Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 17

Ukubali Musaada wa Yehova ili Kupinga Pepo Wachafu

Ukubali Musaada wa Yehova ili Kupinga Pepo Wachafu

“Tunapambana . . . na majeshi ya pepo wachafu katika mahali pa kimbingu.”​—EFE. 6:12.

WIMBO 55 Msiwaogope!

KIFUPI CHA HABARI *

1. Kama vile Waefeso 6:10-13 inaonyesha, Yehova anatumia njia gani moja yenye kugusa moyo sana ili kuonyesha kama anatuhangaikia? Fasiria.

YEHOVA anatusaidia kupinga maadui wetu; hiyo ni njia moja kati ya njia zenye kugusa moyo zaidi zenye anatumia ili kuonyesha kama anatuhangaikia sisi watumishi wake. Maadui wetu wakubwa ni Shetani na pepo wachafu. Yehova anatuonya juu ya maadui hao, na anatupatia mambo yenye tuko nayo lazima ili kuwapinga. (Soma Waefeso 6:10-13.) Wakati tunakubali musaada wa Yehova na kumutegemea kabisa, tunaweza kumupinga Ibilisi. Tunaweza kuwa na uhakika wenye mutume Paulo alikuwa nao. Aliandika hivi: “Kama Mungu iko upande wetu, ni nani atatushinda?”​—Ro. 8:31.

2. Tutazungumuzia nini mu habari hii?

2 Sisi Wakristo wa kweli, hatukaze sana akili yetu juu ya Shetani na pepo wachafu. Tunakaza zaidi akili yetu juu ya kujifunza kumuhusu Yehova na kumutumikia. (Zb. 25:5) Lakini, tunapaswa kujua mambo yenye Shetani anafanyaka. Juu ya nini? Ili tuepuke kudanganywa kupitia ujanja wake. (2 Ko. 2:11) Katika habari hii, tutazungumuzia njia kubwa yenye Shetani na pepo wachafu wanatumia ili kujaribu kudanganya watu. Tutazungumuzia pia mambo yenye tunaweza kufanya ili kuwapinga kabisa.

NAMNA PEPO WACHAFU WANADANGANYA WATU

3-4. (a) Kupashana habari na pepo wachafu, maana yake nini? (b) Watu wengi wanaamini tendo la kupashana habari na pepo wachafu. Ni nini inaonyesha vile?

3 Kupashana habari na pepo wachafu njo njia kubwa yenye Shetani na pepo wachafu wanatumia ili kujaribu kudanganya watu. Wale wenye kupashana habari na pepo wachafu wanasema kama wanajua mambo yenye wanadamu hawawezi kujua ao wako na uwezo juu ya mambo yenye wanadamu hawana uwezo juu yake. Kwa mufano, watu fulani wanasema kama wanaweza kujua mambo ya wakati wenye kuja kwa kutumia uaguzi ao elimu ya nyota. Wengine wanaweza kutenda kama vile wako wanazungumuza na watu wenye wamekufa. Watu fulani wanafanya uchawi, na wanaweza kujaribu kuloga mutu mwingine. *

4 Watu wengi wanaamini kama kupashana habari na pepo wachafu kuko na uwezo fulani. Uchunguzi wenye ulifanywa mu inchi 18 katika Amerika ya Kusini na Karibea ulionyesha kama karibu mutu mumoja kati ya watu tatu anaamini uchawi ao ulozi. Na karibu watu hao wote wanaamini kama inawezekana kuzungumuza na roho. Uchunguzi mwingine ulifanywa katika inchi 18 za Afrika. Katika inchi hizo, kwa kukadiria, zaidi ya nusu ya watu wenye waliulizwa maulizo walisema kama wanaamini uchawi. Kwa kweli, tunapaswa kujilinda na tabia ya kupashana habari na pepo wachafu hata kama tunaishi wapi. Shetani anatafuta kudanganya “dunia yote yenye kuikaliwa na watu.”​—Ufu. 12:9.

5. Yehova iko na mawazo gani juu ya tabia ya kupashana habari na pepo wachafu?

5 Yehova ni “Mungu wa ukweli.” (Zb. 31:5) Kwa hiyo, iko na mawazo gani juu ya tabia ya kupashana habari na pepo wachafu? Anachukia tabia hiyo! Yehova aliambia Waisraeli hivi: “Asipatikane katikati yako mutu yeyote mwenye kupitisha mutoto wake mwanaume ao mutoto wake mwanamuke katika moto, mutu yeyote mwenye kufanya uaguzi, mutu yeyote mwenye kufanya uchawi, mutu yeyote mwenye kutafuta alama za mambo yenye yatatokea, mulozi, mutu yeyote mwenye anafunga wengine kwa uchawi, mutu yeyote mwenye anatafuta shauri kwa mutu mwenye kupashana habari na pepo wachafu ao mutu mwenye kutabiri matukio, ao mutu yeyote mwenye kuuliza habari kwa wafu. Kwa maana kila mutu mwenye kufanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.” (Kum. 18:10-12) Wakristo hawaongozwe na Sheria yenye Yehova alipatia Waisraeli. Lakini, tunajua kama mawazo yake juu ya tabia ya kupashana habari na pepo wachafu haijabadilika.​—Mal. 3:6.

6. (a) Namna gani Shetani anatumia tabia ya kupashana habari na pepo wachafu ili kutendea watu mubaya? (b) Kulingana na Muhubiri 9:5, kweli juu ya hali ya watu wenye wamekufa ni gani?

6 Yehova anatuonya juu ya tabia ya kupashana habari na pepo wachafu kwa sababu anajua kama Shetani anatumia tabia hiyo ili kutendea watu mubaya. Shetani anatumia tabia ya kupashana habari na pepo wachafu ili kueneza uongo, kama vile fundisho la uongo lenye kusema kama watu wenye wamekufa wanaishi mahali pengine. (Soma Muhubiri 9:5.) Pia, Shetani anatumia tabia ya kupashana habari na pepo wachafu ili kufanya watu waendelee kuogopa na kuwafanya wasimukaribie Yehova. Kusudi lake ni hili: anapenda watu wenye kupashana habari na pepo wachafu watumainie pepo wachafu kuliko kumutumainia Yehova.

MAMBO YA KUFANYA ILI TUPINGE PEPO WACHAFU

7. Yehova anatuambia nini?

7 Kama vile tumekwisha kuona, Yehova anatuambia mambo yenye tuko na lazima ya kujua ili tuepuke kudanganywa na Shetani na pepo wachafu. Tuzungumuzie basi mambo fulani yenye tunaweza kufanya ili kupinga Shetani na pepo wachafu.

8. (a) Njia kubwa ya kupinga pepo wachafu ni gani? (b) Namna gani andiko la Zaburi 146:4 linafunua uongo wa Shetani juu ya watu wenye wamekufa?

8 Usome na kufikiri sana juu ya Neno la Mungu. Hiyo njo njia kubwa ya kupinga uongo wenye pepo wachafu wanaeneza. Neno la Mungu liko kama upanga wenye kuwa makali wenye unaweza kukata ao kufunua uongo wenye Shetani anaeneza. (Efe. 6:17) Kwa mufano, Neno la Mungu linafunua kama fundisho lenye kusema kama watu wenye wamekufa wanaweza kuzungumuza na watu wenye wako wazima, ni la uongo. (Soma Zaburi 146:4.) Linatukumbusha pia kama ni Yehova tu njo mwenye anaweza kutabiri bila kudanganyika mambo yenye itatokea wakati wenye kuja. (Isa. 45:21; 46:10) Kama tunasoma na kufikiri sana juu ya Neno la Mungu kwa ukawaida, tutakuwa tayari kukataa na kuchukia uongo wenye pepo wachafu wanapenda tuamini.

9. Tunaepuka mambo gani yenye kuwa na upatano na tabia ya kupashana habari na pepo wachafu?

9 Uepuke kufanya jambo lolote lenye kuwa na upatano na tabia ya kupashana habari na pepo wachafu. Sisi Wakristo wa kweli, tunaepuka kila aina ya kupashana habari na pepo wachafu. Kwa mufano, hatuende kuona watu wenye kupashana habari na pepo wachafu ao kujaribu kuzungumuza kwa njia yoyote na watu wenye wamekufa. Kama vile tulizungumuzia mu habari yenye kutangulia, tunaepuka desturi za maziko zenye kutegemea imani yenye kuonyesha kama watu wenye wamekufa wanaendelea kuishi mahali fulani. Na hatutumie elimu ya nyota ao kujaribu kutabiri matukio ili kutafuta kujua mambo ya wakati wenye kuja. (Isa. 8:19) Tunajua kwamba desturi hizo zote ziko hatari sana na zinaweza kutufanya tukuwe na uhusiano na Shetani na pepo wachafu.

Uige Wakristo wa wakati wa mitume kwa kuachana na kila kitu chenye unaweza kuwa nacho chenye kuwa na upatano na uchawi, na kwa kuepuka mambo ya kujifurahisha yenye kuwa na upatano na tabia ya kupashana habari na pepo wachafu (Picha hii inapatana na fungu la 10-12)

10-11. (a) Watu fulani wa wakati wa mitume walifanya nini wakati walijifunza kweli? (b) Kulingana na 1 Wakorinto 10:21, juu ya nini tunapaswa kuiga mufano wa Wakristo wa wakati wa mitume, na namna gani tunaweza kufanya vile?

10 Achana kabisa na vitu vyenye kuwa na upatano na uchawi. Watu fulani wenye waliishi katika muji wa Efeso wakati wa mitume, walikuwa wanapashana habari na pepo wachafu. Wakati walijifunza kweli, walikamata hatua kubwa. Biblia inasema kama “hesabu kubwa ya wale wenye walizoea kufanya uchawi wakakusanya vitabu vyao pamoja na wakaviteketeza kwa moto mbele ya watu wote.” (Mdo. 19:19) Watu hao walifanya nguvu yao yote ili kupinga pepo wachafu. Vitabu vyao vya mambo ya uchawi vilikuwa vya bei sana. Lakini kuliko kupana ao kuuzisha vitabu hivyo, waliviunguza. Walihangaikia sana kumupendeza Yehova, kuliko bei ya vitabu hivyo.

11 Namna gani tunaweza kuiga mufano wa Wakristo hao wa wakati wa mitume? Ni jambo la hekima kuachana kabisa na kila kitu chenye tunaweza kuwa nacho chenye kuwa na upatano na uchawi. Vitu hivyo ni vitu kama vile hirizi, ao vitu vingine vyenye watu wako navyo ao vyenye wanavaa juu ya kujaribu kujilinda na pepo wachafu.​—Soma 1 Wakorinto 10:21.

12. Ni maulizo gani yenye tunapaswa kujiuliza juu ya mambo yetu ya kujifurahisha?

12 Uchunguze kwa uangalifu mambo yako ya kujifurahisha. Ujiulize hivi: ‘Ninasomaka vitabu, magazeti, ao habari ku Enternete juu ya mambo ya uchawi? Halafu miziki yenye ninasikilizaka, vipindi vya televizyo vyenye ninaangaliaka, ao michezo ya video yenye ninachezaka? Kati ya ile mambo, kuko jambo fulani lenye kuwa na upatano na tabia ya kupashana habari na pepo wachafu? Linaonyesha mambo kama vile wanyonya-damu, maiti zenye kutembea, na mambo yenye haiko ya kawaida? Linafanya uchawi, ulozi, ao laana vionekane kuwa ni mambo ya kujifurahisha yenye haina hatari?’ Kwa kweli, hatuwezi kusema kama mambo yote ya kujifurahisha yenye kuonyesha mambo ya kuwazia ao hadisi za kuwazia, inapatana kabisa na tabia ya kupashana habari na pepo wachafu. Wakati unachunguza mambo yako ya kujifurahisha, uazimie kukamata maamuzi yenye itakusaidia kuepuka kabisa mambo yenye Yehova anachukia. Tunapenda kufanya nguvu yetu yote ili “kuendelea kuwa na zamiri safi” mbele ya Mungu wetu.​—Mdo. 24:16. *

13. Tunapaswa kuepuka kufanya nini?

13 Uepuke kueleza habari juu ya pepo wachafu. Juu ya jambo hilo, tunapaswa kuiga mufano wa Yesu. (1 Pe. 2:21) Mbele Yesu akuje ku dunia, aliishi mbinguni, na alijua mambo mingi juu ya Shetani na pepo wachafu. Lakini hakueleza habari juu ya mambo yenye pepo hao wachafu walikuwa wamefanya. Yesu alipenda kutoa ushahidi juu ya Yehova, hakupenda akuwe mutu wa kueneza habari juu ya Shetani. Tunaweza kumuiga Yesu kwa kuepuka kueneza habari juu ya pepo wachafu. Lakini, tunaonyesha kupitia maneno yetu kama “moyo [wetu] umechangamushwa na jambo moja la muzuri,” ni kusema, ile kweli.​—Zb. 45:1.

Hatuna sababu ya kuogopa pepo wachafu. Yehova, Yesu, na malaika wako na uwezo mwingi zaidi kuwapita (Picha hii inapatana na fungu la 14-15) *

14-15. (a) Juu ya nini hatupaswe kuogopa pepo wachafu? (b) Kuko ushuhuda gani wenye kuonyesha kama Yehova analinda watu wake leo?

14 Usiogope pepo wachafu. Katika ulimwengu huu muovu, mambo ya mubaya inaweza kutupata. Aksidenti, ugonjwa, ao kifo vinaweza kutokea bila kutazamia. Lakini hatupaswe kuwaza kama roho wenye hawaonekane njo wanatuletea ile mambo. Biblia inaonyesha kama “wakati na matukio yenye hayatazamiwe” vinaweza kumufikia kila mutu. (Muh. 9:11) Na kuhusu pepo wachafu, Yehova ameonyesha kama iko na uwezo zaidi kuwapita. Kwa mufano, Mungu hakumuruhusu Shetani amuue Yobu. (Yob. 2:6) Wakati wa Musa, Yehova alionyesha kama iko na uwezo zaidi kupita makuhani wenye walikuwa wanafanya mambo ya uchawi katika inchi ya Misri. (Kut. 8:18; 9:11) Yesu mwenye alikuwa ametiwa nguvu na kutukuzwa na Yehova, alionyesha kama iko na uwezo kupita Shetani na pepo wachafu wakati aliwafukuza kutoka mbinguni na kuwatupa ku dunia. Na hivi karibuni, watatupwa mu abiso, kwenye hawatakuwa na uwezo wa kutendea mubaya mutu yeyote.​—Ufu. 12:9; 20:2, 3.

15 Tunaona ushuhuda mwingi wenye kuonyesha kama Yehova analinda watu wake leo. Fikiria jambo hili: Tunahubiri na kufundisha kweli katika dunia yote. (Mt. 28:19, 20) Kwa hiyo, tunafunua matendo ya mubaya ya Ibilisi. Kwa kweli, kama Shetani angekuwa na uwezo, angesimamisha kazi yetu yote, lakini hawezi. Kwa hiyo, hatupaswe kuogopa pepo wachafu. Tunajua kama “macho ya Yehova yanaenda huku na huku katika dunia yote ili kuonyesha nguvu zake kwa ajili ya wale wenye moyo wao ni kamili kumuelekea yeye.” (2 Ny. 16:9) Kama tuko waaminifu kwa Yehova, pepo wachafu hawawezi kututendea kitu chochote chenye kinaweza kutufanya tukose uzima wa milele.

BARAKA KWA AJILI YA WALE WENYE KUKUBALI MUSAADA WA YEHOVA

16-17. Ni mufano gani wenye kuonyesha kama inaomba kuwa hodari ili kupinga pepo wachafu?

16 Inaomba kuwa hodari ili kupinga pepo wachafu, zaidi sana wakati watu wa familia ao marafiki wenye hawana nia ya mubaya wanatupinga. Lakini Yehova anabariki wale wenye kuonyesha uhodari kama huo. Fikiria mufano wa dada mwenye kuitwa Erica, mwenye kuishi katika inchi ya Ghana. Erica alikuwa na miaka 21 wakati alikubali kujifunza Biblia. Kwa sababu Baba yake alikuwa kuhani mwenye kufanya mambo ya uchawi, Erica alipaswa kujiunga na wengine katika desturi ya uchawi yenye ilitia ndani kula nyama yenye ilitolewa zabihu kwa miungu ya baba yake. Wakati Erica alikataa, watu wa familia yake waliona jambo hilo kuwa tendo la kutukana miungu. Watu wa familia yake waliamini kama miungu ingewapatia malipizi kwa kuwaletea magonjwa ya akili ao ya kimwili.

17 Watu wa familia ya Erica walijaribu kumukaza afuate desturi hiyo, lakini alikataa, hata kama alijua kuwa angefukuzwa kwao. Mashahidi fulani walimukaribisha ili aishi pamoja nao. Katika njia hiyo, Yehova alimubariki Erica kwa kumupatia familia ya mupya, ni kusema, waamini wenzake wenye walikuwa sasa ndugu na dada zake. (Mk. 10:29, 30) Hata kama watu wa jamaa yake walimukana na wakaunguza hata vitu vyake, Erica alibakia mushikamanifu kwa Yehova, akabatizwa, na sasa iko painia wa kawaida. Haogope pepo wachafu. Na kuhusu watu wa familia yake, Erica anasema hivi: “Ninasali kila siku ili watu wa familia yangu nao wapate furaha ya kujua Yehova na kuwa na uhuru wenye mutu anapata wakati anamutumikia Mungu wetu mwenye upendo.”

18. Tunapata baraka gani wakati tunamutegemea Yehova?

18 Haiko sisi wote njo tutapambana na jaribu kubwa la imani kama hilo. Lakini, sisi wote tunapaswa kupinga pepo wachafu na kumutegemea Yehova. Kama tunafanya vile, tutapata baraka mingi na tutaepuka kudanganywa na uongo wa Shetani. Tena, hatutaacha kumutumikia Yehova kwa sababu ya kuogopa pepo wachafu. Zaidi ya yote, tutatia nguvu urafiki wetu pamoja na Yehova. Mutume Yakobo aliandika hivi: “Mujitiishe wenyewe kwa Mungu lakini mumupinge Ibilisi, naye atawakimbia ninyi. Mumukaribie Mungu, naye atawakaribia ninyi.”​—Yak. 4:7, 8.

WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi

^ fu. 5 Kwa upendo, Yehova ametuonya juu ya pepo wachafu na hatari yenye wanaweza kuleta. Pepo wachafu wanatumia njia gani ili kujaribu kudanganya watu? Tunaweza kufanya nini ili kupinga pepo wachafu? Habari hii itazungumuzia namna Yehova anatusaidia ili wasitudanganye.

^ fu. 3 MAFASIRIO YA MANENO FULANI: Tendo la kupashana habari na pepo wachafu linazungumuzia imani na mazoea yenye kuwa na upatano na pepo wachafu. Linatia ndani fundisho lenye kuonyesha kama kisha mwili kufa, roho za wanadamu zinaendelea kuishi, na kama zinazungumuza na watu wenye kuishi, zaidi sana kupitia mutu fulani (mutu mwenye kupashana habari na pepo wachafu). Uchawi na uaguzi ni njia zingine za kupashana habari na pepo wachafu. Mu habari hii, neno uchawi linazungumuzia mazoea yenye kuwa na upatano na mambo yenye haiko ya kawaida. Linatia ndani kulaani na kuloga ao kuzuia ulozi. Haihusu muchezo wa kudanganya wenye kufanywa haraka kwa kutumia mikono, wenye watu fulani wanafanya ili tu kufurahisha watu.

^ fu. 12 Wazee hawana ruhusa ya kuweka sheria juu ya mambo ya kujifurahisha. Lakini, kila Mukristo anapaswa kutumia zamiri yake yenye kuzoezwa na Biblia ili kuchagua mambo yenye atasoma, mambo yenye ataangalia, ao michezo yenye atacheza. Vichwa vya familia wenye hekima wanahakikisha kama mambo ya kujifurahisha yenye watu wa familia yao wanachagua inapatana na kanuni za Biblia.​—Ku jw.org® ona habari “Je, Mashahidi wa Yehova Huwakataza Wafuasi Wao Sinema, Vitabu, au Nyimbo Fulani?” Fungua sehemu KUTUHUSU > MASWALI YANAYOULIZWA MARA NYINGI.

^ fu. 54 MAFASIRIO YA PICHA: Picha yenye kuonyesha Yesu Mufalme wetu wa mbinguni mwenye nguvu akiongoza jeshi la malaika. Kiti cha ufalme cha Yehova kiko juu yao.