Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mapainia George Rollston na Arthur Willis wanasimama ili kujaza maji katika radiatere ya motokari yao. —Eneo la Kaskazini, 1933

VITU VYA MAANA SANA VYA HISTORIA YETU

“Hakuna Barabara ya Mubaya Sana ao ya Murefu Sana”

“Hakuna Barabara ya Mubaya Sana ao ya Murefu Sana”

TAREHE 26 Mwezi wa 3, 1937, wanaume wawili wenye kuchoka sana waliingia polepole na motokari yao yenye kujaa vumbi katika muji wa Sydney, Australia. Mwaka moja ulikuwa umepita tangu wakati waliondoka Sydney, walikuwa wamesafiri zaidi ya kilometre 19300 katika maeneo fulani yenye kuwa na majiwe-majiwe ya Australia. Wanaume hao hawakufanya safari hiyo ili kuvumbua maeneo ya mupya ao kujifurahisha tu. Arthur Willis na Bill Newlands walikuwa kati ya mapainia wenye bidii wenye waliazimia kufikisha habari njema ya Ufalme wa Mungu katika maeneo ya mbali sana ya Australia.

Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1920, hesabu kidogo ya Wanafunzi wa Biblia * katika Australia walikuwa wamehubiri zaidi sana katikati na pembeni-pembeni ya miji yenye kuwa pembeni ya bahari. Hesabu kidogo ya watu wanatawanyika, ni kusema, wanaishi mbali na wengine katika eneo kubwa lenye kuwa katikati ya Australia; eneo hilo lenye kuwa kama jangwa liko na ukubwa wa zaidi ya nusu ya inchi ya Amerika. Lakini ndugu walijua muzuri kama wanafunzi wa Yesu walipaswa kutoa ushahidi juu yake ‘mupaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia,’ hata katika maeneo ya mbali ya Australia. (Matendo 1:8) Hata hivyo, namna gani wangeweza kufanya kazi hiyo kubwa? Kwa sababu walikuwa kabisa na imani kuwa Yehova angebariki kazi yao, waliazimia kuifanya kwa bidii.

MAPAINIA WANAFUNGUA NJIA

Katika mwaka wa 1929, makutaniko ya Queensland na ya Australia ya Mangaribi yalitengeneza hesabu fulani ya magari yenye kuwa na vyombo vya lazima ili kuenda kuhubiri katika maeneo hayo yenye kuwa katikati ya Australia. Motokari hizo zilitumiwa na mapainia wenye nguvu wenye wangeweza kuvumilia hali ngumu na kutengeneza motokari hizo wakati zinaharibika. Mapainia hao walitembelea maeneo mengi yenye yalikuwa hayajahubiriwa hata kidogo.

Mapainia wenye hawangeweza kuwa na motokari walienda katika maeneo hayo ya mbali kwa kutumia kinga. Kwa mufano katika mwaka wa 1932, Bennett Brickell mwenye alikuwa na miaka 23 aliondoka Rockhampton, Queensland, na kufanya safari ya kuhubiri ya miezi tano kupitia sehemu ya mbali ya kaskazini ya jimbo hilo. Kwenye kinga yake alibeba blanketi, manguo, chakula, na vitabu vingi; vitu hivyo vilikuwa na uzito. Wakati magurudumu (pneus) ya kinga yake yaliharibika, aliendelea na safari, na alikuwa hakika kama Yehova angemuongoza. Alisukuma kinga yake kilometre 320 yenye ilikuwa imebakia kwa kupitia katika maeneo kwenye zamani watu walikuwa wamekufa kwa sababu ya kiu ya maji. Kwa miaka ingine 30 yenye ilifuata, Ndugu Brickell alisafiri mamia ya maelfu ya kilometre katika Australia kwa kutumia kinga, pikipiki, ao motokari. Alikuwa wa kwanza kuhubiria wakaaji wa kwanza-kwanza wa Australia (Aborigènes) na alisaidia kuanzisha makutaniko mapya; hilo lilifanya ajulikane sana na kuheshimiwa katika maeneo ya mbali ya Australia.

KUPIGANISHA MAGUMU

Australia iko kati ya inchi zenye kuwa na hesabu kidogo zaidi ya watu katika dunia, na zaidi sana katika maeneo ya mbali kwenye watu wanatawanyika. Kwa hiyo, watu wa Yehova wameonyesha kuwa wameazimia kutafuta watu wenye kuishi katika sehemu za mbali za eneo hilo.

Mapainia Stuart Keltie na William Torrington walionyesha kuwa wameazimia kufanya hivyo. Katika mwaka wa 1933, walivuka Jangwa la Simpson, jangwa kubwa lenye marundo ya muchanga, ili kuhubiri katika muji wa Alice Springs, wenye kuwa katikati kabisa mwa Australia. Wakati motokari yao ndogo iliharibika na walipaswa kuiacha, Ndugu Keltie mwenye alikuwa na muguu wa mbao, aliendelea na safari ya kuhubiri kwa kutumia ngamia! Bidii ya mapainia hao ilikuwa na matokeo ya muzuri wakati walikutana na musimamizi mumoja wa hoteli katika eneo fulani la mbali kwenye treni ilikuwa inasimama. Musimamizi huyo wa hoteli, Charles Bernhardt, alifikia kukubali kweli, akauzisha hoteli yake, na akakuwa painia na kuhubiri yeye mwenyewe kwa miaka 15 katika sehemu za mbali zaidi za Australia zenye kuwa kama jangwa.

Arthur Willis anajitayarisha kuenda katika safari ya kuhubiri katika maeneo ya mbali ya Australia.—Perth, Australia ya Mangaribi, 1936

Kwa kweli, mapainia wa kwanza-kwanza walipaswa kuwa na ujasiri na uvumilivu ili waweze kupambana na magumu mengi yenye walipata. Katika safari yao ya kuhubiri katika maeneo ya mbali ya Australia, Arthur Willis na Bill Newlands, wenye tulitaja kwenye mwanzo wa habari hii, wakati fulani walitumika sana ili kufanya safari ya juma mbili ya kilometre 32 kwa sababu mvua kubwa ilikuwa imegeuza jangwa kuwa bahari ya matope. Wakati fulani walitokwa jasho na kujikaza sana wakati wa joto ili kusukuma motokari yao juu ya marundo makubwa ya muchanga. Walipita katika mabonde yenye majiwe-majiwe na ndani ya mito yenye kuwa na muchanga. Mara kwa mara wakati motokari yao iliharibika, walienda katika muji wenye kuwa karibu kwa muguu ao kwa kutumia kinga, kisha walingojea kwa majuma mengi ili wapate vyombo vya mupya vya kutia kwenye motokari yao. Hawakuvunjika moyo hata kama walipata magumu hayo. Kwa kurudilia maneno yenye yaliandikwa wakati fulani katika gazeti L’Âge d’Or, Arthur Willis alifikia kusema hivi: “Hakuna barabara ya mubaya sana ao ya murefu sana.”

Charles Harris mwenye alifanya kazi ya upainia kwa miaka mingi alieleza kama kuwa katika maeneo ya mbali na kupambana na magumu katika maeneo hayo, kulimusaidia kumukaribia Yehova zaidi. Aliongezea hivi: “Ni muzuri zaidi kujikaza sana kuwa na vitu kidogo katika maisha. Ikiwa Yesu alikuwa tayari kulala inje wakati ilikuwa lazima kufanya hivyo, tunapaswa pia kufurahia kufanya hivyo ikiwa mugawo wetu unatuomba kufanya jambo hilo.” Na mapainia wengi walifanya hivyo. Kwa sababu ya kazi yao yenye bidii, habari njema ilifika katika maeneo yote ya Australia, na kusaidia watu wengi waunge mukono Ufalme wa Mungu.

^ fu. 4 Wanafunzi wa Biblia walianza kutumia jina Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 1931.—Isaya. 43:10.