Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Umuige Yehova​—Mungu Mwenye Kutia Moyo

Umuige Yehova​—Mungu Mwenye Kutia Moyo

‘Abarikiwe Mungu . . . ambaye anatufariji [anatutia moyo] katika ziki yetu yote.’​—2 KOR. 1:3, 4.

NYIMBO: 7, 3

1. Wakati Adamu na Eva waliasi katika Edeni, Yehova alitolea wanadamu tumaini gani lenye kutia moyo?

TANGU wakati wanadamu walifanya zambi na kupoteza ukamilifu, Yehova ameonyesha kama yeye ni Mungu mwenye kutia moyo. Kisha tu uasi katika shamba la Edeni, alitoa unabii wenye ungetia moyo wazao wa Adamu na kuwapatia tumaini. Wakati ahadi hiyo ya unabii yenye kupatikana katika Mwanzo 3:15 ingeeleweka, ingepatia wanadamu tumaini kwamba mwishowe ule “nyoka wa zamani,” ni kusema, Shetani Ibilisi, angeharibiwa pamoja na kazi zake zote zenye uovu.​—Ufu. 12:9; 1 Yoh. 3:8.

YEHOVA ALITIA MOYO WATUMISHI WAKE WA ZAMANI

2. Namna gani Yehova alimutia moyo Noa?

2 Noa, mutumishi wa Yehova aliishi kati ya watu wenye hawakukuwa wanamutumikia Mungu, yeye na familia yake tu ndio walikuwa wanamutumikia Yehova. Kwa sababu watu wenye walimuzunguka walizoea kufanya mambo ya jeuri na ya uasherati, pengine Noa angeweza kuvunjika moyo. (Mwa. 6:4, 5, 11; Yuda 6) Lakini Yehova alimupatia habari yenye ilimutia moyo ili aendelee kuwa na bidii ya ‘kutembea pamoja na Mungu.’ (Mwa. 6:9) Yehova aliambia Noa kama ataharibu ulimwengu huo muovu na akamuambia mambo yenye anapaswa kufanya ili familia yake iokoke. (Mwa. 6:13-18) Yehova alijionyesha kuwa Mungu mwenye kutia moyo kwa Noa.

3. Namna gani Yehova alimutia Yoshua moyo? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

3 Yoshua pia alikuwa na kazi kubwa ya kuingiza watu wa Mungu katika Inchi ya Ahadi. Alipaswa kupigana vita na kushinda majeshi yenye nguvu ya mataifa yenye yalikuwa yanaishi katika inchi hiyo. Yoshua alikuwa na sababu ya kuogopa. Yehova alijua jambo hilo; kwa hiyo, aliamuru Musa amutie moyo Yoshua. Mungu alisema hivi: ‘Nawe umupe Yoshua utume na kumutia moyo na kumwimarisha, kwa maana yeye ndiye atakayevuka mbele ya watu hawa naye ndiye atakayewafanya wariti inchi utakayoiona.’ (Kum. 3:28) Mbele Yoshua aanze kazi yake, Yehova alimutia moyo kwa kumuambia hivi: ‘Je, mimi sikukuamuru wewe? Ukuwe hodari na mwenye nguvu. Usitetemeke wala usikuwe na hofu [woga], kwa maana Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe kila mahali unapoenda.’ (Yos. 1:1, 9) Maneno hayo ni yenye kutia moyo kabisa!

4, 5. (a) Namna gani Yehova alitia moyo watu wake wa zamani? (b) Namna gani Yehova alitia moyo Mwana wake?

4 Zaidi ya kutia moyo watu mumoja-mumoja, Yehova alisema pia maneno yenye kutia moyo juu ya watu wake wakiwa kikundi. Katika maneno ya unabii yenye yangetia moyo Wayahudi wenye walikuwa katika uhamisho katika muji wa Babiloni, Yehova alisema hivi: ‘Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mukono wangu wa kuume wa uadilifu.’ (Isa. 41:10) Wakristo wa kwanza-kwanza walikuwa na uhakikisho huo, na leo pia watu wa Mungu wako na uhakikisho huo.​—Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.

5 Hata Yesu alitiwa moyo na Baba yake. Wakati wa ubatizo wake, Yesu alisikia sauti kutoka mbinguni yenye ilisema hivi: ‘Huyu ni Mwanangu, mupendwa, ambaye nimemukubali.’ (Mt. 3:17) Maneno hayo yalipaswa kumutia Yesu nguvu katika utumishi wake wote katika dunia!

YESU ALITIA WENGINE MOYO

6. Namna gani mufano wa talanta unatutia moyo?

6 Yesu aliiga mufano wa Baba yake. Mufano wa talanta wenye Yesu alitoa katika unabii wake juu ya mwisho wa ulimwengu huu muovu, unatutia moyo tukuwe waaminifu. Katika mufano huo, bwana alionyesha kama anapendezwa na kila mutumishi wake muaminifu, kwa kumuambia hivi: ‘Vema, mutumwa mwema na muaminifu! Ulikuwa muaminifu juu ya mambo machache. Nitakuweka juu ya mambo mengi. Ingia katika shangwe ya bwana wako.’ (Mt. 25:21, 23) Maneno hayo yanatutia moyo kabisa tuendelee kumutumikia Yehova kwa uaminifu!

7. Namna gani Yesu alitia moyo mitume wake, na zaidi sana Petro?

7 Mara nyingi mitume wa Yesu walibishana juu ya nani alikuwa mukubwa zaidi kati yao, lakini Yesu aliwatia moyo kwa uvumilivu wakuwe wanyenyekevu na wakuwe watumishi wa wengine, hapana mabwana juu ya wengine. (Lu. 22:24-26) Zaidi sana Petro alimuhuzunisha Yesu mara nyingi. (Mt. 16:21-23; 26:31-35, 75) Lakini, kuliko kumukataa Petro, Yesu alimutia moyo na hata alimupatia mugawo wa kutia moyo ndugu zake.​—Yoh. 21:16.

WATU WA MUNGU WA ZAMANI WALITIA MOYO WENGINE

8. Namna gani Hezekia alitia moyo wakubwa wa jeshi na watu wa Yuda?

8 Hata mbele Mwana wa Yehova akuje katika dunia na kuweka mufano mukamilifu juu ya namna ya kutia wengine moyo, watumishi wa Yehova waaminifu walijua kama ni jambo la lazima kutia wengine moyo. Wakati Waashuru waliogopesha Wayahudi, Mufalme Hezekia alikusanya wakubwa wa jeshi na watu wa Yuda ili kuwatia moyo. “Na watu wakaanza kujitegemeza [kutiwa nguvu] juu ya maneno [yake].”​—Soma 2 Mambo ya Nyakati 32:6-8.

9. Kitabu cha Ayubu kinatufundisha nini juu ya kutia wengine moyo?

9 Hata kama alikuwa na lazima ya kutiwa moyo, Ayubu alifundisha wafariji wake watatu wa uwongo namna ya kutia wengine moyo. Aliwaambia kama ikiwa ni yeye alikuja kuwafariji, ‘angewatia wao nguvu kwa maneno ya kinywa chake, na faraja ya midomo yake mwenyewe ingewatuliza.’ (Ayu. 16:1-5) Mwishowe, Elihu alimutia Ayubu moyo na Yehova mwenyewe alifanya hivyo.​—Ayu. 33:24, 25; 36:1, 11; 42:7, 10.

10, 11. (a) Sababu gani binti ya Yeftha alikuwa na lazima ya kutiwa moyo? (b) Ni nani wenye kuwa na lazima ya kutiwa moyo leo?

10 Mufano mwingine wenye kuwa katika Biblia wa mutu mwenye alikuwa na lazima ya kutiwa moyo, ni wa binti ya Yeftha. Mbele ya kuenda kupigana vita na Waamoni, muamuzi Yeftha aliahidi Yehova kwamba ikiwa anamupatia ushindi, mutu wa kwanza mwenye angekuja kumupokea kisha vita, angeenda kumutumikia Yehova kwenye tabenakulo. Yeftha alipata ushindi, na binti yake, mutoto mumoja tu mwenye alikuwa naye, ndiye alikuja kumupokea na kufurahia ushindi wake pamoja naye. Moyo wa Yeftha ulivunjika. Lakini alitimiza ahadi yake na akatuma binti yake mwenye alikuwa bikira aende Shilo ili atumike kwenye tabenakulo maisha yake yote.​—Amu. 11:30-35.

11 Hata kama hilo lilikuwa jambo ngumu sana kwa Yeftha, lilipaswa kuwa jambo ngumu zaidi kwa binti yake mwenye alikuwa tayari kutenda kulingana na ahadi ya baba yake. (Amu. 11:36, 37) Kwa hiyo, aliachana na haki yake ya kuolewa, kuzaa watoto, na kuendeleza jina la familia na uriti. Kwa kweli, alihitaji kufarijiwa na kutiwa moyo. Biblia inasema hivi: ‘Nayo ikawa sharti [desturi] katika Israeli: Mwaka baada ya mwaka binti za Israeli wakawa wakienda kumupongeza binti ya Yeftha Mugileadi, siku ine kwa mwaka.’ (Amu. 11:39, 40) Kwa kweli, Wakristo wenye hawajaoa ao kuolewa wenye wanahangaikia sana “mambo ya Bwana” wanastahili pia kupongezwa na kutiwa moyo.​—1 Kor. 7:32-35.

MITUME WALITIA MOYO NDUGU ZAO

12, 13. Namna gani Petro ‘alitia nguvu ndugu zake’?

12 Katika usiku wa kifo chake, mbele auawe Yesu alimuambia Petro hivi: “Simoni, Simoni, tazama! Shetani amedai kuwapata ninyi ili awapepete kama ngano. Lakini nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isififie; na wewe, mara tu utakapokuwa umerudi, watie nguvu ndugu zako.”​—Lu. 22:31, 32.

Barua za mitume zilitia moyo sana makutaniko ya wakati wa mitume, na zinaendelea kutujenga mupaka leo (Picha hizi zinapatana na fungu la 12-17)

13 Petro alifikia kuwa kati ya wale wenye waliongoza katika kutaniko la Kikristo la kwanza-kwanza. (Gal. 2:9) Alitia moyo ndugu zake kupitia mufano wake wenye uhodari kwenye Pentekoste na kuendelea. Wakati alikuwa anakaribia mwisho wa utumishi wake wa muda murefu, aliandikia Wakristo wenzake. Ili kuwaelezea sababu gani aliwaandikia, alisema hivi: ‘Nimewaandikia ninyi kwa maneno machache, ili kutoa kitia-moyo na ushahidi wa bidii kwamba hizi ndizo fazili zisizostahiliwa za Mungu zilizo za kweli; katika hizo simameni imara.’ (1 Pet. 5:12) Barua hizo za Petro zenye ziliongozwa na roho ya Mungu zimeendelea kutia moyo Wakristo tangu wakati huo mupaka leo. Tuko na lazima kabisa ya vitia moyo hivyo wakati tunangojea utimizo wa ahadi za Yehova!​—2 Pet. 3:13.

14, 15. Namna gani vitabu vya Biblia vyenye mutume Yohana aliandika vimetia Wakristo moyo?

14 Mutume Yohana alikuwa pia kati ya watu wenye waliongoza katika kutaniko la Kikristo la kwanza-kwanza. Habari ya Injili yenye kufurahisha yenye aliandika juu ya utumishi wa Yesu imetia moyo Wakristo kwa mamia ya miaka; na inatutia moyo pia leo. Ni Injili yake tu ndiyo iko na maneno ya Yesu yenye kusema kama upendo ndio alama yenye kutambulisha wanafunzi wake wa kweli.​—Soma Yohana 13:34, 35.

15 Barua tatu za Yohana ziko na mali ingine ya kiroho. Kwa kweli, wakati zamiri yetu inatusumbua sana kwa sababu ya zambi, tunatiwa moyo wakati tunasoma kama ‘damu ya Yesu . . . inatusafisha kutoka katika zambi yote.’ (1 Yoh. 1:7) Na ikiwa moyo wetu unaendelea kutuhukumu, kwa kweli, tunatiwa moyo na kuonyesha shukrani sana wakati tunasoma kama ‘Mungu ni mukubwa kuliko mioyo yetu.’ (1 Yoh. 3:20) Ni Yohana tu ndiye aliandika kama “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8, 16) Barua yake ya pili na ya tatu zinapongeza Wakristo wenye wanaendelea ‘kutembea katika kweli.’​—2 Yoh. 4; 3 Yoh. 3, 4.

16, 17. Namna gani mutume Paulo alitia moyo Wakristo wa kwanza-kwanza?

16 Wakati wa mitume, pengine mutume mwenye alitia sana moyo ndugu zake ni mutume Paulo. Inaonekana kama muda mufupi kisha kifo cha Yesu, mitume wengi walibakia katika muji wa Yerusalemu, kwenye kulikuwa baraza lenye kuongoza. (Mdo. 8:14; 15:2) Wakristo katika Yudea walihubiri juu ya Kristo kwa watu wenye walikuwa tayari wanaamini Mungu mumoja. Lakini, mutume Paulo alitumwa na roho takatifu ili aende kuhubiria watu wa mataifa ya Wagiriki na Waroma, wenye walikuwa wanaabudu miungu mingi.​—Gal. 2:7-9; 1 Tim. 2:7.

17 Paulo alisafiri sana katika eneo lenye kuitwa leo Uturuki, na pia katika Ugiriki na Italia, na huko alianzisha makutaniko ya Kikristo kati ya watu wenye hawakukuwa Wayahudi. Wakristo hao wapya ‘waliteseka mikononi mwa wanainchi wenzao’ na walikuwa na lazima ya kutiwa moyo. (1 Tes. 2:14) Katika mwaka wa 50 hivi kisha kuzaliwa kwa Yesu, Paulo aliandikia kutaniko mupya la Thesalonike hivi: ‘Sikuzote sisi tunamushukuru Mungu tunapowataja ninyi nyote katika sala zetu, kwa maana daima sisi tunakumbuka akilini kazi yenu ya uaminifu na kazi yenu ya jasho yenye upendo na uvumilivu wenu.’ (1 Tes. 1:2, 3) Aliwatia pia moyo watiane nguvu kwa kuwaambia hivi: ‘Muendelee kufarijiana na kujengana.’​—1 Tes. 5:11.

BARAZA LENYE KUONGOZA LINATIA WENGINE MOYO

18. Namna gani baraza lenye kuongoza la wakati wa mitume lilitia moyo Filipo?

18 Baraza lenye kuongoza la wakati wa mitume lilitia moyo wale wenye walikuwa wanaongoza na Wakristo wote kwa ujumla. Wakati mweneza-injili Filipo alihubiria Wasamaria juu ya Kristo, ndugu wa baraza lenye kuongoza walimutegemeza kabisa. Walituma wawili kati yao, ni kusema, Petro na Yohana, wasali kwa ajili ya Wakristo hao wapya ili wapate roho takatifu. (Mdo. 8:5, 14-17) Kwa kweli, Filipo na wale wenye alisaidia kuwa Wakristo walipaswa kutiwa moyo kuona namna baraza lenye kuongoza liliwategemeza!

19. Wakristo wa kwanza-kwanza walijisikia namna gani kisha kusoma barua kutoka kwa baraza lenye kuongoza?

19 Kisha, baraza lenye kuongoza lilikutana ili kuamua ikiwa Wakristo wenye hawakukuwa Wayahudi walipaswa kutahiriwa, kama vile sheria ya Musa iliomba Wayahudi. (Mdo. 15:1, 2) Kwa uongozi wa roho takatifu na kisha kuchunguza Maandiko, ndugu wenye kuongoza waliamua kama haikukuwa tena lazima kufanya hivyo, na waliandikia makutaniko barua yenye kufasiria jambo hilo. Wajumbe wa baraza lenye kuongoza walitumwa katika makutaniko ili kupeleka barua hiyo. Hilo lilileta matokeo gani? “Baada ya kuisoma, walishangilia juu ya kitia-moyo hicho.”​—Mdo. 15:27-32.

20. (a) Namna gani Baraza Lenye Kuongoza leo linatia moyo ndugu na dada katika dunia yote? (b) Tutajibia ulizo gani katika habari yenye kufuata?

20 Leo, Baraza Lenye Kuongoza la Mashahidi wa Yehova linatia moyo ndugu na dada wa familia ya Beteli, na watumishi wa pekee wa wakati wote wenye kutumika katika shamba, na linatia moyo pia ndugu na dada wote katika dunia yote. Hilo linaleta matokeo gani? Kama wakati wa mitume, wanashangilia wakati wanatiwa moyo! Zaidi ya hilo, katika mwaka wa 2015, Baraza Lenye Kuongoza lilitoa broshua Umurudilie Yehova, yenye imetia moyo sana watu wengi katika dunia yote. Lakini, wale tu wenye kuongoza ndio wanapaswa kumuiga Yehova ili kutia wengine moyo? Tutajibia ulizo hilo katika habari yenye kufuata.