Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Wazazi, Munasaidia Watoto Wenu Wafikie Ubatizo?

Wazazi, Munasaidia Watoto Wenu Wafikie Ubatizo?

“Kwa nini unakawia? Simama, ubatizwe.”​—MDO. 22:16.

NYIMBO: 51, 135

1. Wazazi Wakristo wanapenda kuhakikisha jambo gani mbele watoto wao wabatizwe?

DADA mumoja mwenye kuitwa Blossom Brandt alieleza hivi juu ya uamuzi wake wa kubatizwa: “Kwa miezi mingi niliambia Baba na Mama yangu kama ninapenda kubatizwa, na mara kwa mara walizungumuza pamoja na mimi juu ya jambo hilo. Walipenda kuhakikisha kama nilielewa kwamba huo ni uamuzi muzito sana. Tarehe 31 Mwezi wa 12, 1934, ilikuwa siku ya tukio hilo la maana sana katika maisha yangu.” Leo, kama wazazi wa dada huyo, wazazi Wakristo wanapenda kusaidia watoto wao wakamate maamuzi yenye hekima. Kukawia-kawia ao kuchelewesha bila sababu ubatizo, kunaweza kuleta matatizo ya kiroho. (Yak. 4:17) Hata hivyo, kwa hekima wazazi wanapenda kuhakikisha kama mbele watoto wao wabatizwe, wako tayari kutimiza daraka la kuwa mwanafunzi wa Kristo.

2. (a) Waangalizi fulani wa muzunguko wameona tatizo gani? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?

2 Waangalizi fulani wa muzunguko wameona kama vijana wengi wenye wanakaribia kueneza miaka 20 hivi hawajabatizwa, hata kama wamekomalia katika familia za Kikristo. Mara nyingi, vijana hao wanahuzuria mikutano na kuhubiri. Wanajiona kuwa Mashahidi wa Yehova. Lakini, kwa sababu fulani wanajizuia kutoa maisha yao kwa Yehova na kubatizwa. Sababu gani? Katika hali fulani, wazazi wamewaambia wangojee kwanza mbele ya kubatizwa. Katika habari hii, tutazungumuzia mambo ine yenye yamezuia wazazi fulani Wakristo kusaidia watoto wao wafikie ubatizo.

MUTOTO WANGU ALISHAKOMAA KABISA?

3. Wazazi wa Blossom walikuwa na wasiwasi juu ya jambo gani?

3 Wazazi wa Blossom mwenye kuzungumuziwa katika fungu la kwanza, walikuwa wanajiuliza ikiwa mutoto wao alikuwa amekomaa kabisa ili kuelewa maana na uzito wa ubatizo. Namna gani wazazi wanaweza kujua ikiwa mutoto iko tayari kujitoa kwa Mungu?

4. Namna gani amri ya Yesu yenye kupatikana kwenye Mathayo 28:19, 20 inaweza kusaidia wazazi wakati wanafundisha watoto wao?

4 Soma Mathayo 28:19, 20. Kama vile tuliona katika habari yenye kutangulia, Biblia haitaje miaka yenye mutu anapaswa kuwa nayo ili abatizwe. Lakini, wazazi wanaweza kupata faida kwa kufikiri juu ya maana ya kufanya mwanafunzi. Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa ‘kufanya wanafunzi’ katika Mathayo 28:19, liko na maana ya mutu kufundisha akiwa na kusudi la kufanya mwanafunzi. Mwanafunzi ni mutu mwenye kujifunza na kuelewa mafundisho ya Yesu na mwenye anaazimia kuyashika. Kwa hiyo, wazazi wote Wakristo wanapaswa kuwa na muradi wa kufundisha watoto wao tangu wakati wangali wadogo sana na kuwasaidia wakuwe wanafunzi wa Kristo wenye kubatizwa. Kwa kweli, mutoto mudogo sana hastahili kubatizwa. Lakini, Biblia inaonyesha kama hata watoto wenye wamekomaa kwa kiasi fulani wanaweza kuelewa na kupenda kweli za Biblia.

5, 6. (a) Mambo yenye Biblia inasema juu ya Timotheo yanatusaidia kuelewa nini juu ya ubatizo wake? (b) Namna gani wazazi wenye kuwa na utambuzi wanaweza kusaidia watoto wao?

5 Timotheo alikuwa mwanafunzi mwenye aliamua kumutumikia Yehova wakati alikuwa angali mudogo. Mutume Paulo alisema kama Timotheo alijifunza kweli ya Maandiko tangu wakati alikuwa mutoto mudogo. Hata kama baba ya Timotheo hakumutumikia Yehova, mama yake mwenye alikuwa Muyahudi na tate (nkambo) yake walimusaidia apendezwe na Maandiko. Kwa hiyo, imani yake ilikuwa yenye nguvu. (2 Tim. 1:5; 3:14, 15) Wakati alifikia kuwa na miaka 20 hivi, Timotheo alikuwa mwanafunzi Mukristo mwenye alistahili kupewa mapendeleo katika kutaniko.​—Mdo. 16:1-3.

6 Kwa kweli, watoto wako tofauti; wamoja wanakomaa kiroho haraka kuliko wengine. Watoto fulani wanaelewa kweli ya Biblia na wanakamata maamuzi yenye hekima wakati wangali wadogo na wanaonyesha kama wanapenda kubatizwa. Wengine wanaweza kuwa tayari kubatizwa wakati wamekomaa kwa kadiri fulani. Kwa hiyo, wazazi wenye kuwa na utambuzi hawakaze watoto wao wabatizwe. Lakini, wanasaidia kila mutoto afanye maendeleo ya kiroho kulingana na namna yake ya kukomaa na uwezo wake. Wazazi wanaweza kufurahi wakati mutoto anakamata kwa uzito mawazo yenye kupatikana kwenye Methali 27:11. (Soma.) Hata hivyo, hawapaswe kusahau kusudi lao, ni kusema, kusaidia watoto wao wakuwe wanafunzi Wakristo. Wakati wanakumbuka jambo hilo, wazazi wanapaswa kufikiria ulizo hili, ‘Mutoto wangu iko na ujuzi wa kutosha ili kujitoa kwa Mungu na kubatizwa?’

MUTOTO WANGU IKO NA UJUZI WA KUTOSHA?

7. Ni lazima mutu wenye anapenda kubatizwa ajue mambo yote yenye kuwa katika Biblia? Eleza.

7 Wakati wazazi wanafundisha watoto wao katika familia, wanapenda watoto wao wakuwe na ujuzi wa musingi wenye utawasaidia wajitoe kwa Yehova. Lakini, haiko lazima mutu ajue mambo yote yenye kuwa katika Biblia ili ajitoe kwa Mungu na kubatizwa. Kisha kubatizwa, wanafunzi wote wanapaswa kuendelea kukomaa katika ujuzi. (Soma Wakolosai 1:9, 10.) Sasa, mutu anapaswa kuwa na ujuzi kwa kadiri gani mbele ya kubatizwa?

8, 9. Mufano wa Paulo na mulinzi wa gereza unaweza kutufundisha nini?

8 Mufano wa familia moja ya wakati wa mitume unaweza kufundisha wazazi mambo fulani. (Mdo. 16:25-33) Wakati wa safari yake ya pili ya umisionere katika mwaka wa 50 hivi kisha kuzaliwa kwa Yesu, Paulo alitembelea muji wa Filipi. Wakati alikuwa huko, yeye na mwenzake Sila walishitakiwa mambo ya uwongo na kufungwa katika gereza. Wakati wa usiku, tetemeko la inchi lilitikisa misingi ya gereza na kufungua milango yote. Kwa sababu mulinzi wa gereza aliogopa kwamba wafungwa wamekimbia, alitaka kujiua wakati mutume Paulo alimuita. Paulo na Sila walipata nafasi ya kuhubiria mulinzi huyo na familia yake. Kwa sababu walipendezwa na kweli zenye walijifunza juu ya Yesu hilo liliwachochea wakamate hatua gani? Walibatizwa bila kukawia. Habari hii inaweza kutufundisha nini?

9 Pengine mulinzi huyo wa gereza alikuwa zamani katika jeshi la Roma. Hakukuwa anajua Maandiko. Kwa hiyo, ili akuwe na ujuzi wa musingi juu ya Maandiko, alipaswa kujifunza kweli za musingi za Biblia, kuelewa maana ya kuwa mutumishi wa Mungu, na kuazimia kushika mambo yenye Yesu alifundisha. Kwa muda mufupi, ujuzi wa musingi wa Maandiko wenye alipata na upendo wake juu ya mambo yenye alijifunza, vilimuchochea kubatizwa. Kwa kweli, aliendelea kuongeza ujuzi wake kisha kubatizwa. Kulingana na mufano huo, munaweza kufanya nini wakati mutoto wenu anaonyesha kama anapendezwa na mafundisho ya musingi ya Maandiko, na anaelewa maana ya kujitoa kwa Mungu na kubatizwa? Wazazi Wakristo, munaweza kumuambia kwamba anaweza kuzungumuza na wazee wa kutaniko ili wachunguze ikiwa anatimiza mambo yenye kuombwa ili astahili kubatizwa. * Kama wanafunzi wengine wenye kubatizwa, ataendelea kuongeza ujuzi wake juu ya kusudi la Yehova katika maisha yake yote, na hata milele.​—Rom. 11:33, 34.

NI ELIMU GANI YENYE KUWA YA MUZURI ZAIDI KWA MUTOTO WANGU?

10, 11. (a) Wazazi fulani wako na mawazo gani? (b) Muzazi anapaswa kwanza kuhangaikia nini?

10 Wazazi fulani wameona kama inaweza kuwa muzuri zaidi mutoto wao asome kwanza masomo ya juu na akuwe na kazi ya muzuri mbele ya kubatizwa. Wazazi hao wanaweza kuwa na nia ya muzuri, lakini masomo hayo yatasaidia mutoto wao akuwe na maisha ya muzuri kabisa? Na jambo la maana zaidi, mawazo hayo yanapatana na Maandiko? Neno la Mungu linatutia moyo tutumie namna gani maisha yetu?​—Soma Mhubiri 12:1.

11 Ni jambo la maana kukumbuka kama ulimwengu huu na mambo yote yenye kuwa ndani vinapingana na mawazo ya Yehova na mambo yenye anapenda. (Yak. 4:7, 8; 1 Yoh. 2:15-17; 5:19) Ikiwa mutoto iko na urafiki wa sana pamoja na Yehova, hilo litamusaidia kupinga Shetani, ulimwengu wake, na mawazo ya mubaya. Ikiwa muzazi anachochea mutoto afuatie sana vitu vya kimwili, hilo linaweza kufanya mutoto afikiri kama kufuatia mambo ya kimwili ndilo jambo la maana zaidi, na hilo linaweza kuwa hatari. Je, wazazi Wakristo wenye upendo watapenda kabisa ulimwengu huu ufundishe mutoto wao namna ya kupata furaha ya kweli? Kwa kweli, tunapata furaha ya kweli wakati tu tunamutia Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu.​—Soma Zaburi 1:2, 3.

HALAFU, MUTOTO WANGU AKIFANYA ZAMBI?

12. Sababu gani wazazi fulani wanapenda mutoto wao angojee kwanza mbele ya kubatizwa?

12 Wakati alikuwa anaeleza sababu gani aliambia mutoto wake mwanamuke asibatizwe, mama mumoja Mukristo alisema hivi: “Ninasikia haya ya kusema kama sababu kubwa ilikuwa mupango wa kutengwa na kutaniko.” Kama dada huyo, wazazi fulani wamefikiri kama ni muzuri zaidi mutoto wao asibatizwe kwanza mupaka wakati atakuwa amekomaa vya kutosha na kuacha tabia za utoto. (Mwa. 8:21; Met. 22:15) Wanaweza kuwaza hivi, ‘Mutoto wangu hawezi kutengwa na kutaniko kwa sababu hajabatizwa.’ Sababu gani mawazo hayo ni ya udanganyifu?​—Yak. 1:22.

13. Ikiwa mutu hajabatizwa, hilo linamaanisha kama hatatoa hesabu kwa Yehova? Eleza.

13 Kwa kweli, wazazi Wakristo hawawezi kupenda mutoto wao abatizwe ikiwa hajakuwa tayari kutoa maisha yake kwa Yehova. Lakini, inaweza kuwa makosa kufikiri kama kwa sababu mutoto hajabatizwa hatatoa hesabu kwa Yehova. Haiko lazima mutu abatizwe ili atoe hesabu kwa Yehova. Lakini, ikiwa mutoto anajua mambo yenye Yehova anaona kuwa sawa na yenye anachukia, atatoa hesabu kwa Mungu. (Soma Yakobo 4:17.) Kwa hiyo, kuliko kuvunja mutoto moyo asibatizwe, wazazi wenye kuwa na hekima wanajikaza sana kuonyesha mufano muzuri. Wanapenda kusaidia mutoto wao tangu wakati angali mudogo apendezwe na kanuni za mwenendo za Yehova za juu. (Lu. 6:40) Kupendezwa na kanuni za Yehova ni ulinzi muzuri zaidi, kwa sababu mutoto wako atachochewa kutii njia za Yehova zenye kuwa sawa.​—Isa. 35:8.

WENGINE WANAWEZA KUSAIDIA

14. Namna gani wazee wanaweza kutegemeza wazazi wenye wako wanasaidia watoto wao wafikie ubatizo?

14 Kwa sababu wazee wa kutaniko ni wachungaji wa kiroho, wanaweza kutegemeza wazazi kwa kusema mambo ya muzuri juu ya miradi ya kiroho. Dada mumoja mwenye alifanya kazi ya upainia kwa zaidi ya miaka 70, alikumbuka namna mazungumuzo yenye alifanya pamoja na Ndugu Russell yalimusaidia wakati alikuwa na miaka sita tu. Alisema hivi: “Alitumia dakika 15 ili kuzungumuza na mimi juu ya miradi yangu ya kiroho.” Kwa kweli, maneno yenye kujenga na yenye kutia moyo yanaweza kuwa na matokeo ya muda murefu. (Met. 25:11) Wazee pia wanaweza kufanya mipango ili wazazi na watoto wao wasaidie katika kazi mbalimbali za Jumba la Ufalme, kwa kupatia vijana kazi mbalimbali kulingana na miaka yao na uwezo wao.

15. Ni katika njia gani wengine katika kutaniko wanaweza kutia moyo vijana?

15 Ndugu na dada katika kutaniko wanaweza kusaidia kwa kuonyesha kama wanapendezwa sana na vijana. Wanaweza kufanya hivyo kwa kuwa waangalifu juu ya mambo yenye kuonyesha kama kijana anafanya maendeleo ya kiroho. Je, kijana ametoa maelezo yenye kutoka moyoni na yenye kujenga ao ametoa mugawo fulani kwenye mukutano wa katikati ya juma? Kijana alishinda jaribu fulani la ushikamanifu ao ametumia nafasi yenye alipata ili kuhubiri kwenye masomo? Ukuwe tayari kumupongeza kwa moyo wote. Unaweza kujiwekea muradi wa kuzungumuza na kijana mumoja mbele ao kisha kila mukutano, na kumuonyesha kama unapendezwa kabisa naye. Katika njia hizi na zingine, vijana wanaweza kuona kama wako sehemu ya “kutaniko kubwa.”​—Zab. 35:18.

SAIDIA MUTOTO WAKO AFIKIE UBATIZO

16, 17. (a) Sababu gani ni jambo la maana watoto wafikie kubatizwa? (b) Wazazi wote Wakristo wanapenda kuwa na furaha gani? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

16 Kukomalisha mutoto katika ‘nizamu na muongozo wa akilini wa Yehova’ ni pendeleo kubwa sana lenye muzazi Mukristo iko nalo. (Efe. 6:4; Zab. 127:3) Tofauti na watoto katika taifa la zamani la Israeli, watoto wa wazazi Wakristo hawazaliwe wakiwa wenye kutolewa kwa Yehova. Zaidi ya hilo, mutoto hariti kutoka kwa wazazi wake kupenda Mungu na kupenda kweli. Tangu wakati mutoto anazaliwa, wazazi wanapaswa kuwa na kusudi la kumufanya kuwa mwanafunzi, kumusaidia ajitoe kwa Mungu, na kuwa mutumishi wa Yehova mwenye kubatizwa. Hilo ndilo jambo la maana zaidi. Kwa kweli, wakati wa ziki kubwa yenye kuja mutu atatiwa alama kwa ajili ya wokovu kwa sababu alijitoa kwa Mungu, alibatizwa, na kumutumikia Mungu kwa uaminifu.​—Mt. 24:13.

Wazazi wanapaswa kuwa na muradi wa kusaidia mutoto wao afikie kuwa mwanafunzi (Picha hizi zinapatana na fungu la 16, 17)

17 Wakati Blossom Brandt aliamua kubatizwa, wazazi wake wenye kumuogopa Mungu walitaka kuhakikisha kama alikuwa tayari kukamata uamuzi wa maana zaidi katika maisha yake. Wakati walikuwa hakika kwamba alikuwa tayari, waliunga mukono uamuzi wake. Usiku wenye ulitangulia siku ya kubatizwa kwake, baba yake alifanya jambo la muzuri sana. Blossom alieleza hivi: “Alituambia sisi wote tupige magoti, na akasali. Aliambia Yehova kwamba alifurahia sana uamuzi wa mutoto wake mwanamuke wa kumutolea maisha yake.” Kisha kupita miaka zaidi ya 60, Blossom alisema hivi: “Kwa kweli munaweza kuwa hakika kama, kwa miaka yote yenye itakuja, sitasahau hata kidogo usiku huo!” Wazazi, mukuwe basi na furaha ya kuona namna watoto wenu wanajitoa kwa Yehova na kuwa watumishi wake wenye kubatizwa.

^ fu. 9 Wazazi wanaweza kuzungumuza pamoja na mutoto wao juu ya habari zenye zinaweza kuwasaidia zenye kupatikana katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, uku. 304-310. Ona pia “Kisanduku cha Maulizo” katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Mwezi wa 4, 2011, uku. 2.