Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kukaribisha Wageni Kunaleta Furaha na Ni Jambo la Maana Sana!

Kukaribisha Wageni Kunaleta Furaha na Ni Jambo la Maana Sana!

‘Mukaribishane bila kunungunika.’​—1 PET. 4:9.

NYIMBO: 100, 87

1. Wakristo wa wakati wa mitume walipambana na magumu gani?

WAKATI fulani kati ya mwaka wa 62 na 64 kisha kuzaliwa kwa Yesu, mutume Petro aliandikia “wakaaji wa muda waliotawanyika huku na huku katika Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia.” (1 Pet. 1:1) Ndugu hao wenye walikuwa katika makutaniko mbalimbali ya Asia Ndogo wenye walitoka katika desturi mbalimbali, walikuwa na lazima ya kutiwa moyo na kupewa muongozo. Walikuwa wanateswa na kutukanwa. Walipambana na majaribu yenye kuwa kama “moto unaowaka.” Na waliishi wakati wa magumu. Petro aliandika hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia.” Kwa kweli, muji wa Yerusalemu ulikuwa karibu kuharibiwa. Ni nini ingesaidia Wakristo kila mahali wavumilie wakati huo wa magumu?​—1 Pet. 4:4, 7, 12.

2, 3. Sababu gani Petro alitia moyo Wakristo wenzake wakaribishe wageni? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

2 Zaidi ya hilo, Petro alitia moyo ndugu zake hivi: ‘Mukaribishane.’ (1 Pet. 4:9) Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “kukaribisha” linamaanisha “kupendezwa na, ao kuonyesha wema kwa wageni.” Hata hivyo, ona kwamba Petro anatia moyo ndugu na dada zake ‘wakaribishane,’ hata kama tayari walikuwa wanajuana na kufanya mambo pamoja. Namna gani kukaribisha wengine kungewasaidia?

3 Kungefanya wakaribiane zaidi. Fikiria mufano wako mwenyewe. Ulifurahi wakati mutu fulani alikualika katika nyumba yake? Uko na mambo ya muzuri yenye unaendelea kukumbuka juu ya tukio hilo? Wakati ulialika ndugu ao dada fulani wa kutaniko lenu, urafiki wenu ulikomaa tena zaidi? Wakati tunakaribisha ndugu na dada zetu, tunafikia kuwajua muzuri zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Katika siku za Petro, kadiri hali ziliendelea kuharibika, Wakristo walipaswa kukaribiana zaidi. Mambo yako hivyo pia kwa Wakristo katika “siku [hizi] za mwisho.”​—2 Tim. 3:1.

4. Tutazungumuzia maulizo gani katika habari hii?

4 Tuko na nafasi gani za ‘kukaribishana’? Namna gani tunaweza kumaliza mambo yenye kutuzuia kukaribisha wageni? Ni nini inaweza kutusaidia tukuwe wageni wazuri?

NAFASI ZA KUKARIBISHA WAGENI

5. Namna gani tunaweza kukaribisha wageni kwenye mikutano yetu ya Kikristo?

5 Kwenye mikutano: Tunakaribisha watu wote wenye kuhuzuria mikutano yetu ya Kikristo kama wageni wenzetu kwenye chakula cha kiroho. Tunaalikwa na Yehova na tengenezo lake. (Rom. 15:7) Wakati wapya wanahuzuria mikutano, wao pia wanakuwa wageni wa Yehova. Unaweza kuwa tayari kukaribisha watu hao wapya, hata iwe wamevaa na kujipamba namna gani. (Yak. 2:1-4) Je, ikiwa unaona mugeni iko yeye mwenyewe, unaweza kumualika akae pamoja na wewe? Anaweza kufurahi ikiwa unamusaidia kufuata mikutano na pengine kutafuta maandiko yenye kusomwa. Hiyo inaweza kuwa njia ya muzuri ya ‘kufuata mwendo wa ukaribishaji-wageni.’​—Rom. 12:13.

6. Ni nani wenye tunapaswa kukaribisha kwanza?

6 Kwa ajili ya chakula: Zamani, mara nyingi kukaribisha wageni kulitia ndani mutu kualika mugeni nyumbani kwake na kumupatia chakula. (Mwa. 18:1-8; Amu. 13:15; Lu. 24:28-30) Kualika mutu kwa ajili ya chakula ilikuwa njia ya kuonyesha urafiki na amani. Ni nani wenye tunapaswa kualika kwanza? Wale wenye tunazoea kuonana nao katika maisha yetu, ni kusema, ndugu na dada katika kutaniko letu. Wakati magumu yanatokea, kwa kweli, tunapaswa kutegemezana. Tunapenda kuwa na urafiki mushikamanifu na amani pamoja nao wote. Jambo la kupendeza ni kwamba katika mwaka wa 2011, Baraza Lenye Kuongoza lilibadilisha programu ya Funzo la Munara wa Mulinzi la familia ya Beteli ya Amerika kutoka saa 12:45 ya mangaribi na kuwa 12:15 ya mangaribi. Sababu gani? Tangazo lilisema kama pengine hilo litasaidia Wanabeteli kukaribishana wakati mukutano unamalizika mbele ya wakati. Biro zingine za tawi zilifuata mufano huo. Mupango huo umesaidia ndugu wa familia ya Beteli wakaribiane zaidi.

7, 8. Namna gani tunaweza kukaribisha wajumbe wa tengenezo la Yehova?

7 Tunapata nafasi za kukaribisha wageni wakati tunatembelewa na wasemaji wageni wenye kutoka katika makutaniko mengine, waangalizi wa muzunguko, na wakati fulani wajumbe kutoka kwenye biro ya tawi ya eneo letu. Hilo linatutolea nafasi ya kukaribisha ndugu hao wenye kututembelea. (Soma 3 Yohana 5-8.) Njia moja ya muzuri ya kukaribisha wageni, ni kuwatolea chakula. Unaweza kuwakaribisha?

8 Dada mumoja katika Amerika, anakumbuka hivi: “Kwa miaka mingi, mimi na bwana yangu tumepata nafasi ya kukaribisha katika nyumba yetu wasemaji wengi wageni na bibi zao. Kila wakati hilo limekuwa lenye kufurahisha, na jambo la maana zaidi, kujenga kiroho. Hatujute hata kidogo juu ya jambo hilo.”

9, 10. (a) Ni nani wenye wanaweza kuwa wageni wa kubakia kwa muda fulani? (b) Wale wenye hawana nyumba kubwa wanaweza kusaidia pia? Toa mufano.

9 Wageni wenye wanabakia kwa muda fulani: Zamani, mara nyingi kukaribisha wageni kulitia ndani kupatia wageni fulani makao. (Ayu. 31:32; Flm. 22) Katika siku zetu pia, wageni fulani wako na lazima ya makao. Mara nyingi waangalizi wa muzunguko wako na lazima ya makao wakati wanatembelea makutaniko. Wanafunzi wa masomo mbalimbali ya kiteokrasi na ndugu na dada wenye kujitolea katika kazi ya ujenzi wanaweza kuwa na lazima ya mahali pa kubakia. Misiba ya asili inaweza kufanya familia fulani zikose makao na kwa hiyo wanakuwa na lazima ya mahali pa kubakia mupaka nyumba zao zitengenezwe tena. Hatupaswe kufikiri kama wale wenye kuwa na nyumba za muzuri ndio tu wanaweza kusaidia; pengine wamefanya hivyo mara nyingi. Unaweza kupatia wageni nafasi ya kubakia hata kama nyumba yako ni ya kidogo?

10 Ndugu mumoja katika Korea ya Kusini anafurahi wakati anakumbuka namna alitolea wanafunzi wa masomo mbalimbali ya kiteokrasi nafasi ya kubakia. Anaandika hivi: “Mwanzoni nilisita kwa sababu tulikuwa wapya katika ndoa na tulikuwa tunaishi katika nyumba ndogo. Lakini kubakia pamoja na wanafunzi kulituletea furaha nyingi kabisa. Kwa sababu tulikuwa wapya katika ndoa, tulipata nafasi ya kuona namna gani bibi na bwana wanaweza kuwa na furaha zaidi wakati wanamutumikia Yehova na kufuatia miradi ya kiroho pamoja.”

11. Sababu gani wapya katika kutaniko lenu wanastahili kukaribishwa?

11 Wapya katika kutaniko: Ndugu na dada na familia fulani wanaweza kuhamia katika eneo lenu. Wamoja wanaweza kuja kutumikia mahali kwenye kuwa lazima kubwa ya wahubiri. Mapainia wanaweza kutumwa ili kusaidia katika kutaniko lenu. Hayo ni mabadiliko makubwa kwao. Wanapaswa kuzoea eneo la mupya, kutaniko la mupya, na pengine luga ya mupya ao desturi za mupya. Kuwaalika ili kula chakula pamoja nao ao kutembelea nafasi fulani pamoja nao, kutawasaidia wakuwe na marafiki wapya na wazoee hali zao za mupya.

12. Sababu gani haiko lazima kuwa na mambo mengi ili kukaribisha wageni? Toa mufano.

12 Haiko lazima utayarishe mambo mengi ili kukaribisha wageni. (Soma Luka 10:41, 42.) Wakati anakumbuka siku za kwanza-kwanza za kazi yake ya umisionere, ndugu mumoja anasema hivi: “Tulikuwa vijana, hatukukuwa na uzoefu, na tulikumbuka sana nyumbani kwetu. Mangaribi moja bibi yangu alikuwa anakumbuka sana nyumbani kwetu na nilikuwa ninajikaza kumusaidia lakini sikuweza. Kisha, karibu saa 1:30 ya mangaribi, mutu fulani aligonga kwenye mulango wetu. Alikuwa mwanafunzi mumoja wa Biblia mwanamuke na alituletea machungwa (oranges) tatu. Alikuja kukaribisha wamisionere wapya. Tulimukaribisha ndani na tukamupatia maji ya kunywa. Kisha tukafanya chai na shokola ya moto. Tulikuwa hatujajua Kiswahili, naye hakukuwa anajua Kiingereza. Lakini, tukio hilo lilitusaidia kuanza kufanya urafiki na ndugu na dada wa eneo na hilo lilituletea furaha.”

KUMALIZA MAMBO YENYE KUTUZUIA KUKARIBISHA WAGENI

13. Tunaweza kupata faida gani wakati tunakaribisha wageni?

13 Umekwisha kujizuia kukaribisha wageni? Kama ni ndiyo, pengine ulipoteza nafasi ya kufurahia pamoja na marafiki na nafasi ya kufanya urafiki wenye kuendelea. Kukaribisha wageni ni kati ya njia za muzuri zaidi za kupiganisha hali ya mutu kujisikia kuwa peke yake. Lakini unaweza kujiuliza hivi: ‘Sababu gani mutu anaweza kujizuia kukaribisha wageni?’ Kunaweza kuwa sababu nyingi.

14. Tunaweza kufanya nini ikiwa hatuna wakati ao nguvu ya kutosha ili kukubali mualiko ao kuonyesha ukaribishaji wageni?

14 Wakati na nguvu: Watumishi wa Yehova wako na mambo mengi ya kufanya na mara nyingi wako na madaraka mengi. Wamoja wanaweza kuwaza tu kama hawana wakati na nguvu ya kukaribisha wageni. Ikiwa uko katika hali kama hiyo, inaweza kuwa muzuri uchunguze programu ya mambo yenye unafanya sasa. Unaweza kufanya mabadiliko fulani ili ukuwe na wakati na nguvu ya kukaribisha wageni ao kukubali wakati unaalikwa? Maandiko yanatia moyo Wakristo wakaribishane. (Ebr. 13:2) Haiko mubaya kupanga wakati wa kufanya hivyo; hilo ndilo jambo la muzuri la kufanya. Kwa kweli, unaweza kupunguza wakati wenye unatumia ili kufanya mambo yenye hayako ya lazima.

15. Sababu gani watu fulani wanaweza kuwaza kama hawawezi kukaribisha wageni?

15 Namna wewe mwenyewe unajiona: Umekwisha kupenda kukaribisha wageni lakini ukajisikia kama hautaweza? Watu fulani ni wenye haya na wanaogopa kama hawataweza kuzungumuza ao wageni hawatafurahia mazungumuzo. Wengine hawana feza za kutosha na wanaona kama hawawezi hata kidogo kutoa mambo yenye wengine katika kutaniko wanaweza kutoa. Kumbuka kama haiko lazima nyumba ikuwe na vitu vya hali ya juu. Lakini wageni wako watafurahi ikiwa nyumba yako inapangwa muzuri, iko safi, na uko tayari kufanya urafiki.

16, 17. Unaweza kufanya nini ikiwa unaogopa kukaribisha wageni?

16 Ikiwa unaogopa kupokea wageni, haiko wewe peke yako. Muzee mumoja katika Uingereza, anasema hivi: “Mutu anaweza kuwa na wasiwasi kwa kadiri fulani wakati anajitayarisha kupokea wageni. Lakini, kama mambo mengine yote yenye kuhusu utumishi wetu kwa Yehova, faida na kutosheka vyenye tunapata, vinashinda woga wowote wenye tunaweza kuwa nao. Nimefurahia kukaa tu pamoja na wageni na kuzungumuza nao na kunywa kahawa pamoja nao.” Ukumbuke kama kupendezwa na wageni kunasaidia sikuzote. (Flp. 2:4) Karibu kila mutu anapenda kuzungumuzia mambo yenye amekutana nayo katika maisha. Wakati tunakutana na wengine unaweza kuwa tu ndio wakati wenye wanaweza kutuuliza mambo yenye tumekutana nayo katika maisha. Muzee mwingine aliandika hivi: “Kualika nyumbani ndugu na dada wa kutaniko letu kunanisaidia kuwaelewa muzuri zaidi na kunanitolea nafasi ya kuwajua muzuri, zaidi sana namna walijua kweli.” Kupendezwa na wengine kunaweza kufanya kila mutu afurahi.

17 Dada mumoja painia mwenye alitolea wanafunzi wa masomo mbalimbali ya kiteokrasi nafasi ya kubakia, anasema hivi: “Mwanzoni nilikuwa na wasiwasi kwa sababu nyumba yangu ni ya hali ya chini na iko na vitu vyenye vilikuwa vimekwisha kutumiwa. Bibi ya mwalimu mumoja wa masomo hayo alinisaidia nisihangaikie mambo hayo. Alisema kama wakati yeye na bwana yake wanafanya kazi ya muzunguko, majuma ya muzuri zaidi ni majuma yenye wanakaa pamoja na watu wenye hawana vitu vingi vya kimwili lakini wanakaza akili yao kama wao juu ya kumutumikia Yehova na kuishi maisha mepesi. Hilo lilinikumbusha mambo yenye mama yangu alizoea kutuambia wakati tulikuwa tungali watoto. Alikuwa anatuambia hivi: ‘Afazali chakula cha mboga za majani mahali penye upendo.’” (Met. 15:17) Acha basi upendo uchochee sifa yako ya kukaribisha wageni, na usikuwe na wasiwasi.

18, 19. Namna gani kukaribisha wageni kunaweza kutusaidia kumaliza mawazo ya mubaya juu ya wengine?

18 Namna unaona wengine: Je, kuko mutu fulani mwenye haufurahiake katika kutaniko lenu? Mwanzoni unaweza kuwa na mawazo yenye hayafae juu ya mutu huyo na yanaweza kuendelea kama haufanye jambo fulani ili kuyabadilisha. Tofauti kati ya utu zinaweza kuzuia tamaa yako ya muzuri ya kukaribisha wageni. Ao pengine mutu fulani alikukosea zamani, na unaona kama ni vigumu kusahau.

19 Ili tukuwe na uhusiano wa muzuri na wengine, hata na maadui wetu, Biblia inatuomba tukaribishe wageni. (Soma Methali 25:21, 22.) Ikiwa unaalika mutu katika nyumba yako, hilo linaweza kukusaidia kumaliza mawazo ya mubaya juu yake. Linaweza kutusaidia kuona sifa za muzuri za mugeni wetu, sifa zenye Yehova aliona wakati alimuvuta katika kweli. (Yoh. 6:44) Ikiwa tunamutolea kwa upendo mualiko wenye hakutazamia, huo unaweza kuwa mwanzo wa urafiki muzuri. Namna gani unaweza kuwa hakika kwamba upendo ndio unakuchochea kabisa? Njia moja ni kufuata shauri lenye kutia moyo lenye kupatikana kwenye Wafilipi 2:3 lenye kusema hivi: ‘Kwa unyenyekevu wa akili muwaone wengine kuwa ni bora [wazuri zaidi] kuliko ninyi.’ Tutafute njia zenye kuonyesha kama ndugu ao dada zetu ni bora kuliko sisi pengine kupitia imani, uvumilivu, ujasiri wao, ao sifa zingine za Kikristo. Hilo litafanya tuwapende zaidi na kutuchochea tuwakaribishe.

NAMNA YA KUWA MUGENI MUZURI

Mara nyingi wale wenye kualika wageni wanajitayarisha muzuri ili kuwapokea (Picha hii inapatana na fungu la 20)

20. Sababu gani na namna gani tunapaswa kuheshimia mualiko wenye tumekubali?

20 Muandikaji wa zaburi Daudi aliuliza hivi: ‘Ee Yehova, ni nani atakayekuwa mugeni katika hema lako?’ (Zab. 15:1) Alijibia ulizo hilo kwa kuzungumuzia sifa za kiroho zenye Mungu anapenda wageni wake waonyeshe. Sifa moja ni kutimiza maneno yetu. Alisema hivi: ‘Ameapa juu ya jambo lililo mbaya kwake, na bado yeye habadilike.’ (Zab. 15:4) Ikiwa tunakubali mualiko tusikose kufika bila sababu ya maana. Pengine mutu mwenye alitualika alifanya matayarisho, na bidii yake yote inaweza kuonekana kuwa ya bure ikiwa tunakosa kufika bila sababu. (Mt. 5:37) Wamoja wamekosa kufika kwenye mualiko wa kwanza kusudi wakubali mualiko mwengine wenye kuonekana kuwa muzuri zaidi. Je, kufanya hivyo ni kuonyesha upendo na heshima? Hapana. Lakini, tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa vitu vyovyote vyenye mutu mwenye alitualika anatupatia. (Lu. 10:7) Na ikiwa hali fulani zenye hatuwezi kuepuka zitafanya tukose kuenda kwa mutu mwenye alitualika, tunapaswa kumujulisha bila kukawia, hilo linaonyesha upendo na heshima.

21. Namna gani kuheshimia desturi za eneo kunaweza kutusaidia kuwa wageni wazuri?

21 Ni jambo la lazima pia tuheshimie desturi za eneo. Katika desturi fulani watu wanakaribisha wageni wenye hawakutazamiwa; lakini katika desturi zingine ni muzuri kufanya mipango mbele ya wakati. Katika maeneo fulani, mutu mwenye kukaribisha wageni anahangaikia sana wageni kuliko familia yake; mahali pengine wote wanachangia vitu pamoja. Katika maeneo fulani, wageni wanaleta kitu fulani cha kuchangia; katika maeneo mengine, watu wenye kukaribisha wageni wanafurahi wakati wageni hawalete kitu chochote. Na katika desturi fulani, inaomba mutu akatae kwa upole mualiko wa kwanza ao wa pili; lakini katika maeneo mengine haiko muzuri kukataa mualiko. Basi, tujikaze sana kufurahisha mutu mwenye alitualika.

22. Sababu gani ni jambo la maana sana ‘tukaribishane’?

22 Kuliko wakati mwingine wowote, “mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Pet. 4:7) Tunapambana na majaribu makubwa zaidi yenye hayajatokea hata kidogo katika ulimwengu. Kadiri mikazo inaendelea kuongezeka, tutakuwa na lazima ya kukomalisha upendo kati ya ndugu na dada zetu. Kuliko wakati mwingine wowote, shauri la Petro linafaa kwa Wakristo. Alisema hivi: ‘Mukaribishane,’ sifa yenye kupendeza na ya lazima yenye haitakuwa na mwisho.​—1 Pet. 4:9.