuri, na ule mwenye anatolewa shukrani anajisikiaka pia muzuri. Juu ya nini shukrani inafanya wote wawili wajisikie muzuri? Fikiria mufano huu: Wakati unaona kama wengine wako tayari kukufanyia jambo fulani, hilo linakuonyesha kama wanakuona kuwa unastahili kufanyiwa jambo hilo. Na unaona kama wanakuhangaikia. Wakati unaona vile, hilo linapaswa kufanya ujisikie muzuri. Tunaweza kuwazia kama ilikuwa vile kumuhusu Rutu. Boazi alimuonyesha Rutu ukarimu. Kwa kweli, Rutu alifurahi sana wakati aliona kama mutu fulani alimuhangaikia.​—Rut. 2:10-13.

Ni jambo lenye kufaa zaidi kuwa wenye shukrani kwa Mungu. Kwa kweli, wakati fulani umefikiria zawadi mingi za kiroho na za kimwili zenye ametoa na zenye anaendelea kutoa. (Kum. 8:17, 18; Mdo. 14:17) Usifikiri kidogo tu juu ya wema wa Mungu, lakini utumie wakati fulani ili kufikiri sana juu ya baraka mingi zenye Mungu amekupatia wewe na wapendwa wako. Kufikiri sana juu ya ukarimu wa Muumbaji wako kutafanya umupende zaidi na kutakusaidia ukuwe hakika zaidi kama anakupenda kabisa na anakuona kuwa wa maana sana.​—1 Yo. 4:9.

Kuliko kufikiri tu juu ya ukarimu wake na kuwaza sana juu ya baraka zake; umushukuru Yehova kwa ajili ya wema wake. (Zb. 100:4, 5) Watu fulani wanasema kama “kuonyesha shukrani kunasaidia watu wakuwe na furaha.”

KUONYESHA SHUKRANI KUNAFANYA URAFIKI UKUWE WENYE NGUVU

Sababu ingine ya kukufanya ukuwe mwenye shukrani ni hii: kuonyesha shukrani kunafanya urafiki ukuwe wenye nguvu. Sisi wote tuko na lazima ya kujisikia kuwa wengine wanatupenda. Wakati unamushukuru mutu mwingine kwa moyo wote kwa ajili ya tendo fulani la muzuri, ninyi wawili munakuwa marafiki sana. (Ro. 16:3, 4) Tena, watu wenye shukrani wanaweza kuwa tayari zaidi kusaidia wengine. Wanatambua wakati wengine wanawatendea muzuri, na hilo linawachochea watendee wengine pia muzuri. Kwa kweli, kusaidia wengine kunatuletea furaha. Ni kama vile tu Yesu alisema: “Kuko furaha zaidi katika kutoa kuliko katika kupokea.”​—Mdo. 20:35.

Robert Emmons, kiongozi musaidizi wa uchunguzi fulani juu ya shukrani wenye ulifanywa ku Masomo ya Juu ya Kalifornia, alisema hivi: “Ili tukuwe wenye shukrani, tunapaswa kuelewa kama tuko na lazima ya watu wengine nao wako na lazima yetu. Wakati fulani tunatoa, na wakati fulani tunapokea.” Kwa kweli, ili tuendelee kuishi na kuwa na furaha mu maisha, tuko na lazima ya wengine katika mambo mingi. Kwa mufano, wanaweza kutupatia chakula ao kututunza wakati tunagonjwa. (1 Ko. 12:21) Mutu mwenye shukrani anaonyesha waziwazi kama anapendezwa na mambo yenye wengine wanamufanyia. Kwa hiyo, uko na tabia ya kuonyesha wengine shukrani juu ya mambo yenye wanakufanyia?

KUONYESHA SHUKRANI KUNAFANYA UKUWE NA MAWAZO YA MUZURI JUU YA MAISHA

Sababu ingine yenye kukuchochea ukuwe mwenye shukrani ni hii: kuonyesha shukrani kunakusaidia ukaze akili juu ya mambo ya muzuri kuliko kukaza akili juu ya mambo ya mubaya. Katika njia fulani, akili yako inatumika kama chombo fulani cha kuchuya vitu. Inakuwezesha ukaze akili juu ya mambo fulani na kuzuia mambo ingine isiingie mu akili. Unakuwa na mwelekeo wa kuona zaidi mambo ya muzuri na kuacha kukaza akili sana juu ya magumu yako. Kama uko mwenye shukrani zaidi, utaona zaidi mambo ya muzuri, na kufanya vile kutakusaidia ukuwe mwenye shukrani hata zaidi. Kuwa na roho ya shukrani mu maisha kutakusaidia utende kulingana na maneno hii ya Paulo: “Mufurahi sikuzote katika Bwana.”​—Flp. 4:4.

Utaona kama kuwa mwenye shukrani kunakusaidia usikuwe na mawazo ya mubaya. Haiko mwepesi kuwa mwenye shukrani na wakati uleule ukuwe mwenye wivu, mwenye huzuni, na mwenye kinyongo. Pia, watu wenye shukrani hawafuatilie zaidi vitu vya kimwili. Wanafurahia vitu vyenye wako navyo na hawatafute kuwa na vitu mingi zaidi.​—Flp. 4:12.

FIKIRIA BARAKA ZENYE UMEPATA!

Juu uko Mukristo, unatambua kuwa Shetani anapenda magumu yenye unapata katika siku hizi za mwisho ikufanye ukuwe na huzuni na uvunjike moyo. Atafurahi sana kama unakuwa na mawazo ya mubaya na tabia ya kunungunika-nungunika. Tabia ya namna hiyo inaweza kufanya usipate matokeo ya muzuri katika kazi ya kuhubiri. Kwa kweli, kuko uhusiano sana kati ya kuwa mwenye shukrani na tunda la roho ya Mungu. Kwa mufano, tuko na shangwe wakati tunaona mambo ya muzuri yenye Mungu ametufanyia na tuko na imani kama ahadi zake juu ya wakati wenye kuja zitatimia.​—Gal. 5:22, 23.

Kwa sababu uko mutumishi wa Yehova, inawezekana unakubaliana na mambo yenye imezungumuziwa katika habari hii juu ya shukrani. Lakini, unatambua kama sikuzote haiko mwepesi kuwa mwenye shukrani na kuwa na mawazo ya muzuri. Hata hivyo, usiache jambo hilo likuvunje moyo. Unaweza kuwa mwenye shukrani na kuendelea kuwa na sifa hiyo. Namna gani? Kila siku, tumia wakati fulani ili kufikiri juu ya mambo fulani mu maisha yako yenye unaweza kutolea shukrani. Kama unafanya vile zaidi, utakuwa mwenye shukrani zaidi. Kufanya vile kutakusaidia ukuwe mwenye furaha zaidi kuliko watu wenye wanakaza akili juu ya magumu ya maisha. Fikiria mambo ya muzuri yenye Mungu na watu wengine wanakufanyia yenye inakutia moyo na kukuletea furaha. Unaweza hata kuandika ile mambo katika kitabu fulani. Unaweza kuandika katika kitabu hicho mambo mbili ao tatu yenye inakufanya ukuwe mwenye shukrani kila siku.

Wachunguzi fulani wamevumbua kama wakati tunashukuru wengine kwa ukawaida, jambo hilo linaweza kubadilisha namna ubongo wetu unatumika na kutusaidia tujisikie muzuri zaidi mu maisha yetu. Mutu mwenye shukrani ni mutu mwenye furaha sana. Kwa hiyo, fikiria baraka zenye umepata, furahia mambo ya muzuri yenye inatokea mu maisha yako, na ukuwe mwenye shukrani sikuzote! Kuliko kuona mambo ya muzuri yenye unapata kuwa ya kawaida tu, ‘umushukuru Yehova, kwa maana yeye ni mwema.’ Ndiyo, ‘ushukuru kwa kila jambo.’​—1 Ny. 16:34; 1 Te. 5:18.