Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Yehova Hajaacha Kunisaidia Hata Kidogo!

Yehova Hajaacha Kunisaidia Hata Kidogo!

Nilikuwa kati ya watoto wanawake ine wenye walichaguliwa ili kumupatia Adolf Hitler maua kisha kumaliza kutoa hotuba wakati fulani. Sababu gani nilichaguliwa? Baba yangu alijiingiza sana katika kazi mbalimbali za Wanazi na alikuwa mutu wa kutembeza motokari ya kiongozi wa kikundi cha Wanazi cha eneo letu. Mama yangu aliamini sana dini ya Katoliki na alipenda nikuwe mutawa mwanamuke. Hata kama kulikuwa mambo hayo mawili yenye kuchochea sana, sikufikia kuunga mukono Wanazi na sikukuwa mutawa mwanamuke. Acha niwaambie sababu gani.

NILIKOMALIA katika Graz, Austria (Autriche). Wakati nilikuwa na miaka saba, nilitumwa kwenye masomo ili nipate mazoezi ya dini. Lakini, niliona matendo ya mambo ya uasherati yenye kuchukiza sana kati ya watawa wanaume na watawa wanawake. Kwa hiyo, mama yangu aliniruhusu nitoke kwenye masomo hayo kisha kufanya mwaka moja.

Familia yetu pamoja na Baba na amevaa nguo za askari

Kisha, nilienda kwenye masomo kwenye wanafunzi wanaishi. Usiku moja, Baba yangu alikuja kunikamata ili kunipeleka mahali penye kuwa salama kwa sababu Graz ilikuwa inapigwa mabombe sana. Tulikimbilia katika muji wa Schladming. Kisha kufika katika muji huo na kuvuka kilalo, kilipigwa mabombe na kuharibiwa kabisa. Wakati mwingine, ndege fulani za vita zilitutupia risasi mimi na tate (nkambo) yangu mwanamuke katika kiwanja chetu. Kufikia wakati wenye vita iliisha, ilionekana kuwa dini na serikali vilikuwa vimetuvunja moyo.

NINAJIFUNZA JUU YA MUSAADA WENYE HAUWEZI KUSHINDWA

Katika mwaka wa 1950, Shahidi mumoja wa Yehova alianza kuzungumuza pamoja na mama yangu juu ya ujumbe wa Biblia. Nilikuwa ninasikiliza mazungumuzo yao na hata kusindikiza Mama yangu kwenye mikutano fulani ya kutaniko. Kwa sababu alisadikishwa kama Mashahidi wa Yehova wako na kweli, alibatizwa katika mwaka wa 1952.

Wakati huo, niliona kutaniko la eneo letu kama mahali kwenye wanawake wenye kukomaa wanazoea kukutana. Lakini kisha, tulitembelea kutaniko kwenye kulikuwa vijana wengi; haikukuwa hata kidogo kama mahali kwenye wanawake wenye kukomaa wanazoea kukutana! Wakati tulirudia katika Graz, nilianza kuhuzuria mikutano yote, na bila kukawia mimi pia nilisadiki kama mambo yenye nilikuwa ninajifunza yalikuwa kweli. Pia, nilifikia kumujua Yehova kuwa Mungu mwenye kutolea watumishi wake musaada wenye hauwezi kushindwa. Anafanya hivyo hata wakati tunajisikia kuwa tuko peke yetu wakati tunapambana na hali zenye tunaona kama hatuwezi kushinda hata kidogo.​—Zab. 3:5, 6.

Nilipenda kuzungumuza na wengine juu ya kweli. Nilianza kuhubiria ndugu na dada zangu. Dada zangu wakubwa ine walikuwa tayari wameondoka nyumbani na walikuwa wanafanya kazi ya kufundisha kwenye masomo. Lakini niliwatembelea katika vijiji mbalimbali na kuwatia moyo wajifunze Biblia. Mwishowe, ndugu yangu na dada zangu tano walijifunza Biblia na wakakuwa Mashahidi wa Yehova.

Wakati wa juma langu la pili la kuhubiri nyumba kwa nyumba, nilikutana na mwanamuke mumoja mwenye alikuwa na miaka 30 hivi, na nikaanza kujifunza Biblia naye. Alifanya maendeleo mupaka kufikia ubatizo, na kisha bwana yake na watoto wake wawili pia wakabatizwa. Funzo hilo lilitia nguvu imani yangu. Sababu gani? Kwa sababu hakuna mutu mwenye alikuwa amejifunza na mimi Biblia kwa kufuata programu ya kujifunza. Nilipaswa kutayarisha muzuri kila habari ya kujifunza. Kwa njia fulani, nilifanya hivyo ili kujifundisha kwanza mimi mwenyewe ili niweze kufundisha mwanafunzi wangu! Hilo lilinisaidia kabisa kuelewa muzuri zaidi kweli. Katika Mwezi wa 4, 1954, nilibatizwa katika maji ili kuonyesha kama nimejitoa kwa Yehova.

‘TUNATESWA, LAKINI HATUACHWE KABISA BILA MUSAADA’

Katika mwaka wa 1955, nilihuzuria mikusanyiko ya kimataifa katika Ujerumani, Ufaransa, na Uingereza. Wakati nilikuwa katika muji wa Londres, nilikutana na Albert Schroeder. Alikuwa mwalimu kwenye Masomo ya Biblia ya Gileadi, na kisha alitumikia katika Baraza Lenye Kuongoza. Wakati tulitembelea Jumba la Makumbusho la Uingereza, Ndugu Schroeder alituonyesha maandishi fulani ya Biblia. Yalikuwa na herufi za Jina la Mungu katika Kiebrania, na alituelezea kama maandishi hayo yalikuwa ya maana. Hilo lilinichochea nipende zaidi Yehova na hata kweli, na kunifanya niazimie zaidi kufundisha wengine kweli zenye kuwa katika Neno la Mungu.

Mimi pamoja na mwenzangu (kuume), tuko mapainia wa pekee katika Mistelbach, Austria

Nilianza kazi ya upainia wa kawaida tarehe 1 Mwezi wa 1, 1956. Kisha miezi ine, nilialikwa kuwa painia wa pekee katika Austria. Wakati huo, hakukuwa Mashahidi wa Yehova katika muji wa Mistelbach, kwenye nilipaswa kutumikia. Lakini nilipambana na tatizo fulani la pekee. Mimi na painia mwenzangu tulikuwa tofauti kabisa. Nilikuwa na miaka 19 hivi na nilikomalia katika muji; naye alikuwa na miaka 25 na alikomalia katika kijiji. Nilipenda kuamuka nyuma kila asubui; yeye alipenda kuamuka asubui sana. Wakati wa mangaribi nilipenda kulala nyuma; yeye alipenda kulala mbele ya wakati. Hata hivyo, kutumikisha mashauri ya Biblia, kulitusaidia kutumika pamoja hata kama tulikuwa tofauti na tulifurahia matokeo ya muzuri katika kazi yetu ya upainia.

Kusema kweli, tulipambana na magumu mengine makubwa zaidi. Kulikuwa hata mateso fulani, lakini ‘hatukuachwa kabisa bila musaada.’ (2 Kor. 4:7-9) Siku fulani, wakati tulikuwa tunahubiri katika kijiji kimoja cha mbali, watu walifungua imbwa zao. Bila kukawia mimi na mwenzangu tulizungukwa na imbwa kubwa-kubwa zenye zilikuwa zinafoka na kuonyesha meno zao. Tulikamatana mikono, na hata nilisali hivi: “Yehova, tafazali, wakati zitatufikia, utusaidie tukufe haraka!” Wakati imbwa hizo zilitukaribia, zilisimama, zikatikisa mikiya, na zikaondoka. Tuliona kama Yehova ametulinda. Kisha hapo, tulihubiri kijiji hicho chote, na jambo la kufurahisha ni kwamba, watu walipendezwa sana. Pengine walishangaa kwa sababu imbwa hazikutuumiza ao kwa sababu tuliendelea kufanya kazi yetu hata kama tulipatwa na jambo hilo lenye kuogopesha sana. Mwishowe, wamoja kati yao walifikia kuwa Mashahidi.

Tulipatwa na jambo lingine la kuogopesha. Siku moja mwanaume mwenye alikuwa anatupangisha alikuja nyumbani akiwa mwenye kulewa, alituogopesha kama atatuua na kusema kama tulikuwa na tunasumbua majirani. Bibi yake alijikaza kumutuliza lakini hakuweza. Tulisikia mambo hayo yote wakati tulikuwa kwenye vipandio vya kuenda katika chumba chetu. Mara moja tuliweka viti kwenye mulango wetu na tukaanza kuweka vitu vyetu katika sakoshi zetu. Wakati tulifungua mulango, mwanaume huyo alikuwa mwenye kusimama kwenye mwisho wa vipandio, na alikuwa na kisu cha murefu katika mikono yake. Kwa hiyo, tukakimbia kwa kupitia kwenye mulango wa nyuma na kupita katika njia ya murefu yenye ilikuwa katika bustani pamoja na vitu vyetu vyote, na hatukurudia tena hata siku moja.

Tulienda katika hoteli moja na tukaomba chumba kimoja. Tulibakia hapo kwa mwaka moja hivi, na hilo lilifikia kutusaidia kabisa katika kazi yetu ya kuhubiri. Namna gani? Hoteli hiyo ilikuwa katikati ya muji, na wanafunzi wetu fulani wa Biblia walipenda kujifunzia hapo. Bila kukawia tulianza kufanyia funzo la kitabu na Funzo la Munara wa Mulinzi la kila juma katika chumba chetu katika hoteli, na watu 15 hivi walihuzuria.

Tulibakia katika Mistelbach kwa zaidi ya mwaka mumoja. Kisha nikatumwa katika Feldbach, kusini-mashariki mwa Graz. Nilikuwa na painia mwengine wa mupya wa kutumika naye, lakini tena hakukuwa kutaniko katika eneo hilo. Tuliishi katika chumba kidogo kwenye gorofa ya pili ya nyumba ya mbao. Upepo ulikuwa unaingia ndani ya chumba hicho kwa kupitia katika tundu zenye kuwa kati ya mbao, kwa hiyo tulijaribu kufunika tundu hizo kwa kutumia magazeti ya kutangaza habari. Tulipaswa pia kushota maji katika kisima. Lakini tulipata matokeo ya muzuri. Kisha miezi kidogo, kikundi kilianzishwa. Mwishowe, watu 30 hivi wa familia moja wenye tulijifunza nao wafikia kukubali kweli!

Mambo hayo yalinichochea nikuwe mwenye shukrani juu ya musaada wa Yehova wenye hauwezi kushindwa wenye anatolea wale wenye kufuatia faida za Ufalme. Hata wakati hakuna mwanadamu mwenye anaweza kutusaidia, Yehova iko pale sikuzote ili kutusaidia.​—Zab. 121:1-3.

‘MUKONO WA KUUME WA UADILIFU’ WA MUNGU UNANITEGEMEZA

Katika mwaka wa 1958 mukusanyiko wa kimataifa ulifanywa katika New York City, kwenye uwanja wa Yankee Stadium na Polo Grounds. Nilijaza ombi la kuhuzuria mukusanyiko huo, na beteli ya Austria iliniuliza ikiwa ninapenda kusoma darasa la 32 la Masomo ya Gileadi. Namna gani ningekataa pendeleo hilo? Mara moja nilijibia, “Ndiyo!”

Katika darasa kwenye Gileadi, nilikaa karibu na Martin Poetzinger. Alikuwa amevumilia majaribu makali wakati wa utawala wa Wanazi katika kambi za mateso. Yeye pia alifikia kutumika katika Baraza Lenye Kuongoza. Wakati wa masomo, Martin alikuwa ananiambia hivi wakati fulani kwa sauti ya chini-chini: “Erika, hilo linamaanisha nini katika luga ya Kijerumani?”

Wakati tulifika katikati ya masomo, Nathan Knorr alitangaza migawo yetu. Mugawo wangu ulikuwa wa kutumikia katika Paraguay. Kwa sababu nilikuwa kijana, nilikuwa na lazima ya ruhusa ya baba yangu ili nihamie katika inchi hiyo. Kisha baba kuniruhusu, nilifika katika Paraguay katika Mwezi wa 3, 1959. Nilitumwa kuishi katika nyumba ya wamisionere katika Asunción, pamoja na misionere mwingine.

Bila kukawia, nilikutana na Walter Bright, misionere mwenye alisoma darasa la 30 la Masomo ya Gileadi. Kisha wakati fulani, tulioana na tungeweza kupiganisha magumu ya maisha pamoja. Kila wakati tulikutana na magumu yenye kuogopesha, tulisoma ahadi ya Yehova yenye kupatikana kwenye Isaya 41:10. Inasema hivi: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu.” Ahadi hiyo ilituhakikishia kama ikiwa tunaendelea kubakia waaminifu kwa Mungu na kutia Ufalme pa nafasi ya kwanza, hataacha kutusaidia hata kidogo.

Kisha wakati fulani, tulitumwa katika eneo lenye lilikuwa karibu na mupaka wa Brazili. Huko viongozi wa dini walichochea vijana watupe majiwe kwenye nyumba yetu ya wamisionere, yenye ilikuwa tayari katika hali ya mubaya. Kisha Walter akaanza kujifunza Biblia pamoja na mukubwa mumoja wa polisi. Alihakikisha kama polisi wanabakia karibu na nyumba yetu kwa juma moja, na wale wenye walikuwa wanatutesa hawakutusumbua tena. Kisha muda mufupi, tulihamia katika makao mengine ya muzuri zaidi upande mwingine wa mupaka wa Brazili. Hilo lilituletea faida kwa sababu tungefanya mikutano katika Paraguay na katika Brazili. Mbele tutoke katika mugawo huo, kulikuwa kutaniko mbili ndogo.

Mimi na bwana yangu, Walter, wakati tulikuwa wamisionere katika Asunción, Paraguay

YEHOVA ANAENDELEA KUNITEGEMEZA

Wanganga wangu walikuwa wameniambia kama singeweza kuzaa watoto; kwa hiyo, tulishangaa kujua katika mwaka wa 1962 kama nilikuwa na mimba! Mwishowe tulianza kuishi katika Hollywood, Florida, karibu na watu wa familia ya Walter. Kwa miaka fulani, mimi na Walter hatukuweza kufanya kazi ya upainia. Tulipaswa kuhangaikia familia yetu. Lakini, tuliendelea kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza.​—Mt. 6:33.

Wakati tulifika katika Florida katika Mwezi wa 11, 1962, tulishangaa kuona kama watu wa eneo hilo hawakupenda ndugu na dada wazungu na weusi wakusanyike pamoja nafasi moja, na kama ndugu na dada walihubiri katika maeneo tofauti. Lakini Yehova hana ubaguzi kati ya watu wa rangi mbalimbali ya ngozi, na bila kukawia ndugu na dada wa rangi zote walianza kukusanyika pamoja katika makutaniko. Mukono wa Yehova ulionekana katika mupango huo, kwa sababu leo kuko makutaniko mengi katika eneo hilo.

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, Walter alikufa kwa sababu ya kansere ya ubongo katika mwaka wa 2015. Alikuwa bwana muzuri kwa miaka 55, alimupenda Yehova na alisaidia ndugu wengi. Ninangojea kwa hamu kumuona tena na afya ya mupya wakati atafufuliwa.​—Mdo. 24:15.

Niko mwenye shukrani kwa sababu nimekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka zaidi ya 40, na nimepata mambo mengi yenye kufurahisha na baraka nyingi. Kwa mufano, mimi na Walter tuliweza kusaidia wanafunzi wetu wa Biblia 136 mupaka kufikia ubatizo. Ni kweli kwamba tulipatwa na magumu fulani. Lakini hatukuona magumu hayo kuwa sababu ya kuacha kumutumikia Mungu wetu mwaminifu. Tulimukaribia zaidi, na kutumainia kama atatengeneza mambo kwa wakati wake na kwa njia yenye anapenda. Na alifanya hivyo!​—2 Tim. 4:16, 17.

Ninamukumbuka sana Walter, lakini kazi ya upainia inanisaidia kuvumilia. Ninaona kama kufundisha wengine kunanisaidia sana, zaidi sana kuzungumuza nao juu ya tumaini la ufufuo. Kwa kweli, katika njia nyingi sana zenye siwezi kueleza, Yehova hajaacha kunisaidia. Ametimiza ahadi yake kwa kunitegemeza, kunitia nguvu, na kunishika kwa mukono wake “wa kuume wa uadilifu.”​—Isa. 41:10.