Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sikiliza Nizamu ili Ukuwe na Hekima

Sikiliza Nizamu ili Ukuwe na Hekima

‘Wana [wangu], . . . Musikilize nizamu mupate kuwa na hekima.’​—MET. 8:32, 33.

NYIMBO: 56, 89

1. Namna gani tunapata hekima, na inatuletea faida gani?

YEHOVA ni chanzo cha hekima, na anapatia wengine kwa ukarimu hekima yake. Andiko la Yakobo 1:5 linasema hivi: ‘Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumuomba Mungu, kwa maana yeye anawapatia wote kwa ukarimu na bila kushutumu.’ Njia moja yenye kutusaidia kupata hekima kutoka kwa Mungu ni kukubali nizamu yake. Na nizamu hiyo inaweza kutusaidia kuepuka kufanya mambo ya mubaya na kutusaidia tubakie karibu na Yehova. (Met. 2:10-12) Kwa hiyo, ‘tunajitunza [wenyewe] katika upendo wa Mungu . . . kwa kutazamia uzima wa milele.’​—Yuda 21.

2. Namna gani tunaweza kujifunza kupenda nizamu ya Mungu?

2 Hata hivyo, kwa sababu hatukamilike, namna tulikomaa, na mambo mengine yanaweza kufanya ikuwe vigumu kwetu kukubali nizamu ao kuwa na mawazo ya muzuri juu ya nizamu. Tunapendezwa na nizamu wakati tunajionea faida zake, zenye kutuhakikishia kama Mungu anatupenda. Andiko la Methali 3:11, 12 linasema hivi: ‘Mwana wangu, usikatae nizamu ya Yehova, . . . kwa sababu yeye ambaye Yehova anamupenda anamukaripia.’ Kwa hiyo, tuendelee basi kukumbuka kama Yehova anapenda tukuwe na maisha ya muzuri. (Soma Waebrania 12:5-11.) Kwa sababu Mungu anatujua muzuri sana, sikuzote anajua nizamu yenye kutufaa na yenye tuko nayo lazima. Tuzungumuzie basi mambo ine juu ya nizamu: (1) kujitia nizamu, (2) nizamu yenye wazazi wanatoa, (3) nizamu katika kutaniko la Kikristo, na (4) jambo la mubaya zaidi kuliko maumivu ya muda yenye mutu anapata kwa sababu ya kupewa nizamu.

KUJITIA NIZAMU KUNAONYESHA HEKIMA

3. Namna gani mutoto anaweza kukomalisha sifa ya kujitia nizamu? Toa mufano.

3 Kujitia nizamu kunatia ndani kujizuia ili kufanya mabadiliko katika tabia yetu na mawazo yetu. Hatuzaliwe na sifa ya kujitia nizamu, lakini tunajifunza kufanya hivyo. Kwa mufano: Wakati mutoto anaanza kujifunza kutembeza kinga, mara nyingi muzazi anabana kinga ili mutoto asianguke. Lakini, wakati mutoto anajua kidogo namna ya kutembeza kinga, muzazi anamuacha yeye mwenyewe kwa wakati fulani. Anamuacha kabisa wakati anajua kutembeza kinga muzuri. Vilevile, wakati wazazi wanazoeza watoto kwa uvumilivu na mara kwa mara ‘katika nizamu na muongozo wa akilini wa Yehova,’ wanasaidia pia watoto wao wakomalishe sifa ya kujitia nizamu na wakuwe na hekima.​—Efe. 6:4.

4, 5. (a) Sababu gani sifa ya kujitia nizamu ni sehemu ya maana ya ‘utu mupya’? (b) Sababu gani hatupaswe kuvunjika moyo hata kama ‘tunaanguka mara saba’?

4 Kanuni hizo zinatumika pia kwa wale wenye wamefikia kumujua Yehova wakati wamekwisha kukomaa. Kwa kweli, pengine tayari wamejitia nizamu kwa kadiri fulani. Hata hivyo, katika maana ya kiroho, mwanafunzi mupya angali mutoto kiroho. Lakini pole kwa pole anaweza kukomaa kiroho wakati anajifunza kuvaa ‘utu mupya’ wenye kufanana na wa Kristo. (Efe. 4:23, 24) Kujitia nizamu ni jambo la maana sana lenye litamusaidia kukomaa kiroho. Kwa hiyo, tunajifunza ‘kukataa kabisa kutomuogopa Mungu na tamaa za ulimwengu na kuishi kwa utimamu wa akili [akili nzuri] na uadilifu na ujitoaji-kimungu [kushikamana na Mungu] katikati ya mufumo wa mambo wa sasa.’​—Tito 2:12.

5 Lakini, sisi wote ni watenda zambi. (Mhu. 7:20) Hata hivyo, ikiwa tunafanya makosa, hilo halionyeshe kama tunashindwa kabisa kujitia nizamu ao hatujitie nizamu hata kidogo. Andiko la Methali 24:16 linasema hivi: ‘Muadilifu [anaweza] kuanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.’ Ni nini itamusaidia kusimama tena? Haiko nguvu zake wenyewe, lakini roho ya Mungu ndiyo inaweza kumusaidia. (Soma Wafilipi 4:13.) Sifa za tunda la roho hiyo zinatia ndani kujizuia, sifa yenye kupatana sana na kujitia nizamu.

6. Namna gani tunaweza kuwa wanafunzi wazuri zaidi wa Neno la Mungu? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

6 Pia jambo la maana la kutusaidia tukomalishe sifa ya kujitia nizamu ni kusali kwa moyo wote, kujifunza Biblia, na kutafakari. Lakini utafanya nini ikiwa unaona kuwa ni vigumu kujifunza Neno la Mungu ao pengine haufurahie kujifunza? Usivunjike moyo. Kumbuka kama Yehova atakusaidia kama unamuruhusu afanye hivyo. Anaweza kukusaidia ‘kukuza [kukomalisha] tamaa’ kwa ajili ya Neno lake. (1 Pet. 2:2) Kwanza, umuombe Yehova akusaidie kujitia nizamu ili upate wakati wa kujifunza Neno lake. Kisha, utende kulingana na sala zako, pengine kwa kufanya vipindi vifupi-vifupi vya kujifunza. Kadiri wakati unapita, itakuwa mwepesi kwako kujifunza na utafurahia funzo hilo! Kwa kweli, utatambua kama unapendezwa na wakati wenye unatumia ili kukaza akili yako juu ya mawazo ya Yehova yenye kupendeza sana.​—1 Tim. 4:15.

7. Namna gani kujitia nizamu kunaweza kutusaidia kufikia muradi fulani wa kiroho?

7 Kujitia nizamu kunatusaidia kufikia miradi ya kiroho. Fikiria mufano wa baba mumoja wa familia mwenye aliona kama bidii yake ilikuwa inapunguka kwa kadiri fulani. Kwa sababu alihangaikia jambo hilo, alijiwekea muradi wa kuwa painia wa kawaida na alisoma habari fulani katika magazeti yetu zenye kuzungumuzia kazi hiyo. Kufanya hivyo, na kusali, kulimutia nguvu na kulitia nguvu hali yake kiroho. Pia alifanya mipango ya kuwa painia musaidizi wakati iliwezekana. Alipata matokeo gani? Hata kama kulikuwa vizuizi, alikaza akili yake juu ya muradi wake wa kuwa painia wa kawaida, na mwishowe alifikia muradi wake.

KOMALISHA WATOTO KATIKA NIZAMU YA YEHOVA

Wakati watoto wanazaliwa hawajue mema na mabaya, wanapaswa kuzoezwa (Picha hii inapatana na fungu la 8)

8-10. Nini inaweza kusaidia wazazi Wakristo wazoeze watoto wao ili wamutumikie Yehova? Toa mufano.

8 Wazazi Wakristo wako na pendeleo la maana sana la kukomalisha watoto wao katika ‘nizamu na muongozo wa akilini wa Yehova.’ (Efe. 6:4) Hilo ni daraka nzito kabisa, zaidi sana katika ulimwengu wa leo. (2 Tim. 3:1-5) Kwa kweli, watoto hawajue mema na mabaya wakati wanazaliwa. Wanazaliwa na uwezo wa kutumia zamiri yao, lakini inapaswa kufundishwa na kutiwa nizamu. (Rom. 2:14, 15) Kitabu kimoja chenye kutoa maelezo juu ya Biblia kinasema kama neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “nizamu” linaweza kumaanisha “namna mutoto anakomaa.”

9 Watoto wenye kutiwa nizamu kwa upendo mara nyingi wanajisikia kuwa salama. Wanajifunza kama uhuru uko na mipaka na kama maamuzi na mwenendo wao vinaweza kuwa na matokeo ya muzuri ao ya mubaya. Kwa hiyo, ni jambo la maana wazazi Wakristo wategemee muongozo wa Yehova. Kumbuka kama mashauri juu ya namna ya kulea watoto yanatofautiana katika desturi mbalimbali na yanaendelea kubadilika kadiri wakati unapita. Lakini wazazi wenye kumutegemea Yehova, hawawazie-wazie mambo ya kufanya ili kulea muzuri watoto ao kutegemea uzoefu wao wenyewe ao mawazo ya wanadamu.

10 Ili kuelewa jambo hilo tuzungumuzie mufano wa Noa. Wakati Yehova alimuambia ajenge safina, Noa hangetegemea uzoefu wake mwenyewe. Alikuwa hajajengaka safina hata siku moja. Kwa hiyo, alipaswa kumutegemea Yehova na kufanya “vivyo hivyo,” kama vile tu Yehova alimupatia maagizo. (Mwa. 6:22) Alipata matokeo gani? Hata kama ilikuwa mara yake ya kwanza, Noa alijenga safina muzuri. Kwa kweli alipaswa kufanya hivyo! Pia, Noa alikuwa muzazi muzuri kwa sababu alitegemea hekima yenye kutoka kwa Mungu. Kwa hiyo, alifundisha muzuri watoto wake na kuwaonyesha mufano muzuri; haikuwa mwepesi kufanya hivyo kwa sababu ya uovu wenye ulikuwa mbele ya Garika kufika.​—Mwa. 6:5.

11. Sababu gani wazazi wanapaswa kujikaza sana kuzoeza watoto wao?

11 Wazazi, namna gani munaweza kufanya “vivyo hivyo” mbele za Mungu? Mumusikilize Yehova. Mumuache awafundishe namna ya kukomalisha watoto kupitia Neno lake na muongozo wenye tunapata kupitia tengenezo lake. Kisha wakati fulani, pengine watoto wenu watawashukuru kwa sababu ya kufanya hivyo! Ndugu mumoja aliandika hivi: “Niko mwenye shukrani sana kwa wazazi wangu juu ya namna walinikomalisha. Walijikaza sana kugusa moyo wangu. Wao ndio wanapaswa kusifiwa zaidi juu ya maendeleo ya kiroho yenye nimefanya.” Lakini, hata kama wazazi wanajikaza sana, watoto fulani wanamuacha Yehova. Lakini, wazazi wenye wamejikaza sana kukaza kweli katika moyo wa mutoto wao, wako na zamiri safi. Wanaweza pia kuwa na tumaini kama siku moja mutoto huyo mwenye ameacha kweli atarudia “nyumbani” kwa Yehova.

12, 13. (a) Ikiwa mutoto ametengwa na kutaniko, namna gani wazazi Wakristo wanaonyesha kama wanamutii Mungu? (b) Familia moja ilipata baraka gani kwa sababu wazazi walimutii Yehova?

12 Jaribu kubwa zaidi la utii lenye wazazi fulani wako nalo ni uhusiano wao pamoja na mutoto mwenye ametengwa na kutaniko. Kwa mufano fikiria mama mumoja mwenye mutoto wake mwanamuke mwenye alikuwa ametengwa aliondoka nyumbani. Mama huyo anasema hivi: “Nilitafuta visababu katika vichapo vyetu ili niweze kupitisha wakati pamoja na mutoto wangu na mujukuu (munkana) wangu mwanamuke.” Anaongeza hivi: “Lakini bwana yangu alinisaidia kwa upole kuelewa kama mutoto wetu hakukuwa tena chini ya madaraka yetu na kama tunapaswa kubakia washikamanifu.”

13 Kisha kupita miaka fulani, mutoto wao alirudishwa katika kutaniko. Mama yake alisema hivi: “Sasa ananiita ao kunitumia ujumbe karibu kila siku! Na ananiheshimia sana mimi na bwana yangu kwa sababu anajua kama tulimutii Mungu. Tuko na uhusiano muzuri sana.” Ikiwa mutoto wako ametengwa na kutaniko, ‘utategemea Yehova kwa moyo wako wote, [kuliko] kutegemea uelewaji wako mwenyewe’? (Met. 3:5, 6) Mukumbuke kama nizamu ya Yehova inaonyesha upendo mwingi na hekima nyingi yenye iko nayo. Musisahau hata kidogo kama alitoa Mwana wake kwa ajili ya watu wote, kutia ndani mutoto wenu. Mungu hapendi mutu yeyote aharibiwe. (Soma 2 Petro 3:9.) Kwa hiyo, mutumainie nizamu ya Yehova na muongozo wake. Wazazi, mufanye mambo yenye Yehova anasema hata wakati kufanya hivyo kunawaletea maumivu. Kwa hiyo, mutegemeze nizamu ya Yehova, hapana kuipinga.

KATIKA KUTANIKO

14. Namna gani tunapata faida kupitia mafundisho yenye Yehova anatutolea kupitia ‘musimamizi-nyumba mwaminifu’?

14 Yehova ametoa ahadi ya kuhangaikia, kulinda, na kufundisha kutaniko la Kikristo. Anafanya hivyo kwa njia mbalimbali. Kwa mufano, amepatia Mwana wake daraka la kuhangaikia kutaniko, na Mwana wake pia ameweka ‘musimamizi-nyumba mwaminifu’ ili atoe chakula cha kiroho kwa wakati wenye kufaa. (Lu. 12:42) Chakula hicho chenye kutolewa katika njia mbalimbali, kinatoa mafundisho, ao nizamu yenye kufaa. Ujiulize hivi: ‘Ni mara ngapi hotuba ao habari fulani katika vichapo vyetu imenichochea kufanya mabadiliko katika mawazo ao katika mwenendo wangu?’ Ikiwa ulitenda kulingana na mashauri hayo, unaweza kuwa mwenye furaha! Unamuruhusu Yehova akufinyange, ao akupatie nizamu kwa faida yako.​—Met. 2:1-5.

15, 16. (a) Namna gani tunafaidika na “zawadi katika wanadamu” katika kutaniko? (b) Namna gani tunaweza kusaidia wazee wafanye kazi yao kwa furaha?

15 Pia Kristo alitolea kutaniko “zawadi katika wanadamu,” ni kusema, wazee ili wachunge kundi la Mungu. (Efe. 4:8, 11-13) Namna gani tunaweza kufaidika na zawadi hizo za maana sana? Njia moja ni kuiga imani ya wazee na mufano wao muzuri. Njia ingine ni kufuata mashauri yenye wanatutolea kupitia Maandiko. (Soma Waebrania 13:7, 17.) Kumbuka kama wazee wanatupenda na wanapenda tukomae kiroho. Kwa mufano, ikiwa wanaona kama tuko tunakosa mikutano ao tumepunguza bidii yetu, kwa kweli watatenda haraka ili kutusaidia. Watatusikiliza na kisha watajikaza kututia moyo kwa upendo na kututolea mashauri yenye kutoka katika Maandiko. Unaona kama musaada huo unaonyesha upendo wa Yehova kwako?

16 Kumbuka kama wazee wanaweza kuona kama ni vigumu kutupatia mashauri. Kwa mufano, wazia namna pengine ilikuwa vigumu kwa nabii Nathani kuzungumuza na Mufalme Daudi kisha Daudi kujaribu kuficha zambi nzito yenye alikuwa amefanya! (2 Sam. 12:1-14) Vilevile, kwa kweli mutume Paulo alipaswa kuwa na ujasiri ili kumurekebisha Petro, mumoja kati ya mitume 12, mwenye alionyesha upendeleo kuelekea ndugu zake Wayahudi. (Gal. 2:11-14) Kwa hiyo, namna gani unaweza kusaidia wazee ili wafanye kazi yao kwa vyepesi katika kutaniko lenu? Ukuwe munyenyekevu, mwenye kukaribiwa kwa vyepesi, na mwenye shukrani. Uone musaada wao kuwa njia yenye Mungu anatumia ili kukuonyesha upendo wake. Hilo litakuletea faida na litawafanya wafurahie zaidi kazi yao.

17. Namna gani dada mumoja alifaidika na musaada wenye upendo wenye wazee walimutolea katika kutaniko?

17 Kwa sababu alikuwa na maisha ya mubaya zamani, dada mumoja aliona kuwa ni vigumu kumupenda Yehova. Alisema hivi: “Wakati maisha yangu ya zamani na mambo mengine yalinifanya nivunjike sana moyo, nilijua kama ninapaswa kuzungumuza na wazee. Hawakunifokea ao kunichambua-chambua, lakini walinitia moyo na kunitia nguvu. Kisha kila mukutano wa kutaniko, hata kama walikuwa na kazi nyingi sana, mumoja kati yao alikuwa ananiuliza juu ya hali yangu. Kwa sababu ya maisha yangu ya zamani, ilikuwa vigumu kwangu kuona kama ninastahili kupendwa na Mungu. Lakini mara kwa mara Yehova ametumia kutaniko na wazee ili kuonyesha upendo wake kwangu. Ninasali ili nisimuache hata kidogo.”

JAMBO LA MUBAYA ZAIDI KULIKO MAUMIVU YENYE KULETWA NA NIZAMU

18, 19. Ni jambo gani lenye kuwa la mubaya zaidi kuliko maumivu yoyote yenye kuletwa na nizamu? Toa mufano.

18 Hata kama nizamu inaweza kuleta maumivu, kuko jambo lingine lenye kuleta maumivu hata zaidi, ni kusema, matokeo ya mubaya sana yenye tunaweza kupata kwa sababu ya kukataa nizamu. (Ebr. 12:11) Fikiria mifano mbili, mufano wa Kaini na wa Mufalme Zedekia. Wakati Kaini alichukia sana ndugu yake Abeli na kutaka kumuua, Mungu alimuonya hivi: ‘Kwa nini umewaka hasira na kwa nini uso wako umekunjamana? Ukigeuka utende mema, je, hautainuliwa? Lakini usipogeuka utende mema, kuna zambi inayovizia katika mwingilio, nayo inakutamani wewe. Je, wewe utaishinda?’ (Mwa. 4:6, 7) Kaini hakusikiliza. Kisha akaua ndugu yake. Kwa kweli, Kaini alijiletea yeye mwenyewe maumivu na mateso! (Mwa. 4:11, 12) Ikiwa angesikiliza onyo la Yehova, hangepatwa na mateso hayo yote.

19 Mufalme Zedekia mwenye alikuwa zaifu na muovu alitawala wakati watu wa Yerusalemu walikuwa katika hali ya mubaya. Mara kwa mara nabii Yeremia alimushauria Zedekia aache matendo yake ya mubaya, lakini mufalme huyo alikataa nizamu. Yeye pia, alipatwa na matokeo ya mubaya sana. (Yer. 52:8-11) Yehova hapendi kabisa tupatwe na mateso kama hayo!​—Soma Isaya 48:17, 18.

20. Wale wenye kukubali nizamu ya Mungu na wale wenye kukataa nizamu hiyo, watapatwa na nini?

20 Katika ulimwengu, mara nyingi watu wanazarau nizamu, na sifa ya kujitia nizamu. Lakini karibuni wale wote wenye kukataa nizamu ya Yehova watapatwa na matokeo ya mubaya. (Met. 1:24-31) Kwa hiyo, ‘tusikilize nizamu tupate kuwa na hekima.’ Kama vile Methali 4:13 inasema, ‘shika nizamu; usiiache. Ilinde, kwa maana hiyo ndiyo uzima wako.’