Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 8

Namna ya Kuendelea Kuwa na Furaha Wakati wa Majaribu

Namna ya Kuendelea Kuwa na Furaha Wakati wa Majaribu

“Muone yote kuwa furaha, ndugu zangu, wakati munapata majaribu mbalimbali.”​—YAK. 1:2.

WIMBO 111 Sababu za Kuwa na Shangwe

KIFUPI CHA HABARI *

1-2. Kulingana na Matayo 5:11, tunapaswa kujisikia namna gani wakati tunajaribiwa?

YESU aliambia wanafunzi wake kama watakuwa na furaha ya kweli. Lakini, aliwaambia pia kama watapata magumu. (Mt. 10:22, 23; Lu. 6:20-23) Tuko na furaha kwa sababu tuko wanafunzi wa Kristo. Lakini, unaweza kujisikia namna gani ikiwa watu wa familia yako wanakupinga, ikiwa serikali inakutesa, ao ikiwa wanafunzi wenzako ao wafanyakazi wenzako wanakuchochea ufanye mambo ya mubaya? Kusema kweli, kufikiria ile mambo kunaweza kutuletea mahangaiko.

2 Watu wengi hawaonake kama mateso inaweza kuletea mutu furaha. Lakini, Neno la Mungu linasema kama mateso inaweza kufanya mutu akuwe na furaha. Kwa mufano, mwanafunzi Yakobo aliandika kama kuliko kuhuzunika sana, tunapaswa kufurahi wakati tuko mu majaribu. (Yak. 1:2, 12) Na Yesu alisema kama tunapaswa kufurahi hata wakati watu wanatutesa. (Soma Matayo 5:11.) Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuwa na furaha hata wakati wa majaribu? Tunaweza kujifunza mambo mingi kwa kuchunguza mawazo fulani yenye Yakobo aliandikia Wakristo wa kwanza-kwanza. Tuzungumuzie kwanza majaribu yenye wale Wakristo walipata.

WAKRISTO WA KARNE YA KWANZA WALIPATA MAJARIBU GANI?

3. Muda mufupi kisha Yakobo kuwa mwanafunzi wa Yesu, kulitokea nini?

3 Muda mufupi kisha Yakobo ndugu ya Yesu kuwa mwanafunzi, Wakristo wa Yerusalemu walianza kuteswa. (Mdo. 1:14; 5:17, 18) Na wakati mwanafunzi Stefano aliuawa, Wakristo wengi walikimbia muji na “walitawanywa kila mahali katika maeneo ya Yudea na Samaria,” na hata kufikia maeneo ya mbali sawa vile Kipro na Antiokia. (Mdo. 7:58–8:1; 11:19) Bila shaka, wale wanafunzi walipata magumu mingi sana. Hata vile, waliendelea kuhubiri kwa bidii kila fasi kwenye walienda, na makutaniko ilianzishwa mu utawala wote wa Roma. (1 Pe. 1:1) Lakini kisha pale, walipata magumu ingine ya nguvu sana.

4. Wakristo wa karne ya kwanza walipata magumu ingine gani?

4 Wakristo wa karne ya kwanza walipata magumu mingi sana. Kwa mufano, mu mwaka wa 50 hivi K.K.Y., Mutawala wa Roma Klaudio, aliamuru Wayahudi watoke katika muji wa Roma. Kwa hiyo, Wakristo Wayahudi walilazimika kuacha nyumba zao na kuhamia fasi ingine. (Mdo. 18:1-3) Mu mwaka wa 61 hivi K.K.Y., mutume Paulo aliandika kama Wakristo wenzake walikuwa wametukanwa mbele ya watu, walikuwa wametiwa mu gereza, na kunyanganywa vitu vyao. (Ebr. 10:32-34) Na kama vile tu watu wengine, Wakristo fulani walikuwa wanateseka kwa sababu ya umaskini na magonjwa.​—Ro. 15:26; Flp. 2:25-27.

5. Tutajibia maulizo gani?

5 Wakati Yakobo aliandika barua yake mbele ya mwaka wa 62 K.K.Y., alikuwa anajua muzuri majaribu yenye ndugu na dada zake walikuwa wanapata. Yehova alimuongoza Yakobo aandikie wale Wakristo ili kuwapatia mashauri yenye ingewasaidia waendelee kuwa na furaha hata kama walikuwa wanapata majaribu. Tuchunguze basi barua ya Yakobo na tujibie hii maulizo: Furaha yenye Yakobo alizungumuzia ni furaha ya aina gani? Nini njo inaweza kufanya Mukristo apoteze furaha yake? Namna gani sifa ya hekima, imani, na uhodari zinaweza kutusaidia tuendelee kuwa na furaha hata kama tuko tunapata majaribu?

NI NINI INAFANYAKA MUKRISTO AKUWE NA FURAHA?

Kama vile moto unaendelea kuwaka ndani ya kirauli ao kioo cha taa, furaha ya kweli yenye Yehova anapatia watu wake inaendelea kuwaka ndani ya moyo wao (Ona fungu la 6)

6. Kulingana na Luka 6:22, 23, juu ya nini Mukristo anaweza kuwa na furaha wakati anapata majaribu?

6 Watu wanaweza kuwaza kama mutu mwenye iko na afya ya muzuri, feza mingi, na mwenye iko na uhusiano wa muzuri na watu wa familia yake njo anaweza kuwa na furaha. Lakini furaha yenye Yakobo alizungumuzia ni sehemu ya tunda la roho ya Mungu na haitegemee hali za mutu. (Gal. 5:22) Jambo lenye linafanyaka Mukristo akuwe na furaha, ni kujua kama iko anamufurahisha Yehova na iko anafuata mufano wa Yesu. (Soma Luka 6:22, 23; Kol. 1:10, 11) Kama moto wenye kuwaka ndani ya taa wenye unalindwa na kirauli ao kioo cha taa, ile aina ya furaha inawaka ndani ya moyo wa Mukristo. Haififie wakati anagonjwa ao wakati iko na feza kidogo sana. Pia, haizimike wakati watu wanamucheka ao wakati watu wa familia yake ao watu wengine wanamupinga. Kuliko kuzimika, inawaka sana. Majaribu yenye tunapata kwa sababu ya imani yetu inaonyesha waziwazi kama tuko wanafunzi wa kweli wa Kristo. (Mt. 10:22; 24:9; Yoh. 15:20) Njo maana, Yakobo aliandika hivi: “Muone yote kuwa furaha, ndugu zangu, wakati munapata majaribu mbalimbali.”​—Yak. 1:2.

Juu ya nini majaribu inafananishwa na moto wenye unatumiwa ili kunoa chombo fulani cha chuma? (Ona fungu la 7) *

7-8. Wakati tunapata majaribu, ile inakuwa na matokeo gani juu ya imani yetu?

7 Yakobo anazungumuzia sababu ingine yenye inafanyaka Wakristo wakuwe tayari kuvumilia hata majaribu ya nguvu sana. Anasema hivi: “Sifa yenye imejaribiwa ya imani yenu inatokeza uvumilivu.” (Yak. 1:3) Majaribu inaweza kufananishwa na moto wenye unatumiwa ili kutengeneza chombo fulani cha chuma. Wakati kile chombo kinawekwa ndani ya moto na kisha kupoleshwa, kinakuwa na nguvu zaidi. Vilevile, wakati tunavumilia majaribu, imani yetu inakuwa nguvu zaidi. Njo maana Yakobo aliandika hivi: “Muache uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili mukuwe kamili na bila kosa katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yak. 1:4) Wakati tunaona namna majaribu inafanya imani yetu ikuwe nguvu zaidi, tunaweza kuvumilia ile majaribu bila kupoteza furaha yetu.

8 Mu barua yake, Yakobo anazungumuzia pia mambo fulani yenye inaweza kutufanya tupoteze furaha yetu. Ni mambo gani, na tunaweza kufanya nini ili kuishinda?

MAMBO YA KUFANYA ILI TUSIPOTEZE FURAHA

9. Juu ya nini tuko na lazima ya hekima?

9 Tatizo: Haujue ufanye nini. Wakati tunapata majaribu, ni muzuri tumuombe Yehova atusaidie tukamate maamuzi yenye itamufurahisha, yenye italetea ndugu na dada faida, na yenye itatusaidia tuendelee kuwa waaminifu. (Yer. 10:23) Tuko na lazima ya hekima ili kujua mambo yenye tunapaswa kusema na kufanya wakati watu wanatupinga. Kama hatujue la kufanya, tunaweza kuvunjika moyo, na bila kukawia tunaweza kupoteza furaha yetu.

10. Yakobo 1:5 inasema tunapaswa kufanya nini juu tupate hekima?

10 Jambo la kufanya: Umuombe Yehova akupatie hekima. Ili kuvumilia majaribu bila kupoteza furaha yetu, tunapaswa kwanza kumuomba Yehova atupatie hekima ili tuweze kukamata maamuzi ya muzuri. (Soma Yakobo 1:5.) Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunaona kama Yehova anakawia kujibia sala yetu? Yakobo alisema kama tunapaswa ‘kuendelea kumuomba’ Mungu. Yehova hachoke kutusikiliza wakati tunaendelea kumuomba hekima yake. Hatatukasirikia. Wakati tunamuomba atupatie hekima ya kutusaidia tuvumilie majaribu, Baba yetu wa mbinguni ‘anatupatia kwa ukarimu’ hekima yake. (Zb. 25:12, 13) Anaona majaribu yetu, anasikia mubaya wakati tunateseka, na anapenda sana kutusaidia. Bila shaka, kujua vile kunafanya tukuwe na furaha! Sasa, namna gani Yehova anatupatia hekima?

11. Ni nini ingine tunapaswa kufanya ili tupate hekima?

11 Yehova anatupatia hekima kupitia Neno lake. (Mez. 2:6) Ili tupate ile hekima, tunapaswa kujifunza Neno la Mungu, na vichapo vyenye kutegemea Biblia. Lakini, zaidi ya kuongeza tu ujuzi, tunapaswa kufanya jambo lingine. Tunapaswa kutumikisha mambo yenye tunajifunza. Yakobo aliandika hivi: “Mukuwe watendaji wa neno, hapana wasikiaji tu.” (Yak. 1:22) Kutumikisha mashauri ya Mungu kunatusaidia tukuwe wenye kufanya amani zaidi, wenye usawaziko zaidi, na wenye rehema zaidi. (Yak. 3:17) Zile sifa zinatusaidia kupambana na majaribu yote bila kupoteza furaha yetu.

12. Juu ya nini ni jambo la maana kujua Biblia muzuri?

12 Neno la Mungu liko kama kioo. Linatusaidia kujua mambo yenye tunapaswa kutengeneza na namna tunaweza kuitengeneza. (Yak. 1:23-25) Kwa mufano, kisha kujifunza Neno la Mungu, tunaweza kuvumbua kama tuko na lazima ya kujifunza kuzuia kasirani yetu. Kwa musaada wa Yehova, tunajifunza namna ya kuwa wapole wakati watu ao mambo fulani inatukasirisha. Kuwa wapole kunatusaidia tupambane muzuri zaidi na mahangaiko. Kunatusaidia tufikiri muzuri zaidi na tukamate maamuzi ya muzuri zaidi. (Yak. 3:13) Kwa kweli, ni jambo la maana kujua Biblia muzuri!

13. Juu ya nini tunapaswa kujifunza mifano ya watu wenye Biblia inazungumuzia?

13 Wakati fulani, tunajifunza mambo yenye tunapaswa kuepuka kisha kufanya makosa. Lakini ile ni kujifunza kisha kuteseka. Njia ya muzuri zaidi ya kupata hekima ni kujifunza kupitia mambo ya muzuri yenye wengine walifanya na pia makosa ya wengine. Njo maana Yakobo anatutia moyo tufikirie mifano ya watu wenye Biblia inazungumuzia kama vile Abrahamu, Rahabu, Yobu, na Eliya. (Yak. 2:21-26; 5:10, 11, 17, 18) Wale watumishi washikamanifu wa Yehova walivumilia majaribu yenye ingefanya wapoteze furaha yao. Mifano yao inaonyesha kama kwa musaada wa Yehova tunaweza pia kuvumilia.

14-15. Juu ya nini tunapaswa kuondoa mashaka?

14 Tatizo: Mashaka. Mara kwa mara, tunaweza kushindwa kuelewa mambo yenye Biblia inasema. Ao Yehova anaweza kukosa kujibia sala zetu namna tulitazamia. Ile inaweza kufanya tukuwe na mashaka. Kama hatufanye jambo fulani ili kuondoa ile mashaka, itaregeza imani yetu na kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. (Yak. 1:7, 8) Na inaweza hata kufanya tupoteze tumaini na tuwaze kama Yehova hatatimiza ahadi zake.

15 Mutume Paulo alifananisha tumaini letu na nanga. (Ebr. 6:19) Nanga inasaidiaka mashua isitikisike-tikisike wakati wa upepo mukali na inaizuiaka isiende kujigonga ku miamba. Lakini, nanga inaweza kusaidia ikiwa tu munyororo wenye unaiunganisha na mashua haukatike. Kama vile kutu inaweza kuregeza munyororo wa nanga, mashaka inaweza kuregeza imani yetu. Wakati mutu mwenye kuwa na mashaka anajaribiwa, anaweza kupoteza imani yake na kuwaza kama Yehova hatatimiza ahadi zake. Kama tunapoteza imani, tunapoteza pia tumaini. Kama vile Yakobo alisema, mutu mwenye kuwa na mashaka “ni kama wimbi la bahari lenye linapelekwa huku na huku.” (Yak. 1:6) Mutu wa vile hawezi kuwa na furaha hata kidogo!

16. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tuko na mashaka?

16 Jambo la kufanya: Ondoa mashaka na utie nguvu imani yako. Tenda bila kukawia. Mu siku za nabii Eliya, watu wa Yehova walianza kuwa na mashaka. Eliya aliwaambia hivi: “Mutaendelea kuyumba-yumba kati ya mawazo mbili tofauti mupaka wakati gani? Kama Yehova ndiye Mungu wa kweli, mumufuate; lakini kama ni Baali, mumufuate!” (1 Fa. 18:21) Leo, sisi pia tunapaswa kutenda haraka. Tunapaswa kufanya utafiti ili kujihakikishia kama Yehova njo Mungu wa kweli, Biblia ni Neno lake, na Mashahidi wa Yehova njo watu wake. (1 Te. 5:21) Kufanya vile kutatusaidia tuondoe mashaka na tutie nguvu imani yetu. Kama tuko na lazima ya musaada ili kuondoa mashaka, tunaweza kuomba wazee watusaidie. Tunapaswa kutenda bila kukawia ili tuendelee kumutumikia Yehova kwa furaha!

17. Ni nini inaweza kutokea ikiwa tunapoteza uhodari?

17 Tatizo: Kuvunjika moyo. Neno la Mungu linasema hivi: “Kama unavunjika moyo siku ya taabu, nguvu zako zitakuwa kidogo.” (Mez. 24:10) Neno la Kiebrania lenye linatafsiriwa ‘kuvunjika moyo’ linaweza kumaanisha “kupoteza uhodari.” Ikiwa unapoteza uhodari, bila kukawia utapoteza pia furaha.

18. Uvumilivu, maana yake nini?

18 Jambo la kufanya: Umuombe Yehova akupatie uhodari ili uvumilie. Tuko na lazima ya uhodari ili tuvumilie majaribu. (Yak. 5:11) Neno lenye Yakobo alitumia lenye linatafsiriwa “uvumilivu” linaleta wazo la mutu mwenye anaendelea kusimama fasi kwenye iko. Tunaweza kufikiria askari mwenye, bila kuogopa, anaendelea kusimama fasi kwenye iko na hakimbie wakati maadui wanamushambulia.

19. Mufano wa Paulo unaweza kutufundisha nini?

19 Mutume Paulo alituwekea mufano muzuri wa uhodari na uvumilivu. Wakati fulani, alijisikia kuwa zaifu. Lakini, aliweza kuvumilia kwa sababu alimuomba Yehova amupatie nguvu yenye alikuwa nayo lazima. (2 Ko. 12:8-10; Flp. 4:13) Sisi pia tunaweza kuwa na nguvu na uhodari kama yeye ikiwa kwa unyenyekevu tunamuomba Yehova atusaidie.​—Yak. 4:10.

UMUKARIBIE MUNGU NA UENDELEE KUWA NA FURAHA

20-21. Tunaweza kuwa hakika na jambo gani?

20 Tunaweza kuwa hakika kama majaribu yenye tunapata haiko malipizi kutoka kwa Yehova. Yakobo anatuhakikishia hivi: “Wakati mutu iko katika jaribu, asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu, wala yeye mwenyewe hamujaribu mutu yeyote.” (Yak. 1:13) Kama tunaamini kabisa ile maneno, tutamukaribia zaidi Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo.​—Yak. 4:8.

21 Yehova “habadilike.” (Yak. 1:17) Kama vile tu alisaidia Wakristo wa karne ya kwanza wakati walipata majaribu, atasaidia pia kila mumoja wetu leo. Umuombe sana akusaidie ukuwe na hekima, imani, na uhodari. Atajibia sala zako. Kama unafanya vile, unaweza kuwa hakika kama atakusaidia uendelee kuwa na furaha wakati unapata majaribu!

WIMBO 128 Kuvumilia Mpaka Mwisho

^ fu. 5 Kitabu cha Yakobo kiko na mashauri mingi yenye inaonyesha mambo yenye tunaweza kufanya wakati wa majaribu. Hii habari itazungumuzia mashauri fulani yenye Yakobo alitoa. Ile mashauri itatusaidia tuendelee kutumikia Yehova kwa furaha hata wakati wa majaribu.

^ fu. 59 MAFASIRIO YA PICHA: Polisi wanakuja kumufunga ndugu kwake. Bibi yake na mutoto wake mwanamuke wanaangalia wakati polisi wanaenda naye. Wakati ule ndugu iko mu gereza, ndugu na dada wa mu kutaniko lao wako wanafanya ibada ya familia pamoja na bibi na mutoto wake. Bibi yake na mutoto wake wanasali kwa Yehova kila mara ili awapatie nguvu ya kuvumilia ile jaribu. Yehova anawapatia amani ya moyo na uhodari. Kwa hiyo, imani yao inakuwa nguvu zaidi, na wanavumilia kwa furaha.